Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, ni vibaya kucheza kamari iwapo unatumia pesa kidogo?

Neno la Mungu halizungumzii kwa undani juu ya kucheza kamari, hata hivyo lina habari ya kutosha inayoonyesha kwamba kucheza kamari kunapingana na kanuni za Biblia. * Kwa mfano, ni wazi kwamba kucheza kamari huchochea pupa. Sababu hiyo pekee, inapasa kufanya Wakristo waepuke kamari, kwa kuwa Biblia inasema kwamba “watu wenye pupa” hawataurithi Ufalme wa Mungu, nayo huhusisha tamaa na ibada ya sanamu.—1 Wakorintho 6:9, 10; Wakolosai 3:5.

Kucheza kamari pia huchochea majisifu na roho ya mashindano isiyofaa, tamaa kubwa ya kushinda. Mtume Paulo alionya dhidi ya mambo hayo alipoandika hivi: “Acheni sisi tusiwe wenye majisifu ya bure, wenye kuchochea shindano juu ya mtu na mwenzake, tukihusudiana.” (Wagalatia 5:26) Isitoshe, kucheza kamari huchochea wengine wafuate ushirikina kwa kutegemea bahati nzuri. Wacheza-kamari hufuata kila namna ya ushirikina, huku wakitumaini kupata bahati nzuri. Wanatukumbusha Waisraeli wasio waaminifu ambao walikuwa ‘wakiandika meza kwa ajili ya Bahati, na kuijazia Ajali vyombo vya divai iliyochanganyika.’—Isaya 65:11.

Watu fulani wanaweza kufikiri kwamba kutumia pesa kidogo na kucheza kadi pamoja na watu wa jamaa au marafiki wa karibu ni kujifurahisha tu. Ni kweli kwamba huenda mtu anayecheza kamari kwa kutumia pesa kidogo tu asijione kuwa mwenye pupa, majisifu, kushindana, au mshirikina. Hata hivyo, anaweza kuathirije wale anaocheza kamari nao? Wacheza-kamari wengi ambao ni sugu walianza kwa kutumia pesa kidogo ‘ili kujifurahisha tu.’ (Luka 16:10) Kujifurahisha huko ambako kulionekana kuwa hakuna madhara kuligeuka na kuwa hatari.

Watoto wameathiriwa hasa na jambo hilo. Watoto wengi husisimuka kushinda pesa kidogo na hivyo kushawishiwa kushinda pesa nyingi zaidi. (1 Timotheo 6:10) Uchunguzi uliofanywa kwa muda mrefu na kuchapishwa Marekani na shirika la Arizona Council on Compulsive Gambling unathibitisha kwamba wacheza-kamari wengi ambao ni sugu walianza kucheza walipokuwa wachanga “kwa kutumia pesa kidogo tu ya michezo au kucheza kadi na marafiki au jamaa zao.” Ripoti nyingine inasema kwamba “watoto huanza kucheza kamari nyumbani, mara nyingi kwa kucheza kadi na watu wa familia na marafiki.” Ripoti hiyo inaongeza kusema kwamba “asilimia 30 ya watoto waliocheza kamari walianza kufanya hivyo kabla hawajafikisha umri wa miaka 11.” Matineja wengi wanaocheza kamari hupata pesa za kufanya hivyo kwa kujihusisha na uhalifu au uasherati, kulingana na uchunguzi wenye kichwa Why Do People Gamble Too Much—Pathological and Problem Gambling. Hayo ni matokeo mabaya kama nini yanayoletwa na jambo ambalo lilionekana kuwa halina madhara hapo mwanzoni!

Kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu ambao tayari una mitego na vishawishi vingi, hakuna haja ya kujiongezea mitego na vishawishi zaidi. (Mithali 27:12) Kucheza kamari ni hatari kiroho na kwapaswa kuepukwa watoto wawepo au wasiwepo au iwapo tutatumia pesa kidogo au nyingi. Wakristo wanaopenda kucheza kadi kama tafrija wanapaswa kushauriwa waandike tu matokeo au wacheze mchezo huo ili kujifurahisha tu bila hata kuandika matokeo. Wakristo wenye hekima ambao wanajali hali yao ya kiroho na vilevile ya marafiki wao na familia yao huepuka kucheza kamari—hata kama wanatumia pesa kidogo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kichapo World Book Encyclopedia kinafafanua kucheza kamari kuwa ‘kuweka mapatano ya kimbele kuhusu matokeo ya mchezo au tukio fulani.’ Kichapo hicho kinaongeza kusema kwamba “wacheza-kamari au wachezaji huweka mapatano ya fedha . . . kuhusu michezo ya bahati nasibu, kadi, na dadu.”