Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Shetani Ni Hadithi Tu au Ni Mtu Halisi Mwovu?

Je, Shetani Ni Hadithi Tu au Ni Mtu Halisi Mwovu?

Je, Shetani Ni Hadithi Tu au Ni Mtu Halisi Mwovu?

KISABABISHI cha uovu kimesumbua wataalamu tangu zamani za kale. Kitabu kinachoitwa A Dictionary of the Bible cha James Hastings kinasema hivi: “Mwanadamu alipoanza kufahamu mambo, alijikuta akikabili nguvu ambazo hangeweza kuzidhibiti ambazo zilitokeza madhara.” Kitabu hicho kinaongezea kusema: “Wanadamu wa awali walijaribu kutafuta visababishi vya maovu, wakafikiri kwamba maovu na nguvu nyinginezo za asili zinasababishwa na mtu fulani.”

Kulingana na wanahistoria, tangu nyakati za Mesopotamia ya kale, watu waliamini kwamba kuna miungu ya kishetani na roho waovu. Wababiloni wa kale waliamini kwamba Nergali, mungu mkatili aliyeitwa pia “mwenye kuwaka,” ndiye aliyesimamia “ulimwengu wa wafu.” Wababiloni pia waliwaogopa roho waovu, na walijaribu kuridhisha roho hao kwa nyimbo za kupandisha pepo. Katika hekaya za Wamisri, Set alikuwa mungu wa uovu, “naye aliwakilishwa na mnyama wa ajabu sana mwenye pua ndefu iliyo nyembamba na yenye kupinda kidogo, na masikio yake yalikuwa marefu na yenye umbo la mraba na alikuwa na mkia mgumu unaofanana na uma.”—Larousse Encyclopedia of Mythology.

Ingawa Wagiriki na Waroma walikuwa na miungu mizuri na mibaya, hawakuwa na mungu mmoja mkuu wa uovu. Wanafalsafa wao walifundisha kwamba kuna nguvu mbili zinazopingana. Empedocles aliziita nguvu hizo Upendo na Zogo. Plato naye alifikiri kwamba ulimwengu una “Nafsi” mbili, nafsi moja ikisababisha mema na nafsi nyingine ikisababisha maovu. Na kama Georges Minois anavyotaja katika kitabu Le Diable (Ibilisi), “dini ya kale ya kipagani [ya Wagiriki na Waroma] haikutambua kwamba Ibilisi yuko.”

Nchini Iran, dini ya Zoroaster ilifundisha kwamba mungu mkuu zaidi Ahura Mazda, au Ormazd, alimwumba Angra Mainyu, au Ahriman, aliyeamua kutenda maovu na kuwa Roho Mwangamizi.

Katika Dini ya Kiyahudi, Shetani alifafanuliwa kwa njia rahisi kuwa Mpinzani wa Mungu aliyesababisha dhambi. Lakini baada ya karne nyingi, fundisho hilo likachanganywa na mafundisho ya kipagani. Kitabu Encyclopaedia Judaica kinasema hivi: “Badiliko kubwa lilikuwa limetokea . . . kufikia karne za mwisho-mwisho K.W.K. Nyakati hizo, Dini [ya Kiyahudi] . . . ilikubali dhana nyingi kwamba kuna nguvu mbili zinazopingana mbinguni na duniani. Upande mmoja kuna Mungu na nguvu nyinginezo za wema na kweli, na upande mwingine kuna nguvu za uovu na udanganyifu zenye uwezo sana. Inaonekana walipata dhana hizo katika dini ya Waajemi.” Kitabu The Concise Jewish Encyclopedia kinasema: “Watu walijikinga [na roho waovu] kwa kushika amri na kwa kutumia hirizi.”

Mafundisho ya Wakristo Walioasi

Kama ambavyo Dini ya Kiyahudi ilivyokubali mafundisho yasiyo ya Kimaandiko kuhusu Shetani na roho waovu, Wakristo walioasi pia waliendeleza mafundisho yasiyo ya Kimaandiko. Kitabu The Anchor Bible Dictionary kinasema: “Mojawapo ya mafundisho ya kidini ya kale yaliyo mabaya zaidi yalisema kwamba Mungu alimlipa Shetani ili kuwakomboa watu wake.” Irenayo (karne ya pili W.K.) ndiye aliyeeneza fundisho hilo. Origen (karne ya tatu W.K.) pia aliliendeleza fundisho hilo akidai kwamba “ibilisi alikuwa na haki kisheria kudai malipo juu ya wanadamu” na aliona “kifo cha Kristo . . . kuwa fidia ambayo ibilisi alilipwa.”—History of Dogma, cha Adolf Harnack.

Kitabu The Catholic Encyclopedia kinasema: “Kwa miaka elfu moja hivi [fundisho la kwamba Ibilisi alilipwa fidia] lilikuwa sehemu kuu ya mafundisho ya kidini” na fundisho hilo likabaki likiwa imani ya kanisa. Wakuu wengine wa Kanisa, hata na Augustine (karne ya nne na ya tano W.K.), pia walikubali wazo la kwamba ni Shetani aliyelipwa fidia. Hatimaye, kufikia karne ya 12 W.K., wanatheolojia wa Katoliki Anselm na Abelard walikata kauli ya kwamba ni Mungu aliyelipwa dhabihu ya Kristo na wala si Shetani.

Ushirikina Katika Enzi za Kati

Ingawa mabaraza mengi ya Kanisa Katoliki yalibaki kimya sana kuhusu suala hilo la Shetani, mwaka wa 1215 W.K., Baraza Kuu la Nne la Kanisa lilitokeza fundisho ambalo New Catholic Encyclopedia inaliita “tangazo zito la imani.” Kanuni ya Kwanza inasema: “Ibilisi na roho wengine waovu waliumbwa na Mungu wakiwa wazuri, lakini wao wenyewe wakawa waovu.” Kanuni hiyo inaendelea kusema kwamba wao wanajaribu sana kuwadanganya wanadamu. Hili jambo la kuwadanganya wanadamu liliwasumbua watu sana katika Zama za Kati. Ikawa kwamba ni Shetani aliyekuwa akisababisha jambo lolote lile lililoonekana kuwa si la kawaida, kama vile ugonjwa usioeleweka, kifo cha ghafula, au kukosa mavuno. Mwaka wa 1233 W.K., Papa Gregory wa 9 alitoa amri kadhaa dhidi ya wazushi, kutia ndani amri fulani dhidi ya Walusiferi, wale walioonwa kuwa waabudu wa Shetani.

Kule kuamini kwamba watu wanaweza kupagawa na Ibilisi au roho waovu kulifanya watu waogope sana mambo ya uchawi. Tokea karne ya 13 hadi 17, kotekote Ulaya watu wakaogopa sana wachawi na woga huo ukasambazwa hata Amerika Kaskazini na watu waliotoka Ulaya. Hata watetezi Waprotestanti wa marekebisho ya kidini kama Martin Luther na John Calvin waliidhinisha tabia ya kuwasaka wachawi. Kule Ulaya, mashtaka yaliyotegemea uvumi tu au shutuma zisizo za kweli yalisikilizwa na Mabaraza ya Kuhukumu Wazushi au na mahakama za nchi. Kwa kawaida watu walikuwa wakiteswa ili wakubali “hatia.”

Wale waliopatikana na hatia wangeweza kuhukumiwa kifo kwa kuteketezwa moto, na katika Uingereza na Scotland, hukumu hiyo ingetekelezwa kwa kunyongwa. Kitabu The World Book Encyclopedia kinasema hivi kuhusu idadi ya wale waliohukumiwa: “Kulingana na baadhi ya wanahistoria, tokea mwaka wa 1484 hadi 1782, kanisa la Kikristo liliwaua wanawake wapatao 300,000 kwa kuwashuku kuwa wachawi.” Ikiwa Shetani ndiye aliyechochea ukatili huo, basi alitumia nani kutekeleza mauaji hayo? Je, ni wale waliouawa au aliwatumia wanyanyasi shupavu wa kidini?

Itikadi za Wakati Huu

Katika karne ya 18, kipindi cha Uelewevu kiliibuka. Kitabu Encyclopædia Britannica kinasema: “Falsafa na mafundisho yaliyotokana na ule Uelewevu zilijaribu kufanya Mkristo aamini kwamba ibilisi ni dhana tu katika hadithi za Zama za Kati.” Lakini katika Baraza la Kwanza la Vatican (1869-1870), Kanisa Katoliki lilikataa jambo hilo na kusisitiza kwamba linaamini kuna Shetani Ibilisi, likirudia kutaja msimamo huo katika Baraza la Pili la Vatican (1962-1965), japo wakati huo si kwa bidii kama katika baraza la kwanza.

Kitabu New Catholic Encyclopedia kinakiri kwamba kirasmi “Kanisa linaamini kuna malaika na roho waovu.” Hata hivyo, Théo, ambayo ni kamusi ya Kifaransa ya Ukatoliki, inakiri kwamba “Wakristo wengi leo hawaoni kama maovu yanasababishwa na ibilisi.” Katika miaka ya karibuni wanatheolojia wa Katoliki wamekuwa katika njia panda, wakitatanika kati ya fundisho rasmi la Katoliki na dhana za watu wengi wakati huu kuhusu Shetani. Kitabu Encyclopædia Britannica kinasema kwamba ‘mafundisho ya Kikristo yasiyo ya kishupavu yanasema kwamba Biblia inatumia Shetani kwa njia ya “mfano tu” inaporejelea uovu na basi Shetani hapaswi kuonwa kuwa mtu halisi—yaani, hiyo ni njia tu ya kutumia hadithi kuonyesha kwamba kuna uovu na kwamba uovu huo umeenea ulimwenguni.’ Kitabu hichohicho kinasema hivi kuhusu Waprotestanti: “Uprotestanti wa kisasa usioshikilia sana mambo una mwelekeo wa kuonyesha kwamba si muhimu kuamini ibilisi ni mtu halisi.” Lakini je, Wakristo wa kweli wayaone maoni ya Biblia juu ya Shetani kuwa “mfano tu”?

Maoni ya Maandiko

Falsafa za wanadamu na mafundisho ya kidini hayafafanui vizuri kisababishi cha uovu kama Biblia inavyoonyesha. Mambo ambayo Maandiko yanasema kuhusu Shetani yanatusaidia sana kuelewa chanzo cha uovu na kuteseka kwa wanadamu, na vilevile kuelewa ni kwa nini ujeuri unazidi kuongezeka kila mwaka.

Mtu anaweza kuuliza: ‘Ikiwa Mungu ni Muumba mzuri mwenye upendo, kwa nini alimwumba kiumbe mkatili, Shetani?’ Biblia inataja kanuni ya kwamba kazi zote za Yehova Mungu ni kamilifu na kwamba viumbe wake wote wenye akili wana hiari. (Kumbukumbu la Torati 30:19; 32:4; Yoshua 24:15; 1 Wafalme 18:21) Basi, ni lazima yule mtu mwenye mwili wa roho ambaye baadaye alikuwa Shetani aliumbwa akiwa mkamilifu na ni lazima aliacha njia ya kweli ya uadilifu kwa hiari yake.—Yohana 8:44; Yakobo 1:14, 15.

Uasi wa Shetani unafanana kwa njia nyingi na uasi wa “mfalme wa Tiro,” aliyetajwa kishairi kuwa mwenye “ukamilifu wa uzuri” na ‘mkamilifu katika njia zake zote tangu siku ile alipoumbwa, hata uovu ulipoonekana ndani yake.’ (Ezekieli 28:11-19) Shetani hakubisha ukuu wa Yehova wala hakubisha akisema Yehova si Muumba. Hangeweza kubisha jambo hilo kwani yeye mwenyewe aliumbwa na Mungu! Lakini Shetani alipinga jinsi Yehova anavyotekeleza mamlaka yake akiwa mwenye enzi kuu. Katika bustani ya Edeni, Shetani alidokeza kwamba Mungu alikuwa akiwanyima Adamu na Hawa kitu ambacho ni haki yao na ambacho kingewafaidi. (Mwanzo 3:1-5) Alifaulu kuwafanya Adamu na Hawa waasi dhidi ya enzi kuu adilifu ya Yehova, matokeo yakiwa dhambi na kifo kwao na kwa wazao wao. (Mwanzo 3:6-19; Waroma 5:12) Basi, Biblia inaonyesha kwamba Shetani ndiye msababishi mkuu wa kuteseka kwa wanadamu.

Pindi fulani kabla ya Furiko, malaika wengine walijiunga na maasi ya Shetani. Walitwaa miili ya wanadamu ili kuridhisha tamaa zao za kingono pamoja na binti za wanadamu. (Mwanzo 6:1-4) Wakati wa Furiko, malaika hao waasi walirudi kwenye makao ya roho lakini hawakurudia “cheo chao cha awali” pamoja na Mungu mbinguni. (Yuda 6) Walishushwa kwenye hali ya giza tititi la kiroho. (1 Petro 3:19, 20; 2 Petro 2:4) Wakawa roho waovu ambao sasa hawakuwa wakitii enzi kuu ya Yehova bali Shetani. Ingawa inaonekana hawawezi kutwaa miili ya wanadamu tena, bado wana uwezo mkubwa wa kutawala akili na maisha ya wanadamu, na bila shaka wanasababisha kadiri kubwa ya ujeuri tunaoona leo.—Mathayo 12:43-45; Luka 8:27-33.

Mwisho wa Utawala wa Shetani Umekaribia

Ni wazi kwamba kuna roho waovu ulimwenguni leo. Mtume Yohana aliandika hivi: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.”—1 Yohana 5:19.

Unabii wa Biblia ambao umetimia unaonyesha kwamba Ibilisi anazidisha ole duniani kwa sababu anajua “ana kipindi kifupi cha wakati” cha kueneza maovu kabla ya kufungwa. (Ufunuo 12:7-12; 20:1-3) Mwisho wa utawala wa Shetani utaleta ulimwengu mpya wenye uadilifu, ambamo machozi, kifo, na maumivu ‘hayatakuwapo tena.’ Kisha mapenzi ya Mungu ‘yatatimizwa hapa duniani kama huko mbinguni.’—Ufunuo 21:1-4; Mathayo 6:10, Union Version.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Wababiloni waliabudu mungu mkatili, Nergali (kushoto zaidi); Plato (kushoto) aliamini kwamba kuna “Nafsi” mbili zinazopingana

[Hisani]

Cylinder: Musée du Louvre, Paris; Plato: National Archaeological Museum, Athens, Greece

[Picha katika ukurasa wa 5]

Irenaeus, Origen, na Augustine walifundisha kwamba Ibilisi alilipwa fidia

[Hisani]

Origen: Culver Pictures; Augustine: From the book Great Men and Famous Women

[Picha katika ukurasa wa 6]

Kuhofu wachawi kulizusha mauaji ya mamia ya maelfu ya watu

[Hisani]

From the book Bildersaal deutscher Geschichte