Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maandiko hutoa mwongozo gani kuhusu kulea watoto iwapo mzazi mmoja ni Shahidi wa Yehova na yule mwingine si Shahidi?

Kuna kanuni mbili muhimu za Kimaandiko ambazo hutoa mwongozo wa kulea watoto iwapo mzazi mmoja ni Shahidi na mwenzi wake si Shahidi. Moja ni: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Nyingine ni: “Mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko.” (Waefeso 5:23) Kanuni ya pili inahusu akina dada ambao waume wao ni Mashahidi na vilevile wale ambao waume wao si Mashahidi. (1 Petro 3:1) Mzazi ambaye ni Shahidi anawezaje kusawazisha kanuni hizo anapowafundisha watoto wake?

Ikiwa mume ni Shahidi wa Yehova, ana daraka la kuandalia familia yake mahitaji ya kiroho na ya kimwili. (1 Timotheo 5:8) Ingawa mama asiyeamini huenda akatumia wakati mwingi zaidi na watoto wao, baba ambaye ni Shahidi anapaswa kufundisha watoto wao mambo ya kiroho akiwa nyumbani na kuwapeleka kwenye mikutano ya Kikristo, ambapo watanufaika na mafundisho kuhusu maadili na kuwa na ushirika unaofaa.

Namna gani iwapo mke wake ambaye si Shahidi anasisitiza kuwapeleka watoto katika dini yake, au kuwafundisha imani yake? Huenda kulingana na sheria za nchi mke akawa na haki ya kufanya hivyo. Ufundishaji bora wa kiroho wa baba utawasaidia sana watoto wasishawishiwe kujiunga na ibada hiyo. Watoto wanapozidi kukua, elimu ya Biblia waliyopata kutoka kwa baba yao inapaswa kuwasaidia kufuata kweli ya Neno la Mungu. Mume anayeamini atafurahi kama nini iwapo watoto wake wataamua kuifuata kweli!

Ikiwa mama ni Shahidi wa Yehova, anapaswa kuheshimu kanuni ya ukichwa na vilevile kujali hali njema ya milele ya watoto wake. (1 Wakorintho 11:3) Mara nyingi, mwenzi asiyeamini hatapinga iwapo mke wake ambaye ni Shahidi anawafundisha watoto wao mambo ya maadili na ya kiroho, na mafundisho hayo hupatikana kwenye mikutano ya watu wa Yehova. Mama anaweza kumsaidia mume wake kuona manufaa ya elimu nzuri ambayo watoto wao wanapata kupitia tengenezo la Yehova. Anaweza kukazia kwa busara faida za kufundisha watoto wao kanuni za maadili za Biblia kwa kuwa watoto wanaishi katika ulimwengu ambao maadili yanazorota.

Hata hivyo, huenda mume asiyeamini akasisitiza kwamba watoto wake wawe katika dini yake, huku akienda nao mahali anapoabudu na kuwafundisha imani ya dini yake. Au huenda mume akapinga dini zote na kusisitiza kwamba watoto wake wasifundishwe mambo ya kidini. Akiwa kichwa cha familia, yeye ndiye mwenye daraka hasa la kuamua. *

Huku akitii ukichwa wa mume wake, mke Mkristo aliyejiweka wakfu atakumbuka maoni ya mtume Petro na Yohana, ambao walisema: “Kwa habari yetu, sisi hatuwezi kukoma kusema juu ya mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.” (Matendo 4:19, 20) Kwa sababu ya kujali hali ya kiroho ya watoto wake, mama ambaye ni Shahidi atatafuta fursa za kutoa mwongozo wa maadili. Ana daraka mbele za Yehova la kuwafundisha wengine mambo anayojua kuwa ni ya kweli, na watoto wake wanapaswa kufundishwa mambo hayo pia. (Mithali 1:8; Mathayo 28:19, 20) Mama ambaye ni Shahidi anaweza kushughulikiaje tatizo hili gumu?

Kwa mfano fikiria suala la imani katika Mungu. Huenda mke ambaye ni Shahidi akashindwa kuwa na funzo rasmi la Biblia pamoja na watoto wake kwa sababu ya vizuizi alivyowekewa na mumewe. Je, anapaswa kuepuka kuwaeleza watoto wake jambo lolote kuhusu Yehova kwa sababu ya vizuizi hivyo? La. Maneno na matendo yake yanapaswa kuonyesha kwamba anaamini kuna Muumba. Huenda watoto wake wakawa na maswali kuhusu Muumba. Anapaswa kujihisi huru kutumia uhuru wake wa kidini kwa kuwaeleza wengine kutia ndani na watoto wake imani yake katika Muumba. Hata asipoweza kuongoza funzo la Biblia pamoja na watoto wake au kwenda nao mikutanoni kwa ukawaida, anaweza kuwafundisha juu ya Yehova Mungu.—Kumbukumbu la Torati 6:7.

Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu uhusiano uliopo kati ya Shahidi na mwenzi wake asiyeamini: “Mume asiyeamini hutakaswa katika uhusiano na mke wake, na mke asiyeamini hutakaswa katika uhusiano na huyo ndugu; kama sivyo, watoto wenu kwa kweli wangekuwa si safi, lakini sasa wao ni watakatifu.” (1 Wakorintho 7:14) Yehova huona ndoa hiyo kuwa takatifu kwa sababu ya mwenzi anayeamini, nao watoto huonwa kuwa watakatifu machoni pa Yehova. Mke ambaye ni Shahidi anapaswa kufanya yote awezayo kusaidia watoto wake waelewe kweli, na kuacha mambo mikononi mwa Yehova.

Watoto wanapozidi kukua, itawabidi kuamua msimamo watakaochukua ikitegemea mambo waliyojifunza kutoka kwa wazazi wao. Huenda wakaamua kutenda kupatana na maneno ya Yesu: “Yeye aliye na shauku kubwa zaidi kwa baba au mama kuliko kwangu hanistahili mimi.” (Mathayo 10:37) Pia wanaamriwa: “Watoto, iweni watiifu kwa wazazi wenu katika muungano na Bwana.” (Waefeso 6:1) Vijana wengi wameamua ‘kumtii Mungu kuwa mtawala’ badala ya kumtii mzazi ambaye si Shahidi licha ya kuteswa na mzazi huyo. Mzazi ambaye ni Shahidi atafurahi kama nini ikiwa watoto wataamua kumtumikia Yehova licha ya upinzani!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Haki za kisheria za mke zinazohusu uhuru wa kidini zinatia ndani haki yake ya kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Nyakati nyingine, huenda mume asikubali kutunza watoto wadogo mke anapoenda mikutanoni, kwa hiyo mama mwenye upendo atalazimika kwenda nao kwenye mikutano.