Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Zoeeni Kufanya Mambo Ambayo Mmejifunza

Zoeeni Kufanya Mambo Ambayo Mmejifunza

Zoeeni Kufanya Mambo Ambayo Mmejifunza

“Mambo mliyojifunza na vilevile mkayapokea na kuyasikia na kuyaona kuhusiana nami, zoeeni kuyafanya haya; na Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi.”—WAFILIPI 4:9.

1, 2. Kwa ujumla, je, Biblia inaongoza maisha ya watu wanaodai kuwa wafuasi wa dini? Eleza.

“DINI Inazidi Kupendwa, na Maadili Yanazidi Kuzorota.” Kichwa hicho cha jarida linaloitwa Emerging Trends kilitaja kwa ujumla matokeo ya uchunguzi mmoja uliofanywa kotekote Marekani. Inaonekana kwamba nchi hiyo imekuwa na ongezeko la watu wanaoenda kanisani na wanaodai kwamba dini ni muhimu maishani mwao. Hata hivyo, ripoti hiyo inaendelea kusema: ‘Japo ongezeko hilo, kwa wazi Wamarekani wengi wanatilia shaka uwezo wa dini kubadilisha maisha ya watu na jamii kwa ujumla.’

2 Hali hiyo haihusu nchi moja tu. Ulimwenguni kote, watu wengi wanaodai kuwa wafuasi wa dini na wanaoikubali Biblia hawaongozwi na Maandiko maishani mwao. (2 Timotheo 3:5) Mkuu wa utafiti fulani alisema kwamba ‘bado tunaiheshimu sana Biblia, lakini hatuisomi tena wala hatutumii mambo tunayojifunza humo.’

3. (a) Biblia inawasaidiaje wale wanaokuwa Wakristo wa kweli? (b) Wafuasi wa Yesu hutumiaje ushauri wa Paulo katika Wafilipi 4:9?

3 Hata hivyo, Wakristo wa kweli ni tofauti. Kutumia ushauri wa Neno la Mungu kumebadili fikira zao na mwenendo wao. Na utu wao mpya huonekana wazi. (Wakolosai 3:5-10) Wafuasi wa Yesu hawaioni tu Biblia kuwa kitabu cha kuwekwa kwenye maktaba na kusahauliwa. Badala yake, mtume Paulo aliwaambia hivi Wakristo wa Filipi: “Mambo mliyojifunza na vilevile mkayapokea na kuyasikia na kuyaona kuhusiana nami, zoeeni kuyafanya haya; na Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi.” (Wafilipi 4:9) Mbali na kukubali ukweli wa Neno la Mungu, Wakristo hutenda kupatana na mambo wanayojifunza. Wao hufuata ushauri wa Biblia daima katika familia, kazini, kutanikoni, na katika maeneo mengine yote ya maisha.

4. Kwa nini ni vigumu kuzoea kutii sheria za Mungu maishani?

4 Si rahisi kuzoea kutii sheria na kanuni za Mungu maishani. Tunaishi katika ulimwengu unaoongozwa na Shetani Ibilisi, ambaye Biblia inamwita “mungu wa huu mfumo wa mambo.” (2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 5:19) Kwa hiyo, ni muhimu tujihadhari na kitu chochote ambacho kinaweza kutuzuia tusifuate mwendo wa uaminifu-maadili kwa Yehova Mungu. Tunawezaje kushika uaminifu-maadili?

Shika “Kiolezo cha Maneno Yenye Afya”

5. Maneno ya Yesu ‘mnifuate kwa kuendelea’ yanadokeza nini?

5 Kufanya yale ambayo tumejifunza kunahusisha kutegemeza kwa uaminifu ibada ya kweli licha ya kupingwa na wasioamini. Unahitaji kujitahidi ili uvumilie. “Ikiwa yeyote ataka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuchukua mti wake wa mateso na kunifuata kwa kuendelea,” akasema Yesu. (Mathayo 16:24) Yesu hakusema tumfuate kwa juma moja tu, au mwezi mmoja tu, au mwaka mmoja tu. Badala yake, alisema: ‘Tumfuate kwa kuendelea.’ Maneno yake yanaonyesha kwamba kuwa wanafunzi wake si jambo la muda tu maishani mwetu au ibada ya kipindi kifupi tu. Kutegemeza kwa uaminifu ibada ya kweli kunamaanisha kuendelea kuvumilia kwa uaminifu katika mwendo huu ambao tumechagua, hata hali ziweje. Tunawezaje kufanya hivyo?

6. Ni nini kiolezo cha maneno yenye afya ambacho Paulo aliwafundisha Wakristo wa karne ya kwanza?

6 Paulo alimhimiza hivi mwandamani wake Timotheo: “Fuliza kushika kiolezo cha maneno yenye afya ulichosikia kutoka kwangu pamoja na imani na upendo vinavyohusiana na Kristo Yesu.” (2 Timotheo 1:13) Paulo alimaanisha nini? Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “kiolezo” linamaanisha kihalisi mchoro. Ingawa mchoro kama huo hauna mambo mengi, kwa ujumla unaweza kuona picha iliyochorwa. Vivyo hivyo, kiolezo cha kweli ambacho Paulo alimfundisha Timotheo na wengine hakikukusudiwa kiweze kujibu kila swali hususa. Lakini mafundisho hayo yanayofananishwa na mchoro yana mwongozo unaotosha kuwasaidia wanyofu kutambua matakwa ya Yehova. Ili kumpendeza Mungu, bila shaka wanahitaji kuendelea kushika kiolezo hicho kwa kuzoea kufanya mambo ambayo wamejifunza.

7. Wakristo wanawezaje kufuata kiolezo cha maneno yenye afya?

7 Katika karne ya kwanza, watu kama Himenayo, Aleksanda, na Fileto walifundisha mambo yaliyokiuka “kiolezo cha maneno yenye afya.” (1 Timotheo 1:18-20; 2 Timotheo 2:16, 17) Wakristo wa mapema wangeepukaje kupotoshwa na waasi-imani? Ni kwa kujifunza kwa makini maandiko matakatifu na kuyatumia maishani. Wale waliofuata mfano wa Paulo na waaminifu wengine waliweza kutambua na kukataa jambo lolote ambalo halikupatana na kiolezo cha kweli waliyofundishwa. (Wafilipi 3:17; Waebrania 5:14) Badala ya kuwa ‘wenye maradhi ya kiakili juu ya maswali-maswali na mashindano juu ya maneno,’ wao waliendelea kuonyesha ujitoaji-kimungu. (1 Timotheo 6:3-6) Sisi pia tunafanya hivyo tunapozoea kufuata kweli ambazo tumejifunza. Tunatiwa moyo sana kuona kwamba mamilioni ya watu wanaomtumikia Yehova kotekote duniani wanaendelea kushika kabisa kiolezo cha kweli ya Biblia ambayo wamefundishwa.—1 Wathesalonike 1:2-5.

Kataa “Hadithi Zisizo za Kweli”

8. (a) Shetani anajaribuje kuvunja imani yetu leo? (b) Paulo anatoa onyo gani katika 2 Timotheo 4:3, 4?

8 Shetani hujaribu kuvunja uaminifu wetu wa maadili kwa kutilia shaka mambo ambayo tumefundishwa. Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo waasi-imani na wengine hujaribu kuharibu imani ya wale wasio na ujuzi. (Wagalatia 2:4; 5:7, 8) Nyakati nyingine wao hutumia vyombo vya habari kueneza habari zisizo za kweli au hata uwongo mtupu kuhusu utaratibu ambao watu wa Yehova hufuata na makusudi yao. Paulo alionya kwamba watu wengine wangekengeushwa waache kweli. Aliandika: “Kutakuwako kipindi cha wakati ambapo hawatachukuliana na fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajirundikia walimu kwa ajili yao wenyewe ili wapate kutekenywa masikio yao; nao watageuzia mbali masikio yao kuacha kweli, lakini watageuzwa kando kwenye hadithi zisizo za kweli.”—2 Timotheo 4:3, 4.

9. Inawezekana Paulo alimaanisha nini alipotaja “hadithi zisizo za kweli”?

9 Badala ya kushika kiolezo cha maneno yenye afya, wengine walivutiwa na “hadithi zisizo za kweli.” Hadithi hizo ni zipi? Labda Paulo alimaanisha hekaya kama zile zinazopatikana katika kitabu kinachoitwa Tobiti cha Apokrifa. * Inawezekana hadithi zisizo za kweli zilitia ndani mambo ya kusisimua yaliyokisiwa tu. Kisha kuna wale ambao “kwa kupatana na tamaa zao wenyewe” huenda walidanganywa akili na wale ambao walikuwa wakipuuza kanuni za Mungu au waliokuwa wakiwachambua wenye kuongoza kutanikoni. (3 Yohana 9, 10; Yuda 4) Hata yawe ni mambo gani yaliyohusika, inaonekana wengine walipendelea habari zisizo za kweli badala ya kweli ya Neno la Mungu. Kisha wakaacha kufanya mambo waliyojifunza, wakaangamia kiroho.—2 Petro 3:15, 16.

10. Hadithi zisizo za kweli siku hizi ni zipi, na Yohana alionyeshaje uhitaji wa kujihadhari?

10 Leo, tunaweza kuepuka kuvutiwa na hadithi zisizo za kweli ikiwa tunachunguza na kuchagua kwa uangalifu mambo tunayosikiliza na kusoma. Kwa mfano, mara nyingi vyombo vya habari huonyesha matendo machafu. Watu wengi huendeleza dhana ya kwamba mambo ya Mungu hayajulikani au hata kudai kwamba hakuna Mungu. Wachambuzi wa Biblia wanadai kwamba Biblia haikuandikwa kwa mwongozo wa Mungu. Na waasi-imani wa siku hizi huendelea kujaribu kutilia shaka imani ya Wakristo ili kuivunja. Mtume Yohana alionya hivi kuhusu hatari inayofanana na hiyo ambayo ilitokezwa na manabii wasio wa kweli katika karne ya kwanza: “Wapendwa, msiamini kila usemi uliopuliziwa, lakini jaribuni semi zilizopuliziwa ili kuona kama hizo zatokana na Mungu, kwa sababu manabii wengi wasio wa kweli wameenda kuingia katika ulimwengu.” (1 Yohana 4:1) Basi tunahitaji kujihadhari.

11. Taja njia moja ya kujijaribu na kuona kama tuko katika imani.

11 Paulo aliandika hivi kuhusu habari hiyo: “Fulizeni kujijaribu kama nyinyi mumo katika imani.” (2 Wakorintho 13:5) Mtume huyo alituhimiza tuendelee kujijaribu ili tuone kama tunafuata mafundisho yote ya Kikristo. Ikiwa tuna mwelekeo wa kusikiliza wale wanaolalamika-lalamika, tunahitaji kujichunguza kupitia sala. (Zaburi 139:23, 24) Je, sisi hukosoa-kosoa watu wa Yehova? Ikiwa ndivyo, kwa nini? Je, ni kwa sababu mtu fulani ametuudhi kwa maneno au kwa matendo? Ikiwa ndivyo, je, tunachukulia jambo hilo kwa njia inayofaa? Dhiki yoyote tunayokabili katika mfumo huu ni ya muda tu. (2 Wakorintho 4:17) Hata kama tunapata jaribu fulani kutanikoni, mbona tuache kumtumikia Mungu? Ikiwa jambo fulani limetuudhi, je, haingefaa tujitahidi kwa kadiri tunavyoweza kulisuluhisha na kuliacha mkononi mwa Yehova?—Zaburi 4:4; Mithali 3:5, 6; Waefeso 4:26.

12. Waberoya walituwekeaje mfano mzuri?

12 Badala ya kuwa wachambuzi, na tudumishe maoni mazuri ya kiroho kuhusu habari tunayojifunza katika funzo la binafsi na katika mikutano ya kutaniko. (1 Wakorintho 2:14, 15) Na badala ya kutilia shaka Neno la Mungu, inafaa tuwe na maoni kama yale ya Waberoya wa karne ya kwanza ambao waliyachunguza Maandiko kwa makini. (Matendo 17:10, 11) Basi, na tufanye yale ambayo tunajifunza, tukatae hadithi zisizo za kweli na kushikamana na kweli.

13. Tunawezaje kueneza hadithi zisizo za kweli pasipo kujua?

13 Kuna aina nyingine ya hadithi isiyo ya kweli ambayo tunahitaji kujihadhari nayo. Kuna habari nyingi za kusisimua zinazoenezwa hasa na barua-pepe (E-mail) kupitia kompyuta. Inafaa tujihadhari na habari kama hizo, na hasa kama hatujui chanzo chake. Hata kama Mkristo mwenye sifa nzuri ndiye aliyetutumia jambo fulani lililoonwa au masimulizi fulani, inawezekana kwamba hata yeye alisimuliwa tu habari hizo. Hiyo ndiyo sababu inafaa tujihadhari tusisimulie au kueneza habari ambazo hazijathibitishwa. Haingefaa kusimulia “hekaya zisizo za kimungu,” au “hadithi zisizo za kweli ambazo huhalifu kilicho kitakatifu.” (1 Timotheo 4:7; New International Version) Kwa kuwa sisi pia tuna wajibu wa kuzungumza mambo yaliyo kweli, ni vizuri tuepuke jambo lolote linaloweza kutufanya tueneze bila kukusudia habari zisizo za kweli.—Waefeso 4:25.

Matokeo Mazuri ya Kuzoea Kufuata Kweli

14. Kuna faida zipi za kuzoea kufanya mambo ambayo tumejifunza katika Neno la Mungu?

14 Kuzoea kufanya yale tunayojifunza katika funzo la binafsi la Biblia na katika mikutano ya Kikristo kunaleta faida nyingi. Kwa mfano, uhusiano wetu na ndugu zetu wa kiroho unaweza kuboreka. (Wagalatia 6:10) Utu wetu wenyewe utakuwa bora tunapofuata kanuni za Biblia. (Zaburi 19:8) Isitoshe, kwa kuzoea kufanya mambo tunayojifunza, ‘tunapamba fundisho la Mungu’ na inaelekea tutafanya wengine wavutiwe na ibada ya kweli.—Tito 2:6-10.

15. (a) Msichana mmoja alipataje ujasiri wa kutoa ushahidi shuleni? (b) Tukio hilo limekufundisha nini?

15 Kuna vijana wengi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova wanaozoea kufanya mambo ambayo wamejifunza katika funzo la binafsi la Biblia na katika vichapo vya Kikristo na vilevile katika mikutano ya kutaniko ambayo wanahudhuria kwa ukawaida. Mwenendo wao mzuri ni ushahidi mkubwa kwa walimu na wanafunzi wenzao shuleni. (1 Petro 2:12) Hebu tuchukue mfano wa Leslie, msichana mwenye umri wa miaka 13 anayeishi Marekani. Anakubali kwamba alikuwa akishindwa kuzungumza na wanafunzi wenzake kuhusu imani yake, lakini siku moja alipata ujasiri. “Wanafunzi walikuwa wakizungumza kuhusu jinsi watu hujaribu kuwauzia-uzia wengine vitu. Msichana mmoja akainua mkono akataja Mashahidi wa Yehova kama mfano.” Kwa kuwa Leslie ni Shahidi, alifanyaje? “Nilitetea dini yetu,” akasema, “na nina hakika kila mtu alishangaa kwa sababu kwa kawaida mimi ni mnyamavu sana shuleni.” Ujasiri wake ukawa na matokeo gani? “Mwanafunzi mmoja aliyekuwa na maswali mengine alikubali broshua na trakti,” Leslie akasema. Yehova hupata shangwe iliyoje anapoona vijana wanaozoea kufanya mambo ambayo wamejifunza wakiwa na ujasiri wa kutoa ushahidi shuleni!—Mithali 27:11; Waebrania 6:10.

16. Shahidi mmoja mchanga amefaidikaje na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi?

16 Kuna mfano mwingine wa Elizabeth. Kuanzia wakati alipokuwa na umri wa miaka saba na kuendelea akiwa shule ya msingi, alikuwa akiwaalika walimu kwenye Jumba la Ufalme wakati wowote alipokuwa na hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Ikiwa mwalimu hakuweza kuhudhuria, Elizabeth alibaki shuleni na kumtolea mwalimu hotuba ile. Alipokuwa akimaliza shule ya upili, Elizabeth aliandika ripoti yenye kurasa kumi kuhusu faida za Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na akatoa onyesho mbele ya walimu wanne. Pia aliombwa kutoa mfano wa hotuba zinazokuwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, akachagua kichwa hiki: “Kwa Nini Mungu Ameruhusu Uovu?” Elizabeth amefaidika na programu yenye kuelimisha ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya Mashahidi wa Yehova. Yeye ni mmojawapo wa Wakristo wengi wachanga wanaomsifu Yehova kwa kuzoea kufanya mambo ambayo wanajifunza katika Neno lake.

17, 18. (a) Biblia inatushaurije kuhusu unyofu? (b) Mtu mmoja aliguswaje moyo na unyofu wa Shahidi mmoja?

17 Biblia inawahimiza Wakristo wajiendeshe kwa haki, au kwa unyofu, katika mambo yote. (Waebrania 13:18) Ikiwa sisi si wanyofu tunaweza kuharibu uhusiano wetu na wengine, na jambo baya zaidi, uhusiano wetu na Yehova mwenyewe. (Mithali 12:22) Kuwa wanyofu kunathibitisha kwamba tunafanya mambo ambayo tumejifunza, na mwenendo huo umefanya watu wengi wawaheshimu sana Mashahidi wa Yehova.

18 Hebu fikiria simulizi hili la mwanajeshi mmoja aitwaye Phillip. Alipoteza hundi ambayo tayari alikuwa ameitia sahihi na ambayo haikuwa imejazwa kiasi cha pesa kinachotakikana. Hakutambua ameipoteza mpaka Shahidi mmoja wa Yehova alipoipata na kumtumia. Shahidi huyo aliambatanisha barua fupi pamoja na hundi hiyo akisema kwamba imani yake ilimchochea airudishe. Phillip akashangaa sana, akasema: “Ningepoteza dola 9,000!” Pindi nyingine alifadhaika kofia yake ilipoibiwa kanisani. Inaonekana mtu anayemfahamu aliiba kofia yake, ilhali sasa mtu ambaye hamfahamu kabisa alimrudishia hundi yake ambayo ingemgharimu maelfu ya pesa! Hakika Wakristo wanyofu humletea sifa Yehova Mungu!

Endeleeni Kuzoea Kufanya Mambo Ambayo Mmejifunza

19, 20. Tutapata faida gani tukifanya mambo tunayojifunza katika Maandiko?

19 Wale wanaozoea kufanya mambo ambayo wamejifunza katika Neno la Mungu hupata faida nyingi. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Yeye achunguaye ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru na ambaye hudumu katika hiyo, mtu huyu, kwa sababu amekuwa, si msikiaji msahaulifu, bali mtekelezaji wa kazi, atakuwa mwenye furaha katika kutenda hiyo.” (Yakobo 1:25) Tukifanya mambo tunayojifunza katika Maandiko, tutapata furaha ya kweli na tutaweza kukabiliana na mikazo ya maisha kwa njia bora. Isitoshe, Yehova atatubariki na tutakuwa na tazamio la kuishi milele!—Mithali 10:22; 1 Timotheo 6:6.

20 Basi, endelea kujifunza Neno la Mungu kwa bidii. Kusanyika kwa ukawaida na waabudu wa Yehova, na usikilize kwa makini unapokuwa katika mikutano ya Kikristo. Tumia maishani mambo unayojifunza, endelea kuyafanya, na ‘Mungu wa amani atakuwa pamoja nawe.’—Wafilipi 4:9.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Inawezekana kitabu Tobiti kiliandikwa karne ya tatu K.W.K., nacho kimejaa hadithi zenye ushirikina kuhusu Myahudi aitwaye Tobia. Ilisemekana kwamba alikuwa na uwezo wa kupata nguvu za kuponya na za kuondosha mashetani akitumia moyo, nyongo, na ini la samaki fulani mwenye kutisha.

Je, Unakumbuka?

• Ni nini “kiolezo cha maneno yenye afya,” na tunawezaje kuendelea kukishika?

• Tunapaswa kukataa ‘hadithi zipi zisizo za kweli’?

• Wale wanaozoea kufanya mambo wanayojifunza katika Neno la Mungu hupata faida zipi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wakristo wa mapema wangeepukaje kukengeushwa na waasi-imani?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Vyombo vya habari, Mtandao wa “Internet,” na waasi-imani wa siku hizi wanaweza kuzusha shaka

[Picha katika ukurasa wa 19]

Haifai kueneza habari ambazo hazijathibitishwa

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mashahidi wa Yehova hutumia yale wanayojifunza katika Neno la Mungu wakiwa kazini, shuleni, na kwingineko