Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tii kwa Uaminifu Mamlaka ya Kimungu

Tii kwa Uaminifu Mamlaka ya Kimungu

Tii kwa Uaminifu Mamlaka ya Kimungu

“BWANA ndiye mwamuzi wetu; BWANA ndiye mfanya sheria wetu; BWANA ndiye mfalme wetu.”—ISAYA 33:22.

1. Ni mambo gani yaliyofanya Israeli la kale liwe taifa la pekee?

TAIFA la Israeli lilianzishwa mnamo mwaka wa 1513 K.W.K. Wakati huo, halikuwa na jiji kuu, nchi yake yenyewe, wala mfalme wa kibinadamu. Hapo zamani raia zake walikuwa watumwa. Hata hivyo, taifa hilo jipya lilikuwa la pekee kwa njia nyingine pia kwa kuwa Yehova Mungu ndiye aliyekuwa Mwamuzi, Mfanya Sheria, na Mfalme wake asiyeonekana. (Kutoka 19:5, 6; Isaya 33:22) Hakuna taifa jingine ambalo lingeweza kudai hivyo!

2. Ni swali gani linalotokea kuhusu jinsi Israeli lilivyopangwa, na kwa nini jibu hilo ni la maana kwetu?

2 Kwa kuwa Yehova ni Mungu mwenye utaratibu, na vilevile ni Mungu wa amani, tunatazamia mambo katika taifa analotawala yawe yamepangwa vizuri. (1 Wakorintho 14:33) Ndivyo ilivyokuwa na taifa la Israeli. Lakini tengenezo la kidunia linaloonekana lingewezaje kuongozwa na Mungu asiyeonekana? Tutanufaika tunapochunguza jinsi Yehova alivyotawala taifa hilo la kale, na kuzingatia hasa jinsi umuhimu wa kutii mamlaka ya kimungu unavyokaziwa na namna alivyoshughulika na Israeli.

Jinsi Taifa la Israeli la Kale Lilivyotawaliwa

3. Yehova alifanya mipango gani inayofaa ili kuwaongoza watu wake?

3 Ijapokuwa Yehova alikuwa Mfalme wa Israeli asiyeonekana, aliweka rasmi wanaume waaminifu kuwa wawakilishi wake wenye kuonekana. Kulikuwa na wakuu, vichwa vya nyumba, na wazee waliotumikia watu wakiwa washauri na waamuzi. (Kutoka 18:25, 26; Kumbukumbu la Torati 1:15) Hata hivyo, hatupaswi kukata kauli kwamba bila kuongozwa na Mungu wanaume hao wenye madaraka wangeweza kuamua mambo pasipo kukosea kwa kutumia ufahamu na uelewevu. Hawakuwa wakamilifu, na hawangeweza kusoma mioyo ya waabudu wenzao. Hata hivyo, waamuzi hao wenye kumwogopa Mungu wangeweza kuwapa waabudu wenzao mashauri yanayofaa kwa kuwa yalitegemea Sheria ya Yehova.—Kumbukumbu la Torati 19:15; Zaburi 119:97-100.

4. Ni maelekeo gani ambayo waamuzi waaminifu wa Israeli walipaswa kuyaepuka, na kwa nini?

4 Hata hivyo, mtu hakuhitaji kujua Sheria tu ili awe mwamuzi. Kwa sababu ya hali ya kutokamilika, wazee hao walipaswa kuwa waangalifu ili waepuke maelekeo yasiyofaa—kama vile ubinafsi, upendeleo, na pupa—mambo yanayoweza kupotosha hukumu. Musa aliwaambia hivi: “Msimpendelee mtu yeyote katika kutoa hukumu; mtawasikiliza bila upendeleo, wakubwa kwa wadogo. Msiogopeshwe na sura ya mtu, maana nyinyi mtapaswa kuhukumu kwa niaba ya Mungu.”(Italiki ni zetu.) Naam, waamuzi wa Israeli walikuwa wakiamua kwa niaba ya Mungu. Hilo lilikuwa pendeleo kubwa kama nini!—Kumbukumbu la Torati 1:16, 17, Biblia Habari Njema.

5. Mbali na kuweka waamuzi, Yehova alifanya mipango gani mingine ya kushughulikia watu wake?

5 Yehova alifanya mipango mingine ili kushughulikia mahitaji ya kiroho ya watu wake. Hata kabla hawajafika katika Bara Lililoahidiwa, aliwaamuru wajenge tabenakulo, ambalo lilikuwa kituo cha ibada ya kweli. Pia alifanya mpango kuwe na makuhani wa kufundisha Sheria, kutoa dhabihu za wanyama, na kufukiza uvumba asubuhi na jioni. Mungu alimweka Aroni, kaka yake Musa kuwa kuhani mkuu wa kwanza katika Israeli, kisha akawaweka rasmi wana wa Aroni kumsaidia baba yao katika kazi zake.—Kutoka 28:1; Hesabu 3:10; 2 Mambo ya Nyakati 13:10, 11.

6, 7. (a) Kulikuwa na uhusiano gani kati ya makuhani na Walawi ambao hawakuwa makuhani? (b) Tunaweza kujifunza somo gani kuhusiana na kazi mbalimbali zilizofanywa na Walawi? (Wakolosai 3:23)

6 Haikuwa kazi rahisi kushughulikia mahitaji ya kiroho ya mamilioni ya watu, nao makuhani walikuwa wachache. Kwa hiyo, mipango ilifanywa ili makuhani wasaidiwe na washiriki wengine wa kabila la Lawi. Yehova alimwambia Musa hivi: “Nawe utawapa Haruni na wanawe hao Walawi wawe nao; amepewa watu hao kabisa kwa ajili ya wana wa Israeli.”—Hesabu 3:9, 39.

7 Walawi walikuwa wamepangwa vizuri. Waligawanywa kulingana na familia tatu—wana wa Gershoni, wana wa Kohathi, na wana wa Merari—kila familia ilikuwa imepewa kazi ya kufanya. (Hesabu 3:14-17, 23-37) Huenda kazi fulani zilionekana kuwa muhimu kuliko nyingine, lakini zote zilikuwa za lazima. Wana wa Kohathi walihitaji kufanya kazi karibu na sanduku takatifu la agano na vifaa vya tabenakulo. Hata hivyo, kila Mlawi, awe ni mwana wa Kohathi au la, alikuwa na mapendeleo makubwa. (Hesabu 1:51, 53) Inasikitisha kwamba baadhi yao hawakuthamini mapendeleo yao. Badala ya kutii kwa uaminifu mamlaka ya kimungu, hawakuridhika, walitenda kwa kiburi, kimbelembele, na wivu. Mlawi mmoja anayeitwa Kora alikuwa mmoja wao.

“Je! Mwataka na Ukuhani Pia?”

8. (a) Kora alikuwa nani? (b) Ni nini ambacho huenda kilifanya Kora aanze kuwa na maoni ya kibinadamu kuelekea makuhani?

8 Kora hakuwa mkuu wa kichwa cha nyumba ya Lawi, wala hakuwa kichwa cha familia za Wakohathi. (Hesabu 3:30, 32) Hata hivyo, alikuwa mkuu aliyeheshimiwa Israeli. Huenda ikawa kazi ambazo Kora alifanya zilimwezesha kushirikiana kwa ukaribu na Aroni na wanawe. (Hesabu 4:18, 19) Baada ya kuona udhaifu wa watu hao, huenda Kora aliwaza hivi: ‘Bila shaka makuhani hawa si wakamilifu, na bado ninatazamiwa niwatii! Aroni alikuwa ametengeneza ndama ya dhahabu muda mfupi tu uliopita. Watu wetu walishiriki ibada ya sanamu kwa kuabudu ndama hiyo. Sasa Aroni, nduguye Musa anatumikia akiwa kuhani mkuu! Huo ni upendeleo ulioje! Namna gani wana wa Aroni, Nadabu na Abihu? Kwa kweli, walidharau kabisa migawo yao hivi kwamba ilimbidi Yehova awaue!’ * (Kutoka 32:1-5; Mambo ya Walawi 10:1, 2) Hata iwe Kora alikuwa akiwaza nini, ni wazi kwamba alianza kuwa na maoni ya kibinadamu kuelekea ukuhani. Jambo hilo lilifanya aasi Musa na Aroni, na hatimaye akamwasi Yehova.—1 Samweli 15:23; Yakobo 1:14, 15.

9, 10. Kora na waasi wenzake walimlaumu Musa kwa jambo gani, na kwa nini hawakupaswa kufanya hivyo?

9 Kwa kuwa Kora alikuwa mashuhuri, haikuwa vigumu kutafuta watu waliokuwa na mtazamo kama wake ili wamwunge mkono. Yeye, pamoja na Dathani na Abiramu, walipata watu 250 waliokuwa na maoni kama yake na wote walikuwa wakuu wa mkutano. Wote pamoja walimwendea Musa na Aroni na kusema: “Mkutano wote ni mtakatifu, kila mmoja miongoni mwao, BWANA naye yu kati yao; n’ nini basi kujitukuza juu ya mkutano wa BWANA?”—Hesabu 16:1-3.

10 Waasi hao hawakupaswa kukaidi mamlaka ya Musa kwa kuzingatia yale ambayo walijua tayari. Muda mfupi kabla ya hapo, Aroni na Miriamu walikuwa wamekaidi mamlaka ya Musa. Kwa kweli, walikuwa wamesababu kama Kora! Kulingana na andiko la Hesabu 12:1, 2, Aroni na Miriamu waliuliza hivi: “Je! ni kweli BWANA amenena na Musa tu? hakunena na sisi pia?” Yehova alikuwa akisikiliza. Hivyo akawaamuru Musa, Aroni, na Miriamu wakutanike kwenye lango la hema la kukutania ili aonyeshe amechagua nani awe kiongozi. Kisha Yehova akasema hivi waziwazi: “Akiwapo nabii kati yenu, mimi, BWANA, nitajifunua kwake katika maono, nitasema naye katika ndoto. Sivyo ilivyo kwa mtumishi wangu, Musa; yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote.” Baada ya hapo, Yehova alimpiga Miriamu kwa ukoma kwa muda mfupi.—Hesabu 12:4-7, 10.

11. Musa alishughulikaje na uasi wa Kora?

11 Lazima iwe Kora pamoja na watu waliomwunga mkono walijua kisa hicho. Hawakuwa na sababu ya kuasi. Hata hivyo, Musa alijaribu kusababu nao kwa subira. Aliwasihi wathamini mapendeleo yao hata zaidi, akisema: “Je! mwaona kuwa ni jambo dogo kwenu, kuwa Mungu wa Israeli amewatenga ninyi na mkutano wa Israeli, ili apate kuwakaribisha kwake?” La, halikuwa “jambo dogo”! Tayari Walawi walikuwa na mapendeleo mengi. Wangetamani nini zaidi? Maneno ya Musa yanayofuata yalifunua jinsi walivyokuwa wakisababu mioyoni mwao: “Je! mwataka na ukuhani pia?” * (Hesabu 12:3; 16:9, 10) Hata hivyo, Yehova alitendaje baada ya watu hao kuasi mamlaka yake?

Mwamuzi wa Israeli Aingilia Kati

12. Waisraeli walipaswa kufanya nini ili waendelee kuwa na uhusiano mzuri na Mungu?

12 Yehova alipowapa Waisraeli Sheria, aliwaambia watu kwamba iwapo wangetii, wangekuwa “taifa takatifu” na kwamba taifa hilo lingeendelea kuwa takatifu mradi lingekubali mpango wa Yehova. (Kutoka 19:5, 6) Sasa kwa kuwa walionyesha uasi waziwazi, Mwamuzi na Mfanya Sheria wa Israeli alilazimika kuingilia kati! Musa alimwambia Kora: “Wewe na mkutano wako wote iweni hapa mbele ya BWANA kesho, wewe, na wao, na Haruni; mkatwae kila mtu chetezo chake, na kutia uvumba juu yake, mkavilete mbele za BWANA, vyetezo mia mbili na hamsini; wewe pia, na Haruni, kila mtu na awe na chetezo chake.”—Hesabu 16:16, 17.

13. (a) Kwa nini waasi hao walionyesha kimbelembele kwa kufukiza uvumba mbele za Yehova? (b) Yehova aliwatendeaje waasi hao?

13 Kulingana na Sheria ya Mungu, makuhani peke yao ndio waliopaswa kufukiza uvumba. Waasi hao walipaswa kushtuka kwa kukumbuka kwamba Mlawi asiye kuhani hapaswi kufukiza uvumba mbele za Yehova. (Kutoka 30:7; Hesabu 4:16) Kora na watu waliokuwa wakimwunga mkono hawakushtuka! Siku iliyofuata ‘alikutanisha mkutano wote kinyume chao Musa na Aroni mlangoni pa hema ya kukutania.’ Simulizi hilo linatuambia: “Kisha BWANA akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia, Jitengeni ninyi mkaondoke kati ya mkutano huu, ili nipate kuwaangamiza mara moja.” Lakini Musa na Aroni walimsihi Yehova asiangamize mkutano huo. Yehova alisikiliza maombi yao. Lakini kuhusu Kora na watu waliomwunga mkono, ‘moto ulitoka kwa BWANA, ukawateketeza hao watu mia mbili hamsini waliofukiza uvumba.’—Hesabu 16:19-22, 35. *

14. Kwa nini Yehova alichukua hatua thabiti dhidi ya mkutano wa Israeli?

14 Jambo la kushangaza ni kwamba hata Waisraeli walioona jinsi Yehova alivyoshughulika na waasi hao hawakujifunza somo lolote. “Siku ya pili yake mkutano wote wa wana wa Israeli wakamnung’unikia Musa, na Haruni, wakasema, Ninyi mmewaua watu wa BWANA.” Waisraeli waliwaunga mkono watu hao waliokula njama! Hatimaye, subira ya Yehova ilikoma. Hakuna mtu ambaye angeweza kuwatetea watu hao, wala Musa wala Aroni. Yehova alileta tauni juu ya watu wasiotii, ‘na wale waliokufa kwa tauni walikuwa kumi na nne elfu na mia saba, zaidi ya wale waliokufa kwa jambo la Kora.’—Hesabu 16:41-49.

15. (a) Kwa nini Waisraeli hawakupaswa kusitasita kukubali uongozi wa Musa na Aroni? (b) Simulizi hili limekufundisha nini kuhusu Yehova?

15 Watu hao wote hawangekufa iwapo wangetumia uwezo wao wa kufikiri kuhusiana na mambo hayo ya uongozi. Wangejiuliza maswali kama vile: ‘Ni nani walioenda mbele ya Farao na kuhatarisha maisha yao? Ni nani waliodai Waisraeli waachiliwe? Ni nani pekee aliyealikwa kwenye Mlima Horebu ili kuzungumza na malaika wa Mungu uso kwa uso baada ya Waisraeli kukombolewa?’ Bila shaka Musa na Aroni walithibitisha kwamba walikuwa waaminifu kwa Yehova na kwamba waliwapenda watu. (Kutoka 10:28; 19:24; 24:12-15) Yehova hakufurahia kuwaua waasi hao. Hata hivyo, ilipoonekana wazi kwamba watu hao wangeendelea na uasi wao, Yehova alichukua hatua ya kukata maneno. (Ezekieli 33:11) Simulizi hilo ni muhimu sana kwetu leo. Kwa nini?

Kutambua Njia Inayotumiwa Leo

16. (a) Ni nini kilichopaswa kuwasadikisha Wayahudi wa karne ya kwanza kwamba Yesu alikuwa mwakilishi wa Yehova? (b) Kwa nini Yehova aliondoa ukuhani wa Walawi, naye alianzisha ukuhani gani badala ya huo?

16 Leo, kuna “taifa” jipya ambalo Yehova ndiye Mwamuzi, Mfanya Sheria, na Mfalme wake. (Mathayo 21:43) “Taifa” hilo lilizaliwa katika karne ya kwanza W.K. Kufikia wakati huo, badala ya tabenakulo iliyotumiwa siku za Musa, kulikuwa na hekalu zuri huko Yerusalemu ambako Walawi walikuwa wakifanya kazi. (Luka 1:5, 8, 9) Hata hivyo, katika mwaka wa 29 W.K., hekalu lingine la kiroho lilianzishwa, Yesu Kristo akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu. (Waebrania 9:9, 11) Suala la mamlaka ya kimungu likazuka tena. Yehova angetumia nani kuongoza “taifa” hili jipya? Yesu alithibitisha uaminifu wake kwa Mungu kabisa. Aliwapenda watu. Pia alifanya miujiza mingi. Hata hivyo, sawa na mababu wao wenye shingo ngumu, Walawi wengi walikataa kumkubali Yesu. (Mathayo 26:63-68; Matendo 4:5, 6, 18; 5:17) Hatimaye, Yehova alianzisha ukuhani wa kifalme badala ya ukuhani wa Walawi. Ukuhani huo wa kifalme ungali upo leo.

17. (a) Ni kikundi gani kilicho ukuhani wa kifalme leo? (b) Yehova hutumiaje ukuhani wa kifalme?

17 Ni nani walio ukuhani huo wa kifalme leo? Mtume Petro anajibu swali hilo katika barua yake ya kwanza iliyopuliziwa na Mungu. Petro aliwaandikia hivi watiwa-mafuta ambao ni washiriki wa mwili wa Kristo: “Nyinyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu kwa ajili ya miliki ya pekee, kwamba mpate kutangaza kotekote sifa bora kabisa’ za yeye aliyewaita nyinyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.” (1 Petro 2:9) Kutokana na maneno hayo, ni wazi kwamba, wakiwa kikundi, wafuasi watiwa-mafuta wa Yesu ndio “ukuhani wa kifalme,” ambao Petro aliuita pia “taifa takatifu.” Wao ndiyo njia ambayo Yehova hutumia kuandalia watu wake maagizo na mwelekezo wa kiroho.—Mathayo 24:45-47.

18. Kuna uhusiano gani kati ya wazee waliowekwa rasmi na ukuhani wa kifalme?

18 Ukuhani huo wa kifalme unawakilishwa na wazee waliowekwa rasmi na walio na madaraka katika makutaniko ya watu wa Yehova duniani pote. Tunapaswa kuwaheshimu wanaume hao na kuwaunga mkono kwa moyo wote, wawe wametiwa mafuta au la. Kwa nini? Kwa sababu Yehova ameweka rasmi wazee katika vyeo vyao kupitia roho yake takatifu. (Waebrania 13:7, 17) Hilo linawezekanaje?

19. Wazee wanawekwa rasmi na roho takatifu kwa njia gani?

19 Wazee hawa hutimiza matakwa yaliyo katika Neno la Mungu, ambalo liliandikwa kupitia roho ya Mungu. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9) Kwa hiyo tunaweza kusema kwamba wamewekwa rasmi na roho takatifu. (Matendo 20:28) Wazee wanapaswa kulifahamu kabisa Neno la Mungu. Wazee wanapaswa kuepuka kabisa upendeleo wanapotoa hukumu kwa kumwiga Mwamuzi Mkuu Kuliko Wote ambaye amewaweka rasmi.—Kumbukumbu la Torati 10:17, 18.

20. Wewe unathamini nini kuhusu wazee wanaofanya kazi kwa bidii?

20 Badala ya kupinga mamlaka yao, tunathamini kikweli wazee wetu wanaofanya kazi kwa bidii! Tunachochewa kuwa na imani katika wazee kwa sababu ya utumishi wao wa uaminifu wa miaka mingi. Wao hutayarisha na kuongoza mikutano ya kutaniko kwa uaminifu, huhubiri ‘habari njema ya Ufalme’ pamoja nasi, na kutupatia shauri la Kimaandiko tunapolihitaji. (Mathayo 24:14; Waebrania 10:23, 25; 1 Petro 5:2) Wanatutembelea tunapokuwa wagonjwa na kutufariji tunapoomboleza. Wao hutegemeza masilahi ya Ufalme kwa uaminifu na pasipo ubinafsi. Wana roho ya Yehova na kibali chake.—Wagalatia 5:22, 23.

21. Wazee wanapaswa kutambua jambo gani na kwa nini?

21 Bila shaka, wazee si wakamilifu. Wanapofikiria udhaifu wao, wao huepuka kupiga ubwana juu ya kundi ambalo ni “urithi wa Mungu.” Badala yake, wao hujichukulia kuwa ‘wafanyakazi wenzi kwa shangwe ya ndugu zao.’ (1 Petro 5:3; 2 Wakorintho 1:24) Wazee wanyenyekevu, na wanaofanya kazi kwa bidii humpenda Yehova, nao wanajua kwamba kadiri wanavyozidi kumwiga kwa ukaribu, ndivyo watakavyoweza kulinufaisha kutaniko. Kwa kuzingatia jambo hilo, wao hujitahidi daima kusitawisha sifa za kimungu kama vile upendo, huruma, na subira.

22. Imani yako katika tengenezo la Yehova linaloonekana imeimarishwaje baada ya kuchunguza simulizi la Kora?

22 Tunafurahi kama nini kwamba Yehova ndiye Mtawala wetu asiyeonekana, Yesu Kristo ndiye Kuhani wetu wa Cheo cha Juu, washiriki watiwa-mafuta wa ukuhani wa kifalme ndio walimu wetu, na wazee Wakristo walio waaminifu ndio washauri wetu! Ingawa hakuna tengenezo linaloelekezwa na wanadamu linaloweza kuwa kamilifu, tunafurahi kumtumikia Mungu pamoja na waabudu wenzetu waaminifu, ambao hufurahia kutii mamlaka ya kimungu!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Wana wale wengine wawili wa Aroni, Eleazari na Ithamari, waliweka kielelezo kizuri katika kumtumikia Yehova.—Mambo ya Walawi 10:6.

^ fu. 11 Dathani na Abiramu ambao walikula njama pamoja na Kora walikuwa wana wa Reubeni. Kwa hiyo, inaonekana hawakutamani ukuhani. Wao walichukia tu uongozi wa Musa, na kwamba kufikia wakati huo taraja lao la kuingia katika Bara Lililoahidiwa halikuwa limetimizwa.—Hesabu 16:12-14.

^ fu. 13 Nyakati za wazee wa ukoo, kila kichwa cha familia aliwakilisha mke na watoto wake mbele za Mungu, na hata kutoa dhabihu kwa niaba yao. (Mwanzo 8:20; 46:1; Ayubu 1:5) Hata hivyo, Sheria ilipotolewa, Yehova alichagua wanaume kutoka familia ya Aroni kuwa makuhani ambao wangewatolea watu dhabihu. Yaonekana waasi hao 250 hawakutaka kukubali badiliko lililofanywa katika mpango huo.

Umejifunza Nini?

• Yehova aliandaa nini kwa upendo ili kushughulikia Waisraeli?

• Kwa nini Kora hakuwa na sababu ya kumwasi Musa na Aroni?

• Tunajifunza nini kuhusiana na jinsi Yehova alivyotendea waasi hao?

• Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini mipango ya Yehova leo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Je, wewe huona mgawo wowote katika utumishi wa Yehova kuwa pendeleo?

[Picha katika ukurasa wa 10]

“N’ nini basi kujitukuza juu ya mkutano wa BWANA?”

[Picha katika ukurasa wa 13]

Wazee waliowekwa rasmi huwakilisha ukuhani wa kifalme