Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tuyaoneje Majaribu?

Tuyaoneje Majaribu?

Tuyaoneje Majaribu?

MAJARIBU hupata kila mtu. Majaribu hayo yanaweza kusababishwa na tofauti za nyutu, matatizo ya kiuchumi, afya mbaya, vishawishi, kukazwa na marika wako ufanye maovu, mnyanyaso, magumu yanayotokana na msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote, na kadhalika. Mara nyingi majaribu hututia wasiwasi hata yawe yanasababishwa na nini. Tunawezaje kukabiliana nayo kwa mafanikio? Je, majaribu hutunufaisha kwa njia yoyote?

Utegemezo Bora Zaidi

Mfalme Daudi wa zamani alipatwa na majaribu mengi maishani, lakini alikufa akiwa mwaminifu. Aliweza kuyavumiliaje? Alionyesha mahali alipopata nguvu aliposema: “BWANA ndiye mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu.” Kisha akasema: “Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, sitaogopa mabaya; kwa maana wewe upo pamoja nami, gongo lako na fimbo yako vyanifariji.” (Zaburi 23:1, 4) Naam, utegemezo wa Yehova hauna mipaka. Alimwongoza Daudi wakati wa mikazo mikali, naye yu tayari kututegemeza inapohitajika.

Tunawezaje kupata utegemezo wa Yehova? Biblia inaonyesha jinsi tunavyoweza kuupata inaposema: “Onjeni mwone ya kuwa BWANA yu mwema.” (Zaburi 34:8) Huo ni mwaliko wenye fadhili, lakini unamaanisha nini? Mwaliko huo unatutia moyo tumtumikie Yehova na kuishi kupatana na mapenzi yake. Kuishi hivyo kunamaanisha kujinyima uhuru fulani, na kudhabihu mambo fulani. Katika hali fulani, maisha hayo yanaweza hata kusababisha majaribu—mnyanyaso na mateso. Hata hivyo, wale wanaokubali mwaliko wa Yehova kwa moyo wote hawahitaji kujuta kwamba walifanya hivyo. Yehova atawaonyesha fadhili. Atawaongoza na kuwatunza kiroho. Atawategemeza wanapopatwa na majaribu kupitia Neno lake, roho yake takatifu, na kutaniko la Kikristo. Naye hatimaye atawapa zawadi ya uhai udumuo milele.—Zaburi 23:6; 25:9; Isaya 30:21; Waroma 15:5.

Wale ambao huamua kubadili njia yao ya maisha na kushikamana na uamuzi huo ili kumtumikia Yehova, huona kwamba Yehova hutimiza ahadi zake zote. Waisraeli waliofuatana na Yoshua hadi Bara Lililoahidiwa walijionea jambo hilo. Baada ya kuvuka Yordani, iliwabidi kuvumilia majaribu, kupigana vita, na kujifunza kupitia hali ngumu. Lakini kizazi hicho kilikuwa chenye imani nyingi kuliko baba zao, waliotoka Misri na kufa nyikani. Kwa hiyo, Yehova aliwategemeza wale waliokuwa waaminifu, nayo Biblia inasema hivi kuhusu hali yao baada ya Yoshua kufa: ‘Yehova aliwapa raha pande zote, sawasawa na hayo yote aliyokuwa amewaapia baba zao. Halikuanguka neno lolote katika jambo lolote lililokuwa ni jema ambalo Yehova alikuwa amelinena katika habari ya nyumba ya Israeli; yalitimia mambo yote.’ (Yoshua 21:44, 45) Yehova anaweza pia kutimiza ahadi zake zote tunapomtegemea kabisa wakati wa majaribu na nyakati nyingine zote.

Ni nini kinachoweza kudhoofisha uhakika wetu katika Yehova? Yesu alitaja sababu moja aliposema: “Hakuna awezaye kutumikia kama mtumwa mabwana-wakubwa wawili . . . Hamwezi kutumikia kama watumwa Mungu na Utajiri.” (Mathayo 6:24) Tukimtumaini Yehova, hatutatafuta usalama katika vitu vya kimwili kama wengi katika ulimwengu wanavyofanya. Yesu aliwashauri wafuasi wake: “Fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi [vya lazima] mtaongezewa.” (Mathayo 6:33) Mkristo anayeamua kudumisha usawaziko kuhusiana na vitu vya kimwili na kuweka Ufalme wa Mungu kwanza maishani mwake, anafanya jambo linalofaa. (Mhubiri 7:12) Huenda akahitaji kudhabihu mambo fulani ili afanye hivyo. Huenda hata akadhabihu vitu vya kimwili. Hata hivyo, atapata thawabu nyingi naye Yehova atamtegemeza.—Isaya 48:17, 18.

Tunayojifunza Kutokana na Majaribu

Bila shaka, uamuzi wa ‘kuonja na kuona ya kuwa BWANA yu mwema’ haumlindi mtu asipatwe na hali zisizotazamiwa maishani; wala hautukingi kabisa na mashambulio ya Shetani na wawakilishi wake wa kibinadamu. (Mhubiri 9:11) Kwa sababu hiyo, huenda unyofu na azimio la Mkristo likajaribiwa. Kwa nini Yehova huwaacha waabudu wake wapatwe na majaribu hayo? Mtume Petro alitoa sababu moja alipoandika: “Kwa muda kidogo mmetiwa kihoro wakati wa sasa, ikiwa ni lazima, kwa namna mbalimbali za majaribu, ili ubora wa imani yenu uliojaribiwa, ulio na thamani kubwa zaidi sana kuliko dhahabu ambayo huharibika ijapokuwa kuthibitishwa kwayo na moto, upatikane kuwa sababu ya sifa na utukufu na heshima wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo.” (1 Petro 1:6, 7) Naam, majaribu hutuwezesha kuonyesha ubora wa imani yetu na upendo wetu kwa Yehova. Nayo husaidia kujibu lawama na mashtaka ya Shetani Ibilisi.—Mithali 27:11; Ufunuo 12:10.

Majaribu pia hutusaidia kusitawisha sifa nyingine za Kikristo. Kwa mfano, fikiria maneno haya ya mtunga-zaburi: “[Yehova] amwona mnyenyekevu, naye amjua mwenye kujivuna tokea mbali.” (Zaburi 138:6) Wengi wetu si wanyenyekevu kiasili, lakini majaribu yanaweza kutusaidia kusitawisha sifa hiyo muhimu. Kumbuka pindi moja siku za Musa ambapo Waisraeli fulani walichoka kula mana juma baada ya juma na mwezi baada ya mwezi. Yaonekana hali hiyo iliwatia katika jaribu, hata ingawa mana iliandaliwa kimuujiza. Ni nini lililokuwa kusudi la jaribu hilo? Musa aliwaambia hivi: ‘Yehova alikulisha jangwani kwa mana, ili apate kukutweza, apate kukujaribu.’—Kumbukumbu la Torati 8:16.

Unyenyekevu wetu unaweza kujaribiwa kwa njia kama hiyo. Jinsi gani? Sisi huitikiaje kunapokuwa na marekebisho katika tengenezo? (Isaya 60:17) Je, tunaunga mkono kwa moyo wote kazi ya kuhubiri na kufundisha? (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Je, tunakubali kwa utayari ufafanuzi wa kweli ya Biblia unaotolewa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”? (Mathayo 24:45-47; Mithali 4:18) Je, tunakataa kabisa mikazo ya kuwa na vifaa, mitindo ya nguo, au gari la karibuni zaidi? Mtu mnyenyekevu ataweza kujibu ndiyo kwa maswali hayo.—1 Petro 1:14-16; 2 Petro 3:11.

Majaribu hutusaidia kusitawisha sifa nyingine pia—uvumilivu. Mwanafunzi Yakobo alisema; “Fikirieni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mkutanapo na majaribu ya namna mbalimbali, kama mjuavyo kwamba ubora huu uliojaribiwa wa imani yenu hutokeza uvumilivu.” (Yakobo 1:2, 3) Tukifanikiwa kuvumilia majaribu mbalimbali kwa kumtegemea Yehova kabisa, tutasitawisha sifa kama uimara, uthabiti, na uaminifu-maadili. Kufanya hivyo pia hutuimarisha kukinza mashambulio ya wakati ujao ya Shetani, mungu wa ulimwengu huu mwenye hasira.—1 Petro 5:8-10; 1 Yohana 5:19; Ufunuo 12:12.

Dumisha Maoni Yanayofaa Kuhusu Majaribu

Mwana mkamilifu wa Mungu, Yesu Kristo, alikabili majaribu mengi alipokuwa duniani naye alinufaika sana kwa kuyavumilia. Paulo aliandika kwamba Yesu “alijifunza utii kutokana na mambo aliyoteseka.” (Waebrania 5:8) Kwa kudumisha uaminifu-mshikamanifu hadi kifo Yesu alililetea sifa jina la Yehova na akaweza kutoa thamani ya uhai wake mkamilifu ukiwa fidia kwa ajili ya wanadamu. Dhabihu hiyo inawapa watu wanaoonyesha imani katika Yesu tazamio la kupata uhai udumuo milele. (Yohana 3:16) Kwa sababu Yesu alidumisha uaminifu chini ya majaribu, sasa yeye ni Kuhani wetu wa Cheo cha Juu na Mfalme aliyetawazwa.—Waebrania 7:26-28; 12:2.

Namna gani sisi? Tunapata baraka nyingi pia tunapodumisha uaminifu-mshikamanifu wakati wa majaribu. Biblia inasema hivi kuhusu wale walio na tumaini la kwenda mbinguni: “Mwenye furaha ni mtu afulizaye kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uhai, ambalo Yehova aliahidi wale waendeleao kumpenda.” (Yakobo 1:12) Wale walio na tumaini la kuishi duniani wanahakikishiwa kwamba wakivumilia kwa uaminifu, watapata uhai udumuo milele katika dunia paradiso. (Ufunuo 21:3-6) Na lililo muhimu hata zaidi ni kwamba wanapovumilia kwa uaminifu wanaliletea sifa jina la Yehova.

Tunapofuata hatua za Yesu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tunaweza kushinda majaribu yote tunayokabili katika ulimwengu huu. (1 Wakorintho 10:13; 1 Petro 2:21) Jinsi gani? Kwa kumtegemea Yehova ambaye hutoa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” kwa wale wanaomtegemea. (2 Wakorintho 4:7) Na tuwe na imani kama ya Yobu, ambaye ingawa alivumilia majaribu makali alisema hivi kwa uhakika: “Akisha kunijaribu, nitatoka kama dhahabu.”—Ayubu 23:10.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Yesu alililetea sifa jina la Yehova kwa kudumisha uaminifu-mshikamanifu chini ya majaribu. Sisi pia tunaweza kufanya vivyo hivyo