Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, kununua jengo la dini nyingine na kulirekebisha kuwa Jumba la Ufalme ni kuchanganya imani?

Kwa kawaida, Mashahidi wa Yehova huepuka kununua majengo ya dini nyingine. Hata hivyo, ununuzi kama huo si kuchanganya imani. Huenda ununuzi huo ukaonekana kuwa jambo linalofanywa mara moja tu na basi. Hiyo haimaanishi kwamba kutaniko la Mashahidi wa Yehova linashirikiana na dini nyingine kujenga nyumba ya ibada watakayotumia kwa pamoja.

Ni tendo gani ambalo Yehova huliona kuwa kuchanganya imani? Ona agizo ambalo mtume Paulo alitoa: “Msiwe wenye kufungwa nira isiyosawazika pamoja na wasio waamini. Kwa maana uadilifu na uasi-sheria vina ushirika gani? Au nuru ina ushiriki gani na giza? Na zaidi, kuna upatano gani kati ya Kristo na Beliali? Au mtu mwaminifu ana fungu gani na asiye mwamini? Na hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu? . . . ‘Kwa hiyo tokeni miongoni mwao, na jitengeni wenyewe,’ asema Yehova, ‘na komeni kugusa kitu kisicho safi’; ‘na hakika mimi nitawakaribisha ndani.’” (2 Wakorintho 6:14-17) Paulo alimaanisha nini kwa kutumia neno “ushirika” na “ushiriki”?

Ushirika unaotajwa na Paulo bila shaka unahusu ibada na shughuli za kiroho pamoja na waabudu-sanamu na wasioamini. Aliwaonya Wakorintho ‘wasishiriki meza ya roho waovu.’ (1 Wakorintho 10:20, 21) Kwa hiyo, kuchanganya imani ni kushiriki ibada pamoja au kushiriki mambo ya kiroho na dini nyingine. (Kutoka 20:5; 23:13; 34:12) Jengo lililokuwa likitumiwa na dini nyingine linaponunuliwa, kusudi hasa ni kupata jengo litakalotumiwa kama Jumba la Ufalme. Kabla halijaanza kutumiwa kama Jumba la Ufalme, kitu chochote kinachohusiana na ibada isiyo ya kweli huondolewa. Baada ya marekebisho hayo kufanywa, linawekwa wakfu kwa Yehova kwa kusudi la kumwabudu. Hakuna ushirika kati ya ibada ya kweli na ibada isiyo ya kweli.

Mazungumzo kuhusu ununuzi wa jengo hilo, yapaswa kufanywa mara chache iwezekanavyo na yahusu tu shughuli ya ununuzi. Washiriki wa kutaniko la Kikristo wanapaswa kuzingatia onyo la Paulo kuhusu ‘kutofungwa nira isiyosawazika pamoja na wasio waamini.’ Ijapokuwa hatujioni kuwa bora kuliko watu wa dini nyingine, tunaepuka kushirikiana nao au kushawishiwa kujiunga na ibada yao. *

Maandiko yanaonyesha nini kuhusu kukodi jengo la dini nyingine? Kwa kawaida, kukodi jengo kama hilo kunamaanisha kufanya mapatano ya kibiashara kwa ukawaida na watu wa dini nyingine, jambo linalopaswa kuepukwa. Kabla baraza la wazee halijakodi jengo kama hilo hata kama litatumiwa mara moja tu, linapaswa kufikiria mambo yafuatayo: Je, kutakuwa na sanamu zozote na mifano ya kidini ndani au nje ya jengo hilo? Watu watakuwa na maoni gani wanapoona tukitumia jengo hilo? Je, yeyote kutanikoni atakwazwa kwa kuona tukitumia jengo hilo? (Mathayo 18:6; 1 Wakorintho 8:7-13) Wazee wanapaswa kuchanganua mambo hayo na kufikia uamuzi unaofaa. Wanapaswa kufikiria dhamiri yao na ile ya kutaniko kwa ujumla wanapoamua iwapo watanunua jengo fulani na kulirekebisha kuwa Jumba la Ufalme.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona Mnara wa Mlinzi, Aprili 15, 1999, ukurasa wa 28 na 29, kwa habari inayohusu jinsi ya kufanya biashara kwa njia inayofaa na matengenezo yasiyokubaliwa na Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Jengo hili, ambalo lilikuwa sinagogi, lilinunuliwa na kurekebishwa kuwa Jumba la Ufalme