Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Uwe Ukijizoeza Mwenyewe”

“Uwe Ukijizoeza Mwenyewe”

“Uwe Ukijizoeza Mwenyewe”

HARAKA zaidi, juu zaidi, kwa ujasiri zaidi! Hivyo ndivyo viwango ambavyo wanariadha katika Ugiriki na Roma ya kale walitamani kuvifikia. Kwa karne nyingi mashindano ya riadha yenye fahari yalifanywa huko Olympia, Delphi, Nemea na kwenye shingo ya nchi iitwayo Isthmus ya Korintho. Mashindano hayo yalifanywa kwa “baraka” za miungu na mbele ya mashabiki wengi sana. Ili kupata pendeleo la kushiriki mashindano hayo mtu alihitaji kujizoeza kwa bidii na kwa miaka mingi. Ushindi ungeleta sifa kuu kwa washindi na majiji yao.

Katika hali hiyo, si ajabu kwamba waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo walilinganisha shindano la mbio la Wakristo na mashindano ya riadha. Mtume Petro na Paulo walitumia kwa ustadi mifano ya mashindano hayo ili kufundisha mambo muhimu. Leo, shindano hilo kali la mbio la Kikristo bado linaendelea. Wakristo wa karne ya kwanza walilazimika kushindana na mfumo wa mambo wa Wayahudi; sisi leo ‘tunashindana’ na mfumo wa ulimwenguni pote unaokaribia kuharibiwa. (2 Timotheo 2:5; 3:1-5) Huenda wengine wakaona kwamba ‘shindano lao la mbio za imani’ linaendelea tu na linachosha. (1 Timotheo 6:12, Biblia Habari Njema) Tutanufaika sana kwa kuchunguza ufanani kati ya mashindano hayo ya riadha na shindano la mbio la Kikristo.

Mzoezaji Bora

Ushindi wa mwanariadha unategemea sana mzoezaji wake. Kuhusu mashindano hayo ya kale, kichapo Archaeologia Graeca kinasema: “Walioshindana walipaswa kuapa kwamba walifanya mazoezi kwa muda wa miezi kumi.” Wakristo pia wanahitaji kujizoeza kwa bidii. Paulo alimshauri hivi Timotheo, aliyekuwa mzee Mkristo: “Uwe ukijizoeza mwenyewe ujitoaji-kimungu ukiwa shabaha yako.” (1 Timotheo 4:7) Ni nani ambaye humzoeza “mwanariadha” Mkristo? Ni Yehova Mungu mwenyewe! Mtume Petro aliandika: “Mungu wa fadhili yote isiyostahiliwa . . . yeye mwenyewe atamaliza mazoezi yenu, atawafanya imara, atawafanya kuwa wenye nguvu.”—1 Petro 5:10.

Maneno “atamaliza mazoezi yenu” yanatokana na kitenzi cha Kigiriki ambacho kulingana na kichapo Theological Lexicon of the New Testament, kinamaanisha hasa “kufanya kitu [au mtu] kifae kazi ambayo kinakusudiwa, kukitayarisha na kukitengeneza ili kitumike kwa njia inayofaa.” Vivyo hivyo, kichapo Greek-English Lexicon cha Liddell na Scott kinaeleza kwamba kitenzi hicho kinaweza kufafanuliwa kuwa “kutayarisha, kuzoeza, au kuandaa kikamili.” Ni katika njia zipi Yehova ‘hututayarisha, hutuzoeza, au kutuandaa kikamili’ kwa ajili ya shindano la mbio la Kikristo ambalo ni gumu? Ili kuelewa ufanani huo, na tuchunguze njia fulani ambazo wazoezaji walitumia.

Kitabu The Olympic Games in Ancient Greece kinasema: “Wale waliowazoeza vijana walitumia njia mbili hasa. Njia ya kwanza ilikusudiwa kumtia moyo yule anayejizoeza ajitahidi iwezekanavyo kushinda, nayo ya pili ilikusudiwa kuboresha mbinu na njia yake ya kushinda.”

Vivyo hivyo, Yehova hututia moyo na kutuimarisha ili tutende kwa uwezo wetu wote na kuboresha ustadi wetu katika utumishi wake. Mungu wetu hututia nguvu kupitia Biblia, tengenezo lake la kidunia, na Wakristo wenzetu waliokomaa. Mara kwa mara yeye hutuzoeza kupitia nidhamu. (Waebrania 12:6) Wakati mwingine, huenda akaruhusu majaribu na magumu fulani yatupate ili tuweze kusitawisha uvumilivu. (Yakobo 1:2-4) Naye huandaa nguvu tunazohitaji. Nabii Isaya anasema: “Wamngojeao BWANA watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.”—Isaya 40:31.

Zaidi ya yote, Mungu hutupatia roho yake takatifu kwa kiwango kikubwa, ambayo hutuimarisha kuendelea kumtolea utumishi wenye kukubalika. (Luka 11:13) Mara nyingi watumishi wa Mungu—wanaume na wanawake wa kawaida kama sisi—wamevumilia kwa muda mrefu majaribu makali ya imani. Watumishi hao wameweza kuvumilia kwa kumtegemea Mungu kabisa. Naam, ‘nguvu ipitayo iliyo ya kawaida ni ya Mungu na si ile ya kutoka katika wao wenyewe.’—2 Wakorintho 4:7.

Mzoezaji Mwenye Huruma

Mojawapo ya majukumu ya mzoezaji wa kale ilikuwa ‘kuamua kila mwanariadha angehitaji mazoezi ya aina gani na angejizoeza mara ngapi kwa ajili la mchezo fulani,’ anasema msomi mmoja. Mungu anapotuzoeza, yeye huzingatia hali, uwezo, utu, na udhaifu wa kila mmoja wetu. Yehova anapotuzoeza, mara nyingi sisi humsihi kama Ayubu alivyomsihi: “Kumbuka, nakusihi ulivyonifinyanga kama vile udongo.” (Ayubu 10:9) Mzoezaji wetu mwenye huruma anaitikiaje? Daudi aliandika hivi kumhusu Yehova: “Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.”—Zaburi 103:14.

Huenda una tatizo baya sana la kiafya ambalo hukuzuia kufanya mengi katika huduma, au unapambana na hali ya kuhisi kwamba hufai. Labda unajitahidi kuacha zoea fulani baya, au huenda ukahisi kwamba huwezi kupambana na mkazo wa marika wako katika eneo unamoishi, kazini, au shuleni. Hata hali zako ziweje, usisahau kamwe kwamba Yehova huelewa matatizo yako vema zaidi ya mtu mwingine yeyote—hata wewe mwenyewe! Kwa kuwa Yehova ni mzoezaji anayejali, yeye yuko tayari wakati wote kukusaidia iwapo utamkaribia.—Yakobo 4:8.

Wazoezaji wa kale ‘wangeweza kutofautisha uchovu au udhaifu uliotokana na mazoezi na ule uliotokana na hali ya akili, moyo mzito, kushuka moyo na kadhalika. Wazoezaji walikuwa na mamlaka kubwa juu ya wanariadha hivi kwamba wangeweza kuchunguza maisha yao ya faraghani na hata kuingilia kati ilipohitajika.’

Je, nyakati nyingine unahisi ukiwa mchovu au dhaifu kwa sababu ya mikazo na majaribu yasiyokoma ya ulimwengu huu? Mzoezaji wako Yehova anakujali sana. (1 Petro 5:7) Anaweza kutambua haraka ishara yoyote ya udhaifu wa kiroho au uchovu. Ingawa Yehova anatambua kwamba tuna uhuru wa kuchagua, yeye hutoa msaada na masahihisho ya kutosha inapohitajika, kwa kuwa anataka hali yetu iwe nzuri milele. (Isaya 30:21) Jinsi gani? Kupitia Biblia na vichapo vinavyozungumzia Biblia, wazee wa kiroho kutanikoni, na ndugu zetu wenye upendo.

“Kujidhibiti Katika Mambo Yote”

Bila shaka, mengi zaidi ya kuwa na mzoezaji mzuri yalihitajiwa ili mwanariadha ashinde. Mengi yalitegemea mwanariadha mwenyewe na jinsi alivyojitoa kufanya mazoezi kwa bidii. Mazoezi hayo yalikuwa makali, kwa kuwa mwanariadha alihitajika kujinyima kabisa vitu kama vile ngono na pombe, na kula chakula maalum. Horace, mshairi mmoja wa karne ya kwanza K.W.K., alisema kwamba wale walioshindana “waliepuka wanawake na divai” ili “kupata ushindi waliotamani sana.” Naye msomi mmoja wa Biblia F. C. Cook anasema kwamba iliwabidi washiriki wa mashindano hayo ‘wajidhibiti na kula chakula maalum kwa miezi kumi.’

Paulo alitumia ufanani huo alipowaandikia Wakristo wa Korintho, ambao waliyafahamu Mashindano ya Isthmus yaliyofanywa karibu na jiji hilo: “Kila mtu anayeshiriki katika shindano hutumia kujidhibiti katika mambo yote.” (1 Wakorintho 9:25) Wakristo wa kweli huepuka maisha ya ulimwengu huu ya kufuatia vitu vya kimwili, ambayo hayana maadili na ni machafu. (Waefeso 5:3-5; 1 Yohana 2:15-17) Pia ni lazima waache kabisa mwenendo mwovu usiopatana na Maandiko na badala yake wawe na sifa kama za Kristo.—Wakolosai 3:9, 10, 12.

Tunawezaje kufanya hivyo? Kwanza, ona jibu la Paulo alilotoa kwa kutumia mfano unaofaa sana: “Napiga-piga mwili wangu ngumi na kuuongoza kama mtumwa, ili, baada ya mimi kuwa nimewahubiria wengine, mimi mwenyewe nisiwe mwenye kukataliwa kwa njia fulani.”—1 Wakorintho 9:27.

Hapa Paulo alitaja jambo linalofaa kama nini! Hakuwa akipendekeza tujipige kihalisi. Bali alikiri kwamba yeye mwenyewe alikuwa na pambano ndani yake. Mara kwa mara alifanya mambo ambayo hangetaka kufanya na kutofanya yale ambayo angetaka kufanya. Lakini alijitahidi sana asishindwe na udhaifu wake. ‘Aliupiga mwili wake,’ yaani, alijitahidi sana kudhibiti tamaa na maelekeo ya mwili.—Waroma 7:21-25.

Wakristo wote wanahitaji kufanya vivyo hivyo. Paulo alitaja mabadiliko yaliyofanywa na watu fulani huko Korintho ambao awali walikuwa wakifanya uasherati, wakiabudu sanamu, wakifanya ngono na watu wa jinsia zao, wakiiba, na kadhalika. Ni nini kilichowasaidia kubadilika? Nguvu ya Neno la Mungu na roho takatifu pamoja na azimio lao la kuishi kupatana na Neno hilo. Paulo alisema, “Lakini mmeoshwa mkawa safi, lakini mmetakaswa, lakini mmetangazwa kuwa waadilifu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo na kwa roho ya Mungu wetu.” (1 Wakorintho 6:9-11) Petro pia aliandika maneno yanayofanana na hayo kuhusu wale walioacha tabia hizo mbaya. Wakristo hao wote walikuwa wamefanya mabadiliko ya kweli.—1 Petro 4:3, 4.

Jitihada Zilizoelekezwa Vizuri

Paulo alitoa mfano kuhusu azimio lake na jinsi alivyozingatia miradi ya kiroho aliposema: “Jinsi ninavyoelekeza ngumi zangu ni ili nisiwe nikipiga hewa.” (1 Wakorintho 9:26) Mshindani angeelekezaje ngumi zake? Kitabu The Life of the Greeks and Romans kinajibu: “Kilichohitajiwa si kuelekeza ngumi kwa nguvu tu, bali pia kuwa macho sana kutambua udhaifu wa mtu unayepigana naye. Mbinu fulani za kuelekeza ngumi kwa uharaka ambazo zilifunzwa kwenye shule za mieleka, zilikuwa muhimu pia.”

Mwili wetu usio mkamilifu ni adui yetu. Je, tumetambua ‘udhaifu wetu mbalimbali’? Je, tuko tayari kujiona vile wengine watuonavyo—hasa kama vile Shetani anavyoweza kutuona? Hilo linahitaji tujichunguze kwa unyofu na kuazimia kufanya mabadiliko. Tunaweza kujidanganya kwa urahisi. (Yakobo 1:22) Ni rahisi kama nini kujitetea kuhusu mwenendo fulani usio wa hekima! (1 Samweli 15:13-15, 20, 21) Hiyo ni sawa na ‘kupiga hewa.’

Katika siku hizi za mwisho, wale wanaotaka kumpendeza Yehova na kupata uhai wanapaswa kuchagua mara moja kati ya mema na mabaya, kati ya kutaniko la Mungu na ulimwengu uliopotoka. Wanapaswa kuepuka kuyumbayumba, ‘kusitasita kuamua, na kutokuwa imara katika njia zao zote.’ (Yakobo 1:8) Hawapaswi kutumia nguvu zao kufuatia mambo yasiyo na manufaa. Mtu anapojiendesha kwa unyofu na kwa kujitoa kabisa, atakuwa mwenye furaha na ‘kusonga mbele kwake kutapata kuwa dhahiri kwa watu wote.’—1 Timotheo 4:15.

Naam, shindano la mbio la Wakristo linaendelea. Yehova—Mzoezaji wetu Mkuu—anatuandalia kwa upendo mafundisho na msaada tunaohitaji ili kuvumilia na hatimaye kupata ushindi. (Isaya 48:17) Kama wanariadha wa zamani, tunahitaji kusitawisha nidhamu, kujidhibiti, na kujitoa kabisa katika kupigania imani. Jitihada zetu zifaazo zitathawabishwa sana.—Waebrania 11:6.

[Sanduku katika ukurasa wa 31]

‘Mpake Mafuta’

Mpaka-mafuta alitimiza sehemu fulani wakati wa mazoezi ya wanariadha katika Ugiriki ya kale. Kazi yake ilikuwa kuipaka mafuta miili ya wanaume waliokuwa karibu kuanza mazoezi. Wazoezaji “waliona kwamba kuna manufaa fulani zinazotokana na kukanda misuli vizuri kabla ya kuanza mazoezi, na kwamba kumkanda mwanariadha kwa makini na kwa wororo baada ya kufanya mazoezi ya muda mrefu, kunamsaidia kupata nguvu tena,” kinasema kichapo The Olympic Games in Ancient Greece.

Kama vile kujipaka mafuta kunavyoweza kutuliza na hata kuponya, kutumia Neno la Mungu kunaweza kumsahihisha, kumfariji, na kumponya “mwanariadha” Mkristo aliyechoka. Hivyo, wazee wa kutaniko wanaoongozwa na Yehova wanashauriwa wasali kwa ajili ya Mkristo kama huyo “wakimpaka mafuta katika jina la Yehova.” Hiyo ni hatua muhimu inayomsaidia kupona kiroho.—Yakobo 5:13-15; Zaburi 141:5.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Baada ya kutoa dhabihu, wanariadha waliapa kwamba walikuwa wamefanya mazoezi kwa miezi kumi

[Hisani]

Musée du Louvre, Paris

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 29]

Copyright British Museum