Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Hubariki Jitihada Yenye Bidii Wakati Gani?

Yehova Hubariki Jitihada Yenye Bidii Wakati Gani?

Yehova Hubariki Jitihada Yenye Bidii Wakati Gani?

“NIACHE, niende, maana kunapambazuka.”

“Sikuachi, usiponibariki.”

“Jina lako n’nani?”

“Yakobo.”

“Jina lako hutaitwa tena Yakobo, ila Israeli, maana umeshindana na Mungu, na watu, nawe umeshinda.”—Mwanzo 32:26-28.

Mazungumzo hayo yenye kupendeza sana yalionyesha jinsi Yakobo mwenye umri wa miaka 97 alivyokuwa na uwezo usio na kifani wa nguvu za kimwili. Ijapokuwa Biblia haisemi kwamba alikuwa mshindanaji, alishindana mweleka na malaika usiku kucha. Kwa nini? Kwa sababu Yakobo alihangaikia sana urithi wake, yaani ahadi ya Yehova kwa babu yake.

Miaka mingi mapema, Esau alimwachia ndugu yake Yakobo haki yake ya mzaliwa wa kwanza kwa kubadilishana na bakuli la mchuzi. Sasa Yakobo anapata habari kwamba Esau akiwa na wanaume 400 anamkabili. Inaeleweka kwamba Yakobo aliogopa na hivyo akataka kuhakikishiwa kuhusu ahadi ya Yehova kwamba familia yake ingefanikiwa katika nchi iliyo ng’ambo ya Mto Yordani. Kulingana na sala zake, Yakobo anafanya tendo lenye kukata maneno. Alituma zawadi nyingi kwa Esau aliyekuwa anakaribia. Anatafuta pia njia ya kujilinda kwa kugawanya watu wake katika vikundi viwili na kusafirisha wake zake na watoto ng’ambo ya kivuko cha Yaboki. Kwa bidii na machozi mengi, sasa anajikakamua mwenyewe zaidi kwa kushindana mweleka usiku kucha na malaika ili “apate kujiombea kibali kwa bidii.”—Hosea 12:4 NW; Mwanzo 32:1-32.

Fikiria mfano wa Raheli, mke wa pili wa Yakobo na aliyependwa sana. Raheli alijua vizuri ahadi ya Yehova ya kumbariki Yakobo. Dada yake Lea, mke wa kwanza wa Yakobo, amebarikiwa kuwa na wana wanne huku Raheli abaki tasa. (Mwanzo 29:31-35) Badala ya kujisikitikia, anaendelea kumsihi Yehova katika sala na kutenda kulingana na sala zake. Kama nyanya yake Sara alivyofanya na Hajiri, Raheli amletea Yakobo, Bilha mjakazi wake awe mke wake wa pili ili kama vile alivyosema, “nami nipate uzao kwa yeye.” * Bilha akamzalia Yakobo wana wawili—Dani na Naftali. Raheli atangaza hivi jitihada zake wakati wa kuzaliwa kwa Naftali: “Kwa mashindano makuu nimeshindana na ndugu yangu, nikashinda!” Raheli abarikiwa zaidi kuzaa wana wawili ambao ni wake mwenyewe, Yosefu na Benyamini.—Mwanzo 30:1-8; 35:24.

Kwa nini Yehova alibariki jitihada yenye bidii ya kimwili na ya kihisia-moyo ya Yakobo na Raheli? Walitanguliza mapenzi ya Yehova na kuthamini sana urithi wao. Walisali kwa unyofu ili wabarikiwe katika maisha yao na wakatenda kulingana na mapenzi ya Mungu na kulingana na maombi yao.

Kama Yakobo na Raheli, wengi leo watakubali kwamba jitihada yenye bidii inahitajiwa ili kupata baraka za Yehova. Wengi hujitahidi kwa machozi, kuvunjika moyo, na kukata tamaa. Mama mmoja Mkristo aitwaye Elizabeth, akumbuka jitihada aliyohitaji kufanya ili kuanza kuhudhuria tena mikutano ya Kikristo kwa ukawaida baada ya kuacha kwa muda mrefu. Haikuwa rahisi kwa vile alikuwa na wavulana watano wachanga, mume asiyeamini, na alilazimika kusafiri mwendo wa kilometa 30 kwenda kwenye Jumba la Ufalme lililokuwa karibu zaidi. “Kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kulihitaji nidhamu, ambayo nilijua ingenifaidi mimi na wana wangu. Iliwasaidia kuona kwamba huo ulikuwa mwendo uliofaa kufuatwa.” Yehova alibariki jitihada zake. Kati ya wana wake watatu wenye bidii katika kutaniko la Kikristo, wawili ni watumishi wa wakati wote. Akifurahia maendeleo yao ya kiroho, yeye asema: “Wamenipita kwa ukuzi wa kiroho.” Jinsi alivyobarikiwa kwa jitihada yenye bidii!

Jitihada Yenye Bidii Ambayo Yehova Huthawabisha

Bila shaka kujitahidi na kufanya kazi kwa bidii kunathawabisha. Kadiri tunavyojitahidi kufanya jambo au mgawo fulani, ndivyo tunavyopata uradhi. Hivyo ndivyo Yehova alivyotuumba. “Ni karama ya Mungu kila mtu apate kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote,” akaandika Mfalme Solomoni. (Mhubiri 3:13; 5:18, 19) Hata hivyo, ili kupata baraka kutoka kwa Mungu, lazima tuhakikishe kwamba tunajitahidi katika mambo yanayofaa. Kwa mfano, je, mtu anaweza kutazamia kupata kibali cha Yehova iwapo anatanguliza njia yake ya maisha na kuweka mambo ya kiroho mahali pa pili? Je, Mkristo aliyejiweka wakfu aweza kutazamia baraka za Yehova iwapo anakubali kazi au cheo ambacho kitafanya akose mafundisho na ushirika wenye kujenga imani katika mikutano ya Kikristo?—Waebrania 10:23-25.

Mtu hawezi “kujiburudisha kwa mema” iwapo anafuatia sana kazi ya kimwili au utajiri na kupuuza mambo ya kiroho. Katika mfano wake wa mpanzi, Yesu alifafanua matokeo ya jitihada zinazoelekezwa kwa mambo yasiyofaa. Kuhusu ile mbegu, ‘iliyopandwa katikati ya miiba,’ Yesu alieleza kwamba “huyo ndiye anayelisikia neno, lakini hangaiko la mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu wa mali hulisonga neno, naye huwa asiyezaa matunda.” (Mathayo 13:22) Paulo pia alionya kuhusu mtego huo na akaongezea kwamba wale wanaofuatia mambo ya kimwili “huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo.” Kuna suluhisho gani kwa maisha hayo yanayodhuru kiroho? Paulo aliendelea: ‘Kimbia mambo hayo na uweke tumaini lako, si juu ya mali zisizo hakika, bali juu ya Mungu, ambaye hututolea sisi vitu vyote kwa utajiri kwa ajili ya ufurahio wetu.’—1 Timotheo 6:9, 11, 17.

Bila kujali umri wetu au muda ambao tumemtumikia Yehova, sote tunaweza kufaidika kwa kuiga jitihada yenye bidii iliyoonyeshwa na Yakobo na Raheli. Katika jitihada zao za kutafuta kibali cha Mungu, hawakusahau urithi wao, hata kama hali yao ingekuwa yenye kutisha au kukatisha tamaa. Mikazo na magumu yanayotupata leo huenda yakawa yenye kutisha, kuvunja moyo au hata kufadhaisha. Ni rahisi kushawishika kuacha pigano na kuwa windo la Shetani. Yeye aweza kutumia njia yoyote, iwe ni vitumbuizo, michezo, kazi au utajiri ili kutimiza kusudi lake. Mara nyingi watu huahidiwa kwamba watapata matokeo mazuri lakini mara nyingi hayatimizwi. Mara nyingi wanaoshawishiwa au kuvutiwa na kujihusisha katika mambo hayo, huishia kukata tamaa. Na tukuze roho ya mshindanaji mwenye bidii kama Yakobo na Raheli wa kale na kushinda mbinu za Shetani.

Ibilisi angependa sana tushindwe, tuhisi kwamba ‘hakuna tumaini. Hakuna suluhisho. Hakuna haja ya kuendelea kujaribu.’ Inafaa kama nini, sote kulinda dhidi ya mwelekeo hatari wa kushindwa na kufikiri kwamba ‘hakuna anayenipenda’ na kwamba ‘Yehova amenisahau.’ Kuwa na mawazo kama hayo huleta madhara. Je, inawezekana kwamba tumeacha kushindana mpaka tutakapopokea baraka? Kumbuka, Yehova hubariki jitihada yetu yenye bidii.

Endelea Kushindania Baraka za Yehova

Hali yetu ya kiroho tukiwa watumishi wa Yehova hutegemea hasa kuthamini kweli mbili za msingi maishani. (1) Kila mtu hupatwa na matatizo, magonjwa au magumu maishani, na (2) Yehova husikia vilio vya wale wanaomwomba kwa bidii ili kupata msaada na baraka.—Kutoka 3:7-10; Yakobo 4:8, 10; 1 Petro 5:8, 9

Hata hali yako iwe ngumu namna gani au unahisi kupungukiwa, usikubali kushindwa na “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi,” yaani kukosa imani. (Waebrania 12:1) Endelea kushindana mpaka upate baraka. Uwe mwenye subira, ukimkumbuka mzee Yakobo aliyeshindana mweleka usiku kucha ili abarikiwe. Kama mkulima anayepanda wakati wa mvua na kungoja mavuno, endelea kungoja kwa subira baraka ya Yehova katika utendaji wako wa kiroho, hata kama unahisi utendaji huo ni wa kiwango cha chini kadiri gani. (Yakobo 5:7, 8) Na kila wakati kumbuka maneno haya ya mtunga-zaburi: “Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha.” (Zaburi 126:5; Wagalatia 6:9) Simama imara, na ubaki miongoni mwa wale washindanao.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Desturi ya kuwa na masuria ilikuwako kabla ya agano la Sheria nayo iliruhusiwa na kufanywa chini ya Sheria. Mungu aliwalinda masuria kulingana na Sheria kwani wakati wa kurudisha kiwango chake alichoanzisha katika shamba la Edeni cha kuoa mke mmoja haukuwa umefika mpaka wakati Yesu Kristo angekuja. Bila shaka desturi hiyo ilisaidia kuongeza idadi ya Waisraeli upesi.