Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Roho Wanaosababisha Maovu?

Je, Kuna Roho Wanaosababisha Maovu?

Je, Kuna Roho Wanaosababisha Maovu?

“Ulimwengu umechanganyikiwa, ni kana kwamba kuna nguvu fulani zinazozidi uwezo wa kibinadamu zinazojaribu kuufunga kabisa.”—Mwandishi wa habari Jean-Claude Souléry.

‘Hali ya kusikitisha ya watu inafanya ionekane kwamba kuna uovu mkuu unaotawala.’—Mwanahistoria Josef Barton.

ULE msiba wenye kutisha wa Septemba 11, 2001, uliosababishwa na mashambulizi ya magaidi ulifanya watu wengi wafikirie sana. Michael Prowse alisema hivi katika gazeti moja la Uingereza liitwalo Financial Times: “Hakuna mnyama yeyote anayeweza kutenda kinyama hivyo.” Mhariri mmoja katika gazeti la New York Times aliandika kwamba mbali na kufikiria mipango iliyofanywa ili kutekeleza mashambulizi hayo, inafaa “kufikiria pia chuki mbaya sana iliyowasukuma watu hao kufanya mashambulizi hayo. Hiyo ni chuki mbaya mno inayozidi sana vita vya kawaida, ni chuki isiyo na kifani, na ni chuki ambayo haitaki mapatano yoyote.”

Wafuasi wa dini tofauti-tofauti walifikiri kwamba huenda ikawa kuna roho fulani anayesababisha matendo ya ukatili. Mfanyabiashara mmoja wa Sarajevo aliyejionea ukatili wa vita vya kikabila kule Bosnia alisema hivi: “Baada ya mwaka mmoja wa vita vya Bosnia, naamini kwamba Shetani ndiye anayeongoza mambo hayo. Hali hii yote ni ukichaa.”

Mwanahistoria Jean De-lumeau alijibu hivi alipoombwa aeleze maoni yake kumhusu Ibilisi: “Siwezi kamwe kusema kwamba hakuna Ibilisi kwa sababu ya mambo ambayo nimeona tangu nizaliwe na yale yanayoendelea sasa: Ile vita ya ulimwengu ya pili iliyosababisha vifo vya watu zaidi ya milioni 40; kambi ya kifo ya Auschwitz na nyinginezo; machinjo makubwa nchini Cambodia; utawala mkatili wa Ceauşescu; na mbinu za kutesa watu ambazo zinatumiwa na serikali nyingi ulimwenguni. Matendo ya ukatili ni mengi sana. . . . Ninaamini hatukosei tunaposema kwamba matendo hayo ‘ni ya kishetani.’ Na matendo hayo hayachochewi na Ibilisi mwenye pembe na kwato bali yanachochewa na Ibilisi anayewakilisha roho na nguvu ya uovu inayoongoza duniani.”

Kama Jean Delumeau, watu wengi pia wanaona kwamba matendo ya ukatili yanayotendeka katika jamii leo, katika familia na hata kati ya mataifa, “ni ya kishetani.” Hiyo inamaanisha nini? Je, matendo hayo ya ukatili yanasababishwa na nguvu fulani tu za uovu, au yanasababishwa na kiumbe mwovu anayewachochea wanadamu kutenda matendo ya kinyama ambayo kwa kawaida binadamu hawezi kuyatenda? Je, nguvu hizo huongozwa na mkuu wa uovu, Shetani Ibilisi?

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

Children: U.S. Coast Guard photo