Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwige Mwalimu Mkuu

Mwige Mwalimu Mkuu

Mwige Mwalimu Mkuu

“Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu . . . , kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.”—MATHAYO 28:19, 20.

1, 2. (a) Sisi sote ni walimu kwa njia gani? (b) Wakristo wa kweli wana daraka gani la pekee inapohusu kufundisha?

JE, WEWE ni mwalimu? Kwa njia fulani, sisi sote ni walimu. Kila mara unapomwelekeza msafiri aliyepotea njia, unapomwonyesha mfanyakazi mwenzako jinsi ya kufanya kazi fulani, au unapomweleza mtoto jinsi ya kufunga kamba za viatu, unafundisha. Kusaidia watu kwa njia hizo huleta uradhi, sivyo?

2 Wakristo wa kweli wana daraka la pekee inapohusu kufundisha. Tumeagizwa ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu . . . , kuwafundisha.’ (Mathayo 28:19, 20) Katika kutaniko pia, tunapata fursa za kufundisha. Wanaume wanaostahili huwekwa rasmi ili kutumikia wakiwa “wachungaji na walimu,” kwa kusudi la kujenga kutaniko. (Waefeso 4:11-13) Katika shughuli zao za Kikristo za kila siku, wanawake waliokomaa wanapaswa kuwa “walimu wa lililo jema” wa wanawake vijana. (Tito 2:3-5) Sote tunahimizwa kuwatia moyo waamini wenzetu, na tunaweza kutii himizo hilo kwa kutumia Biblia kuwajenga wengine. (1 Wathesalonike 5:11) Ni pendeleo lililoje kuwa mwalimu wa Neno la Mungu na kuwaeleza wengine mambo ya kiroho yenye thamani yanayoweza kuwanufaisha milele!

3. Tunawezaje kufanya ufundishaji wetu uwe na matokeo tukiwa walimu?

3 Hata hivyo, tunawezaje kuboresha ufundishaji wetu ili uwe wenye matokeo? Hasa, ni kwa kumwiga Mwalimu Mkuu, Yesu. ‘Lakini tunawezaje kumwiga Yesu?’ huenda wengine wakajiuliza. ‘Yeye alikuwa mkamilifu.’ Ni kweli kwamba hatuwezi kuwa walimu wakamilifu. Hata hivyo, licha ya uwezo wetu, tunaweza kufanya yote tuwezayo kuiga jinsi ambavyo Yesu alifundisha. Na tuchunguze tuone jinsi tunavyoweza kuiga njia nne alizotumia—kufundisha kwa njia rahisi, kutumia maswali kwa njia yenye matokeo, kusababu kwa kutumia akili, na vielezi vinavyofaa.

Fundisha kwa Njia Rahisi

4, 5. (a) Kwa nini ni muhimu kufundisha kweli ya Biblia kwa njia rahisi? (b) Ili kufundisha kwa njia rahisi, kwa nini tunapaswa kuzingatia maneno tunayotumia?

4 Kweli za msingi za Neno la Mungu si ngumu. Yesu alisema hivi katika sala: “Nakusifu wewe hadharani, Baba, . . . kwa sababu umewaficha mambo haya wenye hekima na wenye akili na umeyafunua kwa vitoto.” (Mathayo 11:25) Yehova amefunua makusudi yake kwa watu wanyofu na wanyenyekevu. (1 Wakorintho 1:26-28) Kwa hiyo ni muhimu kufundisha kweli ya Biblia kwa njia rahisi.

5 Unapoongoza funzo la Biblia la nyumbani au kurudia watu waliopendezwa, unawezaje kufundisha kwa njia rahisi? Tulijifunza nini kutoka kwa Mwalimu Mkuu? Ili wasikilizaji wake ambao wengi wao walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida,” wapate kumwelewa, Yesu alitumia lugha rahisi ambayo wangeweza kuelewa. (Matendo 4:13) Kwa hiyo ili kufundisha kwa njia rahisi, tunapaswa kwanza kufikiria maneno tutakayotumia. Si lazima tutumie maneno ya kujionyesha ili kusadikisha wengine ukweli wa Neno la Mungu. ‘Usemi huo wenye kupita kiasi’ unaweza kuogopesha, hasa wale wenye elimu ndogo au uwezo mdogo. (1 Wakorintho 2:1, 2) Mfano wa Yesu unaonyesha kwamba maneno rahisi yaliyochaguliwa vizuri yanaweza kufundisha kweli kwa njia yenye matokeo sana.

6. Tunawezaje kuepuka kumweleza mwanafunzi wa Biblia habari nyingi mno?

6 Ili kufundisha kwa njia rahisi, ni lazima pia tuwe waangalifu tusimweleze mwanafunzi wa Biblia habari nyingi kupita kiasi. Yesu alifikiria uwezo wa wanafunzi wake. (Yohana 16:12) Ni lazima sisi pia tumfikirie mwanafunzi. Kwa mfano, tunapoongoza funzo tukitumia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, si lazima tueleze kila jambo. * Wala haifai kupitia habari hiyo harakaharaka, kana kwamba kumaliza mafungu fulani ndilo jambo kuu. Badala yake, uwezo na mahitaji ya mwanafunzi ndiyo yatakayoamua kiasi cha habari tutakayojifunza. Mradi wetu ni kumsaidia mtu tunayejifunza naye awe mwanafunzi wa Kristo na mwabudu wa Yehova. Tunahitaji kutumia muda wowote unaohitajiwa ili kumsaidia mwanafunzi anayependezwa aelewe vizuri mambo anayojifunza. Hivyo, ukweli unaweza kugusa moyo wake na kumchochea kutenda.—Waroma 12:2.

7. Ni madokezo gani yanayoweza kutusaidia kufundisha kwa njia rahisi tunapotoa hotuba katika kutaniko?

7 Tunapotoa hotuba katika kutaniko, hasa kunapokuwa na wageni, tunawezaje kutumia usemi ‘unaoeleweka kwa urahisi’? (1 Wakorintho 14:9) Fikiria madokezo matatu yanayoweza kusaidia. Kwanza, eleza maneno yoyote yasiyofahamika ambayo utatumia. Tumepata maneno ya pekee kwa sababu ya kulielewa Neno la Mungu. Tukitumia maneno kama vile “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” “kondoo wengine,” na “Babiloni Mkubwa,” huenda tukalazimika kuyaeleza zaidi kwa kutumia maneno rahisi. Pili, epuka kutumia maneno mengi sana. Maneno mengi sana yaliyo magumu, yanaweza kufanya wasikilizaji wasipendezwe na hotuba yako. Tunaweza kufundisha kwa urahisi kwa kutotumia maneno yasiyo ya lazima. Tatu, usijaribu kuzungumzia habari nyingi kupita kiasi. Huenda tukapata mambo mengi sana yenye kupendeza baada ya kufanya utafiti. Ni afadhali kupanga hotuba katika mambo makuu kadhaa, kisha kuyazungumzia katika muda uliowekwa kwa kutumia tu habari yenye kusadikisha na yenye kueleweka vizuri.

Kutumia Maswali kwa Njia Yenye Matokeo

8, 9. Tunawezaje kuchagua swali litakalofaa hali za mwenye nyumba? Toa mifano.

8 Kumbuka kwamba Yesu alikuwa stadi sana katika kutumia maswali ili kufanya wanafunzi wake waeleze yaliyokuwa akilini mwao. Pia alitumia maswali kuwachochea na kuwazoeza kufikiri. Kupitia maswali yake, Yesu aliwafikia mioyo na kuwachochea kwa upole. (Mathayo 16:13, 15; Yohana 11:26) Kama Yesu, tunawezaje kutumia maswali kwa njia yenye matokeo?

9 Tunapohubiri nyumba kwa nyumba, tunaweza kutumia maswali kuamsha kupendezwa, na hivyo kuweka msingi wa kuzungumza juu ya Ufalme wa Mungu. Tunawezaje kuchagua swali litakalofaa hali za mwenye nyumba? Uwe macho. Unapokaribia nyumba, tazama mazingira. Je, kuna vitu vya kuchezea, jambo linaloonyesha kwamba kuna watoto katika nyumba hiyo? Ikiwa vipo, huenda tukauliza, ‘Je, umewahi kujiuliza ulimwengu utakuwaje wakati watoto wako watakapokuwa watu wazima?’ (Zaburi 37:10, 11) Je, kuna makufuli kadhaa kwenye mlango wa mbele, au kuna ulinzi mkali? Tunaweza kuuliza: ‘Je, unafikiri kuna wakati ambapo watu kama vile mimi na wewe tutakuwa na usalama nyumbani mwetu na barabarani?’ (Mika 4:3, 4) Je, kuna jambo fulani linaloonyesha kwamba kuna mgonjwa? Huenda tukauliza: ‘Je, kuna wakati ambapo kila mtu atakuwa na afya njema?’ (Isaya 33:24) Madokezo mengi yanaweza kupatikana katika kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko. *

10. Tunawezaje kutumia maswali ‘kuteka’ mawazo na hisia za moyo wa mwanafunzi wa Biblia, lakini tunapaswa kukumbuka nini?

10 Tunawezaje kutumia maswali kwa njia yenye matokeo tunapoongoza mafunzo ya Biblia? Tofauti na Yesu, hatuwezi kusoma mioyo. Hata hivyo, maswali ya busara na ya utambuzi yanaweza kutusaidia ‘kuteka’ mawazo na hisia za moyo wa mwanafunzi. (Mithali 20:5) Tuseme, tunajifunza sura yenye kichwa “Kwa Nini Kuishi Maisha ya Kimungu Huleta Furaha,” katika kitabu Ujuzi. Sura hiyo inazungumzia maoni ya Mungu kuhusu ukosefu wa unyofu, uasherati, na mambo mengine. Mwanafunzi anaweza kujibu kwa usahihi maswali yaliyochapishwa, lakini je, anakubali mambo anayojifunza? Huenda tukauliza: ‘Je, unaona kwamba maoni ya Yehova kuhusu mambo hayo yanafaa?’ ‘Unawezaje kutumia kanuni hizo za Biblia katika maisha yako?’ Hata hivyo, kumbuka kwamba unahitaji kumheshimu na kumpa adhama mwanafunzi. Hatungependa kuuliza maswali ambayo yatamwaibisha au kumfedhehesha mwanafunzi wa Biblia.—Mithali 12:18.

11. Watoaji wa hotuba za watu wote wanawezaje kutumia maswali kwa njia yenye matokeo?

11 Watoaji wa hotuba za watu wote wanaweza pia kutumia maswali kwa njia yenye matokeo. Maswali ambayo wasikilizaji wetu hawahitaji kuyajibu kwa sauti yanaweza kuwasaidia wafikiri na watumie akili. Yesu alitumia maswali hayo mara kwa mara. (Mathayo 11:7-9) Kwa kuongezea, baada ya utangulizi, huenda msemaji akatumia maswali kutokeza mambo makuu atakayozungumzia. Anaweza kusema: “Katika hotuba yetu leo, tutazungumzia majibu ya maswali yafuatayo . . .” Kisha, anapomalizia, anaweza kutaja tena maswali hayo ili kurudia mambo makuu.

12. Toa mfano unaoonyesha jinsi wazee Wakristo wanavyoweza kutumia maswali kusaidia mwabudu mwenzao apate faraja kutoka kwa Neno la Mungu.

12 Katika kazi yao ya uchungaji, wazee Wakristo wanaweza kutumia maswali kusaidia ‘nafsi iliyoshuka moyo’ kupata faraja kutoka kwa Neno la Yehova. (1 Wathesalonike 5:14) Kwa mfano, ili kusaidia mtu aliyeshuka moyo, mzee anaweza kutumia andiko la Zaburi 34:18. Andiko hilo linasema: “BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” Ili kuhakikisha kwamba mtu aliyeshuka moyo anaona jinsi andiko hilo linavyomhusu, huenda mzee akauliza: ‘Yehova yu karibu na nani? Je, nyakati nyingine wewe huhisi kuwa “umevunjika moyo” na “kupondeka roho”? Ikiwa, kama vile isemavyo Biblia, Yehova yu karibu na watu hao, je, hiyo haimaanishi kwamba yu karibu nawe pia?’ Uhakikisho huo mwororo unaweza kumchochea mtu aliyevunjika moyo.—Isaya 57:15.

Kusababu kwa Njia ya Kutumia Akili

13, 14. (a) Huenda tukasababu jinsi gani na mtu anayesema kwamba haamini kuna Mungu kwa sababu hawezi kumwona? (b) Kwa nini tusitazamie kwamba kila mtu atasadiki yale tusemayo?

13 Tunapokuwa katika huduma, tungependa kufikia mioyo ya watu kwa kusababu nao kwa njia inayofaa na yenye kushawishi. (Matendo 19:8; 28:23, 24) Je, hii inamaanisha kwamba tunapaswa kutumia njia ya kusababu kiakili ya hali ya juu kusadikisha wengine kuhusu kweli ya Neno la Mungu? Sivyo. Si lazima tusababu na watu kwa njia yenye kutatanisha. Hoja zinazotolewa kwa njia ya kiakili na iliyo rahisi mara nyingi huwa na matokeo. Fikiria mfano mmoja.

14 Tunaweza kujibuje mtu anaposema kwamba haamini kuna Mungu kwa kuwa hawezi kumwona? Tunaweza kusababu kwa kutumia sheria ya asili ya kisababishi na matokeo. Tunapoona matokeo, tunakubali kwamba lazima kuwe na kisababishi. Huenda tukasema: ‘Ikiwa ungekuwa mahali fulani mbali na watu na kupata nyumba iliyojengwa vizuri na iliyojaa chakula (matokeo), ungekubali mara moja kwamba mtu fulani (kisababishi) alijenga nyumba hiyo na kujaza chakula kwenye kabati zake. Kwa hiyo, pia tunapoona muundo unaoonekana katika vitu vya asili na chakula tele katika “kabati” (matokeo), je, si jambo linalopatana na akili kukubali kwamba Mtu fulani (kisababishi) ndiye aliyefanya hivyo?’ Biblia hueleza jambo hilo kwa njia iliyo wazi: “Bila shaka, kila nyumba imejengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyejenga vitu vyote ni Mungu.” (Waebrania 3:4) Hata hivyo, hata tusababu kwa njia nzuri namna gani, si wote watakaosadiki tunayosema. Biblia hutukumbusha kwamba ni wale tu ‘walio na mwelekeo ufaao’ ambao watakaokuwa waamini.—Matendo 13:48; 2 Wathesalonike 3:2.

15. Tunaweza kutumia njia gani ya kusababu ili kukazia sifa na njia za Yehova, na ni mifano gani miwili inayoonyesha jinsi tunavyoweza kutumia njia hiyo ya kusababu?

15 Tunapofundisha, iwe ni katika huduma ya shambani au kutanikoni, tunaweza kusababu kwa njia ya kiakili ili kukazia sifa na njia za Yehova. Mara kwa mara, Yesu alitumia njia hii ya kusababu, ‘si zaidi sana’ ambayo ilikuwa na matokeo sana. (Luka 11:13; 12:24) Njia hii ya kusababu ambayo inategemea kutofautisha hali, inaweza kufanya mtu afikiri sana. Ili kuonyesha jinsi fundisho la moto wa mateso lisivyopatana na akili, huenda tukasema: ‘Baba mwenye upendo hawezi kumwadhibu mtoto wake kwa kuingiza mkono wake motoni. Je, si kweli kwamba wazo la kuchoma watu katika moto linamchukiza zaidi sana Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo?’ (Yeremia 7:31) Ili kufundisha kwamba Yehova anajali kila mmoja wa watumishi wake, tunaweza kusema: ‘Ikiwa Yehova anajua kila moja ya mabilioni ya nyota kwa jina, ni lazima awe anajali zaidi wanadamu wanaompenda ambao walinunuliwa kwa damu yenye thamani ya Mwana wake.’ (Isaya 40:26; Matendo 20:28) Kusababu kwa njia hiyo yenye kusadikisha kunaweza kutusaidia tufikie mioyo ya wengine.

Vielezi Vinavyofaa

16. Kwa nini vielezi ni muhimu katika kufundisha?

16 Vielezi vyenye matokeo vinaweza kufanya ufundishaji wetu uvutie zaidi. Kwa nini vielezi ni muhimu katika kufundisha? Mwalimu mmoja alisema: “Uwezo wa kufikiri bila kupiga picha akilini ni mojawapo ya mambo magumu zaidi kwa wanadamu.” Vielezi hutokeza picha muhimu akilini mwetu, na kutusaidia tuelewe kikamili mambo mapya. Yesu alitumia vielezi kwa njia yenye kutokeza. (Marko 4:33, 34) Na tufikirie jinsi tunavyoweza kutumia njia hiyo ya kufundisha.

17. Ni mambo gani manne yanayofanya kielezi kiwe na matokeo?

17 Ni nini hufanya kielezi kiwe chenye matokeo? Kwanza, kinapaswa kifae wasikilizaji wetu, kihusu hali ambazo wasikilizaji wetu wanaweza kuzifahamu kwa urahisi. Tunakumbuka kwamba Yesu alitoa vielezi vyake kutokana na mambo ya kawaida ambayo wasikilizaji wake waliyafahamu. Pili, kielezi kinapaswa kilingane na jambo linalozungumziwa, la sivyo kielezi hicho kitapotosha wasikilizaji wetu. Tatu, kielezi hakipaswi kuwa na habari nyingi mno zisizo muhimu. Kumbuka kwamba ilipohitajika, Yesu alitoa habari hususa na hakutaja habari zisizo muhimu. Nne, tunapotumia kielezi, lazima tuhakikishe kwamba matumizi yake yanaeleweka vizuri. La sivyo, huenda wengine wasielewe jambo kuu.

18. Tunawezaje kupata vielezi vinavyofaa?

18 Tunawezaje kupata vielezi vinavyofaa? Si lazima tufikirie hadithi ndefu zenye mambo mengi. Vielezi vifupi vinaweza kuwa na matokeo sana. Jaribu kufikiria mifano inayohusu jambo linalozungumziwa. Kwa mfano, tuseme tunazungumzia msamaha wa Mungu, na tunataka kutoa kielezi kwa hoja inayotajwa katika andiko la Matendo 3:19, ambalo linasema kwamba Yehova ‘hufuta’ makosa yetu. Taarifa hiyo yenyewe inatumia lugha ya mfano, lakini tunaweza kutumia mfano gani halisi kueleza jambo hilo—kifuto? sponji? Huenda tukasema: ‘Yehova anapotusamehe dhambi zetu, ni kana kwamba anachukua sponji (au kifuto) na kuzifuta kabisa.’ Si vigumu kuelewa jambo linalokaziwa na kielezi hicho rahisi.

19, 20. (a) Tunaweza kupata wapi vielezi vinavyofaa? (b) Ni baadhi ya vielezi gani vyenye matokeo ambavyo vimechapishwa katika vichapo vyetu? (Ona pia sanduku.)

19 Unaweza kupata wapi vielezi vinavyofaa, kutia ndani mifano inayohusu maisha halisi? Vitafute maishani mwako au katika mazingira mbalimbali na mambo yaliyoonwa na waabudu wenzako. Vielezi vinaweza kuchaguliwa kutokana na vitu vingi, kutia ndani vitu vilivyo hai na visivyo hai, vifaa vya nyumbani, au tukio la karibuni linalojulikana na watu katika jumuiya. Njia moja yenye matokeo ya kupata vielezi vinavyofaa ni kuwa macho, “kutazama kwa uangalifu” hali za kila siku zinazotuzunguka. (Matendo 17:22, 23) Kitabu kimoja cha kitaalamu kinasema hivi kuhusu kutoa hotuba hadharani: ‘Msemaji ambaye ni makini kuona watu na kazi mbalimbali wanazofanya, huzungumza na watu wa aina zote, huchunguza mambo kwa makini na kujiuliza maswali hadi aelewe, hukusanya habari nyingi itakayomsaidia sana kwa vielezi.’

20 Pia tunaweza kupata vielezi vingi sana vyenye matokeo kutoka kwa Mnara wa Mlinzi, Amkeni!, na vichapo vingine vinavyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Unaweza kujifunza mengi kwa kuchunguza jinsi vichapo hivyo vinavyotumia vielezi. * Kwa mfano, fikiria kielezi kilichotumiwa katika kitabu Ujuzi sura ya 17 fungu la 11. Kinalinganisha nyutu mbalimbali kutanikoni na magari mbalimbali yanayosafiri yakielekea upande mmoja. Kwa nini ni chenye matokeo? Ona kwamba kinahusu hali za kawaida maishani, kinalingana na jambo linalotajwa, na matumizi yake ni wazi. Huenda tukatumia vielezi vinavyopatikana katika vichapo vyetu tunapofundisha, labda kwa kuvitumia vifae mahitaji ya mwanafunzi wa Biblia au kuvitumia kwenye hotuba.

21. Ni thawabu gani tunazopata kwa kuwa walimu wenye matokeo wa Neno la Mungu?

21 Kuna thawabu nyingi za kuwa mwalimu mwenye matokeo. Tunapofundisha, tunatoa baadhi ya rasilimali zetu kuwasaidia wengine. Utoaji huo huleta furaha, kwa kuwa Biblia inasema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Furaha ambayo walimu wa Neno la Mungu hupata ni ile shangwe ya kujua kwamba tunatoa kitu fulani chenye thamani halisi na ya kudumu—kweli kuhusu Yehova. Pia tunaweza kupata uradhi unaotokana na kujua kwamba tunamwiga Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 9 Ona sehemu “Matangulizi ya Kutumia Katika Huduma ya Shambani,” kwenye ukurasa wa 9-15.—Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 20 Ili kupata mifano, ona Watch Tower Publications Index 1986-2000, chini ya kichwa “Illustrations (Vielezi).”—Kimechapishwa katika lugha kadhaa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Tunawezaje kufundisha kwa njia rahisi tunapoongoza funzo la Biblia la nyumbani? tunapotoa hotuba kutanikoni?

• Tunawezaje kutumia maswali kwa matokeo tunapohubiri nyumba kwa nyumba?

• Tunawezaje kusababu kwa njia ya kiakili ili kukazia sifa na njia za Yehova?

• Tunaweza kupata wapi vielezi vinavyofaa?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

Je, Unakumbuka Vielezi Hivi?

Hapa pana vielezi vichache vyenye matokeo. Mbona usichunguze vichapo vinavyotajwa na kuona jinsi kielezi kilivyokazia hoja inayozungumziwa?

Kama vile wanaume wawili wanaopakua makatoni mazito ya bidhaa, ndoa yenye mafanikio hutegemea hasa wenzi wanaopatana.—Mnara wa Mlinzi, Mei 15, 2001, ukurasa wa 16.

Kueleza hisia zako ni sawa na kutupa mpira. Unaweza kuurusha kwa uanana au kuuvurumisha kwa nguvu na kuumiza mtu.—Amkeni!,

Januari 8, 2001, ukurasa wa 10.

Kujifunza kuonyesha upendo ni kama vile kujifunza lugha mpya.—Mnara wa Mlinzi, Februari 15, 1999, ukurasa wa 18, 22-23.

Dhambi tuliyorithi inaweza kulinganishwa

na kile kinachotukia wakati faili za kompyuta zinapovurugwa na kasoro fulani.—Je, Kuna Muumba Anayekujali?, ukurasa wa 156.

Uwasiliani-roho husaidia roho waovu kama vile chambo husaidia wawindaji. Huvutia windo.—Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, ukurasa wa 111.

Yesu anayeokoa wazao wa Adamu anaweza kulinganishwa na mfadhili tajiri anayelipa deni la kampuni (lililosababishwa na meneja asiye mnyoofu) na kufungua upya kiwanda hicho, na hivyo kunufaisha wafanyakazi wengi.—Mnara wa Mlinzi, Februari 15, 1991, ukurasa wa 13.

Kama vile watu wanaopenda sanaa hujitahidi sana ili kurudisha upya mchoro ulioharibiwa, Yehova anaweza kutusamehe kasoro zetu, kuona wema wetu, na hatimaye kuturudisha katika hali ya ukamilifu iliyopotezwa na Adamu.—Mnara wa Mlinzi, Februari 15, 1990,

ukurasa wa 22.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Wakristo wa kweli ni walimu wa Neno la Mungu

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wazee wanaweza kutumia maswali kusaidia waamini wenzao wapate faraja kutoka kwa Neno la Mungu