Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunachochewa na “Mambo Yenye Fahari ya Mungu”

Tunachochewa na “Mambo Yenye Fahari ya Mungu”

Tunachochewa na “Mambo Yenye Fahari ya Mungu”

“Twawasikia wakisema katika lugha zetu juu ya mambo yenye fahari ya Mungu.”—MATENDO 2:11.

1, 2. Ni jambo gani la kushangaza lililotukia Yerusalemu siku ya Pentekoste 33 W.K.?

ASUBUHI moja mnamo mwaka wa 33 W.K., jambo la kushangaza liliwapata wanafunzi wa Yesu Kristo, wanaume na wanawake waliokuwa wamekusanyika katika nyumba ya mtu fulani huko Yerusalemu. “Kwa ghafula kukatokea kutoka mbinguni kelele sawa na ile ya pepezi yenye nguvu inayovuma kwa kasi, nayo ikajaza nyumba yote ambayo katika hiyo walikuwa wameketi. Na ndimi kama kwamba za moto zikawa zenye kuonekana kwao . . . , nao wote wakawa wenye kujazwa roho takatifu wakaanza kusema katika lugha tofauti.”—Matendo 2:2-4, 15.

2 Umati mkubwa ulikusanyika mbele ya nyumba hiyo. Miongoni mwa umati huo mlikuwemo Wayahudi waliozaliwa ugenini, “wanaume wenye kumhofu Mungu” waliokuwa wamekuja Yerusalemu kusherehekea sikukuu ya Pentekoste. Walishangaa kwa sababu kila mmoja wao alisikia wanafunzi hao wakisema katika lugha yao wenyewe “juu ya mambo yenye fahari ya Mungu.” Ingewezekanaje ilhali wote waliokuwa wakizungumza walikuwa Wagalilaya?—Matendo 2:5-8, 11.

3. Mtume Petro alitolea umati ujumbe gani siku ya Pentekoste?

3 Miongoni mwa Wagalilaya hao mlikuwemo mtume Petro. Alieleza kwamba majuma machache yaliyotangulia, Yesu Kristo alikuwa ameuawa na watu wasio waadilifu. Hata hivyo, Mungu alikuwa amemfufua Mwana wake kutoka kwa wafu. Baada ya hapo, Yesu aliwatokea wanafunzi wake wengi, kutia ndani Petro na wengineo waliokuwa hapo. Siku kumi tu kabla ya tukio hilo, Yesu alikuwa amepaa mbinguni. Yeye ndiye aliyekuwa amewamwagia wanafunzi wake roho takatifu. Je, jambo hilo lilikuwa na maana yoyote kwa watu waliokuwa wakisherehekea sikukuu ya Pentekoste? Ndiyo. Kifo cha Yesu kilifanya iwezekane kusamehewa dhambi zao na kupokea “zawadi ya bure ya roho takatifu” iwapo wangedhihirisha imani kwake. (Matendo 2:22-24, 32, 33, 38) Kwa hiyo watazamaji hao waliitikiaje “mambo yenye fahari ya Mungu” waliyosikia? Simulizi hili linawezaje kutusaidia kuchanganua utumishi tunaomtolea Yehova?

Wachochewa Kutenda!

4. Ni unabii gani wa Yoeli uliotimizwa siku ya Pentekoste 33 W.K.?

4 Mara tu baada ya kupokea roho takatifu, wanafunzi waliokuwa Yerusalemu walianza kuwatangazia wengine habari njema ya wokovu, wakianza na umati uliokuwa umekusanyika asubuhi siku hiyo. Mahubiri yao yalitimiza unabii wenye kutokeza, uliokuwa umeandikwa na Yoeli mwana wa Pethueli karne nane mapema: “Nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume kwa wake, watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono; tena juu ya watumishi wenu, wanaume kwa wanawake, katika siku zile, nitamimina roho yangu . . . kabla haijaja hiyo siku ya BWANA iliyo kuu na itishayo.”—Yoeli 1:1; 2:28, 29, 31; Matendo 2:17, 18, 20.

5. Wakristo wa karne ya kwanza walitabiri katika maana gani? (Ona kielezi-chini.)

5 Je, hii ilimaanisha kwamba Mungu angetokeza manabii wa kiume na wa kike kama Daudi, Yoeli, na Debora, na kuwatumia kutabiri mambo ya wakati ujao? La. ‘Wana waume kwa wake, watumishi wanaume na wanawake’ Wakristo wangetabiri katika maana ya kwamba wangechochewa na roho ya Yehova kutangaza “mambo yenye fahari” ambayo Yehova alikuwa amefanya na ambayo bado angefanya. Kwa hiyo wangetumikia wakiwa wasemaji wa Aliye Juu Zaidi. * Hata hivyo, umati ulitendaje?—Waebrania 1:1, 2.

6. Baada ya kusikia hotuba ya Petro, wengi kati ya umati walichochewa kufanya nini?

6 Baada ya umati kusikia maelezo ya Petro, wengi wao walichochewa kutenda. ‘Walikubali neno lake kwa ukunjufu wa moyo’ na “wakabatizwa, na katika siku hiyo nafsi karibu elfu tatu zikaongezwa.” (Matendo 2:41) Watu hao walikuwa na ujuzi wa msingi wa Maandiko kwa kuwa baadhi yao walikuwa Wayahudi na wengine walikuwa watu waliogeuzwa imani wakawa wafuasi wa dini ya Wayahudi. Ujuzi huo pamoja na imani katika mambo waliyofundishwa na Petro, yaliwawezesha kubatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” (Mathayo 28:19) Baada ya kubatizwa, ‘waliendelea kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume.’ Wakati huohuo, wakaanza kueleza wengine kuhusu imani yao mpya. Kwa kweli, “siku baada ya siku walikuwa wakihudhuria daima kwenye hekalu kwa umoja, . . . wakimsifu Mungu na kupata upendeleo kwa watu wote.” Kwa sababu ya kazi hiyo ya kuhubiri, “Yehova a[li]endelea kuongeza kwao kila siku wale wenye kuokolewa.” (Matendo 2:42, 46, 47) Makutaniko ya Kikristo yalianzishwa upesi katika nchi nyingi ambako waumini hawa wapya waliishi. Yaelekea ongezeko hilo lilipatikana kwa sababu walijitahidi sana kuhubiri “habari njema” waliporudi nyumbani.—Wakolosai 1:23.

Neno la Mungu Lina Nguvu

7. (a) Ni nini huwavuta watu wa mataifa yote kwenye tengenezo la Yehova leo? (b) Huenda kukawa na ongezeko gani zaidi ulimwenguni pote na katika eneo lenu? (Ona kielezi-chini.)

7 Namna gani wale wanaotamani kuwa watumishi wa Mungu leo? Wao pia wanahitaji kujifunza Neno la Mungu kwa makini. Wanapojifunza Neno hilo wanapata kufahamu kwamba Yehova ni Mungu “mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.” (Kutoka 34:6; Matendo 13:48) Wanajifunza juu ya mpango wa Yehova wenye fadhili wa fidia ya Yesu Kristo, ambaye damu yake iliyomwagwa inaweza kuwatakasa na dhambi zote. (1 Yohana 1:7) Pia wanashukuru kufahamu kusudi la Mungu la ‘kufufua waadilifu na wasio waadilifu pia.’ (Matendo 24:15) Kwa sababu ya upendo kwa aliye Chanzo cha “mambo [hayo] yenye fahari” mioyo yao huwachochea kuhubiri kweli hizi zenye thamani. Kisha wao wanakuwa watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu na kubatizwa, nao huendelea “kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.” *Wakolosai 1:10b; 2 Wakorintho 5:14.

8-10. (a) Simulizi la mwanamke fulani Mkristo linathibitishaje kwamba Neno la Mungu “hukazia nguvu”? (b) Simulizi hilo limekufunza nini kuhusu Yehova na jinsi anavyowatendea watumishi wake? (Kutoka 4:12)

8 Ujuzi ambao watumishi wa Mungu hupata kwa kujifunza Biblia si wa kijuujuu tu. Ujuzi huo huchochea mioyo yao, hubadili namna wanavyofikiri, na kuwa sehemu ya maisha yao. (Waebrania 4:12) Kwa mfano, mwanamke mmoja anayeitwa Camille aliajiriwa kazi ya kutunza wazee. Martha, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alikuwa miongoni mwa watu hao waliohitaji kutunzwa. Kwa kuwa Martha alikuwa na ugonjwa mbaya wa akili, alihitaji kutunzwa daima. Alihitaji kukumbushwa kula—hata kumeza chakula. Hata hivyo, kama tutakavyoona, kuna jambo moja ambalo Martha hakusahau kamwe.

9 Siku moja, Martha alimwona Camille akilia kwa sababu ya matatizo fulani ya kibinafsi. Martha alimwekea Camille mikono na kumwomba ajifunze Biblia pamoja naye. Lakini je, mtu mwenye ugonjwa kama wa Martha angeweza kuongoza funzo la Biblia? Ndiyo! Ingawa hangeweza kukumbuka mambo mengi, Martha hakumsahau Mungu wake mtukufu; wala hakusahau kweli nzuri alizojifunza katika Biblia. Wakati wa funzo, Martha alimtia moyo Camille asome kila fungu, asome Maandiko yaliyotajwa, kisha asome swali, na kulijibu. Walifanya hivyo kwa muda, na licha ya tatizo la Martha, Camille aliendelea kupata ujuzi wa Biblia. Martha alitambua kwamba Camille alipaswa kushirikiana na watu wanaopenda kumtumikia Mungu. Kwa kufikiria jambo hilo, alimpa mwanafunzi wake Camille, rinda na viatu ili awe amevalia ifaavyo atakapohudhuria mkutano kwa mara ya kwanza kwenye Jumba la Ufalme.

10 Camille alichochewa na upendo wa kibinafsi, kielelezo, na imani ya Martha. Alikata kauli kwamba habari ambayo Martha alikuwa akimfundisha kutoka kwenye Biblia ni muhimu sana, kwa kuwa Martha alikuwa amesahau karibu mambo yote isipokuwa habari alizojifunza kutoka katika Maandiko. Baadaye, Camille alipohamishwa kwenda kwenye makao mengine ya kutunzia wazee, aliona kwamba anapaswa kuchukua hatua fulani. Mara tu alipopata fursa, alienda kwenye Jumba la Ufalme, akiwa amevalia rinda na viatu alivyopewa na Martha, na kuomba funzo la Biblia. Camille alifanya maendeleo na kubatizwa.

Wachochewa Kudhihirisha Viwango vya Yehova

11. Mbali na kuwa wenye bidii katika kazi ya kuhubiri, tunaweza kuonyeshaje kwamba tumechochewa na ujumbe wa Ufalme?

11 Leo, kuna Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni sita, ambao sawa na Martha na vilevile Camille, wanahubiri ‘habari njema ya ufalme’ ulimwenguni pote. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Sawa na Wakristo wa karne ya kwanza, wanachochewa sana na “mambo yenye fahari ya Mungu.” Wanashukuru kwa pendeleo lao la kutangaza jina la Yehova na kwamba amewamwagia roho yake. Kwa hiyo wanajitahidi kadiri wawezavyo ‘kutembea kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili,’ huku wakitii viwango vyake katika maisha yao yote. Kati ya viwango vya Mungu wanavyoheshimu ni vile vinavyohusu mavazi na mapambo.—Wakolosai 1:10a; Tito 2:10.

12. Tunapata shauri gani hususa kuhusu mavazi na mapambo katika andiko la 1 Timotheo 2:9, 10?

12 Naam, Yehova ameweka viwango kuhusu jinsi tunavyovaa na kujipamba. Mtume Paulo alionyesha baadhi ya matakwa ya Mungu kuhusiana na sura. “Natamani wanawake wajirembe wenyewe katika mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili, si kwa mitindo ya kusuka nywele na dhahabu au lulu au mvao ulio ghali sana, bali katika njia inayofaa wanawake wanaodai kumstahi Mungu, yaani, kupitia kazi zilizo njema.” * Tunajifunza nini kutokana na maneno hayo?—1 Timotheo 2:9, 10.

13. (a) Inamaanisha nini kuvalia “mavazi yenye mpangilio mzuri”? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba si vigumu kutii viwango vya Yehova?

13 Maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba Wakristo wanapaswa “wajirembe wenyewe katika mavazi yenye mpangilio mzuri.” Hawapaswi kuvalia ovyoovyo. Kila mtu hata wale wenye mapato madogo wanaweza kutimiza viwango hivyo ambavyo si vigumu kwa kuhakikisha kwamba mavazi yao ni safi, nadhifu, na ya kuheshimika. Kwa mfano, kila mwaka Mashahidi katika nchi moja ya Amerika Kusini hutembea kilometa kadhaa kupitia msituni, kisha wanasafiri kwa mtumbwi kwa muda wa saa kadhaa ili kuhudhuria kusanyiko lao la wilaya. Wakati wa safari hiyo ni jambo la kawaida watu kuanguka kwenye mto au mavazi yao kuraruliwa na miti. Kwa hiyo ndugu hao wanapofika kwenye kusanyiko, mara nyingi hawaonekani wakiwa nadhifu. Kwa hiyo wanatumia muda fulani kushona vifungo, zipu, kufua na kupiga pasi nguo watakazovalia kwenye kusanyiko. Wanathamini mwaliko wa kula kwenye meza ya Yehova, nao hutaka kuvalia kwa njia inayofaa.

14. (a) Inamaanisha nini kuvalia kwa “kiasi na utimamu wa akili”? (b) Kuvalia ‘kama watu wanaodai kustahi Mungu’ kunahusisha nini?

14 Paulo pia alionyesha kwamba tunapaswa kuvaa kwa “kiasi na utimamu wa akili.” Hii inamaanisha kwamba hatupaswi kuvalia mavazi ya kujionyesha, ya kiajabu-ajabu, yanayochochea nyege, yanayofunua uchi, au ya mitindo inayopita kiasi. Kwa kuongezea, tunapaswa kuvalia kwa njia ya ‘kumstahi Mungu.’ Hilo ni jambo linalotufanya tutafakari, sivyo? Hatupaswi kuvalia tu kwa njia inayofaa wakati tunapohudhuria mikutano na kuvalia ovyoovyo nyakati nyingine. Sikuzote mavazi yetu yanapaswa kuonyesha staha na heshima kwa kuwa sisi ni Wakristo na wahudumu wakati wote. Bila shaka, mavazi yetu ya shule na ya kazini yanapaswa kuwa mavazi yanayofaa kupatana na kazi tunayofanya. Hata hivyo, tunapaswa kuvaa kwa kiasi na kwa heshima. Ikiwa nyakati zote mavazi yetu yanaonyesha kwamba tunamwamini Mungu, hatutasita kutoa ushahidi wa vivi hivi kwa sababu ya kuaibikia mavazi yetu.—1 Petro 3:15.

‘Msiwe Mkipenda Ulimwengu’

15, 16. (a) Kwa nini ni muhimu tuepuke kuiga ulimwengu kuhusu mavazi na mapambo? (1 Yohana 5:19) (b) Tuna sababu gani inayofaa ya kujiepusha na mitindo ya kisasa ya mavazi na mapambo?

15 Shauri linalopatikana katika andiko la 1 Yohana 2:15, 16 linatoa mwongozo pia kuhusu mavazi na mapambo tunayochagua. Twasoma hivi: “Msiwe mkipenda ama ulimwengu ama vitu vilivyo katika ulimwengu. Ikiwa yeyote aupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo katika yeye; kwa sababu kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na wonyesho wa mtu wa kujivunia njia yake ya kutegemeza maisha—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.”

16 Shauri hilo ni la wakati unaofaa kama nini! Katika kipindi hiki chenye msongo mwingi wa marika, hatupaswi kuruhusu ulimwengu utuamulie mavazi tutakayovaa. Katika miaka ya karibuni, mapambo na mitindo ya mavazi imezorota. Wakristo hawawezi kufuata viwango vya mavazi vinavyowekwa na wafanyabiashara na wataalamu kwa kuwa viwango hivyo havitegemeki. Hii ni sababu nyingine ambayo hufanya sikuzote tuwe waangalifu ‘tukome kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo,’ iwapo tunataka kuishi kulingana na viwango vya Mungu na hivyo “kuremba fundisho la Mwokozi wetu, Mungu, katika mambo yote.”—Waroma 12:2; Tito 2:10.

17. (a) Tunaweza kujiuliza maswali gani tunaponunua mavazi au tunapochagua mtindo fulani? (b) Kwa nini vichwa vya familia wahangaikie mavazi ya washiriki wa familia?

17 Kabla hujaamua kununua vazi fulani, lingekuwa jambo la hekima kujiuliza: ‘Kwa nini ninavutiwa na mtindo huu? Je, mtindo huu unahusianishwa na mtumbuizaji fulani mashuhuri—mtu fulani ninayempenda? Je, magenge ya mitaani au kikundi cha watu fulani wenye roho ya kujitegemea na ya uasi wanapendelea mtindo huu?’ Tunapaswa pia kuchunguza vazi hilo kwa makini. Ikiwa ni rinda au sketi, ni refu kadiri gani? Mshono wake ukoje? Je, vazi hilo ni la kiasi, linafaa, na lenye kuheshimika, au linabana sana, linachochea nyege, au ni vazi ovyo? Jiulize, ‘Je, nikivaa vazi hili nitawakwaza wengine?’ (2 Wakorintho 6:3, 4) Kwa nini tuhangaikie mambo hayo? Kwa sababu Biblia inasema: “Hata Kristo hakujipendeza mwenyewe.” (Waroma 15:3) Wakristo ambao ni vichwa vya familia wanapaswa kuhangaikia jinsi familia zao wanavyovalia. Kwa sababu tunamheshimu Mungu mtukufu tunayemwabudu, vichwa vya familia hawapaswi kusita kutoa shauri thabiti na la upendo inapokuwa lazima.—Yakobo 3:13.

18. Ni nini ambacho hukuchochea kuwa mwangalifu kuhusu mavazi na mapambo yako?

18 Ujumbe tunaohubiri unatoka kwa Yehova ambaye ni mfano halisi wa adhama na utakatifu. (Isaya 6:3) Biblia hutuhimiza tumwige ‘tukiwa watoto wapendwa.’ (Waefeso 5:1) Mavazi na mapambo yetu yanaweza kumletea Baba yetu wa kimbingu sifa nzuri au mbaya. Bila shaka tunataka kuufurahisha moyo wake!—Mithali 27:11.

19. Tunapata manufaa gani kwa kuwajulisha wengine “mambo yenye fahari ya Mungu”?

19 Unayaonaje “mambo yenye fahari ya Mungu” ambayo umejifunza? Kwa kweli, tunapaswa kushukuru kwamba tumejifunza kweli! Kwa sababu tunadhihirisha imani katika damu iliyomwagwa ya Yesu Kristo, tunasamehewa dhambi zetu. (Matendo 2:38) Kwa sababu hiyo, tuna uhuru wa kusema mbele za Mungu. Hatuogopi kifo kama watu wasio na tumaini. Badala yake, Yesu anatuhakikishia kwamba siku moja “wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Yehova amekuwa mwema kwa kutufunulia mambo haya yote. Zaidi ya hilo, ametumwagia roho yake. Kwa hiyo, tunapaswa kuonyesha kwamba tunashukuru kwa zawadi hizi zote nzuri kwa kuheshimu viwango vyake vya juu na kumsifu kwa bidii, huku tukiwatangazia wengine “mambo yenye fahari.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Yehova alipowachagua Musa na Aroni wakazungumze na Farao kwa niaba ya watu wake, Yeye alimwambia Musa hivi: ‘Nimekufanya wewe kuwa kama Mungu kwa Farao; na huyo ndugu yako Haruni atakuwa nabii wako.’ (Kutoka 7:1, italiki ni zetu.) Aroni alitumikia akiwa nabii, si kwa kutabiri mambo ya wakati ujao, bali kwa kuwa msemaji wa Musa.

^ fu. 7 Wengi wa mamilioni ya watu waliohudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana unaoadhimishwa kila mwaka na ambao ulifanywa Machi 28, 2002, hawamtumikii Yehova. Twasali kwamba hivi karibuni mioyo ya watu hao wengi wenye kupendezwa itawachochea wapige hatua na kufikia pendeleo la kuwa watangazaji wa habari njema.

^ fu. 12 Ingawa maneno ya Paulo yalielekezwa kwa wanawake Wakristo, kanuni hizohizo zinawahusu wanaume Wakristo na vijana.

Ungejibuje?

• Ni ‘mambo gani yenye fahari’ ambayo watu walisikia siku ya Pentekoste 33 W.K., nao walitendaje?

• Mtu hupataje kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo, nao uanafunzi unahusisha nini?

• Kwa nini ni muhimu kuhangaikia mavazi na mapambo yetu?

• Ni mambo gani yanayopaswa kufikiriwa tunapoamua vazi au mtindo unaofaa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Petro alitangaza kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu

[Picha katika ukurasa wa 17]

Je, mavazi na mapambo yako yanamletea sifa Mungu unayeabudu?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wazazi Wakristo wanapaswa kuhangaikia jinsi familia zao wanavyovalia