Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sisi Sote Tunahitaji Kupongezwa

Sisi Sote Tunahitaji Kupongezwa

Sisi Sote Tunahitaji Kupongezwa

SIKU hiyo ilikuwa yenye kupendeza kwa yule msichana mdogo. Ijapokuwa alihitaji kutiwa nidhamu mara nyingine, siku hiyo, alikuwa amejitahidi kujiendesha vizuri. Hata hivyo, usiku huo baada ya msichana huyo kulala, mamake alimsikia akilia. Alipomwuliza ni kwa nini alilia, msichana huyo alisema hivi machozi yakimtiririka: “Je, sijawa mtoto mzuri leo?”

Swali hilo lilimchoma mamake moyoni. Kwa kawaida mama huyo alikuwa akimtia binti yake nidhamu mara alipokosea. Lakini sasa, ingawa alikuwa ameona jinsi binti yake alivyokuwa amejaribu sana kujiendesha vizuri, hakumpongeza hata kidogo.

Si wasichana wadogo pekee wanaohitaji kupongezwa na kutiwa moyo. Sisi sote tunahitaji kupongezwa kama vile tunavyohitaji kushauriwa na kutiwa nidhamu mara kwa mara.

Tunahisije mtu mwingine anapotupongeza kutoka moyoni? Tunatiwa moyo na kuchangamka sana. Bila shaka tunahisi kwamba mtu yule alitambua jitihada zetu, na kwamba anatujali. Inatuhakikishia kwamba kile tulichofanya kilikuwa cha maana, na inatutia moyo tujitahidi pia wakati ujao. Si ajabu kwamba mara nyingi sisi huvutiwa na mtu ambaye hutusifu kutoka moyoni na kututia moyo.—Mithali 15:23.

Yesu Kristo alielewa kwamba ni muhimu kuwapongeza wengine. Katika mfano kuhusu talanta, bwana (ambaye ni mfano wa Yesu mwenyewe) anamsifu kwa moyo kila mmoja wa watumwa wawili waaminifu akisema hivi: “Vema, mtumwa mwema na mwaminifu!” Jambo hilo linatia moyo sana! Ijapokuwa watumwa hao walikuwa na vipawa na matokeo tofauti sana, wanasifiwa kwa maneno yaleyale.—Mathayo 25:19-23.

Kwa hiyo, tumkumbuke mamake yule msichana mdogo. Hatupaswi kungoja hadi wengine walie kabla ya kuwapongeza. Badala yake, tunaweza kutafuta fursa za kuwapongeza wengine. Naam, tuna sababu nzuri za kuwapongeza wengine kila inapofaa kufanya hivyo.