Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tukio Lenye Kufurahisha Katika Nchi za Balkan

Tukio Lenye Kufurahisha Katika Nchi za Balkan

Tukio Lenye Kufurahisha Katika Nchi za Balkan

Mnamo mwaka wa 1922, Wanafunzi wa Biblia Wenye Bidii, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, walifanya mkutano huko Innsbruck, Austria. Kijana mmoja aliyeitwa Franz Brand, kutoka mji wa Apatin, Vojvodina, huko Serbia, alikuwa miongoni mwa watu waliohudhuria mkutano huo. Mara tu msemaji alipotaja jina la Mungu, Yehova, kikundi fulani cha watu kilianza kumzomea, akashindwa kuendelea, hivyo mkutano huo ukavunjwa. Lakini Franz aliguswa moyo sana na habari hiyo, akaanza kuhubiri habari njema za Ufalme. Huo ulikuwa mwanzo mdogo wa ukuzi wa kiroho wenye kusisimua katika mojawapo ya nchi za Balkan.

WATU wengi leo wanaposikia jina Yugoslavia wanakumbuka mauaji mabaya sana ya vita yaliyotukia huko. Jina hilo huwakumbusha visa vyenye kuhuzunisha sana vya watu wengi waliouawa kikatili, wakimbizi wanaoteseka, nyumba zilizoharibiwa, na mayatima wanaotaabika. Vita vilivyokumba eneo la Balkan kuanzia mwaka wa 1991 hadi 1995 vilisababisha maumivu na mateso makali sana yasiyoelezeka. Vita hivyo vilididimiza kabisa jitihada za wanadamu za kuleta wakati ujao wenye furaha na ufanisi. Vita hivyo viliwaletea wakazi wa iliyokuwa Yugoslavia magumu ya kiuchumi na umaskini mkubwa. *

Ni vigumu kutarajia kupata watu wenye furaha katika nchi hiyo kwa sababu ya matatizo yanayokumba eneo hilo. Hata hivyo, amini usiamini kuna watu wenye furaha nchini humo. Mwishoni mwa karne ya 20, watu hao walikuwa na furaha ya pekee. Franz Brand, kijana aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, alichangiaje furaha hiyo?

Ukuzi wa Kiroho Katika Nchi za Balkan

Franz Brand alisisimuliwa sana na kweli mpya alizosikia, akaazimia kueneza habari njema. Aliajiriwa kazi ya kinyozi katika mji wa Maribor, nchini Slovenia karibu na mpaka wa Austria. Alianza kuwahubiria wateja wake ambao kwa kawaida waliketi kwa utulivu na kumsikiliza huku wakinyolewa. Kwa sababu ya jitihada zake, kikundi kidogo cha wahubiri wa Ufalme kilianzishwa katika mji wa Maribor mwishoni mwa miaka ya 1920. Hotuba zinazotegemea Biblia zilitolewa katika mkahawa mmoja ambao uliitwa jina lifaalo, Mkahawa wa Novi svet (Ulimwengu Mpya) Unaopika Chakula Kinachotoka Baharini.

Baada ya muda, habari njema zilihubiriwa katika nchi yote. Kutumiwa kwa “Photo-Drama of Creation” (onyesho la saa nane la filamu, slaidi, na rekodi) kulisaidia sana ukuzi huo. Mapainia Wajerumani waliotorokea Yugoslavia wakati Mashahidi wa Yehova walipokuwa wakiteswa vikali nchini Ujerumani katika miaka ya 1930, waliwatia nguvu Mashahidi nchini Yugoslavia. Walijitoa kabisa kuhubiri maeneo yaliyo mbali sana katika nchi hiyo yenye milima-milima bila kujali mapendezi yao ya kibinafsi. Mwanzoni, watu wengi hawakukubali ujumbe wao. Mapema miaka ya 1940, ni wahubiri 150 tu waliotoa ripoti ya utumishi wa shambani.

Walinyanyaswa vikali sana kuanzia mwaka wa 1941 hadi 1952. Hatimaye kulikuwa na furaha kubwa sana mnamo Septemba 9, 1953, wakati serikali ya Kikomunisti ya Jenerali Tito ilipowaandikisha kisheria Mashahidi wa Yehova. Mwaka huo, wahubiri wa habari njema walikuwa 914 na waliongezeka kwa haraka. Kufikia mwaka wa 1991, idadi ya wahubiri ilikuwa imeongezeka hadi 7,420, na watu 16,072 walihudhuria Ukumbusho mwaka huo.

Kusanyiko la kwanza la kimataifa la Mashahidi wa Yehova lilifanywa nchini humo kuanzia Agosti 16 hadi 18, mwaka wa 1991, huko Zagreb, Kroatia. Wajumbe 14,684 walihudhuria kusanyiko hilo kutoka nchini na sehemu nyinginezo ulimwenguni. Kusanyiko hilo lisilosahaulika liliwatayarisha watu wa Yehova kwa ajili ya majaribu ambayo wangekabili baadaye. Mabasi yaliyokuwa yakiwarudisha wajumbe Waserbia nyumbani baada ya kusanyiko yalikuwa miongoni mwa magari ya mwisho kuvuka mpaka kati ya Kroatia na Serbia. Baada ya basi la mwisho kuvuka, mpaka ulifungwa na vita vikaanza.

Watu wa Yehova Wana Sababu za Kufurahi

Mashahidi wa Yehova katika nchi za Balkan walipata majaribu makali sana wakati wa vita. Hata hivyo, wana furaha kwa sababu Yehova amewabariki watu wake kwa ongezeko kubwa sana. Tangu mwaka wa 1991, idadi ya wahubiri wa Ufalme katika ile iliyokuwa nchi ya Yugoslavia imeongezeka kwa zaidi ya asilimia 80. Wahubiri walifikia kilele cha 13,472 katika mwaka wa utumishi wa 2001.

Ofisi za tawi huko Zagreb na Belgrade (Serbia) zilikuwa zikisimamia kazi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi zote za iliyokuwa nchi ya Yugoslavia. Kwa sababu ya ongezeko hilo na mabadiliko ya kisiasa, ofisi mpya zilihitajika katika Ljubljana (Slovenia), na Skopje (Masedonia), na kulikuwa pia na uhitaji wa kununua ofisi mpya huko Belgrade na Zagreb. Ofisi hizo zina wafanyakazi 140 hivi. Wengi wao ni vijana wenye bidii wanaompenda sana Yehova. Idadi kubwa wanatafsiri vichapo vya Biblia katika Kikroatia, Kimasedonia, Kiserbia, na Kislovenia. Ni jambo lenye kufurahisha sana kuona kwamba magazeti na vichapo vingi vya Mashahidi wa Yehova katika lugha hizo vinachapishwa sambamba na vichapo vya Kiingereza. Vichapo hivi huwasaidia watu wengi kupata faraja na tumaini.

Jambo jingine linalofurahisha ni jinsi watumishi wengi wa wakati wote kutoka nchi nyingine wanavyounga mkono kazi ya kuhubiri. Makutaniko yamekuwa na furaha zaidi kwa sababu Majumba mengi maridadi ya Ufalme yamejengwa katika miaka ya karibuni. Isitoshe, kulikuwa na jambo jingine lenye kufurahisha zaidi. Ni jambo gani hilo?

Mradi wa Pekee

Wahubiri wengi walijiuliza hivi mara nyingi, ‘Je, kweli tutapata Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha yetu?’ Mwaka baada ya mwaka, walitarajia kwa hamu kusikia tangazo hilo kwenye kusanyiko la wilaya. Lakini, kazi hiyo kubwa sana ingefanywaje, tukizingatia kwamba watafsiri wa lugha hizo walikuwa wapya na wachache tu?

Baada ya kuchanganua hali, Baraza Linaloongoza liliidhinisha mradi wa pamoja ambapo watafsiri wa vichapo vya Kimasedonia, Kikroatia, na Kiserbia wangeshirikiana kwa ukaribu na kusaidiana. Kazi hiyo ilisimamiwa na watafsiri wa Kroatia.

Siku ya Shangwe

Mashahidi wa Yehova katika nchi za Balkan hawatasahau kamwe Julai 23, 1999. Mfululizo wa Makusanyiko ya Wilaya ya “Neno la Mungu la Kiunabii” yangefanywa wakati uleule katika jiji la Belgrade, Sarajevo (Bosnia-Herzegovina), Skopje, na Zagreb. Kulikuwa na shaka iwapo kusanyiko lingefanyiwa Belgrade, kwani mikutano ya umma haikuruhusiwa kwa sababu ya mashambulizi ya mabomu ya wanajeshi wa shirika la kujihami la NATO. Akina ndugu walifurahi sana waliposikia kwamba wangeweza kukusanyika pamoja baada ya miezi mingi ya wasiwasi. Hata hivyo, yaliyotokea kwenye makusanyiko hayo yalikuwa makubwa kuliko walivyotarajia.

Siku ya Ijumaa alasiri, tangazo la pekee lilitolewa kwenye makusanyiko yote manne. Wajumbe 13,497 waliohudhuria walisikiliza tangazo hilo kwa hamu kubwa. Hatimaye msemaji alipotangaza kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ya lugha ya Kikroatia na Kiserbia na aliposema kwamba kazi ya kutafsiri tafsiri ya Kimasedonia ilikuwa ikiendelea vizuri, wajumbe hao walishindwa kujizuia. Walipiga makofi kwa kishindo sana hivi kwamba msemaji hakuweza kumaliza tangazo hilo. Kwenye kusanyiko la Sarajevo, wasikilizaji walinyamaa kimya huku wakiwa wamepigwa na bumbuazi. Halafu wakapiga makofi kwa muda mrefu. Wasikilizaji wengi huko Belgrade walitiririkwa na machozi ya furaha, na msemaji alikatizwa na makofi alipokuwa akitoa tangazo hilo. Kila mtu alifurahi sana.

Zawadi hiyo ilithaminiwa hata zaidi kwa sababu Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepata haki za kuchapisha tafsiri ya Biblia ya Kikroatia na vilevile ya Kiserbia. Kwa hiyo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha hizo mbili iliunganishwa na tafsiri ya Maandiko ya Kiebrania iliyokuwa imetafsiriwa katika lugha hizo. Zaidi ya hayo, Biblia ya Kiserbia ilichapishwa kwa herufi za Kirumi na Kisirili.

Watu wa Yehova katika nchi za Balkan wanashukuru sana kwa ajili ya zawadi zote nzuri na mwongozo wote waliopokea, wanathamini sana maneno haya ya Daudi: “Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, sitaogopa mabaya; kwa maana Wewe [Yehova] upo pamoja nami.” Licha ya magumu yote ambayo wangali wanakabili, wameazimia kufanya ‘furaha ya Yehova iwe nguvu yao.’—Zaburi 23:4; Nehemia 8:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Jamhuri ya Muungano ya Yugoslavia ina nchi sita—Bosnia-Herzegovina, Kroatia, Makedonia, Montenegro, Serbia, na Slovenia.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kikundi cha kwanza cha wahubiri kutoka Maribor, Slovenia, wakihubiri eneo la mbali