Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Hajasema Kamwe Mtu Mwingine Kama Hivi”

“Hajasema Kamwe Mtu Mwingine Kama Hivi”

“Hajasema Kamwe Mtu Mwingine Kama Hivi”

“Wote wakaanza kutoa ushahidi mwema juu yake wakistaajabia maneno yenye uvutio mwingi yenye kutoka kinywani mwake.”—LUKA 4:22.

1, 2. (a) Kwa nini maofisa waliotumwa kumkamata Yesu walirudi mikono mitupu? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba si maofisa peke yao waliovutiwa na mafundisho ya Yesu?

MAOFISA walishindwa kufanya kazi yao. Walitumwa wakamkamate Yesu Kristo, lakini wakarudi mikono mitupu. Makuhani wakuu na Mafarisayo walitaka waelezwe sababu: “Ni kwa nini hamkumleta?” Kwa kweli, kwa nini maofisa hawakumkamata mtu ambaye hangeweza kujikinga? Maofisa walisema: “Hajasema kamwe mtu mwingine kama hivi.” Walivutiwa sana na mafundisho ya Yesu hivi kwamba hawakuona sababu ya kumkamata na kumweka rumande mtu huyo mwenye kupenda amani. *Yohana 7:32, 45, 46.

2 Si maofisa hao peke yao waliovutiwa na mafundisho ya Yesu. Biblia inatuambia kwamba watu wengi walikuja ili kumsikiliza tu akisema. Watu wa kwao walistaajabia “maneno yenye uvutio mwingi yenye kutoka kinywani mwake.” (Luka 4:22) Akiwa kwenye mashua, alizungumza mara kadhaa na umati wa watu waliokusanyika kwenye ufuo wa Bahari ya Galilaya. (Marko 3:9; 4:1; Luka 5:1-3) Pindi moja, “umati mkubwa” ulikaa pamoja naye kwa siku kadhaa, bila kula.—Marko 8:1, 2.

3. Sababu kuu iliyofanya Yesu awe mwalimu mkuu ni ipi?

3 Ni nini kilichofanya Yesu awe mwalimu mkuu? Sababu kuu ni upendo. * Yesu alipenda kweli alizofundisha, na kuwapenda watu aliowafundisha. Hata hivyo, Yesu pia alikuwa na uwezo wa pekee wa kutumia njia mbalimbali za kufundisha. Katika makala za funzo za toleo hili, tutazungumzia baadhi ya njia zenye matokeo alizotumia na jinsi tunavyoweza kuiga njia zake.

Alifundisha kwa Njia Rahisi na Yenye Kueleweka

4, 5. (a) Kwa nini Yesu alitumia lugha rahisi kufundisha, na ni nini kinachotokeza kuhusiana na jambo hilo? (b) Mahubiri ya Mlimani yanaonyeshaje kwamba Yesu alifundisha kwa njia rahisi?

4 Kwa kawaida watu waliosoma sana hutumia lugha isiyoeleweka na wasikilizaji wao. Lakini wengine wasipotuelewa watanufaikaje na ujuzi wetu? Akiwa mwalimu, Yesu hakuzungumza kamwe mambo yasiyoeleweka na wengine. Ebu wazia msamiati ambao angeweza kutumia. Hata hivyo, licha ya ujuzi wake mwingi, aliwafikiria wasikilizaji wake, hakujifikiria mwenyewe. Alijua kwamba wengi wao walikuwa watu “wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Matendo 4:13) Ili waweze kuelewa, alitumia lugha ambayo watu hao wangeweza kuielewa. Huenda maneno aliyotumia yalikuwa rahisi, lakini yalifunua ujuzi na ufahamu mwingi.

5 Kwa mfano, fikiria Mahubiri ya Mlimani, yanayopatikana katika andiko la Mathayo 5:3-7:27. Huenda mahubiri hayo yalimchukua Yesu muda wa dakika 20 tu. Hata hivyo, mafundisho hayo yalikuwa yenye kina, na yaligusia hasa chanzo cha uzinzi, talaka, na kufuatia sana vitu vya kimwili. (Mathayo 5:27-32; 6:19-34) Hata hivyo, hakutumia lugha ngumu. Kwani, hakuna neno hata moja ambalo mtoto angeshindwa kulielewa kwa urahisi! Kwa hiyo tunaweza kuelewa ni kwa nini baada ya kumaliza mahubiri hayo, umati huo, ambao yaelekea ulitia ndani wakulima wengi, wachungaji, na wavuvi—“ulishangaa juu ya njia yake ya kufundisha”!—Mathayo 7:28.

6. Toa mfano unaoonyesha jinsi Yesu alivyotaja mambo muhimu sana kwa kutumia maneno machache.

6 Mara nyingi Yesu alitaja mambo muhimu sana kwa kutumia maneno machache, yaliyo wazi na rahisi. Ona mifano kadhaa: “Hakuna awezaye kutumikia kama mtumwa mabwana-wakubwa wawili; . . . hamwezi kutumikia kama watumwa Mungu na Utajiri.” “Komeni kuhukumu ili msipate kuhukumiwa.” “Kwa matunda yao mtawatambua watu hao.” “Watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua wahitaji.” “Wote wauchukuao upanga wataangamia kwa upanga.” “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mlipeni Mungu vitu vya Mungu.” “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” * (Mathayo 6:24; 7:1, 20; 9:12; 26:52; Marko 12:17; Matendo 20:35) Leo maneno hayo yangali yanakumbukwa ingawa Yesu aliyasema karibu miaka 2,000 iliyopita.

Utumizi wa Maswali

7. Kwa nini Yesu aliuliza maswali?

7 Yesu alitumia maswali kwa njia yenye kutokeza. Mara nyingi alitumia maswali hata wakati ambapo ingechukua muda mfupi zaidi kuwaeleza wasikilizaji wake mambo moja kwa moja. Kwa nini basi aliuliza maswali? Pindi kwa pindi alitumia maswali yenye kupenya ili kufunua nia ya wapinzani wake, na hivyo kuwanyamazisha. (Mathayo 12:24-30; 21:23-27; 22:41-46) Hata hivyo, mara nyingi Yesu alitumia maswali ili kufundisha kweli, kufanya wasikilizaji wake waeleze mambo yaliyokuwa mioyoni mwao, na pia kuwachochea na kuwazoeza wanafunzi wake wafikiri. Sasa na tuchunguze mifano miwili inayohusu mtume Petro.

8, 9. Yesu alitumiaje maswali kumsaidia Petro afikie mkataa unaofaa kuhusu suala la kulipa kodi ya hekalu?

8 Kwanza, kumbuka wakati wakusanya-kodi walipomwuliza Petro ikiwa Yesu analipa kodi ya hekalu. * Petro, ambaye mara nyingine alitenda harakaharaka, alijibu, “Ndiyo.” Hata hivyo, muda mfupi baada ya hapo, Yesu alisababu naye: “‘Wewe wafikiri nini Simoni? Ni kutoka kwa nani wafalme wa dunia hupokea ushuru wa forodhani au kodi ya kichwa? Ni kutoka kwa wana wao au ni kutoka kwa wageni?’ Aliposema: ‘Kutoka kwa wageni,’ Yesu alimwambia: ‘Basi, kwa kweli hao wana hawalipi kodi.’” (Mathayo 17:24-27) Petro alipaswa kuelewa waziwazi kile ambacho Yesu alitaka kumfundisha kupitia maswali. Kwa nini?

9 Katika siku za Yesu, washiriki wa familia za wafalme hawakulipa kodi. Kwa hiyo, Yesu hakupaswa kulipa kodi kwa sababu alikuwa Mwana mzaliwa-pekee wa Mfalme wa kimbingu aliyeabudiwa katika hekalu. Ona kwamba badala ya kumjibu Petro moja kwa moja tu, Yesu alitumia maswali kwa njia yenye matokeo lakini kwa fadhili ili kumsaidia Petro afikie mkataa unaofaa—na labda aone uhitaji wa kufikiri kwa makini zaidi kabla ya kusema.

10, 11. Yesu alifanyaje wakati Petro alipokata sikio la mtu mmoja usiku wa Sikukuu ya Kupitwa mwaka wa 33 W.K., na hilo linaonyeshaje kwamba Yesu alielewa umuhimu wa maswali?

10 Mfano wa pili unahusu jambo lililotukia usiku wa Sikukuu ya Kupitwa mwaka wa 33 W.K. wakati umati ulipokuja kumkamata Yesu. Wanafunzi walimwuliza Yesu iwapo wanapaswa kumpigania. (Luka 22:49) Badala ya kungoja jibu, Petro alikata sikio la mtu mmoja kwa upanga (ingawa huenda Petro alinuia kumjeruhi zaidi mtu huyo). Petro alitenda kinyume cha mapenzi ya bwana wake, kwa kuwa Yesu alikuwa tayari kabisa kukamatwa. Yesu alifanyaje? Kwa kuwa sikuzote Yesu alikuwa mwenye subira, alimwuliza Petro maswali matatu: “Kikombe ambacho Baba amenipa, je, sipaswi kukinywa kwa vyovyote?” “Wafikiri kwamba siwezi kuomba Baba yangu anipe mimi katika dakika hii malejioni zaidi ya kumi na mawili ya malaika? Katika kisa hicho, Maandiko yangetimizwaje kwamba lazima itendeke kwa njia hii?”—Yohana 18:11; Mathayo 26:52-54.

11 Fikiria kidogo simulizi hilo. Yesu, akiwa amezungukwa na umati wenye hasira alijua kwamba kifo chake kilikuwa kimekaribia na kwamba kuondolewa kwa lawama kwa jina la Baba yake na wokovu wa wanadamu ulimtegemea yeye. Hata hivyo, papo hapo alitumia wakati kukazia kweli muhimu akilini mwa Petro kwa kuuliza maswali. Je, si wazi kwamba Yesu alielewa umuhimu wa maswali?

Kutia Chumvi Kimakusudi

12, 13. (a) Utiaji chumvi ni nini? (b) Yesu alitumiaje njia ya kutia chumvi ili kukazia upumbavu wa kuchambua makosa madogo ya ndugu zetu?

12 Katika huduma yake, mara nyingi Yesu alitumia njia nyingine ya kufundisha yenye matokeo—utiaji chumvi. Huo ni utiaji chumvi kimakusudi ili kukazia jambo. Kwa kutia chumvi, Yesu alifanya watu wapige picha akilini mwao ambazo haingekuwa rahisi kuzisahau. Na tuchunguze mifano michache.

13 Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alikazia uhitaji wa ‘kukoma kuhukumu’ wengine, aliposema: “Kwa nini wautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako, lakini hulifikirii boriti lililo katika jicho lako mwenyewe?” (Mathayo 7:1-3) Je, unaweza kupiga picha akilini kuhusu jambo hilo? Mtu ambaye hupenda kuchambua wengine anajitolea kutoa unyasi tu katika “jicho” la ndugu yake. Mchambuzi huyo anadai kwamba ndugu yake hawezi kuona mambo waziwazi na kufikia maamuzi yanayofaa. Lakini uwezo wa mchambuzi huyo wa kuamua mambo umeathiriwa na “boriti”—gogo au mhimili unaoweza kutumiwa kutegemeza paa. Ni njia yenye kutokeza kama nini ya kukazia jinsi lilivyo jambo la upumbavu kuchambua makosa madogo ya ndugu zetu ingawa huenda sisi wenyewe tukawa na makosa makubwa sana!

14. Kwa nini maneno ya Yesu kuhusu kuchuja inzi mwenye kuuma na kumeza ngamia yalikuwa utiaji chumvi usio na kifani?

14 Pindi nyingine, Yesu aliwashutumu Mafarisayo kuwa “viongozi vipofu, ambao humchuja inzi mwenye kuuma lakini humgugumia ngamia.” (Mathayo 23:24) Njia hiyo ya kutia chumvi haikuwa na kifani. Kwa nini? Kulikuwa na tofauti kubwa sana kati ya inzi mwenye kuuma na ngamia, ambaye ni mmojawapo wa wanyama wakubwa zaidi waliojulikana wakati huo na watu waliomsikiliza Yesu. Inakadiriwa kwamba ngamia mmoja ana uzito unaotoshana na inzi wa kuuma milioni 70! Pia, Yesu alijua kwamba Mafarisayo walichuja divai yao kwa kutumia kichujio cha kitambaa. Watu hao wenye kusisitiza sheria walifanya hivyo ili waepuke kumeza inzi mwenye kuuma na hivyo kuwa najisi kisherehe. Hata hivyo, kwa njia ya mfano walimeza ngamia, ambaye pia hakuwa safi. (Mambo ya Walawi 11:4, 21-24) Hoja ya Yesu ilikuwa wazi. Mafarisayo walifuata kwa makini hata yale matakwa madogo kabisa ya Sheria, lakini wakapuuza mambo mazito zaidi—“haki na rehema na uaminifu.” (Mathayo 23:23) Yesu alifunua kabisa utu wao!

15. Yesu alifundisha masomo gani kwa kutumia utiaji chumvi?

15 Katika huduma yake yote, mara nyingi Yesu alitumia utiaji chumvi. Fikiria mifano kadhaa. “Imani yenye ukubwa wa punje ya haradali” ambayo ingeweza kuhamisha mlima—Yesu alikazia kwa njia yenye matokeo sana jinsi imani ndogo inavyoweza kutimiza mambo mengi. (Mathayo 17:20) Mfano wa ngamia mkubwa anayejaribu kujipenyeza kwenye tundu la sindano unaeleza vizuri kama nini jinsi ilivyo vigumu kwa tajiri kumtumikia Mungu huku aking’ang’ania vitu vya kimwili! (Mathayo 19:24) Je, hushangazwi na jinsi Yesu alivyotumia usemi wa kimfano kwa njia yenye kupendeza na kutumia uwezo wake kupata matokeo makubwa kwa maneno machache?

Njia ya Kusababu Kiakili Isiyoweza Kukanushwa

16. Sikuzote Yesu alitumiaje uwezo wake wa kufikiri?

16 Akiwa na akili kamilifu, Yesu alikuwa stadi sana katika kusababu na watu kiakili. Hata hivyo, hakutumia uwezo huo vibaya kamwe. Katika mafundisho yake, sikuzote alitumia uwezo wake wa kufikiri ili kuendeleza kweli. Nyakati nyingine alisababu kwa kutumia akili kwa njia isiyo na kifani kukanusha mashtaka bandia ya wapinzani wake wa kidini. Mara nyingi, alitumia njia ya kusababu kiakili ili kufundisha wanafunzi wake masomo muhimu. Na tuchunguze ustadi wa Yesu wa kusababu kwa kutumia akili.

17, 18. Yesu alitumiaje njia ya kusababu kiakili isiyo na kifani kukanusha shtaka bandia la Mafarisayo?

17 Fikiria pindi ambayo Yesu alimponya mtu aliyepagawa na roho mwovu na ambaye hakuweza kuona wala kuzungumza. Mafarisayo waliposikia kuhusu muujiza huo, walisema: “Jamaa huyu hatoi roho waovu ila kupitia Beelzebubi [Shetani], mtawala wa roho waovu.” Ona kwamba Mafarisayo walikubali kuwa nguvu zinazozidi za kibinadamu zinahitajiwa ili kuwafukuza roho wa Shetani. Hata hivyo, Mafarisayo walisema nguvu za Yesu zilitoka kwa Shetani ili kuzuia watu wasimwamini Yesu. Akionyesha kwamba Mafarisayo hawakuwa wamefikiria vizuri hoja yao ili wafikie mkataa wa kiakili, Yesu alijibu: “Kila ufalme uliogawanyika dhidi yao wenyewe huja kwenye ukiwa, na kila jiji au nyumba iliyogawanyika dhidi yayo yenyewe haitasimama. Katika njia hiyohiyo, ikiwa Shetani afukuza Shetani, amekuwa mwenye kugawanyika dhidi yake mwenyewe; basi, ufalme wake utasimamaje?” (Mathayo 12:22-26) Kwa kweli, Yesu alikuwa akisema: ‘Ikiwa ningekuwa mjumbe wa Shetani kama msemavyo, nikiharibu kazi za Shetani, basi Shetani angekuwa akitenda kinyume cha masilahi yake na angeanguka hivi punde.’ Hiyo ilikuwa njia ya kusababu kiakili isiyo na kifani, sivyo?

18 Kisha Yesu alisababu tena kuhusiana na habari hiyo. Alijua kwamba baadhi ya wanafunzi wa Mafarisayo walikuwa wamefukuza roho waovu. Kwa hiyo, akauliza swali rahisi lakini ambalo liliwashinda: “Ikiwa mimi nafukuza roho waovu kwa njia ya Beelzebubi, ni kwa njia ya nani wana [au wanafunzi] wenu huwafukuza?” (Mathayo 12:27) Kwa njia fulani, hoja ya Yesu ilikuwa: ‘Ikiwa kwa kweli, ninafukuza roho waovu kwa nguvu za Shetani, basi wanafunzi wenu lazima wawe wanawafukuza kwa nguvu hizohizo.’ Mafarisayo wangesemaje? Hawangeweza kukubali kamwe kwamba wanafunzi wao walitumia nguvu za Shetani. Kwa kusababu kiakili kwa njia yenye kusadikisha, Yesu alifanya shtaka lao dhidi yake lionekane kuwa lisilo la akili.

19, 20. (a) Yesu alitumiaje njia ya kusababu kiakili inayofaa? (b) Yesu alitumiaje njia ya kusababu ya ‘si zaidi sana’ alipokuwa akijibu swali la wanafunzi wake walioomba wafundishwe kusali?

19 Mbali na kutumia njia ya kusababu kiakili kunyamazisha wapinzani wake, Yesu pia alitumia hoja za kiakili na zenye kushawishi ili kufundisha kweli zenye kutia moyo na zinazochangamsha kuhusu Yehova. Mara nyingi alitumia njia ya kusababu tunayoweza kuiita “si zaidi sana,” ili kuwasaidia wasikilizaji wake wafanye maendeleo kutokana na kweli walizojua na kupata usadikisho zaidi. Na tuchunguze mifano miwili tu.

20 Wanafunzi wake walipomwomba awafundishe jinsi ya kusali, Yesu aliwajibu kwa kuwasimulia mfano wa mtu ambaye kwa sababu ya “udumifu wake wa ujasiri,” alifaulu kumshawishi rafiki yake ampe vitu alivyotaka. Pia Yesu alitaja utayari wa wazazi ‘kuwapa watoto wao zawadi zilizo bora.’ Kisha akamalizia: “Ikiwa nyinyi, mjapokuwa waovu, mwajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, si zaidi sana yule Baba aliye mbinguni atawapa roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:1-13) Hoja ya Yesu hapa haihusu mambo yaliyo sawa bali tofauti iliyopo kati ya mambo. Ikiwa rafiki ambaye hakuwa na nia ya kusaidia, hatimaye angeweza kushawishiwa amtimizie jirani mahitaji yake, na ikiwa wazazi wa kibinadamu wasio wakamilifu hujali mahitaji ya watoto wao, si zaidi sana Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo atawapa roho takatifu watumishi wake waaminifu wanaosali kwake kwa unyenyekevu!

21, 22. (a) Yesu alisababu kwa kutumia njia gani alipotoa shauri kuhusu kushughulika na mahangaiko kuhusiana na vitu vya kimwili? (b) Baada ya kuchunguza njia chache za Yesu za kufundisha, tunafikia mkataa gani?

21 Yesu alisababu kwa njia hiyohiyo alipotoa shauri la hekima kuhusu jinsi ya kushughulika na mahangaiko kuhusiana na vitu vya kimwili. Alisema: “Angalieni vema kwamba kunguru hawapandi mbegu wala hawavuni, nao hawana bohari wala ghala, na bado Mungu huwalisha. Nyinyi ni wenye ubora zaidi kama nini kuliko ndege? Angalieni vema jinsi mayungiyungi hukua; hayo hayamenyeki wala hayasokoti . . . Ikiwa, basi, Mungu huvisha hivyo mimea shambani ambayo ipo leo na kesho hutupwa ndani ya joko, si zaidi sana atawavisha nyinyi, nyinyi wenye imani kidogo!” (Luka 12:24, 27, 28) Naam, ikiwa Yehova hujali ndege na maua, je, si zaidi sana watumishi wake? Bila shaka, njia hiyo ya kusababu isiyo na kifani na ya fadhili iligusa mioyo ya wasikilizaji wa Yesu.

22 Baada ya kuchunguza njia chache za kufundisha za Yesu, tunaweza kufikia mkataa kwa urahisi kwamba wale maofisa walioshindwa kumkamata hawakuwa wakitia chumvi waliposema: “Hajasema kamwe mtu mwingine kama hivi.” Lakini labda Yesu anajulikana zaidi kwa kutumia vielezi au mifano katika kufundisha. Kwa nini alitumia njia hiyo? Na ni nini kilichofanya vielezi vyake viwe na matokeo sana? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Yaelekea maofisa hao walikuwa wawakilishi wa Sanhedrini chini ya mamlaka ya makuhani wakuu.

^ fu. 3 Ona makala “Niliweka Kiolezo kwa Ajili Yenu” na “Nifuateni kwa Kuendelea,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi, Agosti 15, 2002.

^ fu. 6 Nukuu hili la mwisho linalopatikana katika andiko la Matendo 20:35, limenukuliwa na mtume Paulo peke yake, ijapokuwa maana ya maneno hayo imedokezwa katika vitabu vya Injili. Huenda Paulo alipokea maneno hayo kwa mdomo (ama kutoka kwa mwanafunzi fulani aliyemsikia Yesu akisema maneno hayo au kutoka kwa Yesu aliyefufuliwa) au kwa kufunuliwa na Mungu.—Matendo 22:6-15; 1 Wakorintho 15:6, 8.

^ fu. 8 Wayahudi walitakiwa kulipa kodi ya hekalu ya drakma mbili (karibu mshahara wa siku mbili) kila mwaka. Pesa hizo zilitumiwa kurekebisha hekalu, kwa utumishi uliofanywa huko, na kwa dhabihu za kila siku zilizotolewa kwa niaba ya taifa hilo.

Je, Unakumbuka?

• Ni mifano gani inayoonyesha kwamba Yesu alifundisha kwa njia rahisi na yenye kueleweka?

• Kwa nini Yesu alitumia maswali alipofundisha?

• Utiaji chumvi ni nini, naye Yesu alitumiaje njia hiyo ya kufundisha?

• Yesu alitumiaje njia ya kusababu kiakili ili kufundisha wanafunzi wake kweli zenye kuchangamsha kumhusu Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yesu alitumia lugha rahisi ambayo watu wa kawaida wangeweza kuielewa

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mafarisayo ‘walichuja inzi mwenye kuuma na kugugumia ngamia’