Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakristo Wanaodumisha Msimamo wa Kutokuwamo Katika Siku za Mwisho

Wakristo Wanaodumisha Msimamo wa Kutokuwamo Katika Siku za Mwisho

Wakristo Wanaodumisha Msimamo wa Kutokuwamo Katika Siku za Mwisho

“Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.”—YOHANA 17:16.

1, 2. Yesu alisema wafuasi wake wangekuwa na uhusiano gani na ulimwengu, nayo maneno yake hutokeza maswali gani?

USIKU wa mwisho akiwa mwanadamu mkamilifu, Yesu alitoa sala ndefu huku wanafunzi wake wakisikiliza. Katika sala hiyo, alitaja jambo fulani linalohusu maisha ya Wakristo wote wa kweli. Alisema hivi kuhusu wafuasi wake: “Nimewapa wao neno lako, lakini ulimwengu umewachukia, kwa sababu wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu. Nakuomba wewe, si uwachukue kutoka ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu. Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 17:14-16.

2 Yesu alisema mara mbili kwamba wafuasi wake hawangekuwa sehemu ya ulimwengu. Isitoshe, kujitenga na ulimwengu kungetokeza upinzani—ulimwengu ungewachukia. Hata hivyo, Wakristo hawahitaji kuogopa; Yehova atawalinda. (Mithali 18:10; Mathayo 24:9, 13) Kwa kuzingatia maneno ya Yesu, huenda tukauliza: ‘Kwa nini Wakristo wa kweli si sehemu ya ulimwengu? Inamaanisha nini kutokuwa sehemu ya ulimwengu? Ikiwa Wakristo wanachukiwa na ulimwengu, wanauonaje ulimwengu? Wanaonaje hasa serikali za ulimwengu?’ Majibu ambayo Biblia hutoa kwa maswali hayo ni muhimu kwa sababu yanatuhusu sote.

“Twatokana na Mungu”

3. (a) Ni nini hutufanya tujitenge na ulimwengu? (b) Kuna uthibitisho gani kwamba ulimwengu unakaa “katika nguvu ya mwovu”?

3 Jambo moja linalofanya tusiwe sehemu ya ulimwengu ni uhusiano wetu wa karibu pamoja na Yehova. Mtume Yohana aliandika hivi: “Sisi twajua twatokana na Mungu, lakini ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Maneno ya Yohana kuhusu ulimwengu ni ya kweli kabisa. Vita, uhalifu, ukatili, uonevu, ukosefu wa unyofu, na uasherati ambao umeenea sana leo huthibitisha kwamba ulimwengu uko chini ya uwezo wa Shetani, si wa Mungu. (Yohana 12:31; 2 Wakorintho 4:4; Waefeso 6:12) Mtu anapokuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, hatajihusisha na mazoea hayo au kuyakubali, na jambo hilo humfanya asiwe sehemu ya ulimwengu.—Waroma 12:2; 13:12-14; 1 Wakorintho 6:9-11; 1 Yohana 3:10-12.

4. Tunaonyeshaje kwamba sisi ni wa Yehova?

4 Yohana alisema kwamba, tofauti na ulimwengu, Wakristo ‘wanatokana na Mungu.’ Wote wanaojiweka wakfu kwa Yehova wanakuwa watu wake. Mtume Paulo alisema: “Kwa maana tukiishi, twaishi kwa Yehova, na tukifa, twafa kwa Yehova pia. Kwa hiyo tukiishi na tukifa pia, sisi ni wa Yehova.” (Waroma 14:8; Zaburi 116:15) Kwa kuwa sisi ni wa Yehova, tunamwabudu yeye pekee. (Kutoka 20:4-6) Kwa hiyo Mkristo wa kweli hatumii maisha yake yote kufuatia miradi ya kilimwengu. Na ingawa anaheshimu nembo za kitaifa kama vile bendera, yeye haziabudu kwa matendo au katika moyo. Bila shaka, haabudu wachezaji maarufu au watu wengine wa kisasa walio maarufu. Bila shaka, anaheshimu haki ya wengine ya kufanya watakavyo, lakini yeye humwabudu Muumba pekee. (Mathayo 4:10; Ufunuo 19:10) Jambo hilo pia humfanya ajitenge na ulimwengu.

“Ufalme Wangu Si Sehemu ya Ulimwengu Huu”

5, 6. Kujitiisha kwa Ufalme wa Mungu hututengaje na ulimwengu?

5 Jambo jingine ambalo hufanya Wakristo wasiwe sehemu ya ulimwengu ni kwamba wao ni wafuasi wa Kristo Yesu na raia wa Ufalme wa Mungu. Yesu alipokuwa akihukumiwa mbele ya Pontio Pilato, alisema: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, mahadimu wangu wangalipigana ili nisikabidhiwe kwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu si kutoka chanzo hiki.” (Yohana 18:36) Yehova atatumia Ufalme huo kutakasa jina lake, kuondolea lawama enzi yake, na kufanya mapenzi yake duniani kama ilivyo mbinguni. (Mathayo 6:9, 10) Katika huduma yake yote, Yesu alihubiri habari njema za Ufalme na kusema kwamba habari hizo zingehubiriwa na wafuasi wake hadi mwisho wa mfumo wa mambo. (Mathayo 4:23; 24:14) Mnamo mwaka wa 1914, maneno ya kiunabii ya Ufunuo 11:15 yalitimizwa: “Ufalme wa ulimwengu ulipata kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atatawala akiwa mfalme milele na milele.” Hivi karibuni, Ufalme huo wa mbinguni utakuwa serikali pekee itakayotawala wanadamu. (Danieli 2:44) Wakati utafika ambapo hata viongozi wa ulimwengu watalazimika kukiri mamlaka ya Ufalme huo.—Zaburi 2:6-12.

6 Kwa kuzingatia mambo hayo, Wakristo wa kweli leo ni raia wa Ufalme wa Mungu, nao hutii shauri la Yesu la ‘kufuliza kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wa Mungu.’ (Mathayo 6:33) Hilo halifanyi wasitii sheria za nchi wanamoishi, bali huwafanya wajitenge na ulimwengu kwa njia ya kiroho. Kazi iliyo muhimu zaidi kwa Wakristo leo, kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, ni “kutoa ushahidi kamili kuhusiana na ufalme wa Mungu.” (Matendo 28:23) Hakuna serikali ya kibinadamu iliyo na haki ya kuzuia kazi hiyo ambayo Mungu amesema ifanywe.

7. Kwa nini Wakristo wa kweli hudumisha msimamo wa kutokuwamo, nao wameonyeshaje hivyo?

7 Kwa kuwa Mashahidi ni watu wa Yehova na pia ni wafuasi wa Yesu na raia wa Ufalme wa Mungu, wamedumisha msimamo wa kutokuwamo katika vita vya mataifa na kimataifa katika karne ya 20 na ya 21. Hawaungi mkono upande wowote wa vita, hawatumii silaha dhidi ya mtu yeyote, na hawaenezi habari zisizo za kweli ili kuendeleza mradi fulani wa kilimwengu. Kwa kudhihirisha imani yao kwa njia ya pekee licha ya upinzani mkali sana, wamefuata kanuni walizoelezwa watawala wa Ujerumani ya Nazi mwaka wa 1934: “Hatupendezwi na mambo ya kisiasa, lakini tumejitoa kabisa kwa ajili ya ufalme wa Mungu chini ya Mfalme wake, Kristo. Hatutamdhuru mtu yeyote. Tungependa kuishi kwa amani na kuwatendea watu wote mema tunapopata fursa.”

Mabalozi na Wajumbe wa Kristo

8, 9. Mashahidi wa Yehova leo ni mabalozi na wajumbe jinsi gani, na hilo huathirije uhusiano wao na mataifa?

8 Paulo alisema kwamba yeye pamoja na Wakristo wenzake watiwa-mafuta ni ‘mabalozi walio badala ya Kristo, kama kwamba Mungu alikuwa akisihi sana kupitia wao.’ (2 Wakorintho 5:20; Waefeso 6:20) Tangu mwaka wa 1914, Wakristo watiwa-mafuta wanaweza kuitwa kwa kufaa mabalozi wa Ufalme wa Mungu, nao ni “wana” wa Ufalme huo. (Mathayo 13:38; Wafilipi 3:20; Ufunuo 5:9, 10) Isitoshe, Yehova amekusanya kutoka kwa mataifa “umati mkubwa” wa “kondoo wengine,” yaani Wakristo wenye tumaini la kuishi duniani, ili kuwasaidia wana watiwa-mafuta katika kazi yao ya ubalozi. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) ‘Kondoo hao wengine’ wanaweza kuitwa “wajumbe” wa Ufalme wa Mungu.

9 Balozi na wafanyakazi wake hawaingilii mambo ya nchi wanakotumikia. Vivyo hivyo, Wakristo hawaingilii mambo ya kisiasa ya mataifa ya ulimwengu. Hawapendelei wala kubagua watu kwa sababu ya taifa lao, jamii, au hali yao ya kiuchumi. (Matendo 10:34, 35) Badala yake, ‘wanafanya lililo jema kuelekea wote.’ (Wagalatia 6:10) Kwa kuwa Mashahidi wa Yehova hudumisha msimamo wa kutokuwamo, hakuna mtu ambaye kwa haki anaweza kukataa ujumbe wao akidai kwamba anaunga mkono jamii, taifa, au kabila fulani.

Wanatambulishwa kwa Upendo

10. Upendo ni muhimu kadiri gani kwa Mkristo?

10 Pamoja na mambo yaliyotangulia kutajwa, Wakristo hudumisha msimamo wa kutokuwamo katika mambo ya ulimwengu kwa sababu ya uhusiano wao na Wakristo wengine. Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Upendo wa kidugu ni muhimu sana kwa Mkristo. (1 Yohana 3:14) Mkristo ana uhusiano wa karibu pamoja na Wakristo wengine kwa kuwa hilo linahusisha uhusiano wake pamoja na Yehova na Yesu. Haonyeshi upendo wake kwa washiriki wa kutaniko lake tu, bali pia kwa “ushirika mzima wa ndugu [zake] katika ulimwengu.”—1 Petro 5:9.

11. Upendo uliopo miongoni mwa Mashahidi wa Yehova umekuwa na matokeo gani juu ya mwenendo wao?

11 Leo, Mashahidi wa Yehova hudhihirisha upendo wao wa kidugu kwa kutimiza maneno ya Isaya 2:4: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Kwa sababu ya kufundishwa na Yehova, Wakristo wa kweli wanafurahia amani pamoja naye na pia miongoni mwao wenyewe. (Isaya 54:13) Kwa sababu wanampenda Mungu na ndugu zao, hawawezi kutumia silaha dhidi ya Wakristo wenzao—au mtu mwingine—katika nchi nyingine. Amani na umoja walio nao ni sifa muhimu katika ibada yao, nazo huonyesha kwamba kwa kweli wana roho ya Mungu. (Zaburi 133:1; Mika 2:12; Mathayo 22:37-39; Wakolosai 3:14) Wao hujitahidi ‘kutafuta amani na kuifuatia,’ wakijua kwamba “macho ya BWANA huwaelekea wenye haki.”—Zaburi 34:14, 15.

Jinsi Wakristo Wanavyouona Ulimwengu

12. Mashahidi wa Yehova huiga mtazamo gani wa Yehova kuelekea watu wa ulimwengu, na wanafanya hivyo jinsi gani?

12 Yehova ametangaza hukumu kali dhidi ya ulimwengu huu, lakini bado hajahukumu watu wote ulimwenguni. Atawahukumu kupitia Yesu katika wakati Wake unaofaa. (Zaburi 67:3, 4; Mathayo 25:31-46; 2 Petro 3:10) Kwa sasa, anaonyesha upendo mwingi kwa wanadamu. Hata alimtoa Mwana wake mzaliwa-pekee ili kila mtu aweze kupata fursa ya kupokea uhai udumuo milele. (Yohana 3:16) Tukiwa Wakristo, tunaiga upendo wa Mungu kwa kuwaeleza wengine kuhusu maandalizi ya wokovu, hata ikiwa mara nyingi jitihada zetu za kufanya hivyo hukataliwa.

13. Tunapaswa kuwaonaje watawala wa ulimwengu?

13 Tunapaswa kuwaonaje watawala wa ulimwengu? Paulo alijibu swali hilo alipoandika hivi: “Acheni kila nafsi iwe katika ujitiisho kwa mamlaka zilizo kubwa, kwa maana hakuna mamlaka ila kwa njia ya Mungu; mamlaka zilizopo zimesimama zikiwa zimewekwa na Mungu katika mahali pa vyeo vyazo vyenye kuhusu.” (Waroma 13:1, 2) Wanadamu wana vyeo vya mamlaka “vyenye kuhusu” (vyeo fulani ni vikubwa kuliko vingine, lakini vyote ni vidogo vikilinganishwa na cheo cha Yehova) kwa sababu Mweza Yote anawaruhusu wawe navyo. Mkristo hujitiisha kwa mamlaka ya ulimwengu kwa sababu kufanya hivyo kunahusisha kumtii Yehova. Hata hivyo, namna gani matakwa ya serikali ya kibinadamu yakipingana na matakwa ya Mungu?

Sheria ya Mungu na ya Kaisari

14, 15. (a) Danieli aliwezaje kuepuka hali yenye kutatanisha kuhusu utii? (b) Waebrania watatu walichukua msimamo gani wakati hali yenye kutatanisha kuhusu utii haingeweza kuepukwa?

14 Danieli na wenzake watatu wanaweka kielelezo kizuri cha kuonyesha usawaziko katika kutii serikali za wanadamu na kutii mamlaka ya Mungu. Wakati Waebrania hao wanne walipojikuta uhamishoni Babiloni, walitii sheria za nchi hiyo na mara moja wakachaguliwa ili wapewe mazoezi ya pekee. Danieli alipotambua kwamba mazoezi hayo yangeweza kupingana na Sheria ya Yehova, alizungumzia jambo hilo na maofisa waliohusika. Kwa hiyo, mipango hususa ikafanywa kwa kuzingatia dhamiri za Waebrania hao wanne. (Danieli 1:8-17) Mashahidi wa Yehova huiga kielelezo cha Danieli wanapoeleza kwa busara msimamo wao mbele ya maofisa ili waepuke matatizo yasiyo ya lazima.

15 Hata hivyo, pindi fulani baadaye, hali yenye kutatanisha kuhusu utii haingeweza kuepukwa. Mfalme wa Babiloni alisimamisha sanamu kubwa kwenye uwanda wa Dura na kuwaamuru maofisa wa ngazi za juu, kutia ndani wasimamizi wa wilaya za utawala, wakusanyike pamoja wakati wa mzinduo. Wakati huo, marafiki watatu wa Danieli walikuwa wameteuliwa kuwa wasimamizi wa wilaya ya utawala ya Babiloni, kwa hiyo walihitaji kutii amri hiyo. Wakati fulani sherehe hiyo ilipokuwa ikiendelea, wote waliokusanyika walipaswa kuinamia sanamu hiyo. Lakini Waebrania hao walijua kwamba kufanya hivyo kungepingana na sheria ya Mungu. (Kumbukumbu la Torati 5:8-10) Kwa hiyo waliendelea kusimama, kila mtu alipoinama. Wangeuawa kikatili kwa sababu ya kutotii amri ya mfalme, lakini waliokolewa kimuujiza tu; waliona ni afadhali kufa kuliko kutomtii Yehova.—Danieli 2:49–3:29.

16, 17. Mitume walisemaje walipoamriwa waache kuhubiri, na kwa nini?

16 Katika karne ya kwanza, mitume wa Yesu Kristo waliitwa mbele ya viongozi Wayahudi huko Yerusalemu na kuamriwa waache kuhubiri katika jina la Yesu. Walifanya nini? Yesu ‘alikuwa amewaagiza wafanye wanafunzi kutoka kwa mataifa yote, kutia ndani Yudea. Pia aliwaambia wawe mashahidi wake katika Yerusalemu na vilevile sehemu zote za dunia. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8) Mitume hao walijua kwamba kutimiza amri za Yesu kulikuwa sawa na kufanya mapenzi ya Mungu. (Yohana 5:30; 8:28) Kwa hiyo, walisema: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 4:19, 20; 5:29.

17 Mitume hawakuwa waasi. (Mithali 24:21) Hata hivyo, watawala wa kibinadamu walipowakataza wasifanye mapenzi ya Mungu, walisema, ‘Lazima tumtii Mungu, si mwanadamu.’ Yesu alisema kwamba tunapaswa ‘kulipa Kaisari vitu vya Kaisari, lakini tumlipe Mungu vitu vya Mungu.’ (Marko 12:17) Tukivunja amri ya Mungu kwa sababu mwanadamu fulani anatuambia tufanye hivyo, tutakuwa tumempa mwanadamu vitu vya Mungu. Badala ya kufanya hivyo, tumlipe Kaisari vitu vyake vyote, lakini tutambue mamlaka kuu ya Yehova. Yeye ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu, Muumba, Chanzo cha mamlaka.—Ufunuo 4:11.

Tutasimama Imara

18, 19. Ndugu wengi wamechukua msimamo gani mzuri, nasi tunawezaje kufuata kielelezo chao?

18 Wakati wa sasa, serikali nyingi zinatambua msimamo wa kutokuwamo wa Mashahidi wa Yehova, nasi tunashukuru kwa sababu hiyo. Hata hivyo, katika nchi fulani, Mashahidi wamepingwa vikali. Katika karne ya 20 na hata sasa, baadhi ya ndugu na dada zetu wamepambana vikali wakipigana kwa njia ya kiroho “pigano bora la imani.”—1 Timotheo 6:12.

19 Tunawezaje kusimama imara kama wao? Kwanza, tunakumbuka kwamba lazima tutazamie upinzani. Hatupaswi kushtuka au hata kushangaa upinzani unapotokea. Paulo alimwonya Timotheo hivi: “Wote wale wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watanyanyaswa pia.” (2 Timotheo 3:12; 1 Petro 4:12) Tutakosaje kupingwa katika ulimwengu unaotawalwa na Shetani? (Ufunuo 12:17) Maadamu sisi ni waaminifu, watu fulani ‘watatatanishwa na kuendelea kutusema kwa maneno yenye kuudhi.’—1 Petro 4:4.

20. Tunakumbushwa kweli gani yenye kuimarisha?

20 Pili, tunasadiki kwamba Yehova na malaika zake watatutegemeza. Kama Elisha wa kale alivyosema, “walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao.” (2 Wafalme 6:16; Zaburi 34:7) Huenda ikawa Yehova huruhusu tuendelee kupingwa kwa muda akiwa na kusudi zuri. Hata hivyo, atatupatia nguvu tunazohitaji ili kuvumilia. (Isaya 41:9, 10) Wengine wameuawa, lakini hilo halituogopeshi. Yesu alisema: “Msiwe wenye kuwahofu wale wauuao mwili lakini hawawezi kuiua nafsi; lakini badala ya hivyo mhofuni yeye awezaye kuangamiza vyote viwili nafsi na mwili katika Gehena.” (Mathayo 10:16-23, 28) Sisi ni “wakazi wa muda” tu katika mfumo huu wa mambo. Tunatumia wakati wetu hapa ‘tupate kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi,’ uhai udumuo milele katika dunia mpya ya Mungu. (1 Petro 2:11; 1 Timotheo 6:19) Hakuna mwanadamu anayeweza kutunyima thawabu hiyo maadamu tunadumu tukiwa waaminifu kwa Mungu.

21. Tunapaswa kukumbuka nini daima?

21 Kwa hiyo, na tukumbuke uhusiano wetu wenye thamani pamoja na Yehova Mungu. Sikuzote na tuthamini faida tunazopata kwa kuwa wafuasi wa Kristo na raia wa Ufalme. Na tuwapende ndugu zetu kwa moyo wote, sikuzote na tufurahie upendo wanaotuonyesha. Zaidi ya yote, na tutii maneno ya mtunga-zaburi: “Umngoje BWANA, uwe hodari, upige moyo konde, naam, umngoje BWANA.” (Zaburi 27:14; Isaya 54:17) Kisha, kama vile Wakristo walioishi kabla yetu tutaweza kusimama imara tukiwa na tumaini hakika—Wakristo waaminifu wanaodumisha msimamo wa kutokuwamo katika ulimwengu.

Je, Unaweza Kueleza?

• Uhusiano wetu pamoja na Yehova hututengaje na ulimwengu?

• Tukiwa raia wa Ufalme wa Mungu, tunadumishaje msimamo wa kutokuwamo katika ulimwengu huu?

• Ni katika njia zipi kuwapenda ndugu zetu hufanya tudumishe msimamo wa kutokuwamo na kujitenga na ulimwengu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kunyenyekea Ufalme wa Mungu kunaathirije uhusiano wetu na ulimwengu?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Mhutu na Mtutsi wakifanya kazi pamoja kwa furaha

[Picha katika ukurasa wa 17]

Ndugu wa Kikristo Wayahudi na Waarabu

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wakristo Waserbia, Wabosnia, na Wakroatia wanafurahia ushirika pamoja

[Picha katika ukurasa wa 18]

Tunapaswa kuchukua hatua gani inayofaa watawala wanapotuamuru tuvunje amri ya Mungu?