Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Somo Kutoka kwa Korongo

Somo Kutoka kwa Korongo

Somo Kutoka kwa Korongo

“KWELI, korongo ya mbinguni anajua wakati wake . . . lakini watu wangu hawajui amri za BWANA.” (Yeremia 8:7, Zaire Swahili Bible) Kwa maneno hayo nabii Yeremia alitoa hukumu ya Yehova dhidi ya watu wa Yuda walioasi imani, ambao walimwacha Yehova Mungu wao na kuanza kuabudu miungu ya kigeni. (Yeremia 7:18, 31) Kwa nini Yeremia alichagua mfano wa korongo ili kuwafundisha Wayahudi wasio waaminifu?

Waisraeli walijua korongo, na hasa korongo weupe, kwa kuwa ndege hao walipitia mabara ya Biblia wakati wao wa kuhama. Jina la Kiebrania la ndege huyo mkubwa wa majini, mwenye miguu mirefu, linatokana na neno linalomaanisha jinsia ya kike linalomaanisha “mwaminifu-mshikamanifu; mwenye fadhili-upendo.” Jina hilo linamfaa ndege huyo kwa kuwa tofauti na ndege wengine, korongo dume na jike hawaachani kamwe. Baada ya kutoroka baridi kali na kukaa sehemu zenye joto kidogo, korongo wengi hurudi walikotoka mwaka baada ya mwaka na mara nyingi hurudi kwenye kiota kilekile.

Tabia ya kisilika ya korongo huonyesha sifa ya uaminifu-mshikamanifu katika njia mbalimbali za kipekee. Korongo dume na jike hushirikiana kulalia mayai na kulisha makinda. Kitabu Our Magnificent Wildlife kinaeleza hivi: ‘Korongo ni wazazi waaminifu sana. Huko Ujerumani, korongo mmoja wa kiume alikufa baada ya kuruka na kugusa nyaya fulani za umeme. Mwenzake aliendelea kulalia mayai peke yake kwa muda wa siku tatu naye aliacha kiota mara moja tu wakati alipotoka kwa muda mfupi kwenda kutafuta chakula. Katika kisa kingine, korongo dume alilea watoto wakati mwenzake alipouawa kwa kupigwa risasi.’

Naam, kwa kuwa mwaminifu kisilika na kwa kutunza makinda wake kwa upendo, korongo hutimiza maana ya jina lake—“mwaminifu-mshikamanifu.” Hivyo, korongo walikuwa mfano mzuri kwa Waisraeli wakaidi na wasio waaminifu.

Watu wengi leo huona uaminifu-mshikamanifu kuwa sifa ya kizamani—yenye kupendeza lakini isiyofaa. Kuongezeka kwa talaka, kuachana kwa wenzi wa ndoa, wizi wa pesa kwa kutumia udanganyifu, na udanganyifu wa aina nyingine, huonyesha kwamba watu hawathamini sifa ya uaminifu-mshikamanifu hata kidogo. Kinyume cha hilo, Biblia huonyesha kwamba uaminifu-mshikamanifu ni sifa yenye thamani ambayo huchochewa na upendo na fadhili. Biblia huwatia moyo Wakristo ‘wavae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.’ (Waefeso 4:24) Naam, ingawa utu mpya hutusaidia kuwa waaminifu-washikamanifu, korongo wanaweza pia kutufundisha somo fulani kuhusu uaminifu-mshikamanifu.