Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Dumisheni Mwenendo Wenu Ukiwa Bora Miongoni mwa Mataifa”

“Dumisheni Mwenendo Wenu Ukiwa Bora Miongoni mwa Mataifa”

“Dumisheni Mwenendo Wenu Ukiwa Bora Miongoni mwa Mataifa”

“Heshimuni watu wa namna zote, iweni na upendo kwa ushirika mzima wa ndugu.”—1 PETRO 2:17.

1, 2. (a) Mwandishi fulani wa gazeti alisema nini kuhusu Mashahidi wa Yehova? (b) Kwa nini Mashahidi wa Yehova hujitahidi kudumisha viwango vya juu vya mwenendo?

MIAKA kadhaa iliyopita, mwandishi wa gazeti fulani huko Amarillo, Texas, Marekani, alizuru makanisa mbalimbali katika eneo hilo kisha akachapisha ripoti yake. Aliona kikundi kimoja kilichokuwa tofauti. Alisema: “Kwa miaka mitatu, nilihudhuria makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova yanayofanywa kila mwaka huko Amarillo Civic Center. Nilipochangamana nao, sikuona kamwe mtu yeyote akiwasha sigareti, akifungua mkebe wa pombe, au kutumia lugha chafu. Walikuwa watu safi, wenye adabu, nadhifu, na wenye fadhili kuliko watu ambao nimewahi kukutana nao.” Mara nyingi maoni kama hayo kuhusu Mashahidi wa Yehova yamechapishwa. Kwa nini mara nyingi Mashahidi husifiwa na watu ambao si wa dini yao?

2 Kwa kawaida, watu wa Mungu husifiwa kwa sababu ya mwenendo wao bora. Ingawa kwa ujumla viwango vinazidi kuzorota, Mashahidi wa Yehova wanatakiwa kuwa na mwenendo mzuri kwani unahusiana na ibada yao. Wanajua kwamba matendo yao huathiri maoni ya wengine kuhusu Yehova na ndugu zao Wakristo na kwamba mwenendo wao unaweza kufanya wengine wavutiwe na kweli wanayohubiri. (Yohana 15:8; Tito 2:7, 8) Basi, na tuone jinsi tunavyoweza kudumisha mwenendo bora na hivyo kudumisha sifa nzuri ya Yehova na Mashahidi wake na jinsi tunavyonufaika kwa kufanya hivyo.

Familia ya Kikristo

3. Familia za Kikristo zinapaswa kulindwa dhidi ya nini?

3 Fikiria mwenendo wetu katika familia. Kitabu kinachohusu uhuru wa kidini (Die Neuen Inquisitoren: Religionsfreiheit und Glaubensneid) cha Gerhard Besier na Erwin K. Scheuch, chasema: “[Mashahidi wa Yehova] huona kwamba familia inapaswa kulindwa sana.” Maneno hayo ni ya kweli, na leo familia inahitaji kulindwa dhidi ya hatari nyingi. Kuna watoto ambao ‘hawatii wazazi’ na watu wazima ambao ‘hawana shauku ya kidugu’ au ‘wasio na hali ya kujidhibiti.’ (2 Timotheo 3:2, 3) Wenzi wa ndoa hutendewa kijeuri katika familia, wazazi huwatendea watoto wao vibaya au kuwapuuza, nao watoto huasi, huanza kutumia dawa za kulevya na kufanya uasherati, au kutoroka nyumbani. Yote hayo hutokea kwa sababu ya uvutano mbaya wa ‘roho ya ulimwengu.’ (Waefeso 2:1, 2) Tunahitaji kulinda familia zetu dhidi ya roho hiyo. Jinsi gani? Kwa kutii shauri la Yehova na mwelekezo anaotoa kwa familia.

4. Washiriki wa familia za Kikristo wana daraka gani kuelekea mmoja na mwenzake?

4 Wakristo waliofunga ndoa wanatambua kwamba wanapaswa kutimiziana mahitaji ya kihisia-moyo, kiroho, na kimwili. (1 Wakorintho 7:3-5; Waefeso 5:21-23; 1 Petro 3:7) Wazazi Wakristo wana madaraka mazito kuelekea watoto wao. (Mithali 22:6; 2 Wakorintho 12:14; Waefeso 6:4) Nao watoto katika nyumba za Kikristo wanapokua, wanatambua kwamba wao pia wana madaraka fulani. (Mithali 1:8, 9; 23:22; Waefeso 6:1; 1 Timotheo 5:3, 4, 8) Ili kutimiza madaraka ya familia, jitihada, azimio, na roho ya upendo na ya kujidhabihu inahitajiwa. Hata hivyo, washiriki wote wa familia wanapotimiza madaraka yao waliyopewa na Mungu, wananufaika na kunufaisha kutaniko. Jambo la maana zaidi ni kwamba wanamletea Yehova Mungu sifa, aliye Mwanzilishi wa familia.—Mwanzo 1:27, 28; Waefeso 3:15.

Udugu wa Kikristo

5. Tunapata manufaa gani kwa kushirikiana na Wakristo wenzetu?

5 Tukiwa Wakristo, sisi pia tuna wajibu fulani kuelekea waamini wenzetu kutanikoni na, wale wanaofanyiza “ushirika mzima wa ndugu . . . ulimwenguni.” (1 Petro 5:9) Uhusiano wetu na kutaniko ni muhimu ili kuwa na afya ya kiroho. Tunaposhirikiana na Wakristo wenzetu, tunafurahia ushirika wao wenye kujenga na pia chakula cha kiroho kinachofaa kutoka kwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Tukiwa na matatizo tunaweza kuwaendea ndugu zetu ili kupata shauri linalofaa ambalo linategemea kanuni za Kimaandiko. (Mithali 17:17; Mhubiri 4:9; Yakobo 5:13-18) Ndugu zetu hawatuachi tunapokuwa na uhitaji. Ni baraka iliyoje kuwa katika tengenezo la Mungu!

6. Paulo alionyeshaje kwamba tuna wajibu fulani kuelekea Wakristo wengine?

6 Hata hivyo, hatuko kutanikoni ili kupokea tu; tuko huko ili kutoa pia. Kwa kweli, Yesu alisema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Mtume Paulo alikazia nia ya kutoa alipoandika hivi: “Acheni tushike sana tangazo la hadharani la tumaini letu bila kuyumbayumba, kwa maana yeye ni mwaminifu aliyeahidi. Na acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali kutiana moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri mwonavyo siku ikikaribia.”—Waebrania 10:23-25.

7, 8. Tunaonyeshaje roho ya kutoa katika kutaniko letu na kwa ajili ya Wakristo katika nchi nyinginezo?

7 Katika kutaniko, tunafanya “tangazo la hadharani la tumaini letu” tunapotoa maelezo kwenye mikutano au kushiriki katika programu hiyo kwa njia nyinginezo. Bila shaka jitihada hizo huwatia moyo ndugu zetu. Pia tunawatia moyo kwa mazungumzo yetu kabla na baada ya mikutano. Huo ndio wakati tunapoweza kuwaimarisha walio dhaifu, kuwaliwaza walioshuka moyo, na kuwafariji wagonjwa. (1 Wathesalonike 5:14) Wakristo wanyofu hutoa kwa wingi katika njia hiyo, na ndiyo sababu wengi wanaohudhuria mikutano yetu kwa mara ya kwanza huvutiwa na upendo wanaoona miongoni mwetu.—Zaburi 37:21; Yohana 15:12; 1 Wakorintho 14:25.

8 Hata hivyo, upendo wetu hauhusishi tu kutaniko letu. Unatia ndani ushirika mzima wa ndugu zetu ulimwenguni pote. Ndiyo sababu, katika kila Jumba la Ufalme kuna sanduku la michango kwa ajili ya Hazina ya Majumba ya Ufalme. Huenda tukawa na Jumba zuri la Ufalme, lakini tunajua kwamba maelfu ya Wakristo wenzetu katika nchi nyinginezo hawana mahali pazuri pa kukutania. Tunapotoa michango kwa ajili ya Hazina ya Majumba ya Ufalme, tunaonyesha kwamba tunawapenda ndugu zetu hata ingawa huenda tusiwajue.

9. Ni kwa sababu gani kuu Mashahidi wa Yehova wanapendana?

9 Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanapendana? Yesu aliwaamuru wafanye hivyo. (Yohana 15:17) Na upendo ulio kati yao unathibitisha kwamba roho ya Mungu i juu yao wakiwa mtu mmoja-mmoja au kikundi. Upendo ni sehemu ya “matunda ya roho.” (Wagalatia 5:22, 23) Mashahidi wa Yehova wanapojifunza Biblia, wanapohudhuria mikutano ya Kikristo, na kusali kwa Mungu daima, linakuwa jambo la kawaida kupendana licha ya kwamba wanaishi katika ulimwengu ambao ‘upendo wa idadi kubwa umepoa.’—Mathayo 24:12.

Kushughulika na Ulimwengu

10. Tuna daraka gani kuelekea ulimwengu?

10 Paulo anatukumbusha daraka lingine anapotaja “tangazo la hadharani la tumaini letu.” Tangazo hilo la hadharani linahusisha kazi ya kuhubiri habari njema kwa watu ambao si ndugu zetu Wakristo. (Mathayo 24:14; 28:19, 20; Waroma 10:9, 10, 13-15) Kazi hiyo ya kuhubiri ni tendo lingine la kutoa. Tunahitaji wakati, nguvu, matayarisho, mazoezi, na rasilimali ili kushiriki kazi hiyo. Hata hivyo, Paulo aliandika hivi pia: “Kwa Wagiriki na kwa Wabaribari pia, kwa wenye hekima na kwa wasio na akili pia mimi ni mdeni: kwa hiyo kuna hamu upande wangu kuitangaza habari njema kwenu pia mlioko Roma.” (Waroma 1:14, 15) Kama Paulo, na tujitoe kwa moyo kulipa kikamilifu “deni” hilo.

11. Uhusiano wetu na ulimwengu unategemea kanuni gani mbili za Kimaandiko, hata hivyo tunatambua jambo gani?

11 Je, tuna daraka lolote kuelekea watu ambao si waamini wenzetu? Bila shaka. Tunatambua kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Tunajua kwamba Yesu alisema hivi kuhusu wanafunzi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.” Hata hivyo, tunaishi katika ulimwengu, tunapata riziki yetu kutoka kwa ulimwengu, na kupokea huduma zake. (Yohana 17:11, 15, 16) Kwa hiyo, tuna daraka fulani kuelekea ulimwengu. Daraka gani? Mtume Petro alijibu swali hilo. Muda mfupi kabla Yerusalemu halijaharibiwa, aliandika barua kwa Wakristo wa Asia Ndogo, na habari fulani katika barua hiyo zinatusaidia tuwe na usawaziko tunaposhughulika na ulimwengu.

12. Wakristo ni “wakaaji wa kigeni na wakazi wa muda,” katika njia gani, na kwa hiyo wanapaswa kujiepusha na nini?

12 Petro alianza kwa kusema: “Wapendwa, nawahimiza nyinyi kwa bidii mkiwa wakaaji wa kigeni na wakazi wa muda mfulize kujiepusha na tamaa za kimwili, ambazo zenyewe ndizo huendesha pambano dhidi ya nafsi.” (1 Petro 2:11) Katika maana ya kiroho, Wakristo wa kweli ni “wakaaji wa kigeni na wakazi wa muda” kwa sababu wanazingatia hasa uhai udumuo milele—watiwa-mafuta mbinguni na “kondoo wengine” katika paradiso ya kidunia itakayokuja. (Yohana 10:16; Wafilipi 3:20, 21; Waebrania 11:13; Ufunuo 7:9, 14-17) Hata hivyo, tamaa za kimwili ni zipi? Zinatia ndani mambo kama vile tamaa ya kuwa tajiri, kuwa mashuhuri, tamaa isiyofaa ya ngono, na tamaa zinazotajwa kuwa “husuda” na ‘kutamani.’—Wakolosai 3:5; 1 Timotheo 6:4, 9; 1 Yohana 2:15, 16.

13. Tamaa za mwili “huendesha pambano dhidi ya nafsi [zetu]” jinsi gani?

13 Kwa kweli, tamaa hizo “huendesha pambano dhidi ya nafsi [zetu].” Zinaharibu uhusiano wetu na Mungu na hivyo kuhatarisha tumaini (“nafsi” zetu au uhai) letu la Kikristo. Kwa mfano, tukianza kupendezwa na mambo yasiyo ya adili, tutawezaje kujitoa ‘kuwa dhabihu iliyo hai, takatifu, na yenye kukubalika kwa Mungu’? Tukinaswa na mtego wa kufuatia vitu vya kimwili ‘tutautafutaje ufalme kwanza’? (Waroma 12:1, 2; Mathayo 6:33; 1 Timotheo 6:17-19) Jambo la busara kufanya ni kufuata kielelezo cha Musa, kukataa vishawishi vya ulimwengu, na kutanguliza utumishi wa Yehova maishani mwetu. (Mathayo 6:19, 20; Waebrania 11:24-26) Hilo ni jambo muhimu la kutusaidia tuwe na usawaziko tunaposhughulika na ulimwengu.

‘Dumisheni Mwenendo Bora’

14. Kwa nini tukiwa Wakristo tunajitahidi kudumisha mwenendo bora?

14 Mwongozo mwingine muhimu unapatikana katika maneno ya Petro yanayofuata: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa bora miongoni mwa mataifa, ili, katika jambo ambalo katika hilo wao wanasema dhidi yenu kuwa watenda-maovu, likiwa tokeo la kazi zenu bora ambazo wamekuwa mashahidi wa kujionea wapate kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.” (1 Petro 2:12) Kwa kuwa sisi ni Wakristo, tunajitahidi kuwa kielelezo kizuri. Tunajifunza kwa bidii shuleni. Tunakuwa wenye bidii na wanyofu kazini—hata ikiwa mwajiri wetu anaonekana kuwa mtu mgumu kushughulika naye. Katika familia zilizogawanyika kidini, mume au mke ambaye ni mwamini hujitahidi kufuata kanuni za Kikristo. Si rahisi kufanya hivyo sikuzote, lakini tunajua kwamba mwenendo wetu bora humpendeza Yehova na mara nyingi huwavutia watu ambao si Mashahidi.—1 Petro 2:18-20; 3:1.

15. Tunajuaje kwamba mwenendo wa kiwango cha juu wa Mashahidi wa Yehova unajulikana sana?

15 Kwa kuchunguza maelezo ambayo yamechapishwa kwa miaka mingi kuhusu Mashahidi wa Yehova, tunaona kwamba wengi wao wamefanikiwa kudumisha viwango bora. Kwa mfano, gazeti Il Tempo la Italia liliripoti hivi: “Watu ambao hufanya kazi pamoja na Mashahidi wa Yehova wanawatambua kuwa wafanyakazi wanyofu, walio na imani yenye nguvu sana; hata hivyo, wanastahili kuheshimiwa kwa sababu ya uaminifu wao wa maadili.” Gazeti Herald la Buenos Aires, Argentina, lilisema: “Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova wamethibitika kuwa raia wanaofanya kazi kwa bidii, wanaochukua mambo kwa uzito, wanaotumia pesa kwa uangalifu, na wanaomwogopa Mungu.” Msomi Mrusi Sergei Ivanenko alisema: “Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kuwa raia wanaotii sheria kabisa, wenye mtazamo mzuri hasa kuhusiana na kulipa kodi.” Meneja wa uwanja fulani unaotumiwa na Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya kusanyiko lao nchini Zimbabwe alisema hivi: “Ninaona Mashahidi wakiokota makaratasi na kusafisha vyoo. Wanaacha uwanja wa maonyesho ukiwa safi kuliko ulivyokuwa awali. Vijana wenu ni waadilifu. Laiti watu ulimwenguni pote wangekuwa Mashahidi wa Yehova.”

Ujitiisho wa Kikristo

16. Tuna uhusiano gani na wenye mamlaka, na kwa nini?

16 Petro anataja pia uhusiano wetu na wenye mamlaka. Anasema: “Kwa ajili ya Bwana jitiisheni wenyewe kwa kila kilichoumbwa na binadamu: kama ni kwa mfalme akiwa mkubwa au kwa magavana wakiwa wametumwa naye kupasisha adhabu juu ya watenda-maovu bali kusifu watenda-mema. Kwa maana ndivyo mapenzi ya Mungu yalivyo, kwamba kwa kutenda mema mpate kufunga kinywa yale maongezi yasiyo na ujuzi ya watu wenye kukosa akili.” (1 Petro 2:13-15) Tunashukuru kwa manufaa tunazopata kutokana na serikali zenye utaratibu, na kwa kuongozwa na maneno ya Petro, tunatii sheria za serikali na kulipa kodi. Ingawa tunatambua haki ambayo Mungu ameipa serikali kuadhibu wanaovunja sheria, sababu kuu inayofanya tutii mamlaka ni “kwa ajili ya Bwana.” Ni mapenzi ya Mungu. Isitoshe, hatungependa kuleta suto kwa jina la Yehova kwa kuadhibiwa kwa sababu ya kufanya kosa.—Waroma 13:1, 4-7; Tito 3:1; 1 Petro 3:17.

17. “Watu wenye kukosa akili” wanapotupinga, tunaweza kuwa na uhakika gani?

17 Kwa kusikitisha, watu fulani “wenye kukosa akili” ambao wana mamlaka hutunyanyasa au kutupinga kwa njia nyingine—kama vile kwa kueneza habari zisizo za kweli kutuhusu. Hata hivyo, kwa wakati unaofaa wa Yehova, habari zao zisizo za kweli hufunuliwa, na ‘maongezi yao yasiyo ya ujuzi,’ huzimwa kabisa. Sifa ambayo tumepata kupitia mwenendo wetu wa Kikristo huonyesha ukweli wa mambo. Ndiyo sababu maofisa wa serikali walio wanyofu hutupongeza sisi kuwa watenda mema.—Waroma 13:3; Tito 2:7, 8.

Watumwa wa Mungu

18. Tukiwa Wakristo, tunawezaje kuepuka kutumia uhuru wetu vibaya?

18 Sasa Petro aonya hivi: “Iweni kama watu huru, na bado mkishika uhuru wenu, si kama kisetiri cha ubaya, bali kama watumwa wa Mungu.” (1 Petro 2:16; Wagalatia 5:13) Leo, kuijua kweli ya Biblia hutuweka huru kutokana na mafundisho ya kidini yasiyo ya kweli. (Yohana 8:32) Isitoshe, tuna uhuru wa kuchagua, nasi tunaweza kufanya maamuzi. Hata hivyo, hatutumii uhuru wetu vibaya. Tunapochagua marafiki, mavazi, mapambo, vitumbuizo—hata chakula na vinywaji—tunakumbuka kwamba Wakristo wa kweli ni watumwa wa Mungu, si watu wenye kujipendeza. Tunachagua kumtumikia Yehova badala ya kuwa watumwa wa tamaa zetu za kimwili au mitindo ya kisasa ya ulimwengu.—Wagalatia 5:24; 2 Timotheo 2:22; Tito 2:11, 12.

19-21. (a) Tunawaonaje watu wenye madaraka serikalini? (b) Wengine wameonyeshaje “upendo kwa ushirika mzima wa ndugu”? (c) Daraka letu muhimu zaidi ni lipi?

19 Petro anaendelea kusema: “Heshimuni watu wa namna zote, iweni na upendo kwa ushirika mzima wa ndugu, iweni katika kuhofu Mungu, iweni wenye kumheshimu mfalme.” (1 Petro 2:17) Kwa kuwa Yehova Mungu ameruhusu watu fulani wawe na madaraka, tunawapa watu hao heshima inayostahili. Hata tunasali kwa ajili yao, kusudi turuhusiwe kuendelea na huduma yetu kwa amani na kwa ujitoaji-kimungu. (1 Timotheo 2:1-4) Hata hivyo, wakati huohuo, ‘tuna upendo kwa ushirika mzima wa ndugu.’ Nyakati zote tunataka kuwafaidi ndugu zetu Wakristo, si kuwaumiza.

20 Kwa mfano, wakati taifa moja la Afrika lilipokumbwa na vita ya kikabila, mwenendo wa Kikristo wa Mashahidi wa Yehova ulionekana waziwazi. Gazeti Reformierte Presse la Uswisi liliripoti hivi: “Mnamo mwaka wa 1995, shirika la kutetea haki za Waafrika linaloitwa African Rights . . . lilithibitisha kwamba dini zote zilishiriki [vita hiyo] isipokuwa Mashahidi wa Yehova.” Nchi nyingine zilipopata habari kuhusu msiba huo, Mashahidi wa Yehova huko Ulaya walituma chakula na dawa mara moja kwa ndugu zao na watu wengine walioathiriwa. (Wagalatia 6:10) Walitii maneno ya Mithali 3:27: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.”

21 Hata hivyo, tuna daraka lingine muhimu zaidi ya heshima tunayowapa wenye mamlaka na hata upendo tunaopaswa kuwaonyesha ndugu zetu. Ni daraka gani? Petro alisema: “Iweni katika kuhofu Mungu.” Tuna deni kubwa kwa Yehova kuliko kwa mwanadamu yeyote. Jinsi gani? Nasi tunawezaje kutimiza wajibu wetu kwa Mungu na wakati huohuo kwa wenye mamlaka? Maswali hayo yatajibiwa katika makala inayofuata.

Je, Unakumbuka?

• Wakristo wana madaraka gani katika familia?

• Tunawezaje kuonyesha roho ya kutoa katika kutaniko?

• Tuna wajibu gani kuelekea ulimwengu?

• Tunapata manufaa gani kwa kudumisha viwango vya juu vya mwenendo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Familia ya Kikristo inawezaje kuwa mahali pa shangwe kubwa?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanapendana?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je, tunaweza kuwapenda ndugu zetu hata tusipowajua?