Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mbona Leo Hakuna Majirani Wanaojali?

Mbona Leo Hakuna Majirani Wanaojali?

Mbona Leo Hakuna Majirani Wanaojali?

“Jamii ya kisasa haimtambui jirani,” akasema Benjamin Disraeli, mwanasiasa mashuhuri wa karne ya 19 kutoka Uingereza.

WAKUBA walio wazee huboresha maisha yao kwa njia isiyo ya kawaida: wana vikundi vinavyoitwa círculos de abuelo yaani, vikundi vya mababu na nyanya. Kulingana na ripoti moja ya mwaka wa 1997, Mkuba 1 kati ya kila Wakuba 5 wazee ni mshiriki wa vikundi hivyo. Kwenye vikundi hivyo wazee hao hupata marafiki, utegemezo na msaada ambao huwawezesha kuishi maisha bora. ‘Madaktari wa familia wanapotaka kusambaza habari kuhusu chanjo ya kuzuia ugonjwa fulani, wao huwaendea wazee wa vikundi hivyo ambao wako tayari na wanaweza kuwasaidia,’ linasema gazeti World-Health.

Hata hivyo, inasikitisha kwamba katika nchi nyingi za ulimwengu, hakuna vikundi kama hivyo vinavyojali hali ya wazee. Kwa mfano, fikiria kisa chenye kuhuzunisha cha Wolfgang Dircks, aliyeishi katika nyumba fulani za kupanga huko Ulaya magharibi. Miaka kadhaa iliyopita, gazeti The Canberra Times liliripoti kwamba ingawa familia 17 zilizoishi katika nyumba hizo pamoja na Wolfgang hazikuwa zikimwona, ‘hakuna hata mtu mmoja aliyefikiria kubisha mlango wake.’ Hatimaye wakati mwenye nyumba hizo alipokuja, “aliipata mifupa ya Wolfgang ikiwa imeketi mbele ya televisheni.” Kwenye mapaja yake kulikuwa na orodha ya vipindi vya televisheni ya Desemba 5, 1993. Wolfgang alikuwa amekufa kwa muda wa miaka mitano. Huo ni uthibitisho ulioje kwamba majirani hawajali wenzao! Si ajabu kwamba mwandishi mmoja alisema katika makala moja kwenye gazeti The New York Times Magazine kwamba watu wa mahali anapoishi, sawa na watu wa sehemu nyingine nyingi, ‘hawajuani.’ Je, hali iko hivyo mahali unapoishi?

Ni kweli kwamba jamii fulani za mashambani bado zinafurahia ujirani wa kweli nazo jamii nyingine mijini zinajitahidi kuwasaidia watu wawe wenye kuwajali majirani. Hata hivyo, wakazi wengi wa mijini huhisi wametengwa na pia huhisi wanaweza kupatwa na hatari fulani katika ujirani wao. Wanahisi hivyo kwa kuwa hawajui majirani wao. Jinsi gani?

Kuishi Bila Kujua Jirani

Bila shaka wengi wa majirani wetu wanaishi karibu nasi. Mmemeto wa televisheni, vivuli vya watu wakipita karibu na dirisha, kuwashwa na kuzimwa kwa taa, mngurumo wa magari yakiingia na kutoka, sauti za nyayo za watu wakipitapita ushorobani, milango ikifunguliwa na kufungwa, ni ishara kwamba majirani bado wako “hai.” Hata hivyo, hakuwezi kuwa na ujirani wa kweli ikiwa watu wanaoishi karibu-karibu hawajuani au wanapuuzana kwa sababu ya hekaheka za maisha. Huenda watu wakahisi kwamba hakuna haja ya kujishughulisha na majirani au kuhisi wana daraka lolote kuwaelekea. Gazeti Herald Sun la Australia linakiri hivi: ‘Watu hawajui kinachotendeka katika ujirani wao, na hivyo hawahisi wana daraka lolote kuelekea jamii. Sasa ni rahisi kupuuza au kuwaepuka watu wasiopendeza katika jamii.’

Hali hiyo haishangazi. Katika ulimwengu ambapo watu ni “wenye kujipenda wenyewe,” majirani wameanza kupata matokeo ya maisha yao ya ubinafsi. (2 Timotheo 3:2) Matokeo hayo ni kwamba watu wengi wanakuwa wapweke na wanahisi wametengwa. Hali hiyo hutokeza kutoaminiana, hasa ikiwa kuna jeuri au uhalifu katika ujirani. Nayo hali hiyo ya kutoaminiana hufanya watu wasioneane huruma.

Hata hali iweje katika ujirani wako, bila shaka unakubali kwamba majirani wema wanafaa katika jamii. Watu hutimiza mambo mengi wanaposhirikiana wakiwa na lengo moja. Majirani wema wanaweza pia kuwa baraka. Makala inayofuata itaonyesha jinsi majirani wanavyoweza kuwa baraka.