Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Bila Kielezi Hakuwa Akisema Nao”

“Bila Kielezi Hakuwa Akisema Nao”

“Bila Kielezi Hakuwa Akisema Nao”

‘Yesu alisema kwa umati kwa vielezi. Kwa kweli, bila kielezi hakuwa akisema nao.’—MATHAYO 13:34.

1, 2. (a) Kwa nini vielezi vyenye matokeo havisahauliki kwa urahisi? (b) Yesu alitumia vielezi vya aina gani, na ni maswali gani yanayotokea kuhusiana na matumizi yake ya vielezi? (Ona pia kielezi-chini.)

JE, UNAWEZA kukumbuka kielezi ulichosikia, labda kwenye hotuba ya watu wote miaka mingi iliyopita? Si rahisi kusahau vielezi vyenye matokeo. Mwandishi mmoja alisema kwamba vielezi ‘husaidia wasikilizaji wapige picha akilini juu ya mambo wanayosikia.’ Kwa kuwa tunafahamu mambo vizuri zaidi tunapopiga picha akilini, vielezi vinaweza kufanya iwe rahisi zaidi kuelewa mambo. Vielezi hufanya maneno yaeleweke, na hutufunza mambo ambayo hudumu katika kumbukumbu letu.

2 Hakuna mwalimu yeyote duniani ambaye amewahi kutumia vielezi kwa ustadi kuliko Yesu Kristo. Mifano mingi ya Yesu hukumbukwa kwa urahisi karibu miaka elfu mbili tangu itamkwe. * Kwa nini Yesu alitumia sana vielezi kufundisha? Na ni nini kilichofanya vielezi vyake viwe na matokeo sana?

Kwa Nini Yesu Alifundisha kwa Vielezi?

3. (a) Kulingana na andiko la Mathayo 13:34, 35, ni kwa nini Yesu alitumia vielezi? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anathamini njia hii ya kufundisha?

3 Biblia hutoa sababu mbili muhimu ambazo huonyesha kwa nini Yesu alitumia vielezi. Kwanza, kwa kufanya hivyo alitimiza unabii. Mtume Mathayo aliandika hivi: “Yesu [alisema] kwa umati kwa vielezi. Kwa kweli, bila kielezi hakuwa akisema nao; ili kupate kutimizwa lililosemwa kupitia nabii aliyesema: ‘Hakika mimi nitafungua kinywa changu kwa vielezi.’” (Mathayo 13:34, 35) “Nabii” aliyenukuliwa na Mathayo ni mtungaji wa Zaburi 78:2. Mtunga-zaburi huyo aliandika kwa kuongozwa na roho ya Mungu karne kadhaa kabla Yesu hajazaliwa. Katika lugha ya awali ya Kiebrania, neno “mithali” linaweza kumaanisha pia “vielezi.” Kwa kweli ni muhimu kutambua kwamba miaka mingi mapema, Yehova aliamua kwamba Mwana wake angefundisha kwa kutumia vielezi. Bila shaka, Yehova anathamini njia hii ya kufundisha!

4. Yesu alielezaje sababu iliyofanya atumie vielezi?

4 Pili, Yesu mwenyewe alieleza kwamba alitumia vielezi ili kutenganisha watu waliokuwa na mioyo migumu. Baada ya kusimulia ‘umati huo mkubwa’ ule mfano wa mpanzi, wanafunzi wake walimwuliza: “Ni kwa nini wewe huwaambia kwa utumizi wa vielezi?” Yesu alijibu: “Nyinyi mmeruhusiwa kuzielewa siri takatifu za ufalme wa mbingu, lakini watu hao hawakuruhusiwa. Hii ndiyo sababu nawaambia kwa utumizi wa vielezi, kwa sababu, wakitazama, watazama bure, na wakisikia, wasikia bure, wala hawapati maana yake; na kuwaelekea wao unabii wa Isaya unapata utimizo, ambao husema, ‘Kusikia, mtasikia lakini kwa vyovyote hamtapata maana yake; na, kutazama, mtatazama lakini kwa vyovyote hamtaona. Kwa maana moyo wa watu hawa umekuwa usioitikia.’”—Mathayo 13:2, 10, 11, 13-15; Isaya 6:9, 10.

5. Vielezi vya Yesu vilitenganishaje wasikilizaji wanyenyekevu na wale wenye kiburi?

5 Ni mambo gani katika vielezi vya Yesu yaliyotenganisha watu? Nyakati nyingine, wasikilizaji wake walilazimika kutafuta kwa makini ili kuelewa maneno yake kabisa. Watu wanyenyekevu walitiwa moyo waulize ili wapate habari zaidi. (Mathayo 13:36; Marko 4:34) Wakati huo vielezi vya Yesu vilifunua kweli kwa wale waliokuwa na tamaa ya kujua kweli; na wakati huohuo vielezi vyake vikaficha kweli kwa watu waliokuwa na kiburi. Yesu alikuwa mwalimu mwenye kutokeza kama nini! Sasa na tuchunguze mambo yaliyofanya vielezi vya Yesu viwe na matokeo sana.

Alichagua kwa Uangalifu Habari za Kutumia

6-8. (a) Ni kitu gani ambacho wasikilizaji wa Yesu wa karne ya kwanza hawakuwa nacho? (b) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba Yesu alichagua kwa makini habari za kutumia?

6 Je, umewahi kujiuliza wanafunzi wa karne ya kwanza walihisije kumsikiliza Yesu moja kwa moja akifundisha? Hata ingawa walipendelewa kusikia sauti ya Yesu, hawakuwa na namna ya kufanya utafiti katika Maandiko ili kujikumbusha mambo aliyosema. Badala yake, walipaswa kuweka maneno ya Yesu akilini na moyoni mwao. Kwa kutumia vielezi kwa ustadi, Yesu alifanya iwe rahisi kwao kukumbuka mambo aliyofundisha. Kwa njia gani?

7 Yesu alichagua kwa uangalifu habari alizotumia. Alihakikisha kwamba ametia ndani habari iliyokuwa muhimu katika simulizi fulani au habari iliyohitajiwa ili kukazia maana. Kwa hiyo alitaja idadi hususa ya kondoo waliobaki wakati mchungaji alipoenda kumtafuta kondoo aliyepotea, saa hususa ambazo wafanyakazi walitumia katika shamba la mizabibu, na ni talanta ngapi zilizotolewa kuwa amana.—Mathayo 18:12-14; 20:1-16; 25:14-30.

8 Wakati huohuo, Yesu hakutaja habari zisizo muhimu ambazo zingefanya tusipate maana ya vielezi vyake. Kwa mfano, katika mfano wa mtumwa asiye na huruma hatuelezwi ni jinsi gani mtumwa huyo alivyopata kuwa na deni la dinari 60,000,000. Yesu alikuwa akikazia umuhimu wa kusamehe. Jambo muhimu halikuwa ni jinsi gani mtumwa huyo alivyopata deni hilo, bali jinsi alivyosamehewa, na jinsi baada ya hapo alivyomtendea mtumwa mwenzake aliyekuwa akimdai pesa zake kidogo. (Mathayo 18:23-35) Vivyo hivyo, katika kielezi cha mwana mpotevu, Yesu hakueleza ni kwa nini yule mwana mchanga aliomba urithi wake mara moja na kwa nini aliufuja. Lakini Yesu alifafanua jinsi baba huyo alivyohisi na jinsi alivyotenda wakati mwana wake alipobadili nia yake na kurudi nyumbani. Habari hizo kuhusu itikio la baba zilikuwa muhimu kuhusiana na jambo ambalo Yesu alikuwa akieleza, kwamba Yehova ‘husamehe kabisa.’—Isaya 55:7; Luka 15:11-32.

9, 10. (a) Yesu alikazia nini alipofafanua wahusika katika vielezi vyake? (b) Yesu alifanyaje iwe rahisi kwa wasikilizaji wake na wengineo kukumbuka vielezi vyake?

9 Yesu pia alitumia busara kufafanua wahusika katika mifano yake. Badala ya kutoa habari nyingi kuhusu sura za wahusika hao, mara nyingi Yesu alikazia mambo waliyofanya au jinsi walivyotenda katika visa alivyosimulia. Kwa hiyo, badala ya kufafanua sura ya Msamaria mwema, Yesu alieleza jambo jingine lililo muhimu zaidi—jinsi Msamaria huyo alivyomsaidia kwa huruma Myahudi aliyejeruhiwa, aliyekuwa amelala kando ya barabara. Yesu aliandaa habari iliyohitajiwa ili kufundisha kwamba upendo kwa jirani wapaswa kutia ndani watu ambao si wa jamii yetu au taifa letu.—Luka 10:29, 33-37.

10 Yesu alichagua habari kwa uangalifu ili vielezi vyake viwe vifupi na visiwe na mambo mengi mno. Kwa hiyo alifanya iwe rahisi kwa wasikilizaji wake wa karne ya kwanza na wengine wengi ambao baadaye wangesoma vitabu vya Injili vilivyoandikwa kwa roho ya Mungu, kukumbuka vielezi hivyo na pia mambo ambayo vilifundisha.

Vilihusu Mambo ya Kawaida Maishani

11. Toa mifano inayoonyesha jinsi mifano ya Yesu ilivyotaja vitu ambavyo bila shaka alijionea alipokuwa akikua huko Galilaya.

11 Yesu alikuwa stadi katika kutumia vielezi vilivyohusu maisha ya watu. Mifano yake mingi inahusu vitu ambavyo bila shaka aliviona alipokuwa akikua huko Galilaya. Ebu fikiria kidogo kuhusu maisha yake ya utotoni. Mara nyingi aliona mama yake akitayarisha mkate wenye chachu kwa kuchukua unga wenye chachu uliokuwa umesalia na kuutumia ili kuutia chachu unga aliokanda. (Mathayo 13:33) Mara nyingi aliwaona wavuvi wakishusha nyavu zao katika maji ya Bahari ya Galilaya. (Mathayo 13:47) Mara nyingi aliwaona watoto wakicheza sokoni. (Mathayo 11:16) Bila shaka Yesu alitambua vitu vingine vya kawaida ambavyo alitumia katika vielezi vyake—mbegu zikipandwa, karamu za ndoa zenye furaha, na mashamba ya nafaka zilizokomaa.—Mathayo 13:3-8; 25:1-12; Marko 4:26-29.

12, 13. Mfano wa Yesu wa ngano na magugu unaonyeshaje kwamba alifahamu hali za kwao?

12 Basi, haishangazi kwamba vielezi vingi vya Yesu vilihusu mambo ya kawaida maishani. Kwa hiyo, ili kuelewa kikamili ustadi aliotumia katika njia hii ya kufundisha, inafaa kuchunguza jinsi maneno yake yalivyomaanisha kwa wasikilizaji wake Wayahudi. Na tuchunguze mifano miwili.

13 Kwanza, katika mfano wa ngano na magugu, Yesu alisimulia kuhusu mtu fulani aliyepanda ngano safi katika shamba lake lakini “adui” akalivamia na kupanda magugu katikati ya ngano. Kwa nini Yesu alichagua tendo hilo la uhasama? Kumbuka kwamba Yesu alisimulia kielezi hiki karibu na Bahari ya Galilaya, na yaonekana Wagalilaya wengi walikuwa wakulima. Mkulima angepata madhara makubwa sana iwapo adui angekuja shambani mwake kwa siri na kupanda magugu hatari katikati ya mbegu nzuri. Sheria zilizokuwako wakati huo zinaonyesha kwamba watu walifanya hivyo. Je, si wazi kwamba Yesu alitumia hali ambayo wasikilizaji wake wangeweza kuielewa?—Mathayo 13:1, 2, 24-30.

14. Katika mfano wa Msamaria mwema, kwa nini Yesu alitumia barabara ‘iliyotoka Yerusalemu kwenda Yeriko’ kukazia hoja yake?

14 Pili, kumbuka mfano wa Msamaria mwema. Yesu alianza kwa kusema: “Mtu fulani alikuwa akiteremka kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko akaanguka miongoni mwa wapokonyaji, ambao walimvua nguo na pia kumpiga, wakaenda zao, wakimwacha yeye nusura kufa.” (Luka 10:30) Yesu alitumia barabara ‘iliyotoka Yerusalemu kwenda Yeriko’ kukazia hoja yake. Yesu alisimulia mfano huo akiwa Yudea, karibu na Yerusalemu; kwa hiyo yaelekea wasikilizaji wake walijua barabara hiyo. Barabara hiyo ilikuwa hatari sana hasa kwa mtu aliyetembea peke yake. Ilijipinda-pinda kwa hiyo kulikuwa na sehemu nyingi ambazo wahalifu wangeweza kuotea.

15. Kwa nini hakuna mtu ambaye angeweza kutetea kutojali kwa kuhani na Mlawi katika kielezi cha Msamaria mwema?

15 Pia tunapaswa kutambua jambo jingine ambalo Yesu alitaja kuhusu barabara “kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko.” Kulingana na simulizi hilo, kuhani ndiye aliyekuwa wa kwanza kupita katika barabara hiyo kisha akafuatwa na Mlawi, lakini wote wawili hawakusimama kumsaidia mtu huyo. (Luka 10:31, 32) Makuhani walitumikia hekaluni huko Yerusalemu, na walisaidiwa na Walawi. Makuhani na Walawi wengi walikaa Yeriko wakati ambapo hawakuwa wakifanya kazi hekaluni, kwa kuwa Yeriko lilikuwa umbali wa kilometa 23 tu kutoka Yerusalemu. Kwa hiyo, bila shaka walipita katika barabara hiyo mara kwa mara. Pia, ona kwamba kuhani na Mlawi walikuwa wakitembea katika barabara ‘iliyotoka Yerusalemu,’ hivyo wakielekea mbali na hekalu. * Kwa hiyo hakuna mtu ambaye angeweza kutetea kutojali kwa watu hao kwa kusema, ‘Walikwepa mtu huyo aliyejeruhiwa kwa sababu alionekana ni kama amekufa, na kugusa maiti kungefanya wasitumikie hekaluni.’ (Mambo ya Walawi 21:1; Hesabu 19:11, 16) Je, si wazi kwamba kielezi cha Yesu kilihusu mambo ambayo wasikilizaji wake waliyafahamu?

Vilihusu Uumbaji

16. Kwa nini haishangazi kwamba Yesu alifahamu uumbaji vizuri?

16 Vielezi na mifano mingi ya Yesu inaonyesha kwamba alifahamu mimea, wanyama, na hali ya anga. (Mathayo 6:26, 28-30; 16:2, 3) Alipata wapi ujuzi huo? Bila shaka, alipokuwa akikua huko Galilaya, alipata fursa ya kutosha kuchunguza uumbaji wa Yehova. Isitoshe, Yesu ni “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote,” naye Yehova alimtumia kuwa “stadi wa kazi” kuumba vitu vyote. (Wakolosai 1:15, 16; Mithali 8:30, 31) Je, inashangaza kwamba Yesu alifahamu uumbaji vizuri? Na tuone jinsi alivyotumia ujuzi huo kwa ustadi ili kufundisha.

17, 18. (a) Maneno ya Yesu kwenye Yohana sura ya 10 yanaonyeshaje kwamba alifahamu tabia za kondoo? (b) Watu ambao wametembea katika nchi zinazotajwa katika Biblia wameona kuna uhusiano gani kati ya wachungaji na kondoo wao?

17 Miongoni mwa vielezi vya Yesu vyenye kugusa hisia ni kile kinachopatikana katika Yohana sura ya 10, ambapo analinganisha uhusiano wa karibu kati yake na wafuasi wake na ule uliopo kati ya mchungaji na kondoo zake. Maneno ya Yesu yanaonyesha kwamba alifahamu vizuri tabia za kondoo. Alionyesha kwamba kondoo hukubali kuongozwa, nao humfuata mchungaji wao kwa uaminifu. (Yohana 10:2-4) Wageni ambao wametembelea nchi zinazotajwa katika Biblia wamejionea uhusiano wa pekee uliopo kati ya wachungaji na kondoo. Katika karne ya 19, mwanamazingira H. B. Tristram alisema: “Pindi moja niliona mchungaji akicheza na kondoo wake. Alijifanya kuwa anatoroka; kondoo walimfuata na kumzunguka. . . . Hatimaye kundi lote lilimzunguka na kuanza kuchezacheza kando yake.”

18 Kwa nini kondoo hufuata mchungaji wao? “Kwa sababu wajua sauti yake,” akasema Yesu. (Yohana 10:4) Je, kweli kondoo wanajua sauti ya mchungaji wao? Kutokana na jambo alilojionea, George A. Smith aliandika hivi katika kitabu chake The Historical Geography of the Holy Land: “Mara kwa mara tulifurahia kupumzika mchana kando ya mojawapo ya visima vya Yudea, ambapo wachungaji watatu au wanne walileta kondoo wao. Kondoo hao walichanganyikana, nasi tukajiuliza jinsi ambavyo kila mchungaji angetambua kondoo wake. Lakini baada ya kondoo hao kumaliza kunywa maji na kucheza, kila mchungaji alielekea upande tofauti wa bonde hilo, na kila mmoja akaitana kwa sauti ambayo ingetambuliwa na kondoo wake; nao kondoo wa kila mchungaji walijitenga na hao kondoo wengine na kufuata mchungaji wao kwa utaratibu kama vile walivyokuja.” Yesu alipata njia bora zaidi ya kueleza hoja yake. Tukitambua, kutii mafundisho yake, na kufuata mwongozo wake, basi tunaweza kupata utunzaji mwororo na wenye upendo wa “mchungaji mwema.”—Yohana 10:11.

Vilihusu Mambo Ambayo Wasikilizaji Wake Waliyafahamu

19. Yesu alitumiaje kwa njia yenye matokeo msiba uliotukia ili kupinga wazo lisilo la kweli?

19 Vielezi vyenye matokeo vinaweza kutia ndani mambo yaliyoonwa au mifano inayotufundisha mambo fulani. Pindi moja, Yesu alitumia tukio la karibuni kupinga wazo lisilo la kweli kwamba msiba huwapata watu wanaoustahili. Alisema: “Wale kumi na wanane ambao mnara katika Siloamu uliangukia, kwa njia hiyo ukiwaua, je, mwawazia kwamba walithibitishwa kuwa wadeni [wenye dhambi] wakubwa zaidi kuliko watu wengine wote wenye kukaa Yerusalemu?” (Luka 13:4) Yesu alisababu waziwazi na kupinga wazo la kwamba mambo yanayowapata watu huwa yamepangwa kimbele. Wale 18 hawakufa kwa sababu ya kutenda dhambi fulani iliyomkasirisha Mungu. Badala yake, walipatwa na msiba huo kwa sababu ya wakati na tukio lisilotazamiwa. (Mhubiri 9:11, NW) Kwa hiyo alikanusha fundisho la uwongo kwa kutaja kisa ambacho wasikilizaji wake walikifahamu vizuri.

20, 21. (a) Mafarisayo waliwalaumu wanafunzi wa Yesu jinsi gani? (b) Yesu alitumia simulizi gani la Kimaandiko kuonyesha kwamba Yehova hakukusudia sheria yake ya Sabato itumiwe kwa njia isiyofaa? (c) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

20 Alipokuwa akifundisha, Yesu pia alitumia mifano ya Kimaandiko. Kumbuka wakati Mafarisayo walipowashutumu wanafunzi wake kwa kukwanyua nafaka na kuila siku ya Sabato. Kwa kweli, wanafunzi hawakuvunja Sheria ya Mungu, bali walivunja sheria kali zilizotungwa na Mafarisayo kuhusu kazi zisizopaswa kufanywa siku ya Sabato. Ili kuonyesha kwamba Mungu hakuwa amekusudia sheria yake ya Sabato itumiwe kwa njia hiyo isiyofaa, Yesu alisimulia kisa kinachopatikana katika andiko la 1 Samweli 21:3-6. Alipokuwa na njaa, Daudi na watu wake waliingia katika tabenakulo na kula mikate ya wonyesho ambayo ilikuwa imeondolewa katika tabenakulo. Kwa kawaida, mikate hiyo ya zamani iliwekwa kando ili iliwe na makuhani. Hata hivyo, chini ya hali hizo, Daudi na watu wake hawakushutumiwa kwa kula mikate hiyo. Kwa kweli, hilo ndilo simulizi pekee katika Biblia linaloonyesha kuhusu kuliwa kwa mikate hiyo na watu ambao hawakuwa makuhani. Yesu alijua simulizi ambalo lingefaa kutumiwa, na bila shaka wasikilizaji wake Wayahudi walifahamu simulizi hilo.—Mathayo 12:1-8.

21 Kwa kweli, Yesu alikuwa Mwalimu Mkuu! Bila shaka tunashangazwa na uwezo wake usio na kifani wa kufundisha kweli muhimu kwa njia ambayo wasikilizaji wake wangeweza kuelewa. Hata hivyo, tunawezaje kumwiga tunapofundisha? Habari hii itazungumziwa katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Vielezi vya Yesu vilikuwa vya aina mbalimbali, navyo vilitia ndani mifano, ulinganisho, na maneno ya ufananisho. Anajulikana sana kwa kutumia mifano ambayo imefafanuliwa kuwa ‘masimulizi mafupi ambayo kwa kawaida huwa yamebuniwa nayo hutumiwa kufundisha kweli ya kiroho au ya kiadili.’

^ fu. 15 Yerusalemu lilikuwa katika nyanda za juu kuliko Yeriko. Kwa hiyo kama ilivyotajwa katika mfano huo, msafiri angekuwa “akiteremka” anaposafiri “kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko.”

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini Yesu alifundisha kwa kutumia vielezi?

• Ni mfano gani unaoonyesha kwamba Yesu alitumia vielezi ambavyo wasikilizaji wake wa karne ya kwanza walifahamu?

• Yesu alitumiaje kwa ustadi ujuzi aliokuwa nao juu ya uumbaji katika vielezi vyake?

• Yesu alitumiaje matukio yaliyojulikana na wasikilizaji wake?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yesu alisimulia kuhusu mtumwa aliyekataa kusamehe mwenzake deni ndogo na kuhusu baba aliyemsamehe mwanawe aliyefuja urithi wake wote

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yesu alikazia jambo gani katika mfano wa Msamaria mwema?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Je, kweli kondoo wanajua sauti ya mchungaji wao?