Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anakujali

Yehova Anakujali

Yehova Anakujali

‘Mtupieni [Mungu] hangaiko lenu lote, kwa sababu yeye huwajali nyinyi.’—1 PETRO 5:7.

1. Yehova na Shetani wanatofautiana kabisa katika jambo gani?

YEHOVA na Shetani wanatofautiana kabisa. Yeyote anayevutiwa na Yehova huchukizwa na Ibilisi. Tofauti hiyo inatajwa katika kitabu kimoja cha kitaalamu kinachokubalika. Kuhusu matendo ya Shetani kama yanavyotajwa katika kitabu cha Biblia cha Ayubu, kichapo Encyclopædia Britannica (1970) kinasema: ‘Kazi ya Shetani ni kuzunguka-zunguka duniani pote akitafuta matendo au watu wa kushtaki; hivyo kazi yake ni tofauti na kazi ya “macho ya Bwana,” ambayo huzunguka-zunguka duniani pote kutia nguvu matendo yote ya wema. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Shetani hudai kwa dharau kwamba wanadamu hutenda wema kwa sababu tu za ubinafsi, naye Mungu humruhusu awajaribu chini ya mamlaka na udhibiti Wake.’ Naam, hiyo ni tofauti iliyoje!—Ayubu 1:6-12; 2:1-7.

2, 3. (a) Neno “Ibilisi” linafafanuliwaje vizuri na yale yaliyompata Ayubu? (b) Biblia huonyeshaje kwamba Shetani anaendelea kuwashtaki watumishi wa Yehova duniani?

2 Neno “Ibilisi” linatokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “mshtaki asemaye uwongo,” “mchongezi.” Kitabu cha Ayubu kinafunua kwamba Shetani alimshtaki Ayubu, mtumishi mwaminifu wa Yehova, kwamba alimtumikia Mungu kwa sababu za ubinafsi. Alisema: “Je! huyo Ayubu yuamcha BWANA bure?” (Ayubu 1:9) Masimulizi ya kitabu cha Ayubu yanaonyesha kwamba licha ya majaribu yaliyompata, Ayubu alimkaribia Yehova zaidi. (Ayubu 10:9, 12; 12:9, 10; 19:25; 27:5; 28:28) Baada ya mateso yaliyompata, Ayubu alimwambia Mungu hivi: “Nilikuwa nimesikia habari zako, kwa kusikia kwa masikio; bali sasa jicho langu linakuona.”—Ayubu 42:5.

3 Je, Shetani ameacha kuwashtaki watumishi waaminifu wa Mungu tangu wakati wa Ayubu? La. Kitabu cha Ufunuo kinaonyesha kwamba wakati huu wa mwisho, Shetani anaendelea kuwashtaki ndugu za Kristo waliotiwa mafuta na bila shaka pia waandamani wao waaminifu. (2 Timotheo 3:12; Ufunuo 12:10, 17) Kwa hiyo, sisi sote Wakristo wa kweli tunahitaji kujitiisha chini ya Mungu wetu anayejali, Yehova, na kumtumikia kwa sababu tunampenda sana na hivyo kuthibitisha shtaka la Shetani kuwa la uwongo. Kwa kufanya hivyo, tutaufurahisha moyo wa Yehova.—Mithali 27:11.

Yehova Hutafuta Njia za Kutusaidia

4, 5. (a) Tofauti na Shetani, Yehova hutafuta nini duniani? (b) Tunahitaji kufanya nini ili kupata kibali cha Yehova?

4 Ibilisi huzunguka-zunguka duniani akitafuta mtu wa kushtaki au kunyafua. (Ayubu 1:7, 9; 1 Petro 5:8) Tofauti naye, Yehova hutafuta njia za kuwasaidia wale wanaohitaji nguvu zake. Nabii Hanani alimwambia hivi Mfalme Asa: “Kwa maana macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Kuna tofauti iliyoje kati ya jinsi Shetani anavyotuchunguza kwa chuki na jinsi Yehova anavyotujali kwa upendo!

5 Yehova hatuchunguzi kisiri, akiwa na nia mbaya ya kutupata na kosa. Mtunga-zaburi aliandika: “BWANA, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Jibu linalodokezwa ni: hakuna hata mmoja. (Mhubiri 7:20) Tukimkaribia Yehova kwa moyo wote, macho yake yatakuwa juu yetu, si atushutumu, bali aone jitihada zetu na kujibu sala zetu za kuomba msaada na msamaha. Mtume Petro aliandika: “Macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yaelekea dua zao; bali uso wa Yehova uko dhidi ya wale wanaofanya mambo mabaya.”—1 Petro 3:12.

6. Kisa cha Daudi kinatufariji na kutuonya jinsi gani?

6 Daudi hakuwa mkamilifu naye alifanya dhambi nzito. (2 Samweli 12:7-9) Lakini alimweleza Yehova yote yaliyokuwa moyoni mwake, akimkaribia kwa sala ya bidii. (Zaburi 51:1-12) Yehova alisikiliza sala yake na kumsamehe, ingawa Daudi alipatwa na matokeo mabaya ya dhambi yake. (2 Samweli 12:10-14) Jambo hilo linapaswa kutufariji na vilevile kutuonya. Tunafarijika kujua kwamba Yehova yu tayari kutusamehe dhambi tukitubu kikweli, lakini ni jambo linaloamsha fikira pia kujua kwamba mara nyingi dhambi huwa na matokeo mabaya sana. (Wagalatia 6:7-9) Ikiwa tunataka kumkaribia Yehova, tunapaswa kukaa mbali iwezekanavyo na chochote kisichompendeza.—Zaburi 97:10.

Yehova Huwavuta Watu Wake Kwake

7. Yehova hutazama watu wa aina gani, naye huwavutaje kwake?

7 Daudi aliandika hivi katika mojawapo ya zaburi zake: “Ingawa BWANA yuko juu, amwona mnyenyekevu, naye amjua mwenye kujivuna tokea mbali.” (Zaburi 138:6) Ikizungumzia jambo hilohilo, zaburi nyingine inasema: “Ni nani aliye mfano wa BWANA, Mungu wetu aketiye juu; anyenyekeaye kutazama, mbinguni na duniani? Humwinua mnyonge kutoka mavumbini.” (Zaburi 113:5-7) Naam, Muumba wa ulimwengu wote aliye mweza yote hunyenyekea kuitazama dunia, nayo macho yake humwona “mnyenyekevu,” “mnyonge,” watu ‘wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika.’ (Ezekieli 9:4) Yeye huvuta watu hao kwake kupitia Mwana wake. Alipokuwa duniani, Yesu alisema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye . . . Hakuna awezaye kuja kwangu isipokuwa aruhusiwe na Baba.”—Yohana 6:44, 65.

8, 9. (a) Kwa nini sote tunahitaji kumwendea Yesu? (b) Jambo la pekee sana kuhusu mpango wa fidia ni nini?

8 Wanadamu wote wanapaswa kumwendea Yesu na kuweka imani katika dhabihu ya fidia kwa sababu walizaliwa wakiwa watenda-dhambi, wametengwa na Mungu. (Yohana 3:36) Wanahitaji kupatanishwa na Mungu. (2 Wakorintho 5:20) Mungu hakungoja watenda-dhambi wamsihi afanye mpango fulani ili waweze kuwa na amani pamoja naye. Mtume Paulo aliandika: “Mungu apendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu. . . . Kwa maana, ikiwa tulipokuwa maadui, tulipata kuwa wenye kupatanishwa na Mungu kupitia kifo cha Mwana wake, ni zaidi sana sisi tutaokolewa kwa uhai wake, kwa kuwa sasa tumepata kuwa wenye kupatanishwa.”—Waroma 5:8, 10.

9 Mtume Yohana alithibitisha ukweli mtukufu kwamba Mungu anawapatanisha wanadamu kwake mwenyewe alipoandika: “Kwa hili upendo wa Mungu ulifanywa dhahiri katika kisa chetu, kwa sababu Mungu alituma Mwana wake mzaliwa-pekee kuingia katika ulimwengu ili tuweze kupata uhai kupitia kwake. Upendo uko hivi, si kwamba sisi tumempenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda akamtuma Mwana wake kuwa dhabihu yenye kufunika kwa ajili ya dhambi zetu.” (1 Yohana 4:9, 10) Mungu, wala si mwanadamu, ndiye aliyechukua hatua ya kwanza. Je, unavutiwa na Mungu aliyetuonyesha upendo mwingi hivyo ingawa sisi tulikuwa “watenda-dhambi” na “maadui” wake?—Yohana 3:16.

Tunahitaji Kumtafuta Yehova

10, 11. (a) Ni lazima tufanye nini tukitaka kumtafuta Yehova? (b) Tuuoneje ulimwengu wa Shetani?

10 Kama tujuavyo, Yehova hatulazimishi twende kwake. Ni lazima tumtafute, ‘tupapase-papase tukimtafuta na kwa kweli tumpate, ijapokuwa, kweli, yeye hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.’ (Matendo 17:27) Ni lazima tutambue kwamba Yehova ana haki ya kudai tujitiishe kwake. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Basi, jitiisheni wenyewe kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia. Safisheni mikono yenu, nyinyi watenda-dhambi, na takaseni mioyo yenu, nyinyi wenye kusitasita kuamua.” (Yakobo 4:7, 8) Tunapaswa kuchukua msimamo imara upande wa Yehova na kumpinga Ibilisi kabisa.

11 Kufanya hivyo kunamaanisha kujitenga kabisa na ulimwengu mwovu wa Shetani. Yakobo pia aliandika: “Je, hamjui kwamba urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu? Kwa hiyo, yeyote yule atakaye kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya mwenyewe kuwa adui ya Mungu.” (Yakobo 4:4) Kwa upande mwingine, iwapo tunataka kuwa marafiki wa Yehova, lazima tutazamie kuchukiwa na ulimwengu wa Shetani.—Yohana 15: 19; 1 Yohana 3:13.

12. (a) Daudi aliandika maneno gani yenye kufariji? (b) Yehova alitoa onyo gani kupitia nabii Azaria?

12 Ulimwengu wa Shetani unapotupinga kwa njia fulani hususa, tunahitaji hasa kumwendea Yehova katika sala, tukimwomba atusaidie. Daudi ambaye aliokolewa na Yehova mara nyingi aliandika maneno haya yenye kutufariji: “BWANA yu karibu na wote wamwitao, wote wamwitao kwa uaminifu. Atawafanyia wamchao matakwa yao, naye atasikia kilio chao na kuwaokoa. BWANA huwahifadhi wote wampendao, na wote wasio haki atawaangamiza.” (Zaburi 145:18-20) Zaburi hiyo inaonyesha kwamba Yehova anaweza kutuokoa tunapojaribiwa tukiwa mtu mmoja-mmoja na kwamba ataokoa watu wake kwa ujumla wakati wa “dhiki kuu.” (Ufunuo 7:14) Yehova atakaa karibu nasi iwapo tutakaa karibu naye. Nabii Azaria aliongozwa na “roho ya Mungu,” kueleza ile ambayo tunaweza kuiita kweli ya msingi: “BWANA yu pamoja nanyi, mkiwa pamoja naye; nanyi mkimtafuta ataonekana kwenu; lakini mkimwacha atawaacha ninyi.”—2 Mambo ya Nyakati 15:1, 2.

Lazima Yehova Awe Halisi Kwetu

13. Tunaweza kuonyeshaje kwamba Yehova ni halisi kwetu?

13 Mtume Paulo aliandika kuhusu Musa kwamba “aliendelea akiwa imara kama ambaye anaona Yeye asiyeonekana.” (Waebrania 11:27) Bila shaka, Musa hakumwona Yehova kihalisi. (Kutoka 33:20) Lakini Yehova alikuwa halisi sana kwake, kana kwamba alimwona. Vivyo hivyo, baada ya majaribu yaliyompata, Ayubu alimwona Yehova vizuri zaidi kwa macho ya imani. Alimwona kuwa Mungu anayeruhusu watumishi wake waaminifu wapatwe na majaribu lakini asiyeweza kuwaacha. (Ayubu 42:5) Ilisemwa kuhusu Enoki na Noa kwamba ‘walikwenda pamoja na Mungu.’ Walifanya hivyo kwa kujitahidi kumpendeza Mungu na kumtii. (Mwanzo 5:22-24; 6:9, 22; Waebrania 11:5, 7) Kama Yehova ni halisi kwetu kama alivyokuwa kwa Enoki, Noa, Ayubu, na Musa, ‘tutamkiri yeye’ katika njia zetu zote, naye ‘atayanyosha mapito yetu.’—Mithali 3:5, 6.

14. Inamaanisha nini “kushikamana” na Yehova?

14 Muda mfupi tu kabla ya Waisraeli kuingia Bara Lililoahidiwa, Musa aliwashauri hivi: “Tembeeni kwa kumtafuta BWANA, Mungu wenu; mcheni na kushika maagizo yake na kuisikia sauti yake, nanyi mtumikieni na kushikamana naye.” (Kumbukumbu la Torati 13:4) Walipaswa kumfuata Yehova, kumwogopa, kumtii, na kushikamana naye. Kuhusu neno linalotafsiriwa “kushikamana” kwenye andiko hilo, msomi mmoja wa Biblia anasema kwamba “lugha ya [Kiebrania] inaonyesha uhusiano wa karibu sana.” Mtunga-zaburi alisema: “Mwenyezi-Mungu ni rafiki ya wale wamchao.” (Zaburi 25:14, Biblia Habari Njema) Tutakuwa na uhusiano huo wa thamani na wa karibu pamoja na Yehova iwapo yeye ni halisi kwetu na iwapo tunampenda kiasi cha kwamba tunaogopa kumchukiza kwa njia yoyote.—Zaburi 19:9-14.

Je, Unajua Kwamba Yehova Anakujali?

15, 16. (a) Zaburi ya 34 inaonyeshaje kwamba Yehova anatujali? (b) Tunapaswa kufanya nini iwapo ni vigumu kukumbuka matendo ya wema ambayo Yehova ametutendea?

15 Njia moja ya ujanja ambayo Shetani hutumia ni kutufanya tusahau kwamba Mungu wetu, Yehova, anawajali watumishi wake daima. Mfalme Daudi wa Israeli alijua kwamba Yehova alimlinda hata alipokabili hali hatari sana. Alipolazimika kujifanya kwamba amerukwa na akili mbele ya Mfalme Akishi wa Gathi, Daudi alitunga wimbo, zaburi nzuri sana, iliyokuwa na maneno haya ya imani: “Mtukuzeni BWANA pamoja nami, na tuliadhimishe jina lake pamoja. Nalimtafuta BWANA akanijibu, akaniponya na hofu zangu zote. Malaika wa BWANA hufanya kituo, akiwazungukia wamchao na kuwaokoa. Onjeni mwone ya kuwa BWANA yu mwema; heri mtu yule anayemtumaini. BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa. Mateso ya mwenye haki ni mengi, lakini BWANA humponya nayo yote”.—Zaburi 34:3, 4, 7, 8, 18, 19; 1 Samweli 21:10-15.

16 Je, unaamini kwamba Yehova anaweza kuokoa? Je, unajua kwamba yeye hutumia malaika kukulinda? Je, wewe umeonja na kuona kwamba Yehova ni mwema? Je, unakumbuka hasa mara ya mwisho ambapo Yehova alikutendea jambo fulani jema? Jaribu kukumbuka. Je, ni wakati ulipotembelea nyumba ya mwisho ulipokuwa ukihubiri, ingawa ulikuwa unahisi kwamba huwezi kuendelea zaidi? Labda ulikuwa na mazungumzo mazuri na mwenye nyumba hiyo. Je, ulikumbuka kumshukuru Yehova kwa kukupatia nguvu zaidi ulizohitaji na kwa kukubariki? (2 Wakorintho 4:7) Kwa upande mwingine, huenda ikawa vigumu kwako kukumbuka tendo hususa la wema ambalo Yehova amekutendea. Huenda usiweze kukumbuka kama alitenda hivyo juma moja lililopita, mwezi, mwaka, au hata muda mrefu uliopita. Iwapo una tatizo hilo, kwa nini usijitahidi kumkaribia Yehova zaidi na kujaribu kuona jinsi anavyokuongoza na kukuelekeza? Mtume Petro aliwashauri Wakristo hivi: “Jinyenyekezeni chini ya mkono wa Mungu wenye uweza . . . huku mkitupa hangaiko lenu lote juu yake, kwa sababu yeye huwajali nyinyi.” (1 Petro 5:6, 7) Naam, utashangaa kuona jinsi Yehova anavyokujali!—Zaburi 73:28.

Endelea Kumtafuta Yehova

17. Tunahitaji kufanya nini ili kuendelea kumtafuta Yehova?

17 Ni lazima tuendelee kusitawisha uhusiano wetu na Yehova sikuzote. Yesu alisema hivi aliposali kwa Baba yake: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Tunahitaji kujitahidi daima ili kutwaa ujuzi juu ya Yehova na Mwana wake. Tunahitaji msaada wa sala na roho takatifu ili kuelewa “mambo yenye kina kirefu ya Mungu.” (1 Wakorintho 2:10; Luka 11:13) Tunahitaji pia mwongozo wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ili kulisha akili zetu chakula cha kiroho kinachotolewa “wakati ufaao.” (Mathayo 24:45) Kupitia mtumwa huyo, Yehova ametushauri tusome Neno lake kila siku, tuhudhurie mikutano kwa ukawaida, na kushiriki kwa bidii kazi ya kuhubiri ‘habari njema ya ufalme.’ (Mathayo 24:14) Kwa kufanya hivyo, tutaendelea kumtafuta Yehova, Mungu wetu anayetujali.

18, 19. (a) Tunapaswa kuazimia kufanya nini? (b) Ikiwa tutachukua msimamo imara dhidi ya Ibilisi na kuendelea kumtafuta Yehova, tutabarikiwaje?

18 Shetani anafanya yote awezayo ili kuwanyanyasa, kuwapinga, na kuwaletea watu wa Yehova mikazo kutoka kila upande. Yeye hujaribu kuvuruga amani yetu na kuharibu msimamo wetu mzuri pamoja na Mungu. Shetani hataki tuendelee na kazi yetu ya kutafuta watu wenye mioyo minyofu na kuwasaidia wasimame upande wa Yehova kuhusiana na suala la ni nani mwenye haki ya kutawala ulimwengu wote. Lakini ni lazima tuazimie kuwa waaminifu-washikamanifu kwa Yehova, tukitumaini kwamba atatukomboa na yule mwovu. Kwa kukubali tuongozwe na Neno la Mungu na kwa kuendelea kushirikiana kwa bidii na tengenezo lake linaloonekana, tunaweza kuwa na hakika kwamba ataendelea kutusaidia.—Isaya 41:8-13.

19 Kwa hiyo, sote na tuchukue msimamo imara dhidi ya Ibilisi na njia zake za ujanja, huku tukimtafuta Mungu wetu mwenye upendo, Yehova, ambaye ‘atatufanya imara, atatufanya kuwa wenye nguvu.’ (1 Petro 5:8-11) Hivyo ‘tutajitunza wenyewe katika upendo wa Mungu, huku tukingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa tazamio la uhai udumuo milele.’—Yuda 21.

Ungejibuje?

• Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “Ibilisi” linamaanisha nini, naye Ibilisi hutimizaje maana ya neno hilo?

• Kuna tofauti gani kati ya Yehova na Ibilisi kuhusiana na vile Yeye atazamavyo wakazi wa dunia?

• Kwa nini ni lazima mtu akubali fidia katika kumfikia Yehova?

• Inamaanisha nini “kushikamana” na Yehova, na tunawezaje kuendelea kumtafuta?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Licha ya majaribu yake, Ayubu alikuja kujua kwamba Yehova alimjali

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Kusoma Biblia kila siku, kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na kushiriki kwa bidii kazi ya kuhubiri hutukumbusha kwambaYehova anatujali