Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sitawisha Utii Mwisho Unapokaribia

Sitawisha Utii Mwisho Unapokaribia

Sitawisha Utii Mwisho Unapokaribia

“Kwa [Shilo] kutii kwa watu kutakuwa.”—MWANZO 49:10, Zaire Swahili Bible.

1. (a) Mara nyingi kumtii Yehova kulimaanisha nini zamani? (b) Yakobo alitoa unabii gani kuhusu utii?

MARA nyingi kumtii Yehova kumemaanisha kutii wawakilishi wake. Wawakilishi hao wametia ndani malaika, wazee wa ukoo, waamuzi, makuhani, manabii, na wafalme. Kiti cha wafalme wa Israeli hata kiliitwa kiti cha enzi cha Yehova. (1 Mambo ya Nyakati 29:23) Hata hivyo, inasikitisha kwamba wafalme wengi wa Israeli hawakumtii Mungu, na hivyo wakajiletea msiba pamoja na raia zao. Lakini Yehova hakuwaacha waaminifu wake pasipo tumaini; aliwafariji kwa kuwaahidi kwamba angetawaza Mfalme mnyofu, ambaye waadilifu watafurahia kumtii. (Isaya 9:6, 7) Mzee wa ukoo, Yakobo, aliyekuwa akikaribia kufa alitoa unabii huu kuhusu mfalme huyo wa baadaye, aliposema: “Fimbo haitaondoka katika Yuda, wala gongo la mutawala kati ya miguu yake hata Shilo anakuja; na kwake kutii kwa watu kutakuwa.”—Mwanzo 49:10, ZSB.

2. Neno “Shilo” linamaanisha nini, nao utawala wake ungetia ndani nani?

2 “Shilo” ni neno la Kiebrania linalomaanisha “Yeye Ambaye Ni Yake” au “Yeye Ambaye Ni Mali Yake.” Ndiyo, Shilo angerithi haki kamili ya kuwa mfalme, kama inavyoonyeshwa na ishara ya fimbo, na pia mamlaka, kama inavyoonyeshwa na gongo la mtawala. Isitoshe, utawala wake wa kifalme utatia ndani “watu” wote, si wazao wa Yakobo peke yao. Jambo hilo linapatana na ahadi ambayo Yehova alimpa Abrahamu: “Uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Mwanzo 22:17, 18) Yehova alihakikisha kwamba “mbegu” huyo ametambulishwa mwaka wa 29 W.K. alipomtia mafuta Yesu wa Nazareti kwa roho takatifu.—Luka 3:21-23, 34; Wagalatia 3:16.

Ufalme wa Kwanza wa Yesu

3. Yesu alipokea ufalme gani alipopaa mbinguni?

3 Yesu alipopaa mbinguni, hakuanza kutawala wakazi wa dunia mara moja. (Zaburi 110:1) Hata hivyo, alipokea “ufalme” ambao raia zake walimtii. Mtume Paulo aliutambulisha ufalme huo alipoandika hivi: “[Mungu] alitukomboa kutoka katika mamlaka ya giza na kutuhamisha kuingia katika ufalme wa Mwana wa upendo wake.” (Wakolosai 1:13) Ukombozi huo ulianza Pentekoste 33 W.K., wakati roho takatifu ilipomwagwa juu ya wafuasi waaminifu wa Yesu.—Matendo 2:1-4; 1 Petro 2:9.

4. Wanafunzi wa Yesu wa mapema walionyesha utii kwa njia gani, naye Yesu aliwatambulishaje wakiwa kikundi?

4 Wakiwa “mabalozi walio badala ya Kristo,” kwa utii wanafunzi waliotiwa mafuta kwa roho walianza kukusanya wengine ambao wangekuwa ‘raia wenzao’ katika ufalme huo wa kiroho. (2 Wakorintho 5:20; Waefeso 2:19; Matendo 1:8) Kwa kuongezea, wanafunzi hao walipaswa kubaki wakiwa ‘wameunganishwa kwa kufaa katika akili ileile na fikira ileile’ ili wapate kibali cha Mfalme wao Yesu Kristo. (1 Wakorintho 1:10) Wakiwa kikundi, walifanyiza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” au jamii ya msimamizi-nyumba.—Mathayo 24:45; Luka 12:42.

Wabarikiwa kwa Kutii “Msimamizi-Nyumba” wa Mungu

5. Yehova amewafundishaje watu wake tangu nyakati za kale?

5 Yehova amekuwa akiwaandalia watu wake walimu. Kwa mfano, baada ya Wayahudi kurudi kutoka Babiloni, Ezra na wanaume wengine wanaostahili hawakuwasomea watu Sheria ya Mungu tu, bali ‘walifafanua’ sheria hiyo, ‘wakaeleza maana’ ya Neno la Mungu.—Nehemia 8:8, NW.

6, 7. Jamii ya mtumwa imeandaaje chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa kupitia Baraza lake Linaloongoza, na kwa nini inafaa kutii jamii ya mtumwa?

6 Katika karne ya kwanza, wakati suala la tohara lilipozuka mwaka wa 49 W.K., baraza linaloongoza la jamii hiyo ya mtumwa lilizungumzia jambo hilo kwa sala na kufikia uamuzi unaopatana na Maandiko. Walipotangaza uamuzi wao kupitia barua, makutaniko yalitii mwelekezo uliotolewa na kupata baraka tele za Mungu. (Matendo 15:6-15, 22-29; 16:4, 5) Vivyohivyo, nyakati za kisasa, mtumwa mwaminifu kupitia Baraza Linaloongoza ameelezea masuala muhimu kama vile kutokuwamo kwa Kikristo, utakatifu wa damu, na matumizi ya dawa za kulevya na tumbaku. (Isaya 2:4; Matendo 21:25; 2 Wakorintho 7:1) Yehova aliwabariki watu wake kwa kutii Neno lake na kumtii mtumwa mwaminifu.

7 Kwa kujitiisha kwa jamii ya mtumwa, watu wa Mungu pia huonyesha kwamba wanamtii Bwana wao, Yesu Kristo. Utii huo hudhihirika hata zaidi nyakati za kisasa kwa sababu ya mamlaka ambayo Yesu ameongezewa, kama alivyotabiri Yakobo alipokuwa anakaribia kufa.

Shilo Awa Mfalme wa Dunia Mwenye Haki Kamili

8. Mamlaka ya Kristo iliongezwa jinsi gani na wakati gani?

8 Unabii wa Yakobo ulisema kwamba ‘watu wangemtii’ Shilo. Ni wazi kwamba, utawala wa Kristo ungehusisha wengi zaidi ya Waisraeli wa kiroho. Ungehusisha nani? Andiko la Ufunuo 11:15 linajibu: “Ufalme wa ulimwengu ulipata kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atatawala akiwa mfalme milele na milele.” Biblia huonyesha kwamba Yesu alipokea mamlaka hiyo mwishoni mwa “nyakati saba” za kiunabii—“nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa”—mwaka wa 1914. * (Danieli 4:16, 17; Luka 21:24) Mwaka huo, “kuwapo” kwa Kristo kusikoonekana akiwa Mfalme wa Kimesiya kulianza, na pia wakati wa ‘kuwa na enzi kati ya adui zake.’—Mathayo 24:3; Zaburi 110:2.

9. Yesu alifanya nini alipopokea Ufalme wake, na hilo limewaathirije wanadamu kwa njia isiyo ya moja kwa moja, na hasa wanafunzi wake?

9 Hatua ya kwanza ambayo Yesu alichukua baada ya kupokea mamlaka ya ufalme ni kumvurumisha “chini kwenye dunia” yule anayejulikana sana kwa kutotii—Shetani—pamoja na roho wake waovu. Tangu wakati huo, roho hao waovu wamefanya wanadamu wateseke sana, na pia wanatokeza hali inayofanya iwe vigumu sana kumtii Yehova. (Ufunuo 12:7-12; 2 Timotheo 3:1-5) Kwa kweli, Shetani anapigana vita hasa na watiwa-mafuta wa Yehova, “washikao amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kuhusu Yesu,” na pia wenzao ambao ni “kondoo wengine.”—Ufunuo 12:17; Yohana 10:16.

10. Ni kutimizwa kwa unabii gani kunakohakikisha kwamba Shetani atashindwa katika vita yake dhidi ya Wakristo wa kweli?

10 Hata hivyo, pasipo shaka Shetani atashindwa, kwa sababu hii ni “siku ya Bwana,” na hakuna kitu kinachoweza kumzuia Yesu ‘asikamilishe ushindi wake.’ (Ufunuo 1:10; 6:2) Kwa mfano, atahakikisha kwamba yule wa mwisho kati ya Waisraeli wa kiroho 144,000 ametiwa muhuri. Pia atalinda “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” (Ufunuo 7:1-4, 9, 14-16) Hata hivyo, tofauti na wenzao waliotiwa mafuta, hawa watakuwa raia watiifu wa Yesu watakaoishi duniani. (Danieli 7:13, 14) Kuwapo kwao duniani leo, tayari kunathibitisha kwamba kwa kweli Shilo ni Mfalme juu ya “Ufalme wa ulimwengu.”—Ufunuo 11:15.

Sasa Ndio Wakati wa ‘Kutii Habari Njema’

11, 12. (a) Ni nani pekee watakaookoka mwisho wa mfumo huu wa mambo? (b) Wale wanaofyonza “roho ya ulimwengu” husitawisha tabia gani?

11 Wote wanaotaka kuishi milele, lazima wajifunze kutii, kwa kuwa Biblia inasema waziwazi kwamba “wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu” hawataokoka siku ya Yehova ya kulipiza kisasi. (2 Wathesalonike 1:8) Hata hivyo, mazingira maovu ya ulimwengu wa sasa na roho yake ya uasi dhidi ya sheria na kanuni za Biblia hufanya iwe vigumu kutii habari njema.

12 Biblia hutaja mtazamo huo wa kumwasi Mungu kuwa “roho ya ulimwengu.” (1 Wakorintho 2:12) Akieleza jinsi mtazamo huo unavyowaathiri watu, mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa karne ya kwanza huko Efeso: “Wakati fulani nyinyi mlitembea kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii. Ndiyo, miongoni mwao sisi sote wakati fulani tulijiendesha wenyewe kwa kupatana na tamaa za mwili wetu, tukifanya mambo yanuiwayo na mwili na fikira, nasi kiasili tulikuwa watoto wa hasira ya kisasi sawa na wale wengine.”—Waefeso 2:2, 3.

13. Wakristo wanaweza kufanikiwaje kukinza roho ya ulimwengu, na kupata matokeo gani mazuri?

13 Inafurahisha kwamba Wakristo wa Kutaniko la Efeso hawakuendelea kuwa watumwa wa roho ya kutotii. Badala yake, Wakristo hao walikuwa watoto watiifu wa Mungu kwa kujitiisha kwa roho yake na kutokeza sifa nyingi zinazofaa. (Wagalatia 5:22, 23) Vivyo hivyo leo, roho ya Mungu—nguvu kuu zaidi ulimwenguni—inasaidia mamilioni ya watu wamtii Yehova, ili waweze kupata “uhakikisho kamili wa tumaini hadi mwisho.”—Waebrania 6:11; Zekaria 4:6.

14. Yesu aliwatahadharishaje Wakristo wanaoishi siku za mwisho kuhusu matatizo hususa ambayo yangejaribu utii wao?

14 Pia, kumbuka kwamba Shilo anatuunga mkono kwa nguvu, naye pamoja na Baba yake hataruhusu adui yeyote—awe roho mwovu au mwanadamu—ajaribu utii wetu kuliko tunavyoweza kustahimili. (1 Wakorintho 10:13) Kwa kweli, ili kutusaidia katika vita yetu ya kiroho, Yesu alitaja matatizo hususa ambayo tungekabili siku hizi za mwisho. Aliyataja katika barua saba, alizompa mtume Yohana katika maono. (Ufunuo 1:10, 11) Bila shaka, barua hizo zilikuwa na mashauri muhimu kwa Wakristo wa wakati huo, lakini zinahusu hasa “siku ya Bwana,” tangu mwaka wa 1914. Kwa hiyo inafaa kama nini kwamba tuzingatie ujumbe huo! *

Epuka Kutojali, Ukosefu wa Maadili, na Pupa

15. Kwa nini tujilinde na tatizo lililopata kutaniko la Efeso, na tunawezaje kufanya hivyo? (2 Petro 1:5-8)

15 Barua ya kwanza ya Yesu ilielekezwa kwa kutaniko la Efeso. Baada ya kusifu kutaniko hilo kwa uvumilivu wake, Yesu alisema: “Hata hivyo, nashika hili dhidi yako, kwamba umeacha upendo uliokuwa nao hapo kwanza.” (Ufunuo 2:1-4) Leo, Wakristo fulani waliokuwa na bidii wameacha upendo wao wenye shauku waliokuwa nao kwa Mungu hapo awali. Kuacha upendo huo kunaweza kudhoofisha uhusiano wako na Mungu, kwa hiyo unapaswa kushughulikia jambo hilo haraka. Upendo huo unaweza kuchochewaje upya? Kwa kujifunza Biblia kwa ukawaida, kuhudhuria mikutano, sala, na kutafakari. (1 Yohana 5:3) Kwa kweli, unahitaji ‘jitihada yenye bidii’ ili kutimiza mambo hayo, lakini utanufaika sana. (2 Petro 1:5-8) Ukijichunguza kwa unyofu na kuona kwamba upendo wako umepoa, basi rekebisha hali hiyo mara moja kwa kutii himizo hili la Yesu: “Kumbuka ni kutoka katika nini umeanguka, nawe tubu na kufanya vitendo vya kwanza.”—Ufunuo 2:5.

16. Kulikuwa na uvutano gani hatari kiroho katika makutaniko ya Pergamamu na Thiatira, na kwa nini maneno ambayo Yesu aliambia makutaniko hayo yanafaa leo?

16 Wakristo wa Pergamamu na Thiatira walipongezwa kwa sababu ya uaminifu, uvumilivu, na bidii yao. (Ufunuo 2:12, 13, 18, 19) Hata hivyo, waliathiriwa na watu fulani waliodhihirisha mtazamo mwovu wa Balaamu na Yezebeli, ambao waliwapotosha Waisraeli wa kale kupitia uasherati na ibada ya Baali. (Hesabu 31:16; 1 Wafalme 16:30, 31; Ufunuo 2:14, 16, 20-23) Lakini namna gani wakati wetu—“siku ya Bwana”? Je, uvutano huo mwovu upo? Ndiyo, kwa kuwa watu wengi wa Mungu hutengwa na ushirika kwa sababu ya uasherati. Kwa hiyo, ni muhimu tuepuke kushirikiana na watu wanaoweza kutupotosha kiadili, iwe ni katika kutaniko au nje ya kutaniko. (1 Wakorintho 5:9-11; 15:33) Wale wanaotaka kuwa raia watiifu wa Shilo watajiepusha na vitumbuizo vinavyokiuka maadili na pia ponografia, iwe imechapwa au iwe kwenye vitabu au Internet.—Amosi 5:15; Mathayo 5:28, 29.

17. Maoni na mtazamo wa Wakristo wa Sardisi na Laodikia kuhusu hali yao ya kiroho ulitofautianaje na mtazamo wa Yesu?

17 Kutaniko la Sardisi halikupongezwa hata kidogo isipokuwa washiriki wachache tu. Lilikuwa na “jina,” au lilionekana kuwa hai, lakini lilipuuza mambo ya kiroho sana hivi kwamba Yesu aliliona kuwa “mfu.” Lilitii habari njema kidesturi tu. Lililaumiwa kama nini! (Ufunuo 3:1-3) Hali ya kutaniko la Laodikia ilifanana na hiyo. Lilijidai kuwa tajiri, likisema, “Mimi ni tajiri,” hata ingawa machoni pa Kristo lilikuwa ‘lenye taabu na la kusikitikiwa na maskini na kipofu na uchi.’—Ufunuo 3:14-17.

18. Mtu anawezaje kuepuka kupuuza mambo ya kiroho machoni pa Mungu?

18 Leo, Wakristo fulani waliokuwa waaminifu wakati fulani wamejikuta katika hali hiyo ya kutotii. Labda wameruhusu roho ya ulimwengu ifanye wasahau umuhimu wa nyakati hizi, na hivyo kusitawisha mtazamo wa kupuuza mambo ya kiroho kama vile kujifunza Biblia, kusali, mikutano ya Kikristo, na huduma. (2 Petro 3:3, 4, 11, 12) Wakristo hao wanapaswa kumtii Kristo kwa kutumia utajiri wa kiroho kwa njia inayofaa—naam, ‘kununua kutoka kwa Kristo dhahabu iliyosafishwa sana kwa moto.’ (Ufunuo 3:18) Utajiri huo halisi unahusisha kuwa “matajiri katika kazi zilizo bora, kuwa wakarimu, tayari kushiriki.’ Kwa kutumia utajiri huo wa kiroho kwa njia inayofaa, ‘tunajiwekea wenyewe msingi bora kwa ajili ya wakati ujao, ili tupate kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi.’— 1 Timotheo 6:17-19.

Walipongezwa kwa Utii Wao

19. Yesu alitoa pongezi na himizo gani kwa Wakristo huko Smirna na Filadelfia?

19 Kutaniko la Smirna na Filadelfia ni kielelezo kizuri cha kuonyesha utii, kwa kuwa Yesu hakushutumu makutaniko hayo katika barua alizowaandikia. Alisema hivi kuhusu kutaniko la Smirna: “Najua dhiki na umaskini wako—lakini wewe ni tajiri.” (Ufunuo 2:9) Walikuwa tofauti kama nini na wale wa Laodikia ambao kwa kweli walikuwa maskini ingawa walijigamba kuwa matajiri kimwili! Bila shaka, Ibilisi hakufurahi kuona mtu yeyote akionyesha uaminifu na utii kwa Kristo. Kwa hiyo, Yesu alionya hivi: “Usiogope mambo uliyo karibu kuteseka. Tazama! Ibilisi atafuliza kutupa baadhi yenu ndani ya gereza ili mpate kutiwa kwenye jaribu kikamili, na kwamba mpate kuwa na dhiki siku kumi. Jithibitishe mwenyewe kuwa mwaminifu hata kufikia kifo, nami hakika nitakupa taji la uhai.” (Ufunuo 2:10) Vivyo hivyo, Yesu aliwapongeza wale wa Filadelfia, akisema: “Ulitunza neno langu [au, ulinitii] na hukuthibitika kuwa asiye wa kweli kwa jina langu. Mimi ninakuja upesi. Fuliza kushika sana lile ulilo nalo, ili yeyote asipate kuchukua taji lako.”—Ufunuo 3:8, 11.

20. Mamilioni ya watu leo wametunzaje neno la Yesu, licha ya hali gani?

20 Katika “siku ya Bwana,” iliyoanza mwaka wa 1914, mabaki waaminifu na wenzao wa kondoo wengine, ambao sasa ni mamilioni kadhaa, wametunza pia neno la Yesu kwa kuhubiri kwa bidii na kudumisha uaminifu-maadili. Kama ndugu zao wa karne ya kwanza, wengine wameteseka kwa sababu ya kumtii Kristo, hata kufungwa gerezani na kwenye kambi za mateso. Wengine wametunza neno la Yesu kwa kudumisha ‘jicho sahili,’ licha ya kuzungukwa na watu wenye utajiri na pupa. (Mathayo 6:22, 23) Naam, katika mazingira na hali zote, Wakristo wa kweli wanaendelea kuufurahisha moyo wa Yehova kwa utii wao.—Mithali 27:11.

21. (a) Jamii ya mtumwa itaendelea kutimiza daraka gani la kiroho? (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba kwa kweli tunataka kumtii Shilo?

21 Tunapokaribia dhiki kubwa, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ameazimia kumtii Bwana wake, Kristo. Hii inatia ndani kuwatayarishia watu wa nyumba ya Mungu chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Kwa hiyo, na tuendelee kushukuru kwa ajili ya tengenezo zuri na la kiroho la Yehova na mambo linalotuandalia. Kwa kufanya hivyo, tutathibitisha kwamba tunajitiisha kwa Shilo, atakayewathawabisha raia wake watiifu kwa uhai udumuo milele.—Mathayo 24:45-47; 25:40; Yohana 5:22-24.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kwa habari kamili kuhusu “nyakati saba,” ona sura ya 10 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 14 Kwa habari kamili kuhusu barua zote saba, tafadhali ona kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, kuanzia ukurasa wa 33.

Je, Unakumbuka?

• Yesu angetimiza daraka gani kulingana na unabii uliotolewa na Yakobo alipokuwa anakaribia kufa?

• Tunamtambuaje Yesu kuwa Shilo, nasi tunapaswa kuepuka roho gani?

• Ni mashauri gani yanayotuhusu leo ambayo yanapatikana katika barua zilizoandikiwa makutaniko saba ya Ufunuo?

• Tunaweza kuwaigaje Wakristo katika kutaniko la kale la Smirna na Filadelfia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yehova hubariki watu wake kwa kutii “msimamizi-nyumba” mwaminifu

[Picha katika ukurasa wa 19]

Uvutano wa Shetani hufanya iwe vigumu kumtii Mungu

[Picha katika ukurasa wa 21]

Uhusiano mzuri na Yehova hutusaidia tumtii