Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Wanaoipenda Kweli

Vijana Wanaoipenda Kweli

Vijana Wanaoipenda Kweli

“JINSI gani kijana aisafishe njia yake?” akauliza mtunga-zaburi Mwebrania miaka mingi sana iliyopita. (Zaburi 119:9) Swali hilo bado linafaa leo kwa sababu vijana wanakabili matatizo mengi ulimwenguni. Vijana wengi wamepatwa na UKIMWI kwa sababu ya kufanya ngono ovyoovyo. Nusu ya vijana hao wenye UKIMWI wana umri wa kati ya miaka 15 na 24. Matumizi ya dawa za kulevya pia husababisha matatizo mengi, kutia ndani kifo cha mapema. Vijana huathiriwa sana na muziki unaoshusha heshima, sinema, na vipindi vya televisheni na video vinavyoonyesha jeuri na mambo ya uasherati. Wanaathiriwa sana pia na picha chafu katika Internet. Kwa hiyo, swali ambalo mtunga-zaburi anauliza linawahangaisha sana wazazi na vijana wengi leo.

Mtunga-zaburi huyo anajibu swali lake hivi: “Kwa kutii, akilifuata neno lako.” Ni kweli kwamba Neno la Mungu, Biblia, lina mwongozo mzuri kwa vijana, na wengi wao hufanikiwa maishani wanapoufuata. (Zaburi 119:105) Na tuone mifano ya vijana kadhaa ambao wanampenda Mungu na wanaojitahidi kuendelea kuwa imara kiroho katika ulimwengu unaofuatia anasa na vitu vya kimwili.

Wanashukuru kwa Mwongozo wa Wazazi

Jacob Emmanuel alikuwa painia, yaani, mhudumu wa wakati wote kwa miaka kadhaa, kabla ya kuanza kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Mexico. Yeye hukumbuka kwa shukrani jinsi upendo wake kwa Mungu ulivyositawishwa: “Wazazi wangu na pia ndugu fulani waliokomaa kiroho, ambao ni rafiki zangu, walinisaidia sana. Walinichochea kupenda kazi ya kuhubiri na kunielekeza kwa upole katika njia inayofaa; hawakunikaza.”

David, ambaye tayari ametumikia kwa miaka kadhaa katika huduma ya wakati wote, anakumbuka jinsi alivyochochewa na wazazi wake ambao walianza kutumikia wakiwa mapainia wa pekee wakati yeye na ndugu yake walipokuwa wachanga. Baba yake alipokufa, mama yake aliendelea kutumikia akiwa painia wa pekee. Aliwatunza na vilevile kuhubiri habari njema. “[Wazazi] wangu hawakunikaza niwe painia, lakini tulifurahia upainia tukiwa familia hivi kwamba nilichochewa na ushirika na mazingira hayo kuwa painia,” anasema David. Kuhusu umuhimu wa mwongozo na utunzaji unaofaa wa wazazi, David anasema: “Kila usiku mama yetu alitusomea hadithi katika kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana. * Alisimulia hadithi hizo kwa njia ambayo ilitusaidia kupenda chakula cha kiroho.”

Kuthamini Mikutano

Vijana wengine huona ni vigumu kuthamini mikutano ya Kikristo. Wao huihudhuria tu kwa sababu wazazi wao huandamana nao. Hata hivyo, baadaye wanaweza kuthamini mikutano iwapo wataendelea kuihudhuria. Fikiria Alfredo, aliyeanza utumishi wa wakati wote akiwa na umri wa miaka 11. Yeye anakiri kwamba alipokuwa na umri wa miaka mitano hivi, alijaribu kuepuka kwenda kwenye mikutano kwa kuwa ilimfanya asinzie, lakini wazazi wake hawakumruhusu alale wakati wa mikutano. Yeye anakumbuka: “Kadiri nilivyokua, ndivyo nilivyozidi kupendezwa na mikutano, hasa nilipojua kusoma na kuandika kwa sababu nilianza kutoa maelezo kwa kutumia maneno yangu mwenyewe.”

Cintia, msichana mwenye umri wa miaka 17 ambaye anatumikia akiwa painia wa kawaida, anaeleza jinsi mashirika mazuri yalivyomsaidia sana kupenda utumishi wa Mungu. Yeye anasema: “Uhusiano mzuri na akina ndugu na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida hufanya nisitamani kuwa na marafiki wa ulimwengu au kutamani mambo ambayo vijana wanapenda sana kama vile kwenda disko. Kusikiliza maelezo na mambo yaliyoonwa kwenye mikutano kulinichochea kumpa Yehova vyote nilivyo navyo, na ninaona kwamba ujana wangu ndicho kitu bora zaidi ninachoweza kumpa. Kwa hiyo nimeamua kutumia ujana wangu katika utumishi wake.”

Hata hivyo, Cintia anakiri hivi: “Wakati fulani kabla sijabatizwa, niliona ni rahisi kukosa mikutano kwa kusingizia kwamba nilikuwa na kazi ya kufanyia nyumbani niliyopewa shuleni. Nilikosa mikutano kadhaa, na jambo hilo likaanza kuniathiri kiroho. Nilifanya urafiki na mvulana mmoja ambaye hakuwa akijifunza Biblia lakini kwa msaada wa Yehova nikaachana naye kabla haijawa kuchelewa mno.”

Uamuzi wa Kibinafsi

Pablo, kijana mwingine anayemtumikia Yehova kwa wakati wote, anasema hivi anapoulizwa juu ya jambo kuu lililomsaidia kupenda kweli ya Neno la Mungu: “Ninafikiri kuna mambo mawili: funzo la kibinafsi la ukawaida na bidii katika kuhubiri. Ninawashukuru wazazi wangu kwa kunifunza kweli kumhusu Yehova, nami ninaona kwamba kweli ndiyo kitu bora zaidi ambacho wangeweza kunifunza. Hata hivyo, ninahitaji kujithibitishia ni kwa nini ninampenda Yehova. Ili kufanya hivyo, ni muhimu kujua ‘upana na kina’ cha kweli ya Biblia. Ni kwa njia hiyo tu tunaweza kuanza kulitamani Neno la Yehova ambalo huwasha ‘moto’ ndani yetu unaotuchochea kuwaeleza wengine kulihusu. Bidii hiyo kwa ajili ya kazi ya kuhubiri itafanya tuithamini kweli zaidi.”—Waefeso 3:18; Yeremia 20:9.

Jacob Emmanuel, aliyetajwa hapo awali, anakumbuka pia umuhimu wa kufanya uamuzi wa kibinafsi ili kumtumikia Yehova. Anasema kwamba wazazi wake hawakumkaza abatizwe. “Ninaamini kwamba walifanya vizuri sana kwa sababu ninaona matokeo mazuri ya kutonikaza. Kwa mfano, vijana waliokuwa marafiki wangu wakuu waliamua kubatizwa wote wakati mmoja. Ingawa haikuwa vibaya kufanya hivyo, ningeweza kuona kwamba baadhi yao walibatizwa kwa sababu ya msisimuko tu, na muda mfupi baadaye, bidii yao kwa kazi ya Ufalme ikafifia. Wazazi wangu hawakunikaza nifanye uamuzi wa kujiweka wakfu kwa Yehova. Huo ulikuwa uamuzi wangu binafsi.”

Kutaniko Lilitimiza Nini?

Vijana wengine wamejifunza kweli ya Neno la Mungu bila msaada wa wazazi wao. Kwa kweli si rahisi katika hali kama hizo kujifunza kufanya mambo yanayofaa na kuendelea kuyafanya.

Noé anakumbuka jinsi kweli ilivyomfaidi. Alikuwa mwenye hasira na jeuri tangu alipokuwa mchanga. Alipoanza kujifunza Biblia akiwa na umri wa miaka 14, hasira yake ilianza kupungua. Wazazi wake ambao wakati huo hawakupendezwa na Biblia, walifurahi sana. Noé alipofanya maendeleo ya kiroho, alitaka kutumia maisha yake kikamili zaidi katika kumtumikia Mungu. Sasa anamtumikia kwa wakati wote.

Vivyo hivyo, Alejandro alianza kupendezwa na kweli ya Kikristo alipokuwa mchanga sana hata ingawa wazazi wake hawakupendezwa. Anasema hivi kuonyesha uthamini wake kwa kweli hiyo: “Nililelewa katika familia ya Wakatoliki. Lakini nikaanza kupendezwa zaidi na imani ya Wakomunisti kwamba hakuna Mungu, kwa kuwa kanisa lilishindwa kujibu maswali yaliyokuwa yamenisumbua tangu nilipokuwa mchanga. Tengenezo la Yehova lilinisaidia kumjua Mungu. Liliniokoa kihalisi kwa sababu kama nisingalijifunza Biblia, labda ningalijiingiza katika mambo yasiyo safi kiadili na ningalianza kunywa pombe kupita kiasi, au kutumia madawa ya kulevya. Huenda hata ningalijiunga na kikundi fulani cha wanamageuzi na matokeo yangalikuwa mabaya sana.”

Kijana anawezaje kuendelea kuitafuta kweli na kuifuata bila kuungwa mkono na wazazi wake? Hapana shaka kwamba wazee na ndugu wengine kutanikoni husaidia sana. Noé anakumbuka: “Sijawahi kuhisi mpweke, kwa kuwa Yehova amekuwa karibu sana nami. Pia nimetegemezwa na ndugu na dada wenye upendo ambao wamekuwa baba, mama, na ndugu zangu kiroho.” Sasa yuko Betheli na anatumia wakati wake kumtumikia Mungu. Naye Alejandro anaeleza: “Nitashukuru daima kwa sababu nilinufaika kuwa katika kutaniko lenye wazee waliopendezwa nami kibinafsi. Ninashukuru sana kwa jambo hilo kwa sababu nilipoanza kujifunza Biblia nikiwa na umri wa miaka 16, niliathiriwa na masumbufu yanayowapata vijana. Familia katika kutaniko hazikuniacha. Sikuzote nilikaribishwa nyumbani kwao kwa chakula na nilionyeshwa huruma.” Sasa Alejandro amekuwa mtumishi wa wakati wote kwa miaka zaidi ya 13.

Watu wengine hufikiri kwamba dini ni ya wazee tu. Hata hivyo, vijana wengi wamejifunza kweli ya Biblia wakiwa wachanga na wanampenda Yehova na ni waaminifu kwake. Maneno ya Daudi kwenye Zaburi 110:3 yanaweza kutumiwa kuwahusu: “Watu wako wanajitoa kwa hiari, siku ya uwezo wako; kwa uzuri wa utakatifu, tokea tumbo la asubuhi, unao umande wa ujana wako.”

Vijana wanahitaji kujitahidi sana kujifunza kweli na kuifuata. Inafurahisha kama nini kuona kwamba wengi wameshikamana na tengenezo la Yehova, wanahudhuria mikutano kwa ukawaida, na kujifunza Biblia kwa bidii. Kwa kufanya hivyo, wameweza kusitawisha upendo wa kweli kwa Neno la Mungu na utumishi wake!—Zaburi 119:15, 16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1958 lakini sasa hakichapwi.