Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wakristo Wanapaswa Kuwa na Wivu?

Je, Wakristo Wanapaswa Kuwa na Wivu?

Je, Wakristo Wanapaswa Kuwa na Wivu?

JE, WAKRISTO wanapaswa kukuza sifa ya wivu? Tukiwa Wakristo, tunatiwa moyo ‘kufuatia upendo,’ na tunaambiwa kwamba “upendo hauna wivu.” (1 Wakorintho 13:4; 14:1) Kwa upande mwingine, tunaambiwa kwamba “BWANA . . . ni Mungu mwenye wivu” na tunaamriwa ‘tuwe waigaji wa Mungu.’ (Kutoka 34:14; Waefeso 5:1) Mbona yaonekana kwamba Maandiko hayo yanapingana?

Ni kwa sababu maneno ya Kiebrania na ya Kigiriki yanayotafsiriwa “wivu” katika Biblia yana maana nyingi mbalimbali. Yanaweza kuwa na maana nzuri au maana mbaya, ikitegemea jinsi yanavyotumiwa. Kwa mfano, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “wivu” linaweza kumaanisha “kutaka ujitoaji usiohusisha wengine; kutovumilia ushindani wowote; bidii; shauku; wivu [wa uadilifu au mwovu]; husuda.” Na neno la Kigiriki lina maana hiyohiyo ya neno la Kiebrania. Maneno hayo yanaweza kumaanisha hisia isiyofaa kuelekea mtu anayeonekana kuwa mpinzani au anayedhaniwa kuwa anafaidika. (Mithali 27:4) Maneno hayo yanaweza pia kutumiwa ifaavyo kuelezea sifa ya Mungu kwa kutaka kumlinda mtu umpendaye asipate madhara.—2 Wakorintho 11:2.

Mfano Bora Kabisa

Yehova huonyesha wivu unaofaa kwa njia iliyo bora kabisa. Yeye huwa na nia nzuri ya kuwalinda watu wake wasichafuliwe kiroho na kiadili. Alisema hivi kuhusu watu wake wa kale walioitwa jina la kifumbo, Sayuni: “Mimi nina wivu kwa ajili ya Sayuni, wivu mkuu, nami nina wivu kwa ajili yake kwa ghadhabu kuu.” (Zekaria 8:2) Kama vile baba mwenye upendo anavyokuwa chonjo daima ili kuwalinda watoto wake wasipate madhara, Yehova yu macho kuwalinda watumishi wake dhidi ya hatari ya kimwili na ya kiroho.

Yehova aliwapatia watu wake Neno lake, Biblia ili liwalinde. Lina mashauri mengi ya kuwasaidia waishi kwa hekima, na lina mifano mingi ya watu waliofanya hivyo. Tunasoma hivi kwenye Isaya 48:17: “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.” Ni faraja iliyoje kujua kwamba wivu wake humfanya atutunze na kutulinda! Kama hangelikuwa na wivu huo unaofaa, tungepata madhara mbalimbali kwa sababu hatuna ujuzi wa kutosha. Wivu wa Yehova si wa ubinafsi kamwe.

Basi, tofauti ni nini kati ya wivu wa kimungu na wivu usiofaa? Ili kupata jibu, hebu tuchunguze mfano wa Miriamu na Finehasi. Hebu fikiria kilichowachochea kutenda jinsi walivyotenda.

Miriamu na Finehasi

Miriamu alikuwa dada mkubwa ya Musa na Haruni, ambao waliwaongoza Waisraeli walipokuwa wakitoka Misri. Waisraeli walipokuwa nyikani, Miriamu alimwonea wivu Musa nduguye. Biblia yasema hivi: “Kisha Miriamu na Haruni wakamnenea Musa kwa sababu ya mwanamke Mkushi aliyekuwa amemwoa . . . Wakasema, Je! Ni kweli BWANA amenena na Musa tu? Hakunena na sisi pia?” Inaonekana kwamba Miriamu aliongoza katika kumshutumu Musa, ndiyo sababu Yehova alimwadhibu Miriamu wala si Haruni, kwa kumpiga kwa ukoma kwa muda wa juma moja kwa sababu alikosa heshima.—Hesabu 12:1-15.

Ni nini kilichomchochea Miriamu amshutumu Musa? Je, ni kwa sababu alijali ibada ya kweli na je, alikuwa na nia ya kuwalinda Waisraeli wenzake wasipate madhara? Bila shaka la. Inaonekana kwamba Miriamu alikuwa amesitawisha moyoni mwake tamaa isiyofaa ya umashuhuri na mamlaka. Alikuwa nabii wa kike katika Israeli, na hivyo watu walimheshimu sana, hasa wanawake. Aliwaongoza katika nyimbo na kucheza baada ya Waisraeli kuokolewa kimuujiza katika Bahari Nyekundu. Lakini baada ya muda, yaonekana kwamba Miriamu aliogopa kwamba umashuhuri wake ungemwendea mke wa Musa, ambaye alimwona kuwa mshindani wake. Huku akichochewa na wivu wa kichoyo, alichochea upinzani dhidi ya Musa ambaye aliteuliwa rasmi na Yehova.—Kutoka 15:1, 20, 21.

Finehasi naye alitenda akiwa na nia tofauti. Waisraeli walipokuwa wamepiga kambi kwenye Nyanda za Moabu kabla tu ya kuingia Nchi ya Ahadi, wanawake Wamoabu na Wamidiani waliwashawishi wanaume wengi Waisraeli wafanye uasherati na kuabudu sanamu. Waamuzi wa Israeli waliamuriwa wawaue wanaume wote waliokuwa wameasi, ili kuitakasa kambi na kuizuia hasira kali ya Yehova. Kwa ushupavu, Zimri, mkuu wa kabila la Simeoni alimleta Kozbi, mwanamke Mmidiani katika kambi “mbele ya macho ya mkutano wote wa wana wa Israeli.” Finehasi alichukua hatua mara moja. Huku akichochewa na wivu, au bidii, kwa ajili ya ibada ya Yehova na akiwa na nia ya kudumisha utakatifu wa maadili kambini, aliwaangamiza waasherati hao hemani mwao. Alipongezwa kwa ajili ya kuwa na “hasira ya wivu,” “kutovumilia kamwe ushindani wowote” dhidi ya Yehova. Tendo la haraka la Finehasi lilikomesha pigo ambalo lilikuwa tayari limewaua watu 24,000, naye Yehova akamthawabisha kwa kumpa agano la ukuhani wa milele katika ukoo wake.—Hesabu 25:4-13; The New English Bible.

Wivu wa Miriamu ulitofautianaje na wivu wa Finehasi? Miriamu alimshutumu nduguye kwa sababu alimwonea wivu wa kichoyo, lakini Finehasi alitekeleza haki kwa sababu ya wivu wa kimungu. Nyakati nyingine tunahitaji kuwa kama Finehasi, kwa kulitetea kwa maneno au kwa matendo jina la Yehova, ibada yake, na watu wake.

Wivu Usiofaa

Lakini, je, mtu anaweza kuwa na wivu usiofaa? Ndiyo. Wayahudi wengi katika karne ya kwanza walikuwa na wivu usiofaa. Walilinda kwa wivu Sheria ya Mungu na mapokeo yao. Walijaribu kuilinda Sheria kwa kuweka maagizo na masharti mengi madogo-madogo ambayo yaliwalemea watu sana. (Mathayo 23:4) Kwa kuwa hawakuweza au hawakutaka kutambua kwamba Mungu alikuwa ameiondoa Sheria ya Musa na kuanzisha kile kilichowakilishwa na Sheria hiyo, walichochewa na wivu kuwaghadhibikia vikali wafuasi wa Yesu Kristo. Mtume Paulo, ambaye wakati mmoja alishikilia Sheria kwa wivu usiofaa alisema kwamba watu waliokuwa wakiitetea Sheria walikuwa na “bidii [wivu] kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.”—Waroma 10:2; Wagalatia 1:14.

Hata haikuwa rahisi kwa Wayahudi wengi waliokuja kuwa Wakristo kuacha kabisa bidii hiyo inayozidi mpaka kwa ajili ya Sheria. Baada ya safari yake ya tatu ya kimishonari, Paulo alipeleka ripoti kwa baraza lililokuwa likiongoza kuhusu watu wa mataifa waliogeuzwa imani. Wakati huo, maelfu ya Wakristo Wayahudi walikuwa “wenye bidii kuhusu Sheria.” (Matendo 21:20) Miaka mingi ilikuwa imepita tangu baraza hilo lilipoamua kwamba Wakristo wasio Wayahudi hawakuhitaji kutahiriwa. Mambo fulani kuhusu kushika Sheria yalikuwa yakileta migawanyiko kutanikoni. (Matendo 15:1, 2, 28, 29; Wagalatia 4:9, 10; 5:7-12) Kwa sababu ya kutojua jinsi Yehova alivyoshughulika na watu wake wakati huo, baadhi ya Wakristo Wayahudi walisisitiza maoni yao na kuwachambua wengine.—Wakolosai 2:17; Waebrania 10:1.

Kwa hiyo ni lazima tuepuke hatari ya kujaribu kushikilia tu maoni yetu au kufuata njia ambazo hazitegemei kabisa Neno la Mungu. Tunapaswa kukubali uelewevu mpya wa Neno la Mungu unaotolewa na wale ambao Yehova anatumia leo.

Uwe na Wivu kwa Ajili ya Yehova

Hata hivyo, wivu wa kimungu unafaa katika ibada ya kweli. Tunapoanza kuhangaikia mno sifa au haki zetu, wivu wa kimungu hutufanya tumfikirie Yehova. Hutuchochea tutafute njia za kutangaza ukweli kumhusu, tutetee njia zake na watu wake.

Akiko, mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, alizomewa vikali na mwenye-nyumba ambaye hakujua ukweli juu ya sheria ya Mungu kuhusu damu. Kwa busara, Akiko alilitetea Neno la Mungu, hata alitaja matatizo ya kitiba yanayosababishwa na kutiwa damu mishipani. Akiwa na hamu kubwa ya kusema kuhusu Yehova, Akiko aliyabadili mazungumzo hayo akitilia maanani sababu iliyomfanya mwanamke huyo ampinge—kutoamini kwamba kuna Muumba. Akiko alimwonyesha mwenye-nyumba huyo jinsi uumbaji unavyothibitisha kwamba kuna Muumba. Ushahidi wake wa ujasiri uling’oa chuki isiyo na msingi ya mwanamke huyo naye akakubali kujifunza Biblia pamoja na Akiko. Sasa mwanamke huyo aliyekuwa na hasira hapo awali anamwabudu Yehova.

Wivu unaofaa, au bidii kwa ajili ya ibada ya kweli hutuchochea kuwa macho na kutumia fursa yoyote kuhubiri juu ya imani yetu na kuitetea kazini, shuleni, madukani, na tunaposafiri. Kwa mfano, Midori ameazimia kuwahubiria wafanyakazi wenzake kuhusu imani yake. Mfanyakazi mmoja mwenye umri wa miaka 40 hivi alisema kwamba hapendezwi kamwe na Mashahidi wa Yehova. Baadaye, walipokuwa wakizungumza pindi moja, mwanamke huyo alilalamika kwamba binti yake alikuwa ameanza kuharibika. Midori alimwonyesha kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, * na alijitolea kujifunza na bintiye kitabu hicho. Funzo lilianzishwa, lakini mama yake hakuhudhuria funzo hilo. Midori aliamua kumwonyesha mwanamke huyo video Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name.* Hilo liliondoa maoni yake mengi yasiyofaa. Video hiyo ilimchochea kusema hivi: “Nataka kuwa kama Mashahidi wa Yehova.” Alijiunga na bintiye kujifunza Biblia.

Wivu unaofaa una manufaa kwa kutaniko la Kikristo. Huchangia roho ya upendo na shauku na hutuchochea kukataa katakata mambo ambayo yanaweza kuwaumiza ndugu zetu wa kiroho, kama vile porojo zenye kudhuru na uasi-imani. Wivu wa kimungu hutufanya tuunge mkono maamuzi ya wazee, ambao nyakati nyingine hulazimika kuwakaripia watenda-dhambi. (1 Wakorintho 5:11-13; 1 Timotheo 5:20) Paulo alieleza hivi kuhusu wivu aliokuwa nao kuelekea waamini wenzake wa kutaniko la Korintho: “Nina wivu juu yenu nikiwa na wivu wa kimungu, kwa maana mimi binafsi niliwaposea nyinyi mume mmoja ili nipate kuwatoa nyinyi mkiwa bikira safi kiadili kwa Kristo.” (2 Wakorintho 11:2) Vivyo hivyo, wivu wetu hutuchochea kufanya yote tuwezayo kulinda usafi wa kiroho, wa kiadili na wa mafundisho kutanikoni.

Naam, wivu unaofaa, yaani, wivu wa kimungu huwajenga wengine. Huleta kibali cha Yehova na ni moja ya sifa ambazo Wakristo wanadhihirisha leo.—Yohana 2:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Finehasi alichochewa na wivu wa kimungu kutenda

[Picha katika ukurasa wa 30]

Epuka hatari ya wivu usiofaa

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wivu wa kimungu hutuchochea kuwahubiria wengine kuhusu imani yetu na kuwathamini ndugu zetu