Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mpingeni Ibilisi”

“Mpingeni Ibilisi”

“Mpingeni Ibilisi”

“Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia.”—YAKOBO 4:7.

1. Ni nini kinachoweza kusemwa kuhusu ulimwengu wa sasa, na kwa nini watiwa-mafuta na waandamani wao wanahitaji kuwa waangalifu?

“MUNGU ametoweka, lakini Ibilisi bado yupo.” Maneno hayo ya mwandikaji Mfaransa André Malraux yanaweza kutumiwa kufafanua hali ya ulimwengu tunamoishi. Yaonekana matendo ya wanadamu yanadhihirisha zaidi hila za Ibilisi kuliko mapenzi ya Mungu. Shetani anapotosha watu kwa “kila kazi yenye nguvu na ishara za uwongo na mambo ya ajabu na pamoja na kila udanganyo usio wa uadilifu kwa wale wanaoangamia.” (2 Wathesalonike 2:9, 10) Hata hivyo, katika ‘siku hizi za mwisho,’ Shetani anajitahidi zaidi kupotosha watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, akifanya vita dhidi ya Wakristo watiwa-mafuta “washikao amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kuhusu Yesu.” (2 Timotheo 3:1; Ufunuo 12:9, 17) Watumishi hao watiwa-mafuta wa Mungu pamoja na waandamani wao walio na tumaini la kuishi duniani, wanahitaji kuwa waangalifu.

2. Shetani alimshawishije Hawa, naye mtume Paulo aliogopa nini?

2 Shetani ni mdanganyifu sana. Kwa kutumia nyoka ili asitambulike, Shetani alimdanganya Hawa afikiri kwamba angepata furaha zaidi kwa kutenda bila kumtegemea Mungu. (Mwanzo 3:1-6) Miaka elfu nne baadaye, mtume Paulo aliogopa kwamba Wakristo wa Korintho wangenaswa na Shetani kupitia ujanja wake. Paulo aliandika: “Naogopa kwamba kwa njia fulani, kama nyoka alivyomshawishi Hawa kwa ujanja wake, huenda akili zenu zikafisidiwa kutoka kwenye weupe wa moyo na usafi wa kiadili ambao wamstahili Kristo.” (2 Wakorintho 11:3) Shetani hupotosha akili za watu. Kama vile alivyomshawishi Hawa, anaweza kufanya Wakristo wasababu kwa njia isiyo ya kweli, wakifikiri kwamba furaha yao inategemea jambo fulani ambalo Yehova na Mwana wake wanakataa.

3. Yehova huandaa ulinzi gani dhidi ya Ibilisi?

3 Shetani anaweza kulinganishwa na mnasa-ndege ambaye hutumia mitego kuwanasa ndege wasioitambua. Ili kuepuka mitego ya Shetani, tunahitaji ‘kuketi mahali pa siri pake aliye Juu,’ yaani, mahali pa mfano tunapoweza kupata ulinzi ambao Yehova hutoa kwa wale ambao katika matendo yao hutambua haki yake ya kutawala ulimwengu wote. (Zaburi 91:1-3) Tunahitaji ulinzi wote ambao Mungu huandaa kupitia Neno lake, roho yake, na tengenezo lake ili ‘tuweze kusimama imara dhidi ya mbinu za Ibilisi.’ (Waefeso 6:11) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mbinu” linaweza pia kutafsiriwa “njia za ujanja.” Bila shaka, Ibilisi hutumia njia nyingi za ujanja ili kuwanasa watumishi wa Yehova.

Mitego Aliyotega Shetani Kuwanasa Wakristo wa Mapema

4. Wakristo wa mapema waliishi katika hali ya aina gani?

4 Wakristo wa karne ya kwanza na ya pili W.K. waliishi wakati ambapo Milki ya Roma ilikuwa kwenye upeo wa usitawi wake. Ile Pax Romana (Amani ya Roma) iliwezesha biashara kusitawi. Ufanisi huo uliwaletea watawala starehe nyingi, nao walihakikisha kwamba watu wa kawaida walipata vitumbuizo vingi ili wasiasi. Nyakati fulani, idadi ya siku za mapumziko ilikuwa sawa na siku za kufanya kazi. Viongozi walitumia pesa za umma kuwaandalia watu chakula na vitumbuizo ili wakengeushe akili zao.

5, 6. (a) Kwa nini haikufaa kwa Wakristo kwenda kwenye kumbi na nyanja za maonyesho za Waroma? (b) Shetani alitumia mbinu gani, nao Wakristo wangeweza kuiepukaje?

5 Je, hali hiyo ilihatarisha maisha ya Wakristo wa mapema? Kwa kuzingatia maonyo yaliyoandikwa na waandishi kama Tertullian, ambao waliishi muda mfupi baada ya wakati wa mitume, tunaona kwamba mambo yaliyofanywa wakati wa mapumziko yalikuwa hatari sana kiroho na kiadili kwa Wakristo wa kweli. Kwanza, sherehe na michezo mingi ya umma ilifanywa ili kutukuza miungu ya kipagani. (2 Wakorintho 6:14-18) Kwenye kumbi za maonyesho, hata michezo ya kawaida ya kuigiza ilikuwa na ukosefu mkubwa wa maadili au yenye jeuri na umwagaji damu. Baada ya muda, watu walichoshwa na michezo hiyo ya kuigiza, na badala yake wakataka kuona maonyesho machafu ambapo waigizaji walicheza dansi kwa njia iliyoamsha tamaa ya ngono. Katika kitabu chake Daily Life in Ancient Rome, mwanahistoria Jérôme Carcopino anasema: ‘Katika maonyesho hayo, waigizaji wanawake waliruhusiwa kuvua nguo zote. Damu ilimwagwa kwa wingi. Waigizaji hao walionyesha mambo machafu sana ya kingono ambayo watu wengi wa jiji hilo walikuwa wakifanya. Hawakuchukizwa nayo kwa kuwa hisia zao zilikuwa zimefanywa sugu na kupotoshwa na mauaji ya kinyama waliyokuwa wametazama kwa muda mrefu kwenye nyanja za maonyesho.’—Mathayo 5:27, 28.

6 Katika nyanja hizo, wapiganaji walipigana hadi kufa, au wakapigana na wanyama-mwitu na kuwaua au kuuliwa nao. Wahalifu waliohukumiwa walitupiwa wanyama wakali. Hatimaye Wakristo pia walitupiwa wanyama hao. Hata nyakati hizo za mapema, mbinu ya Shetani ilikuwa kufanya hisia za watu ziwe sugu wasiweze kuchukizwa na jeuri na mambo yasiyo ya kiadili. Kwa sababu hiyo, hayo yakawa mambo ya kawaida yaliyopendwa sana na watu. Njia pekee ya kuepuka mtego huo ilikuwa kutokwenda kwenye kumbi na nyanja hizo za maonyesho.—1 Wakorintho 15:32, 33.

7, 8. (a) Kwa nini halingekuwa jambo la hekima kwa Mkristo kwenda kwenye mashindano ya magari ya kukokotwa? (b) Shetani angeweza kutumiaje mabafu ya Waroma kuwanasa Wakristo?

7 Mashindano ya magari ya kukokotwa yaliyofanywa kwenye nyanja za sarakasi zenye umbo la mstatili yalikuwa yenye kusisimua kwelikweli, lakini Wakristo hawangeenda kwenye mashindano hayo kwa sababu mara nyingi mashabiki walikuwa wenye jeuri. Mwandikaji mmoja wa karne ya tatu aliripoti kwamba baadhi ya watazamaji walipigana, naye Carcopino anasema kwamba “makahaba na watabiri wanaotumia nyota walifanya biashara yao” kwenye vijia vya nyanja hizo za sarakasi. Ni wazi kwamba Wakristo hawangeenda kwenye mashindano hayo ya Waroma.—1 Wakorintho 6:9, 10.

8 Namna gani mabafu ya Waroma yaliyokuwa maarufu? Bila shaka, si vibaya kuoga ili kuwa safi. Lakini mabafu mengi ya Waroma yalikuwa majengo makubwa sana yaliyokuwa na vyumba vya kukandia watu, kufanyia mazoezi, kuchezea kamari, kulia chakula na kunywea. Ingawa ilisemekana kwamba kulikuwa na wakati uliotengewa wanaume au wanawake kutumia mabafu hayo, mara nyingi wanaume na wanawake waliruhusiwa kuoga pamoja. Clement wa Aleksandria aliandika: “Mabafu yamefunguliwa kwa wanaume na wanawake; nao huvua nguo zote ili kufanya mambo ya uasherati.” Hivyo, majengo kama hayo yanayofaa yangeweza kutumiwa na Shetani kwa urahisi kuwanasa Wakristo. Watu wenye hekima hawakwenda kwenye mabafu hayo.

9. Wakristo wa mapema walilazimika kuepuka mitego gani?

9 Milki ya Roma ilipokuwa kwenye upeo wa usitawi wake, watu wengi walipenda kucheza kamari wakati wa mapumziko. Wakristo wa mapema wangeweza kuepuka kucheza kamari wakati wa mashindano ya magari ya kukokotwa kwa kutokwenda kwenye nyanja ambapo mashindano hayo yalifanywa. Uchezaji kamari wa kiwango kidogo pia ulifanywa kinyume cha sheria katika vyumba vya nyuma vya mikahawa na baa. Watu wangecheza kamari kwa kukisia kama idadi ya mawe au mifupa ambayo mtu alishika mkononi ingeweza kugawanywa kwa mbili au la. Kucheza kamari kulifanya maisha yawe yenye kusisimua zaidi, kwa kuwa watu walitumaini kupata pesa bila jitihada nyingi. (Waefeso 5:5) Zaidi ya hayo, mara nyingi wanawake waliohudumu kwenye baa hizo walikuwa makahaba, hivyo kulikuwa na hatari ya kufanya uasherati. Hiyo ni baadhi ya mitego ambayo Shetani alitumia kuwanasa Wakristo walioishi katika majiji ya Milki ya Roma. Je, hali ni tofauti leo?

Mitego ya Shetani Leo

10. Hali ya leo inafananaje na hali zilizoenea katika Milki ya Waroma?

10 Kwa ujumla mbinu za Shetani hazijabadilika katika miaka mingi iliyopita. Paulo aliwashauri vikali Wakristo walioishi katika mji uliopotoka wa Korintho ili ‘wasipate kushindwa na Shetani.’ Alisema: ‘Sisi si wasio na ujuzi kuhusu mbinu za Shetani.’ (2 Wakorintho 2:11) Katika nchi nyingi zilizoendelea, hali leo ni kama ilivyokuwa wakati Milki ya Roma ilipokuwa kwenye upeo wa usitawi wake. Sasa watu wengi wana wakati mwingi zaidi wa kupumzika. Michezo ya bahati nasibu ya serikali huwapa matumaini kidogo hata walio maskini. Kuna vitumbuizo vya malipo ya chini vya kushika akili za watu. Nyanja za michezo hujaa watu, wengine hucheza kamari, na nyakati nyingine mashabiki na hata wachezaji huwa wenye jeuri. Muziki wenye kushusha heshima ni mwingi, nayo michezo ya kuigiza, sinema na vipindi vya televisheni huonyesha mambo machafu. Katika nchi fulani wanawake na wanaume hupenda kuoga pamoja kwenye mabafu ya mvuke au chemchemi za maji moto. Wengine hata huoga wakiwa uchi kwenye fuo fulani za bahari. Kama ilivyokuwa katika karne za mapema za Ukristo, Shetani hujaribu kushawishi watumishi wa Mungu kwa kutumia mambo ambayo hufanywa na watu wa ulimwengu wakati wa mapumziko.

11. Tunakabiliwa na mitego gani tunapotafuta mahali pa kupumzikia?

11 Katika ulimwengu ambamo kuna mkazo mwingi, ni jambo la kawaida kuhisi unahitaji wakati wa kupumzika. Hata hivyo, kama vile mabafu ya Waroma yalivyohusisha mambo ambayo yangeweza kuwa hatari kwa Wakristo wa mapema, Shetani ametumia sehemu fulani ambako watu huenda kupumzika kama mtego wa kuwaingiza Wakristo wa siku hizi katika uasherati au ulevi. Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa Korintho: “Msiongozwe vibaya. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa. Amkeni mwe na utimamu wa akili katika njia ya uadilifu na msizoee dhambi, kwa maana wengine hawana ujuzi juu ya Mungu.”—1 Wakorintho 15:33, 34.

12. Shetani hutumia mbinu gani kunasa watumishi wa Yehova leo?

12 Tumeona jinsi Shetani alivyotumia ujanja kupotoa mawazo ya Hawa. (2 Wakorintho 11:3) Leo, mojawapo ya mitego ambayo Ibilisi hutumia ni kuwafanya Wakristo wafikiri kwamba wanaweza kuwavuta watu wengine kwenye kweli ya Kikristo iwapo watajaribu kuiga njia za ulimwengu kadiri wawezavyo, wakitaka kuonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova si tofauti na watu wengine. Nyakati nyingine wao hupita mipaka, na hali inakuwa kinyume cha walivyotarajia. (Hagai 2:12-14) Mbinu nyingine ambayo Shetani hutumia ni kuwachochea Wakristo waliojiweka wakfu, vijana na watu wazima waishi maisha maradufu na ‘kuitia kihoro roho takatifu ya Mungu.’ (Waefeso 4:30) Wengine wamenaswa na mtego huo kwa kutumia isivyofaa mtandao wa Internet.

13. Ni mtego gani ambao hauonekani kana kwamba unadhuru ambao Ibilisi hutumia kwa ujanja, na ni shauri gani la Mithali linalofaa kuhusiana na mtego huo?

13 Mtego mwingine ambao Shetani hutumia ni uchawi ambao hauonekani kana kwamba unadhuru. Hakuna Mkristo wa kweli anayeweza kujiingiza kimakusudi katika ibada ya Shetani au uwasiliani-roho. Hata hivyo, kwa kutojua wengine wamekosa kuwa waangalifu kuhusu sinema, vipindi vya televisheni, michezo ya video, na hata vitabu vya watoto vinavyotia ndani vitabu vya katuni ambavyo hukazia jeuri na uchawi. Chochote kinachohusiana na mambo ya uchawi kinahitaji kuepukwa kabisa. Mithali yenye hekima inasema: “Miiba na mitego huwa katika njia ya mshupavu; yeye aitunzaye nafsi yake atakuwa mbali nayo.” (Mithali 22:5) Kwa kuwa Shetani ni “mungu wa huu mfumo wa mambo,” anaweza kutumia jambo lolote linalopendwa na wengi kama mtego.—2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 2:15, 16.

Yesu Alimpinga Ibilisi

14. Yesu alipingaje kishawishi cha kwanza cha Ibilisi?

14 Yesu aliweka mfano mzuri wa kumpinga Ibilisi na kufanya atoroke. Baada ya Yesu kubatizwa na kufunga kwa siku 40, Shetani alimshawishi. (Mathayo 4:1-11) Katika kishawishi cha kwanza Shetani alijaribu kutumia njaa iliyompata Yesu baada ya kufunga. Shetani alitaka Yesu afanye muujiza wake wa kwanza ili atosheleze uhitaji wa kimwili. Akinukuu Kumbukumbu la Torati 8:3, Yesu alikataa kutumia nguvu zake kwa ubinafsi, akionyesha kwamba chakula cha kiroho kilikuwa muhimu kuliko chakula cha kimwili.

15. (a) Shetani alitumia tamaa gani ya kiasili kumshawishi Yesu? (b) Ibilisi anatumia sana njia ipi ya ujanja dhidi ya watumishi wa Mungu leo, lakini tunaweza kumpingaje?

15 Jambo fulani lenye kuvuta fikira kuhusiana na kishawishi hicho ni kwamba Ibilisi hakutaka Yesu afanye dhambi ya uasherati. Yaonekana njaa, ambayo kiasili husababisha hamu ya kula, ndiyo tamaa ya kimwili yenye nguvu ambayo Shetani angeweza kutumia wakati huo kumshawishi Yesu. Shetani hutumia vishawishi vipi kuwanasa watu wa Mungu leo? Yeye hutumia vishawishi vingi tofauti-tofauti, lakini vishawishi vya kufanya ngono ni mojawapo ya njia za ujanja anazotumia sana ili kuvunja uaminifu-maadili wa watu wa Yehova. Kwa kumwiga Yesu, tunaweza kumpinga Ibilisi na kukataa vishawishi vyake. Kama vile Yesu alivyoshinda vishawishi vya Shetani kwa kukumbuka maandiko yafaayo, sisi pia tunaweza kukumbuka maandiko kama Mwanzo 39:9 na 1 Wakorintho 6:18 tunaposhawishiwa na Shetani.

16. (a) Shetani alimshawishije Yesu kwa mara ya pili? (b) Ni katika njia zipi huenda Shetani akajaribu kutushawishi tumjaribu Yehova?

16 Halafu, Ibilisi akataka Yesu aruke kutoka kwenye ukuta wa hekalu ili aone kama Mungu anaweza kumlinda kupitia malaika Wake. Akinukuu andiko la Kumbukumbu la Torati 6:16, Yesu alikataa kumjaribu Baba yake. Huenda Shetani asitushawishi turuke kutoka kwenye ukuta wa hekalu, lakini anaweza kutushawishi tumjaribu Yehova. Je, tunashawishiwa kuona ni kwa kadiri gani tunavyoweza kuiga mapambo na mitindo ya mavazi ya kilimwengu bila kushauriwa? Je, tunashawishiwa kuhusiana na vitumbuizo visivyofaa? Huenda tukawa tunamjaribu Yehova. Ikiwa tuna maelekeo kama hayo, huenda Shetani akaendelea kukaa karibu nasi badala ya kutoroka, akijaribu daima kutunasa tujiunge naye katika kumpinga Mungu.

17. (a) Ibilisi alimshawishije Yesu kwa mara ya tatu? (b) Andiko la Yakobo 4:7 linaweza kutimizwaje kwetu?

17 Shetani alipomtolea Yesu falme zote za ulimwengu ili afanye tendo moja tu la ibada, Yesu alimpinga kwa mara nyingine kwa kunukuu Maandiko, akionyesha msimamo wake imara wa kumwabudu Baba yake pekee. (Kumbukumbu la Torati 5:9; 6:13; 10:20) Huenda Shetani asitutolee falme za ulimwengu, lakini yeye hutushawishi daima kwa vitu vya kimwili vinavyoonekana kuwa vyenye kuvutia, na hata kufanya tuwe na ndoto za kuwa matajiri wakubwa. Je, sisi hutenda kama Yesu alivyotenda na kumwabudu Yehova pekee? Ikiwa ndivyo, tutapatwa na yaliyompata. Masimulizi ya Mathayo yanasema: “Ndipo Ibilisi akamwacha.” (Mathayo 4:11) Shetani atatuacha tukimpinga kwa kukumbuka kanuni za Biblia zifaazo na kuzitumia. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia.” (Yakobo 4:7) Mkristo mmoja aliandikia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Ufaransa hivi: “Shetani ni mjanja kwelikweli. Licha ya nia yangu nzuri, ninaona ni vigumu sana kudhibiti hisia na tamaa zangu. Hata hivyo, kwa ujasiri, subira, na zaidi ya yote, msaada wa Yehova, nimeweza kudumisha uaminifu-maadili, na kushikamana na kweli kabisa.”

Tumeandaliwa Vifaa Kikamili Kumpinga Ibilisi

18. Ni silaha gani za kiroho zinazotuandaa kumpinga Ibilisi?

18 Yehova ametuandalia suti kamili ya silaha za kiroho ili tuweze “kusimama imara dhidi ya mbinu za Ibilisi.” (Waefeso 6:11-18) Upendo wetu kwa ile kweli utafunga viuno vyetu, au utatutayarisha, kwa ajili ya kazi ya Kikristo. Azimio letu la kushika viwango vya Yehova vya uadilifu litakuwa kama bamba la kifuani linalolinda moyo wetu. Ikiwa miguu yetu imevishwa kama viatu vifaa vya habari njema, tutashiriki kwa ukawaida kazi ya kuhubiri, na kufanya hivyo kutatuimarisha na kutulinda kiroho. Imani yetu yenye nguvu itakuwa kama ngao kubwa inayotulinda dhidi ya “vishale vyote vinavyowaka moto vya yule mwovu,” yaani, mashambulizi na vishawishi vyake vya ujanja. Tumaini letu hakika kwamba ahadi za Yehova zitatimizwa litakuwa kama kofia ya chuma inayolinda uwezo wetu wa kufikiri na kutupatia amani ya akili. (Wafilipi 4:7) Iwapo tutakuwa stadi katika kutumia Neno la Mungu, litakuwa kama upanga tunaoweza kutumia kuwasaidia watu watoke katika utumwa wa kiroho wa Shetani. Tunaweza pia kuutumia kujikinga, kama vile Yesu alivyoutumia alipokabili kishawishi.

19. Mbali na ‘kumpinga Ibilisi,’ inatupasa kufanya nini pia?

19 Kwa kuendelea kuvaa “suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu” na kuendelea kusali bila kukoma, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatulinda Shetani anapotushambulia. (Yohana 17:15; 1 Wakorintho 10:13) Lakini Yakobo alionyesha kwamba mbali na ‘kumpinga Ibilisi,’ inatupasa pia ‘tujitiishe kwa Mungu’ anayetujali. (Yakobo 4:7, 8) Katika makala inayofuata tutaona jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.

Ungejibuje?

• Wakristo wa mapema walilazimika kuepuka mitego gani ya Shetani?

• Ni njia zipi za ujanja ambazo Shetani hutumia leo kuwanasa watumishi wa Yehova?

• Yesu alipingaje vishawishi vya Ibilisi?

• Ni suti gani ya kiroho ambayo hutuwezesha kumpinga Ibilisi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Yesu alimpinga Ibilisi kabisa

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wakristo wa karne ya kwanza walikataa vitumbuizo vyenye jeuri na ukosefu wa maadili

[Hisani]

The Complete Encyclopedia of Illustration/J. G. Heck