Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tulibaki Mahali Tulipotumwa

Tulibaki Mahali Tulipotumwa

Simulizi la Maisha

Tulibaki Mahali Tulipotumwa

LIMESIMULIWA NA HERMANN BRUDER

Nilikuwa na uchaguzi wa kufanya: kujiandikisha katika Kikosi cha Kigeni cha Ufaransa kwa miaka mitano au kufungwa gerezani nchini Morocco. Acha nieleze jinsi nilivyojikuta katika hali hiyo ngumu.

NILIZALIWA huko Oppenau, Ujerumani, mwaka wa 1911, miaka mitatu tu kabla ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu. Wazazi wangu, Joseph na Frida Bruder, walikuwa na wana na binti 17. Mimi nilikuwa mtoto wao wa 13.

Ninakumbuka kwamba niliwatazama wanamuziki wa jeshi wakitembea kwenye barabara kuu iliyopita katikati ya mji wetu nilipokuwa mdogo sana. Nilivutiwa na muziki wao na nikawafuata hadi kituo cha gari-moshi, ambapo nilimwona Baba na wanaume wengine waliokuwa wamevaa mavazi ya jeshi wakiingia kwenye gari-moshi. Gari-moshi lilipoanza safari, baadhi ya wanawake waliokuja kuwaaga wasafiri wakaanza kulia. Muda mfupi baadaye, kasisi wetu alihubiri kwa muda mrefu kanisani na kutaja majina ya wanaume wanne waliokuwa wameuawa vitani walipokuwa wakilinda nchi yetu. “Sasa wamo mbinguni,” alieleza. Mwanamke mmoja aliyesimama karibu nami alizirai.

Baba alishikwa na homa ya matumbo alipokuwa vitani, mpakani mwa Urusi. Alirudi nyumbani akiwa mgonjwa sana na akalazwa hospitalini mara moja. “Enda kwenye kanisa dogo kando ya makaburi, ukatoe Sala ya Bwana mara 50, na sala ya Maria Mtakatifu mara 50,” kasisi akapendekeza. “Ukifanya hivyo, baba yako atapona.” Nilifuata ushauri wake, lakini Baba akafa kesho yake. Ijapokuwa nilikuwa mvulana mdogo tu, vita hiyo iliniletea huzuni kubwa sana.

Jinsi Nilivyopata Kujua Kweli

Ilikuwa vigumu sana kupata kazi Ujerumani kati ya mwaka wa 1919 hadi 1939. Hata hivyo, baada ya kuacha shule mwaka wa 1928, nilipata kazi ya kutunza bustani huko Basel, Uswisi.

Nilikuwa Mkatoliki mwaminifu kama Baba. Lengo langu lilikuwa kutumikia kama mtawa wa dini ya Capuchin huko India. Aliposikia kuhusu miradi yangu, ndugu yangu Richard ambaye alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alisafiri hadi Uswisi ili kujaribu kunizuia nisifuatie miradi hiyo. Alinionya juu ya hatari ya kutumaini wanadamu, hasa makasisi, na akanitia moyo kusoma Biblia na kuitumaini hiyo tu. Ijapokuwa nilikuwa na mashaka, nilinunua Agano Jipya na nikaanza kuisoma. Hatua kwa hatua niligundua kwamba mambo mengi niliyoamini hayakupatana na mafundisho ya Biblia.

Jumapili moja mwaka wa 1933, nilipokuwa nimemtembelea Richard huko Ujerumani, alinijulisha kwa wenzi wa ndoa waliokuwa Mashahidi wa Yehova. Walipojua kwamba nilikuwa nikisoma Biblia, walinipa kijitabu kimoja kilichoitwa The Crisis. * Niliendelea kukisoma hadi usiku wa manane. Nilisadikishwa kwamba nilikuwa nimepata kweli!

Mashahidi wa Yehova huko Basel walinipa vitabu viwili vinavyoitwa Studies in the Scriptures * pamoja na magazeti na vichapo vingine. Nilivutiwa na yale niliyojifunza, kwa hiyo nikamwendea kasisi wa sehemu hiyo, na kumwomba afute jina langu katika orodha ya majina ya wafuasi wa dini. Kasisi huyo alikasirika sana na kunionya kwamba ningepoteza imani yangu. Lakini, sikupoteza imani hata kidogo. Kwa mara ya kwanza maishani, nilikuwa na imani ya kweli.

Akina ndugu huko Basel walikuwa wakipanga kwenda kuhubiri mpakani mwa Ufaransa mwisho-juma huo. Ndugu mmoja alinieleza kwa fadhili kwamba mimi sikuwa nimealikwa kwa sababu nilikuwa nimejiunga na kutaniko hivi majuzi tu. Sikuvunjika moyo, bali nilimwambia kwamba nilitamani sana kuanza kuhubiri. Baada ya kushauriana na mzee mwingine, alinipatia eneo la kuhubiri nchini Uswisi. Mapema Jumapili asubuhi, nilifunga safari ya kwenda kwa baiskeli kwenye kijiji kimoja karibu na Basel. Nilikuwa na vitabu 4, magazeti 28, na broshua 20 katika mkoba wangu wa mahubiri. Wakazi wengi wa kijiji hicho walikuwa kanisani nilipowasili. Hata hivyo, kufikia saa tano asubuhi nilikuwa nimegawa vichapo vyangu vyote.

Nilipowaambia akina ndugu kwamba nilitaka kubatizwa, waliongea nami kwa uzito na kuniuliza maswali ya kindani kuhusu kweli. Nilivutiwa na bidii yao na uaminifu wao kwa Yehova na tengenezo lake. Ilikuwa majira ya baridi kali, kwa hiyo ndugu mmoja alinibatiza katika beseni ya kuogea. Ninakumbuka kwamba nilihisi furaha isiyoelezeka na ujasiri. Nilibatizwa mwaka wa 1934.

Kufanya Kazi Kwenye Shamba la Ufalme

Mwaka wa 1936 nilisikia kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wamenunua shamba nchini Uswisi. Nilijitolea kufanya kazi kwenye shamba hilo. Kwa furaha yangu nilialikwa kufanya kazi kwenye Shamba la Ufalme huko Steffisburg, umbali wa kilometa 30 kutoka Bern. Kila nilipopata nafasi niliwasaidia wengine kufanya kazi zao kwenye shamba hilo. Huko Betheli nilijifunza umuhimu wa kuwa na roho ya kufanya kazi kwa umoja.

Jambo moja muhimu lililotukia nilipokuwa Betheli kwa miaka kadhaa lilikuwa ziara ya Ndugu Rutherford mwaka 1936. Alipoona jinsi nyanya zetu zilivyokuwa kubwa sana na jinsi shamba hilo lilivyotoa mazao mengi, alitabasamu na kufurahi. Tulimpenda Ndugu Rutherford sana!

Nilipokuwa nimetumikia kwenye shamba hilo kwa miaka mitatu hivi, barua kutoka kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Marekani ilisomwa wakati wa kiamsha kinywa. Barua hiyo ilikazia umuhimu wa kazi ya kuhubiri na yeyote aliyetaka kutumikia nchi za kigeni kama painia alikaribishwa kufanya hivyo. Nilijitolea bila kusita. Mwezi wa Mei 1939 nilijulishwa eneo la kuhubiri ambalo nilikuwa nimegawiwa—Brazili!

Wakati huo nilikuwa nikihudhuria mikutano ya Kutaniko la Thun, karibu na Shamba la Ufalme. Kila Jumapili baadhi yetu tulikwenda kuhubiri katika milima ya Alps. Ilichukua saa mbili kufika kwa baiskeli kutoka Thun. Margaritha Steiner alikuwa mmoja wa kikundi hicho. Ghafula nilipata wazo fulani: Yesu alikuwa amewatuma wanafunzi wake wakiwa wawili-wawili. Nilipomtajia Margaritha kwamba nilikuwa nimetumwa Brazili, aliniambia kwamba hata yeye alitamani kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa. Tulioana Julai 31, 1939.

Safari Yakatizwa Bila Kutazamiwa

Mwishoni mwa Agosti 1939, tulianza safari kutoka Le Havre, Ufaransa, kwenda Santos, Brazili, kwa meli. Vyumba vyote vya watu wawili vilikuwa vimechukuliwa, kwa hiyo hatukulala pamoja katika chumba kimoja. Tulipokuwa safarini tulipata habari kwamba nchi za Uingereza na Ufaransa zilikuwa zimetangaza vita dhidi ya Ujerumani. Mara moja abiria 30 Wajerumani wakaanza kuimba wimbo wa taifa wa Ujerumani. Nahodha alikasirika sana hivi kwamba akageuka na kusafiri hadi Safi, Morocco. Abiria wote wenye pasipoti za Ujerumani, kutia ndani sisi, walipewa dakika tano tu kushuka melini.

Tulikaa kwenye kituo cha polisi siku moja, kisha tukawekwa ndani ya basi kuukuu lililojaa watu na kupelekwa hadi gereza moja huko Marrakech, umbali wa kilometa 140. Siku zilizofuata zilikuwa ngumu. Vyumba vya gereza vilijaa watu na vilikuwa vyenye giza. Choo, kilikuwa shimo sakafuni na kilikuwa kimeziba daima. Kila mmoja wetu alipewa gunia chafu la kulalia, na usiku panya waliguguna miguu yetu. Tulipewa chakula mara mbili kwa siku katika mikebe iliyokuwa imeshika kutu.

Ofisa mmoja wa jeshi aliniambia kwamba ningeachiliwa kama ningekubali kujiandikisha katika Kikosi cha Kigeni cha Ufaransa kwa miaka mitano. Niliteswa vikali sana kwa saa 24 nilipokataa. Nilisali karibu muda huo wote.

Baada ya siku nane, wakuu wa gereza waliniruhusu kumwona Margaritha tena. Alikuwa amekonda sana, na hakuweza kuacha kulia. Nilijitahidi kumtia moyo. Tukahojiwa na kuhamishwa kwa gari-moshi hadi Casablanca ambako Margaritha aliachiliwa. Mimi nilipelekwa hadi kambi ya gereza huko Port Lyautey (sasa Kenitra), umbali wa kilometa 180. Balozi wa Uswisi alimshauri Margaritha arudi Uswisi, lakini kwa uaminifu alikataa katakata kuniacha. Kwa muda wa miezi miwili ambayo nilikaa Port Lyautey, alisafiri kila siku kutoka Casablanca ili kunitembelea na kuniletea chakula.

Mwaka mmoja mapema, Mashahidi wa Yehova walikuwa wamechapisha kitabu Kreuzzug gegen das Christentum (Vita Dhidi ya Ukristo) ili kuwajulisha watu kwamba Mashahidi hawakuunga mkono utawala wa Nazi. Nilipokuwa katika kambi hiyo ya gereza, ndugu kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Bern waliwaandikia wenye mamlaka huko Ufaransa, na kuwatumia kitabu hicho, ili kujaribu kuwasadikisha kwamba sisi hatukuwa Wanazi. Margaritha pia alifanya vyema kuwatembelea maofisa wa serikali na kujitahidi kuwasadikisha kwamba hatukuwa na hatia. Hatimaye, mwishoni mwa 1939, tulipewa ruhusa ya kuondoka Morocco.

Baada ya kufunga safari ya kwenda Brazili tena tuliambiwa kwamba nyambizi za Kijerumani zilikuwa zikishambulia meli zilizosafiri katika Bahari ya Atlantiki na kwamba meli yetu ilikuwa shabaha hasa. Ijapokuwa meli yetu iliyoitwa Jamaique ilikuwa ya biashara, ilikuwa na mizinga mbele na nyuma. Nahodha alisafiri kwa kupinda-pinda wakati wa mchana huku akifyatua mizinga. Hatukuwasha taa usiku ili Wajerumani wasione meli yetu. Tulifurahi kama nini tulipowasili hatimaye kwenye bandari ya Santos, Brazili, Februari 6, 1940, zaidi ya miezi mitano baada ya kutoka Ulaya!

Kurudi Gerezani

Eneo letu la kwanza la kuhubiri lilikuwa Montenegro, mji mmoja kusini mwa Brazili katika jimbo la Rio Grande do Sul. Yaelekea wakuu wa kanisa walikuwa wametaarifiwa juu ya kuja kwetu. Baada ya kuhubiri kwa saa mbili tu, polisi walitukamata na kutunyang’anya sahani za santuri zenye mahubiri ya Biblia, vichapo vyetu vyote, na hata mikoba yetu ya mahubiri iliyotengenezwa kwa ngozi ya ngamia ambayo tulikuwa tumenunua Morocco. Kasisi mmoja na mhubiri mmoja aliyeongea Kijerumani walitusubiri kwenye kituo cha polisi. Walisikiliza wakati mkuu wa polisi aliposambaza hotuba moja ya Ndugu Rutherford kwa kutumia santuri ambayo alikuwa ametunyang’anya. Bila shaka Ndugu Rutherford alitaja mambo waziwazi katika hotuba yake! Alipotaja mambo fulani kuhusu Vatikani, kasisi aliondoka ghafula kwa hasira.

Askofu wa Santa Maria aliwaomba polisi watuhamishe hadi Pôrto Alegre, mji mkuu wa jimbo hilo. Baada ya muda mfupi Margaritha aliachiliwa na akamwomba balozi wa Uswisi msaada. Balozi huyo alipendekeza arudi Uswisi. Tena alikataa kuniacha. Margaritha amekuwa mwenzi mwaminifu siku zote. Siku 30 baadaye nilihojiwa na kuachiliwa. Wakuu wa polisi walitupatia uchaguzi: siku kumi za kuondoka katika jimbo au “tukione cha mtema kuni” tusipoondoka. Ndugu kwenye makao makuu huko Brooklyn walipendekeza tuondoke na twende Rio de Janeiro, nasi tukafanya hivyo.

“Tafadhali Soma Ujumbe Huu”

Ijapokuwa kuhubiri kwetu huku Brazili kulianza kwa njia isiyopendeza, bado tulifurahi sana! Kwa vyovyote, tulikuwa hai, mikoba yetu ilijaa tena vichapo, na jiji lote la Rio de Janeiro lilikuwa eneo letu la kuhubiri. Lakini tulihubirije, hali hatukujua Kireno vizuri? Kwa kutumia kadi ya ushuhuda yenye ujumbe ulioandikwa. Maneno ya kwanza ya Kireno ambayo tulijifunza kutumia katika kazi ya kuhubiri yalikuwa: “Por favor, leia este cartão” (“Tafadhali soma ujumbe huu”). Tulitumia kadi hiyo kwa mafanikio sana. Katika mwezi mmoja tu, tuligawa zaidi ya vitabu 1,000. Wengi ambao walikubali vichapo vyetu vya Biblia walikubali kweli baadaye. Kwa kusema kweli, vichapo vyetu vilitoa ushuhuda kwa matokeo mazuri kuliko sisi. Jambo hilo lilinionyesha umuhimu wa kuwagawia wanaopendezwa vichapo vyetu.

Jiji la Rio de Janeiro lilikuwa jiji kuu la Brazili wakati huo, na tulipata matokeo mazuri hasa tulipohubiri katika majengo ya serikali. Nilikuwa na pendeleo la kumtolea waziri wa fedha na waziri wa jeshi ushuhuda. Katika vipindi hivyo niliona wazi jinsi roho ya Yehova ilivyoongoza mambo.

Wakati mmoja, nilipokuwa nikihubiri katika mtaa fulani katikati ya Rio, niliingia katika Jumba la Sheria. Nilijikuta nimeingia katika chumba kimoja na kuzungukwa na wanaume waliokuwa wamevalia mavazi meusi. Ilionekana kana kwamba walikuwa wakifanya sherehe ya mazishi. Nilimkaribia mwanamume mashuhuri na kumpa kadi yangu ya ushuhuda. Hawakuwa wakifanya sherehe ya mazishi. Nilikuwa nimeingilia kesi ya mahakamani, na nilikuwa ninaongea na hakimu. Alicheka na kuwaashiria walinzi wasichukue hatua yoyote. Alikubali kitabu Children * na kutoa mchango. Nilipokuwa nikitoka nje, mmoja wa walinzi alinionyesha alama kubwa kwenye mlango: Proibida a entrada de pessoas estranhas (Hakuna Ruhusa ya Kuingia Hapa).

Bandari lilikuwa eneo lingine lenye matokeo mazuri. Wakati mmoja nilikutana na baharia fulani aliyekubali vichapo kabla ya kusafiri tena. Baadaye tulikutana naye kwenye kusanyiko moja. Familia yake ilikuwa imekubali kweli, naye mwenyewe alikuwa akifanya maendeleo mazuri. Tulifurahi sana.

Hata hivyo, hali haikuwa shwari sikuzote. Muda wa miezi sita ambao tulikuwa tumeruhusiwa kukaa nchini ulimalizika, na tulikabili uwezekano wa kufukuzwa nchini. Baada ya kutuma barua hadi makao makuu na kueleza hali yetu, tulipokea barua kutoka kwa Ndugu Rutherford. Kwa upendo alitutia moyo kuvumilia na kupendekeza jinsi ya kushughulikia hali hiyo. Tulitamani kubaki Brazili, na hatimaye, kwa msaada wa wakili mmoja, tukapata ruhusa ya kudumu mwaka wa 1945.

Tulikaa kwa Muda Mrefu

Hata hivyo, kabla ya hapo, Jonathan, mwana wetu alizaliwa mwaka wa 1941, Ruth mwaka wa 1943, na Esther mwaka wa 1945. Ili kuruzuku familia yangu iliyoongezeka, nilihitaji kuanza kufanya kazi ya kimwili. Margaritha aliendelea katika utumishi wa wakati wote hadi mtoto wetu wa tatu alipozaliwa.

Tangu mwanzo, tulihubiri pamoja kama familia katika mitaa ya jiji, vituo vya gari-moshi, barabarani, na maeneo ya biashara. Kila Jumamosi usiku tuligawa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! tukiwa pamoja. Tulifurahia sana vipindi hivyo.

Kila mtoto alikuwa na kazi zake za kufanya nyumbani. Jonathan alikuwa na daraka la kusafisha jiko la kupikia na jikoni. Wasichana walisafisha friji, walifagia nje ya nyumba, na kung’arisha viatu. Jambo hilo liliwasaidia kuwa wenye utaratibu na kuzoea kufanya mambo bila kuambiwa. Leo, watoto wetu ni wafanyakazi wenye bidii wanaotunza nyumba zao na vitu vyao vizuri, jambo ambalo hunifurahisha mimi na Margaritha sana.

Tulitarajia pia watoto wetu wajiendeshe vizuri mikutanoni. Kabla ya mkutano kuanza, walikunywa maji na kwenda chooni. Wakati wa mkutano tuliketi kwa mfuatano huu, Jonathan, mimi, Ruth, Margaritha, kisha Esther. Jambo hilo liliwasaidia kukaza fikira na kufaidika na chakula cha kiroho mapema maishani mwao.

Yehova amebariki jitihada zetu. Watoto wetu wote wanaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu na kushiriki kwa furaha katika kazi ya kuhubiri. Jonathan ni mzee katika Kutaniko la Novo Méier, Rio de Janeiro.

Kufikia mwaka wa 1970, watoto wetu wote walikuwa wamefunga ndoa na kuondoka nyumbani, kwa hiyo, mimi na Margaritha tukaamua kuhama ili kutumikia mahali ambapo kulikuwa na uhitaji mkubwa. Eneo la kwanza lilikuwa Poços de Caldas, katika Jimbo la Minas Gerais, ambako kulikuwa na kikundi chenye wahubiri 19 wa Ufalme. Nilipoona kwa mara ya kwanza chumba chao cha kukutania, niliudhika sana. Kilikuwa cha chini ya ardhi, bila madirisha, na kilikuwa kimechakaa sana. Tulianza mara moja kutafuta Jumba la Ufalme linalofaa na baada ya muda mfupi tulipata jengo zuri katika eneo bora. Jambo hilo lilileta matokeo mazuri sana! Miaka minne na nusu baadaye, idadi ya wahubiri ilikuwa imeongezeka hadi 155. Mwaka wa 1989, tulihamia Araruama, Rio de Janeiro, ambako tulitumikia kwa muda wa miaka tisa. Katika kipindi hicho makutaniko mapya mawili yalianzishwa.

Tumebarikiwa kwa Sababu Tulibaki Tulikotumwa

Mwaka wa 1998, tulihamia São Gonçalo, Rio de Janeiro, kwa sababu tulikuwa na matatizo ya afya na tulitaka kuwa karibu na watoto wetu. Ningali ninatumikia kama mzee wa kutaniko. Tunajitahidi tuwezavyo kushiriki katika kazi ya kuhubiri kwa ukawaida. Margaritha hufurahia kuwahubiria watu kwenye duka la kujihudumia lililo karibu, na kutaniko limetenga eneo kwa ajili yetu karibu na nyumba yetu ili tuweze kuhubiri kadiri afya yetu inavyoturuhusu.

Mimi na Margaritha tumekuwa watumishi waliojiweka wakfu wa Yehova kwa zaidi ya miaka 60. Sisi wenyewe tumejionea kwamba “wala serikali wala mambo yaliyo hapa sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala kiumbe kingine chochote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 8:38, 39) Na tumefurahia sana kuona jinsi ambavyo “kondoo wengine,” wamekusanywa, ambao wana tumaini zuri ajabu la kuishi milele kwenye dunia kamilifu, wakifurahia uumbaji mzuri wa Mungu! (Yohana 10:16) Tulipowasili Rio de Janeiro mwaka wa 1940, jiji hilo lilikuwa na kutaniko moja tu lenye wahubiri 28. Leo kuna makutaniko 250 na wahubiri wa Ufalme zaidi ya 20,000 huku.

Tulikuwa na nafasi za kurudi Ulaya na kuishi tena pamoja na jamaa zetu huko. Lakini Yehova alitutuma huku Brazili. Tunashukuru sana kwamba tungali tunatumikia huku!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini hakichapishwi tena.

^ fu. 12 Kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini hakichapishwi tena.

^ fu. 33 Kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kwenye Shamba la Ufalme, Steffisburg, Uswisi, mwishoni mwa 1930 (mimi niko kushoto kabisa)

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kabla tu ya arusi yetu, 1939

[Picha katika ukurasa wa 23]

Casablanca katika miaka ya 1940

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kuhubiri pamoja na familia

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kushiriki kwa ukawaida katika huduma leo