Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tafsiri ya “Septuagint” Ilifaa Zamani na Inafaa Sasa

Tafsiri ya “Septuagint” Ilifaa Zamani na Inafaa Sasa

Tafsiri ya “Septuagint” Ilifaa Zamani na Inafaa Sasa

MWETHIOPIA fulani mashuhuri alikuwa akisafiri kuelekea nyumbani kwao kutoka Yerusalemu. Alikuwa akisoma kwa sauti hatikunjo fulani ya kidini alipokuwa akipita kwa gari lake la kukokotwa kwenye barabara moja ya jangwani. Alipoelezwa maana ya maneno aliyokuwa akisoma, aliguswa moyo sana hivi kwamba maisha yake yalibadilika kuanzia wakati huo na kuendelea. (Matendo 8:26-38) Mtu huyo alikuwa akisoma andiko la Isaya 53:7, 8 katika tafsiri ya Biblia ya kwanza kabisa—Septuagint ya Kigiriki. Tafsiri hiyo imesaidia sana katika kueneza ujumbe wa Biblia kwa karne nyingi hivi kwamba imeitwa tafsiri ya Biblia iliyoubadili ulimwengu.

Tafsiri hiyo ya Septuagint iliandikwa wakati gani na chini ya hali gani? Kwa nini tafsiri hiyo ilihitajiwa? Imethibitikaje kuwa inafaa katika karne zote? Tafsiri ya Septuagint inaweza kutufunza nini leo?

Ilitafsiriwa kwa Ajili ya Wayahudi Waliozungumza Kigiriki

Mnamo mwaka wa 332 K.W.K. Aleksanda Mkuu alikaribishwa kama mkombozi wakati alipovamia Misri baada ya kuharibu Tiro, jiji la Foinike. Huko alianzisha jiji la Aleksandria, lililokuwa kituo cha kujifunza katika ulimwengu wa kale. Akiwa na nia ya kueneza utamaduni wa Kigiriki kwa watu walioishi katika nchi alizozitiisha, Aleksanda alianzisha Kigiriki cha kawaida (Koine) katika milki yake kubwa.

Katika karne ya tatu K.W.K., jiji la Aleksandria lilikuwa na wakazi wengi Wayahudi. Wayahudi wengi waliotawanyika katika koloni mbalimbali nje ya Palestina, hasa baada ya kutoka uhamishoni Babiloni, walihamia Aleksandria. Wayahudi hao walifahamu Kiebrania kwa kadiri gani? Kichapo Cyclopedia ya McClintock na Strong kinasema: ‘Ni wazi kwamba baada ya Wayahudi kurudi kutoka utekwani Babiloni, walikuwa wamesahau maneno mengi ya Kiebrania cha kale, kwa kuwa katika masinagogi ya Palestina vitabu vya Musa vilisomwa na kuelezwa kwa Kikaldayo. Yaelekea Wayahudi walioishi Aleksandria walisahau hata zaidi maneno mengi ya Kiebrania; lugha waliyoifahamu ni Kigiriki cha Aleksandria.’ Yaonekana, ilifaa sana Maandiko ya Kiebrania yatafsiriwe katika Kigiriki huko Aleksandria.

Aristobulus, Myahudi aliyeishi katika karne ya pili K.W.K., aliandika kwamba nakala ya sheria ya Kiebrania ilikuwa imetafsiriwa katika Kigiriki na kukamilishwa wakati wa utawala wa Ptolemy Philadelphus (285-246 K.W.K.). Haijulikani Aristobulus alimaanisha nini alipotaja neno “sheria.” Watu wengine hufikiri kwamba alimaanisha vile vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, ilhali wengine hufikiri alimaanisha Maandiko yote ya Kiebrania.

Vyovyote vile, kulingana na mapokeo, inasemekana kwamba wasomi Wayahudi wapatao 72 walishiriki kuandika na kutafsiri tafsiri ya kwanza ya Maandiko kutoka Kiebrania hadi Kigiriki. Baadaye, namba kamili 70 ikaanza kutumiwa. Kwa hiyo, tafsiri hiyo ikaitwa Septuagint, neno linalomaanisha “70,” nalo huandikwa LXX, katika Kiroma. Mwishoni mwa karne ya pili K.W.K., vitabu vyote vya Maandiko ya Kiebrania vingeweza kusomwa katika Kigiriki. Hatimaye, jina Septuagint likatumiwa kumaanisha Maandiko yote ya Kiebrania yaliyotafsiriwa katika Kigiriki.

Ilifaa Katika Karne ya Kwanza

Tafsiri ya Septuagint ilitumiwa sana na Wayahudi waliozungumza Kigiriki kabla na baada ya enzi ya Yesu Kristo na mitume wake. Wayahudi wengi na watu waliogeuza imani yao ambao walikutanika Yerusalemu siku ya Pentekoste 33 W.K. walitoka wilaya za Asia, Misri, Libya, Roma, na Krete—maeneo ambako watu walizungumza Kigiriki. Bila shaka, walizoea kusoma tafsiri ya Septuagint. (Matendo 2:9-11) Kwa hiyo, tafsiri hii ikawa muhimu katika kueneza habari njema katika karne ya kwanza.

Kwa mfano, alipokuwa akizungumza na watu kutoka Kirene, Aleksandria, Kilikia, na Asia, mwanafunzi Stefano alisema: “Yosefu akatuma watu waite Yakobo baba yake na jamaa zake wote kutoka mahali hapo [Kanaani], wenye kufikia idadi ya nafsi sabini na tano.” (Matendo 6:8-10; 7:12-14) Maandishi ya Kiebrania katika Mwanzo sura ya 46 yanasema kwamba jamaa za Yosefu walikuwa sabini. Lakini tafsiri ya Septuagint husema sabini na tano. Yaonekana, Stefano alinukuu tafsiri ya Septuagint.Mwanzo 46:20, 26, 27, kielezi-chini NW.

Mtume Paulo aliposafiri kotekote katika Asia Ndogo na Ugiriki wakati wa safari yake ya pili na ya tatu ya umishonari, alihubiria watu wengi wasio Wayahudi waliomhofu Mungu na “Wagiriki waliomwabudu Mungu.” (Matendo 13:16, 26; 17:4) Watu hao walianza kumhofu Mungu au kumwabudu kwa sababu walikuwa wamepata ujuzi fulani juu yake kwa kusoma tafsiri ya Septuagint. Paulo alipokuwa akiwahubiria watu hao waliozungumza Kigiriki, mara nyingi alinukuu au kufafanua sehemu fulani za tafsiri hiyo.—Mwanzo 22:18, kielezi-chini NW; Wagalatia 3:8.

Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yana manukuu ya moja kwa moja 320 na jumla ya marejeo yapatayo 890 kutoka Maandiko ya Kiebrania. Mengi ya manukuu hayo yanatoka katika tafsiri ya Septuagint. Kwa hiyo manukuu kutoka tafsiri hiyo, wala si kutoka kwa hatikunjo za Kiebrania, ndiyo yaliyokuwa sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliyoongozwa na Mungu. Hilo lilikuwa jambo la maana kama nini! Yesu alikuwa ametabiri kwamba habari njema ya Ufalme ingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa. (Mathayo 24:14) Ili kutimiza kazi hiyo, Yehova angeruhusu Neno lake lililoongozwa kwa roho litafsiriwe katika lugha mbalimbali zinazozungumzwa ulimwenguni pote.

Inafaa Leo

Tafsiri ya Septuagint inafaa leo, nayo hutumiwa kufunua makosa ya waandishi ambayo huenda yalitokea wakati hatikunjo za Kiebrania ziliponakiliwa baadaye. Kwa mfano, simulizi a Mwanzo 4:8 husema: “Kaini akamwambia Habili nduguye, [Twende uwandani]. Ikawa walipokuwapo uwandani, Kaini akamwinukia Habili nduguye, akamwua.”

Maneno yaliyo katika mabano “twende uwandani” hayapatikani katika hatikunjo za Kiebrania za karne ya kumi W.K. Hata hivyo, yanapatikana katika hatikunjo za zamani kidogo za tafsiri ya Septuagint na katika vitabu vichache vya kitaalamu vya mapema. Hatikunjo za Kiebrania zina neno ambalo kwa kawaida hutangulia mazungumzo, lakini hazina maneno yoyote yaliyosemwa na Kaini. Ni nini kilichotokea? Andiko la Mwanzo 4:8 linarudia neno “uwandani” mara mbili. Kwa kuwa neno la Kiebrania linalomaanisha uwandani linapatikana mara mbili katika mstari huo, Cyclopedia ya McClintock na Strong yadokeza hivi: ‘Huenda mwandishi Mwebrania hakuona neno hilo mahali lilipotumiwa mara ya kwanza na hivyo akanakili tu mahali lilipoonekana mara ya pili.’ Bila shaka, tafsiri ya Septuagint, na vilevile hatikunjo nyingine za zamani zinafaa katika kufunua makosa yaliyo katika nakala za Kiebrania zilizoandikwa baadaye.

Kwa upande mwingine, nakala za tafsiri ya Septuagint zinaweza kuwa na makosa pia, na mara kwa mara maandishi ya Kiebrania hutumiwa ili kusahihisha maandishi hayo ya Kigiriki. Kwa hiyo, kulinganisha hatikunjo za Kiebrania na za Kigiriki na tafsiri za lugha nyingine kunaweza kusaidia kufunua makosa ya utafsiri na vilevile makosa ya waandishi na hivyo tunakuwa na uhakika kwamba Neno la Mungu ni sahihi.

Nakala kamili za tafsiri ya Septuagint zilizopo leo ni za karne ya nne W.K. Hatikunjo hizo na nakala zilizoandikwa baadaye hazina jina la Mungu Yehova, ambalo katika Kiebrania linawakilishwa na Tetragramatoni (YHWH). Nakala hizo zimetumia maneno ya Kigiriki “Mungu” na “Bwana” mahali popote penye Tetragramatoni katika maandishi ya Kiebrania. Hata hivyo, uvumbuzi fulani huko Palestina yapata miaka 50 iliyopita, ulifafanua zaidi habari hiyo. Kikundi cha watu waliokuwa wakifanya utafiti karibu na ufuo wa magharibi wa Bahari ya Chunvi walifukua vipande vya hatikunjo ya kale iliyotengenezwa kwa ngozi ambayo ilikuwa na maandishi ya manabii 12 (Hosea hadi Malaki) iliyoandikwa katika Kigiriki. Hatikunjo hiyo iliandikwa kati ya mwaka wa 50 K.W.K. na 50 W.K. Hatikunjo hiyo ya zamani, ilikuwa na Tetragramatoni badala ya maneno ya Kigiriki yanayomaanisha “Mungu” na “Bwana.” Kwa hiyo, ilithibitishwa kwamba jina la Mungu lilikuweko katika tafsiri ya mapema ya Septuagint.

Mnamo mwaka wa 1971 hatikunjo za mafunjo ya kale (Fouad 266 Papyri) zilianza kuchapishwa. Sehemu hizo za tafsiri ya Septuagint, za karne ya pili au ya kwanza K.W.K. zilifunua nini? Zilikuwa na jina la Mungu pia. Hatikunjo hizo za zamani za tafsiri ya Septuagint huthibitisha kwamba Yesu na wanafunzi wake wa karne ya kwanza walijua na kutumia jina la Mungu.

Leo, Biblia ndicho kitabu ambacho kimetafsiriwa katika lugha nyingi zaidi katika historia. Zaidi ya asilimia 90 ya wanadamu wanaweza kupata Biblia au sehemu fulani ya Biblia katika lugha yao. Tunashukuru sana hasa kwa tafsiri ya kisasa iliyo sahihi ya New World Translation of the Holy Scriptures, inayopatikana ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha zaidi ya 40. Tafsiri ya New World Translation of the Holy Scriptures—With References ina mamia ya vielezi-chini kutoka kwa tafsiri ya Septuagint na hatikunjo nyingine za kale. Kwa kweli, tafsiri ya Septuagint inapendeza na ingali ina manufaa kwa wanafunzi wa Biblia leo.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mwanafunzi Filipo alifafanua kifungu kilichosomwa kutoka kwa tafsiri ya“Septuagint”

[Picha katika ukurasa wa 29]

Mara nyingi mtume Paulo alinukuu tafsiri ya“Septuagint”