Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanafurahi Kwamba Wamejifunza Kusoma!

Wanafurahi Kwamba Wamejifunza Kusoma!

Wanafurahi Kwamba Wamejifunza Kusoma!

KATIKA sehemu fulani za Visiwa vya Solomon, asilimia 80 ya Mashahidi wa Yehova hawakujua kusoma. Tatizo hilo liliwazuia kutoa maelezo kwenye mikutano ya kutaniko inayofanywa kila juma na pia lilifanya iwe vigumu kuwafundisha wengine kweli za Ufalme. Je, kweli inawezekana watu wazima ambao hawajawahi kushika kalamu wajifunze kusoma?

Broshua Jitahidi Kusoma na Kuandika, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova, imetumiwa katika mtaala wa kujifunza kusoma karibu katika makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova kotekote katika Visiwa vya Solomon. Mambo yaliyoonwa yafuatayo yanaonyesha jinsi ambavyo mamia ya watu wamesaidiwa kuboresha uwezo wao wa kusoma kupitia programu hiyo. Jambo lililo muhimu hata zaidi ni kwamba kujifunza kusoma kumewawezesha kutoa ushahidi kuhusu imani yao kwa njia bora zaidi.—1 Petro 3:15.

Mishonari mmoja aliyepewa mgawo wa kushirikiana na kutaniko moja lenye watangazaji wa Ufalme zaidi ya mia moja aliona kwamba wakati wa funzo la Biblia linalofanywa kila juma kwa kutumia gazeti Mnara wa Mlinzi, ni watu wachache tu waliokuwa na nakala, na wale waliotoa maelezo walikuwa wachache hata zaidi. Kwa nini? Hawakujua kusoma. Kutaniko lilipotangaza kuanzishwa kwa shule ya kujifunza kusoma na kuandika, mishonari huyo alifurahia kujitolea kuwa mwalimu. Shule hiyo ilipoanza, ni wanafunzi wachache tu waliohudhuria, lakini punde si punde zaidi ya watu 40 wa kila umri wakaanza kuhudhuria.

Matokeo yakawaje? Mishonari huyo asema: “Muda mfupi tu baada ya mtaala huo kuanzishwa, nilienda sokoni saa kumi na mbili asubuhi kuwanunulia mishonari chakula. Huko nilikuta baadhi ya wanafunzi, hata wale wachanga wakiuza nazi na mboga. Kwa nini? Kwa sababu walitaka kupata pesa za kutosha kununua kalamu na kitabu cha kuandikia ambacho wangetumia kwenye mtaala huo! Pia shule hiyo iliwachochea kuwa na Mnara wa Mlinzi.” Aongeza kusema: “Sasa, wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi la kutaniko, wakubwa kwa wachanga hushiriki, na mazungumzo yetu huwa machangamfu.” Mishonari huyo alifurahi sana wakati wanafunzi wanne walipomwuliza kama wanaweza kushiriki kazi ya kuhubiri kwa sababu walisema, “sasa hatuogopi tena.”

Mbali na kujua kusoma na kuandika, wanafunzi hao wamenufaika zaidi. Kwa mfano, kwa miaka mingi mke asiyeamini wa Shahidi mmoja alihangaisha sana kutaniko. Watu walipomkasirisha kidogo tu, aliwatupia mawe na hata aliwashambulia wanawake wengine kwa ubao. Kwenye mikutano ya Kikristo ambako alihudhuria mara kwa mara akiwa na mumewe, mwanamke huyo alikuwa mwenye wivu sana hivi kwamba mumewe aliamua kuvaa miwani nyeusi ili mkewe asimlaumu kwamba anawaangalia wanawake wengine.

Hata hivyo, muda mfupi baada ya shule hiyo kuanzishwa, mwanamke huyo aliuliza hivi kwa upole: “Je, ninaweza kujiunga na shule hii?” Akaambiwa anaweza. Kuanzia wakati huo na kuendelea hajawahi kukosa kuhudhuria shule hiyo au mkutano wa kutaniko. Alijitahidi sana katika masomo yake, akafanya maendeleo mazuri yaliyomletea furaha nyingi. Baada ya hapo, aliomba mtu wa kumfundisha Biblia. Mume wake alifurahi kuanza kujifunza naye, na anazidi kufanya maendeleo katika kujifunza kusoma na kuandika na pia kujifunza Biblia.

Mtu mwenye umri wa miaka 50 ambaye hajawahi kushika kalamu, huona ni vigumu sana kushika kalamu ili kuandika herufi za alfabeti. Wanapoanza kujifunza kuandika, wengine huchubuka vidole kwa sababu ya kushika kalamu kwa nguvu. Baada ya kung’ang’ana kwa majuma kadhaa kushika kalamu ifaavyo, wanafunzi fulani husema hivi kwa mshangao na kwa tabasamu: ‘Ninaweza kuandika kwa urahisi!’ Walimu hufurahi pia kuona maendeleo ya wanafunzi. Mwalimu mmoja alisema: “Inafurahisha sana kufundisha, nao wanafunzi huonyesha shukrani zao kwa maandalizi haya ya Yehova kwa kupiga makofi baada ya masomo.”

Mashahidi hawa ambao sasa wanajua kusoma na kuandika, wanashangilia pamoja na mishonari. Kwa nini? Kwa sababu sasa wanaweza kutumia uwezo wao wa kusoma na kuandika kumsifu Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Wachanga kwa wakubwa hufurahia mtaala wa kujifunza kusoma