Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ni Vigumu Sana Kuomba Msamaha?

Kwa Nini Ni Vigumu Sana Kuomba Msamaha?

Kwa Nini Ni Vigumu Sana Kuomba Msamaha?

MNAMO Julai mwaka 2000, Baraza la Kutunga Sheria la Jimbo la California nchini Marekani lilipitisha muswada uliokusudiwa kuwaondolea watu hatia iwapo watamwonyesha huruma mtu aliyejeruhiwa kwenye aksidenti ambayo wao wenyewe walihusika. Kwa nini walipitisha muswada huo? Ilionekana kwamba aksidenti inaposababisha majeraha au uharibifu, mara nyingi watu husita kuomba msamaha isije ikaeleweka mahakamani kwamba wamekiri kuwa na hatia. Kwa upande mwingine, huenda wale wanaohisi kwamba wanapaswa kuombwa msamaha mara moja wakaudhika, na huenda aksidenti ndogo tu ikasababisha mgogoro mkubwa.

Bila shaka, si lazima kuomba msamaha kwa aksidenti ambayo hukusababisha. Na huenda nyakati nyingine likawa jambo la hekima kuwa mwangalifu kuhusu yale unayosema. Mithali moja ya zamani inasema: “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.” (Mithali 10:19; 27:12) Lakini, unaweza kuwa mwenye adabu na mwenye kusaidia.

Hata hivyo, je, si kweli kwamba watu wengi wameacha kuomba msamaha, hata katika mambo yasiyohusisha mahakama? Huenda mke akalalamika nyumbani, ‘Mume wangu haombi msamaha kwa jambo lolote.’ Huenda msimamizi akalalamika kazini, ‘Wafanyakazi wangu hawakubali makosa yao, nao huomba msamaha mara chache sana.’ Huenda mwalimu akaripoti shuleni, ‘Watoto hawazoezwi kusema samahani.’

Huenda mtu asiombe msamaha akiogopa kwamba ombi lake litakataliwa. Huenda akakosa kueleza jinsi anavyohisi akiogopa kwamba atapuuzwa. Kwani huenda mtu aliyekosewa akamwepuka kabisa mkosaji na kufanya iwe vigumu sana kusuluhisha mambo.

Huenda wengine wakasita kuomba msamaha kwa sababu ya kutojali hisia za wengine. Huenda wakawaza, ‘Kuomba msamaha hakutarekebisha kosa nililofanya.’ Hata kuna wengine wanaosita kuomba msamaha kwa sababu ya mambo yanayoweza kuwapata wakifanya hivyo. Wanajiuliza, ‘Je, nitahesabiwa makosa na hivyo kuombwa nilipe fidia?’ Hata hivyo, sababu kuu inayofanya watu wasikubali makosa ni kiburi. Mtu aliye na kiburi sana asiweze kusema “naomba msamaha,” anaweza kukata kauli, ‘Sitaki kujiaibisha kwa kukubali kosa langu. Jambo hilo litanishushia cheo.’

Hata sababu iwe nini, wengi huona ni vigumu kuomba msamaha. Lakini je, ni muhimu kweli kuomba msamaha? Kuna manufaa gani kuomba msamaha?

[Picha katika ukurasa wa 3]

‘Watoto hawazoezwi kusema samahani’

[Picha katika ukurasa wa 3]

‘Wafanyakazi wangu hawakubali makosa yao’

[Picha katika ukurasa wa 3]

‘Mume wangu haombi msamaha kwa jambo lolote’