Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Waliounga Mkono Ibada ya Kweli Zamani za Kale na Leo

Watu Waliounga Mkono Ibada ya Kweli Zamani za Kale na Leo

Watu Waliounga Mkono Ibada ya Kweli Zamani za Kale na Leo

JE, UNAKUMBUKA jina la mwanamume fulani aliyelilia jiji la kale la Yerusalemu? Huenda ukajibu ‘Yesu,’ na ni kweli kwamba Yesu alifanya hivyo. (Luka 19:28, 41) Hata hivyo, karne nyingi kabla ya Yesu kuja duniani, mtumishi mwingine mwaminifu wa Mungu alililia Yerusalemu. Jina lake ni Nehemia.—Nehemia 1:3, 4.

Ni nini kilichomfanya Nehemia ahuzunike kiasi cha kwamba alililia Yerusalemu? Alifanyia jiji hilo na wakazi wake nini? Na tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wake? Ili kupata majibu, tujikumbushe mambo kadhaa yaliyotukia siku zake.

Mwanamume Mtendaji na Mwenye Huruma

Nehemia aliwekwa kuwa liwali wa Yerusalemu, lakini kabla ya hapo, alikuwa afisa mkuu katika jumba la Mfalme wa Uajemi jijini Shushani. Ijapokuwa aliishi maisha ya starehe, bado aliwahangaikia ndugu zake Wayahudi waliokuwa mbali huko Yerusalemu. Kwa kweli, wakati kikundi cha Wayahudi kutoka Yerusalemu walipotembelea Shushani, mara moja ‘aliwauliza habari za Wayahudi waliopona, hao watu wa uhamisho waliosalia; na habari za Yerusalemu.’ (Nehemia 1:2) Wageni hao walipojibu kwamba watu wa Yerusalemu walikuwa “katika hali ya dhiki nyingi” na kwamba ukuta wa jiji ulikuwa “umebomolewa,” Nehemia ‘aliketi, akalia, akaomboleza siku kadha wa kadha.’ Baada ya hapo alitoa sala kutoka moyoni na kumweleza Yehova huzuni yake. (Nehemia 1:3-11) Kwa nini Nehemia alikuwa na huzuni sana kiasi hicho? Kwa sababu jiji la Yerusalemu, lililokuwa kituo cha ibada ya Yehova duniani, lilikuwa limeharibika. (1 Wafalme 11:36) Isitoshe, hali ya jiji hilo ilionyesha kwamba wakazi wake hawakuwa na hali nzuri ya kiroho.—Nehemia 1:6, 7.

Nehemia alijitolea kusaidia kwa sababu alihangaikia Yerusalemu na aliwahurumia Wayahudi walioishi huko. Mfalme wa Uajemi alipomruhusu kuchukua likizo, mara moja Nehemia alifunga safari ndefu ya kwenda Yerusalemu. (Nehemia 2:5, 6) Alitaka kutumia nguvu zake, wakati wake, na vipawa vyake katika kazi ya kujenga upya ukuta. Siku chache baada ya kuwasili, tayari alikuwa amepanga jinsi ya kujenga upya ukuta wote wa Yerusalemu.—Nehemia 2:11-18.

Nehemia aliwagawia watu wa familia mbalimbali sehemu ya kazi hiyo kubwa ya kujenga upya ukuta, nao wakaifanya bega kwa bega. * Zaidi ya vikundi 40 tofauti vilipewa kazi ya kujenga upya “sehemu” mbalimbali za ukuta. Matokeo yakawa nini? Kazi hiyo ambayo ilionekana kuwa kubwa mno iliweza kukamilishwa kwa sababu wafanyakazi wengi sana, kutia ndani wazazi pamoja na watoto, walijitolea kutumia wakati na nguvu zao. (Nehemia 3:11, 12, 19, 20) Baada ya kujenga kwa bidii kwa muda wa miezi miwili, walimaliza kujenga upya ukuta wote! Nehemia aliandika kwamba hata wale waliokuwa wamepinga kazi ya kujenga upya ukuta walilazimika kutambua kwamba ‘kazi hiyo ilitendwa na Mungu wetu.’—Nehemia 6:15, 16.

Mfano Tunaopaswa Kukumbuka

Nehemia hakutumia tu wakati na ustadi wake wa kupanga mambo. Alitumia pia mali zake ili kuendeleza ibada ya kweli. Alitumia fedha zake kuwatoa ndugu zake Wayahudi utumwani. Alikopesha fedha bila faida. Hakuwawekea Wayahudi mzigo “mzito” kwa kudai posho lake kama liwali, jambo ambalo lilikuwa haki yake. Badala yake, alikuwa mkarimu, akawalisha “watu mia na hamsini, zaidi ya wale waliotujia kutoka makafiri waliotuzunguka.” Kila siku aliwaandalia wageni wake ‘ng’ombe mmoja, na kondoo wazuri sita; tena kuku.’ Isitoshe, kila baada ya siku kumi aliwapa “akiba ya mvinyo ya namna zote.” Naye ndiye aliyelipa gharama za vitu hivyo.—Nehemia 5:8, 10, 14-18.

Nehemia alionyesha mfano mzuri wa ukarimu kwa watumishi wote wa Mungu wakati wake na hata sasa. Mtumishi huyo jasiri wa Mungu alitumia kwa hiari na kwa ukarimu mali zake kuwaunga mkono wafanya-kazi ili kuendeleza ibada ya kweli. Kwa kufaa, aliweza kumwomba Yehova hivi: ‘Ukumbuke, Ee Mungu wangu, kwa mema, yote niliyowafanyia watu hawa.’ (Nehemia 5:19) Bila shaka Yehova atafanya hivyo.—Waebrania 6:10.

Mfano wa Nehemia Hufuatwa Leo

Tunatiwa moyo kuona kwamba watu wa Yehova leo wanaonyesha huruma na bidii iyo hiyo, na mwelekeo wa kujitoa kwa ajili ya ibada ya kweli. Tunaposikia kwamba waamini wenzetu hupitia magumu, tunawahangaikia sana. (Waroma 12:15) Kama Nehemia, tunamwendea Yehova kwa sala na kuwaombea ndugu zetu wa kiroho wanaoteseka: “Nakusihi, litege sikio lako, uyasikilize maombi ya mtumishi wako, na maombi ya watumishi wako, wanaofurahi kulicha jina lako.”—Nehemia 1:11; Wakolosai 4:2.

Hata hivyo, mahangaiko yetu juu ya hali ya kiroho na ya kimwili ya ndugu zetu Wakristo na juu ya ibada ya kweli hayahusishi hisia zetu tu, bali hutusukuma kutenda. Kama Nehemia, wale ambao hali yao inawaruhusu husukumwa na upendo kuacha nchi zao na kuhamia sehemu nyingine ili kuwasaidia wanaohitaji msaada. Bila kukata tamaa kwa sababu ya hali ngumu ya maisha ambayo watu hao wanaojitolea hukabili katika sehemu nyingine za dunia, wao huendeleza ibada ya kweli huku wakitumikia pamoja na ndugu zao Wakristo. Wanastahili kupongezwa kwa sababu ya roho yao ya kujidhabihu.

Kusaidia Mahali Tulipo

Ni wazi kwamba, wengi wetu hatuwezi kuhamia sehemu nyingine. Sisi huunga mkono ibada ya kweli mahali tunapoishi. Jambo hilo linaonyeshwa pia katika kitabu cha Nehemia. Ona jambo lingine ambalo Nehemia anasema juu ya baadhi ya watu waaminifu walioshiriki katika kazi ya kujenga upya ukuta. Aliandika hivi: ‘Sehemu inayofuata, inayokabiliana na nyumba yake ilijengwa upya na Yedaya, mwana wa Harumafu . . . Benyamini na Hashubu, walijenga upya sehemu inayokabiliana na nyumba yake. Azaria, mwana wa Maaseia, mwana wa Anania, alijenga upya sehemu inayokabiliana na nyumba yao.” (Nehemia 3:10, 23, 28-30, Biblia Habari Njema, italiki ni zetu.) Wanaume hao na familia zao walichangia sana ibada ya kweli kwa kufanya kazi ya kujenga upya sehemu ya ukuta iliyokuwa karibu na nyumba zao.

Leo, wengi wetu huunga mkono ibada ya kweli katika ujirani wetu kwa njia mbalimbali. Sisi hushiriki katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme, husaidia wakati wa msiba, na hasa katika kazi ya kuhubiri Ufalme. Huenda ikawa sisi wenyewe hatuwezi kushiriki katika ujenzi au kusaidia mahali palipo na msiba. Lakini sisi sote hutamani kwa moyo wote kuunga mkono ibada ya kweli kwa kutoa mali zetu, kama vile Nehemia alivyofanya kwa ukarimu.—Ona sanduku “Jinsi ya Kutoa Michango ya Hiari.”

Nyakati nyingine huenda ikaonekana kwamba fedha za kutosha hazitapatikana ili kulipa uchapishaji wetu unaoongezeka, misaada, na huduma nyingine nyingi zinazotolewa duniani pote. Hata hivyo, kumbuka pia kwamba ilionekana kuwa kazi ya kujenga upya ukuta wa Yerusalemu ingeshindwa. (Nehemia 4:10) Lakini, kazi hiyo ilikamilishwa kwa sababu watu wa familia nyingi walikuwa na moyo wa kusaidia. Ndivyo ilivyo leo, fedha nyingi zinazohitajika ili kuendesha kazi yetu ya ulimwenguni pote zitapatikana iwapo kila mmoja wetu atatimiza sehemu yake.

Sanduku “Jinsi Ambavyo Wengine Hutoa Michango” linaonyesha njia kadhaa za kutoa michango ya hiari kwa ajili ya kazi ya Ufalme. Katika mwaka uliopita, wengi kati ya watu wa Mungu walitoa michango, na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova linawashukuru sana wote ambao walisukumwa na moyo wao kutoa kwa hiari. Zaidi ya yote, tunamshukuru Yehova kwa kubariki sana jitihada za moyo wote za watu wake za kuendeleza ibada ya kweli duniani pote. Naam, tunapotafakari jinsi ambavyo Yehova ametuongoza kwa miaka mingi, tunasukumwa kusema kama Nehemia aliyeshukuru kwa kusema hivi: ‘Mkono wa Mungu wangu ulikuwa mwema juu yangu.’—Nehemia 2:18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Andiko la Nehemia 3:5 linasema kwamba baadhi ya Wayahudi mashuhuri, “wakuu,” walikataa kusaidia kufanya kazi hiyo, lakini wengine wote waliiunga mkono. Watu wa malezi mbalimbali kama vile makuhani, mafundi wa dhahabu, mafundi wa manukato, wakuu, na wafanya-biashara, waliunga mkono mradi huo.—Mistari ya 1, 8, 9, 32.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Jinsi Ambavyo Wengine Hutoa Michango

MICHANGO KWA AJILI YA KAZI YA ULIMWENGUNI POTE

Wengi hutenga kiasi fulani cha pesa ambacho wao hutia katika masanduku ya michango yenye alama “Michango kwa Ajili ya Kazi ya Ulimwenguni Pote—Mathayo 24:14.”

Kila mwezi, makutaniko hutuma pesa hizo kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova au kwenye ofisi ya tawi ya nchi yao. Michango ya hiari ya pesa inaweza kutumwa moja kwa moja kwenye Treasurer’s Office, Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, 25 Columbia Heights, Brooklyn, New York 11201-2483, au kwenye ofisi ya tawi ya nchi yenu. Vito au vitu vingine vyenye thamani vinaweza kuchangwa vilevile. Barua fupi inayoonyesha kwamba vitu hivyo ni zawadi ya moja kwa moja inapaswa kuambatanishwa na michango hiyo.

MPANGO WA MICHANGO YENYE MASHARTI

Pesa zinaweza kuchangwa kukiwa na mpango wa kwamba iwapo mtoaji atakuwa na uhitaji wa pekee, pesa hizo zinaweza kurudishwa. Kwa habari zaidi, tafadhali wasiliana na Treasurer’s Office kwa kutumia anwani iliyoonyeshwa hapa juu.

UTOAJI ULIOPANGWA

Mbali na zawadi za moja kwa moja za pesa au vitu vyenye thamani na michango yenye masharti, kuna njia nyinginezo za kutoa kwa ajili ya kazi ya Ufalme duniani pote. Hizo zinatia ndani:

Bima: Watch Tower Society inaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa hati ya bima ya maisha au wa malipo ya kustaafu kazi au ya uzeeni.

Akiba za Benki: Akaunti za benki, hati za amana, au akiba za pesa za kustaafu za mtu mmoja-mmoja zaweza kuwekwa zikiwa amana, au kulipwa wakati wa kifo, kwa Watch Tower Society, kulingana na matakwa ya benki za kwenu.

Hisa na Dhamana: Hisa na dhamana zinaweza kuchangwa kwa Watch Tower Society zikiwa zawadi ya moja kwa moja.

Ardhi na Nyumba: Ardhi au nyumba zinazoweza kuuzwa zinaweza kuchangwa kwa Watch Tower Society zikiwa zawadi ya moja kwa moja au zawadi yenye sharti, yaani, mtoaji anaweza kuendelea kuishi humo hadi kifo chake. Julisha ofisi ya tawi katika nchi yako kabla ya kuchanga ardhi au nyumba.

Malipo-Mwaka: Huo ni mpango wa kutoa pesa, hisa na amana, ziwe mali za Watch Tower Society. Yule anayetoa mchango huo, au mtu fulani aliyechaguliwa na mtoaji, hupata kiasi fulani cha pesa kila mwaka maishani mwake. Mtoaji hupunguziwa kodi ya serikali mwaka ule ambapo mpango huo unaanzishwa.

Wasia na Amana: Watch Tower Society inaweza kuachiwa urithi wa mali au pesa kwa njia ya wasia halali, au Watch Tower Society inaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mkataba wa amana. Kuwa na amana inayofaidi tengenezo la kidini kunaweza kupunguza kwa kiasi fulani kodi ambayo hutozwa na serikali.

Kama vile usemi “utoaji uliopangwa” unavyodokeza, michango ya aina hii kwa kawaida hutaka mtoaji afanye mipango hususa. Watch Tower Society imetayarisha broshua ya Kiingereza na Kihispania yenye kichwa Charitable Planning to Benefit Kingdom Service Worldwide, ili kuwasaidia watu wanaotamani kuendeleza kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kwa njia ya utoaji uliopangwa. Broshua hiyo iliandikwa ili kujibu maswali mengi yaliyopokewa kuhusu zawadi, wasia, na amana. Pia ina habari za ziada zenye mafaa juu ya mipango ya ardhi na nyumba, pesa, na kodi. Inawajulisha watu kuhusu njia mbalimbali za kutoa zawadi sasa au kama urithi mtu anapokufa. Unaweza kupata broshua hiyo kwa kuiomba moja kwa moja kutoka kwenye Charitable Planning Office.

Baada ya kusoma broshua hiyo na kushauriana na Charitable Planning Office, watu wengi wameweza kuwasaidia Mashahidi wa Yehova kotekote duniani, na wakati uleule kupunguziwa kodi kwa sababu ya kufanya hivyo. Charitable Planning Office inapaswa kujulishwa na kupokea hati yoyote ile inayohusiana na yoyote ya mipango hiyo. Ikiwa unapendezwa na mojawapo ya mipango hiyo ya utoaji, unapaswa kuwasiliana na Charitable Planning Office, ama kwa kuandika ama kwa kupiga simu, kwenye anwani iliyoonyeshwa hapa chini, ama kwenye ofisi ya tawi ya nchi yako.

Mashahidi wa Yehova

Box 47788

00100 Nairobi GPO

Kenya

Simu: (02) 573211

[Sanduku katika ukurasa wa 30]

Jinsi ya Kutoa Michango ya Hiari

Katika barua yake kwa Wakorintho, mtume Paulo alitaja mambo matatu muhimu kuhusiana na kutoa michango ya hiari. (1) Alipoandika kuhusu kuchanga fedha, Paulo alitoa agizo hili: “Kila siku ya kwanza ya juma acheni kila mmoja wenu kwenye nyumba yake mwenyewe aweke kando kitu fulani.” (1 Wakorintho 16:2a) Kwa hiyo, kutoa michango kunapaswa kupangwa kimbele, na kufanywa kwa ukawaida. (2) Paulo aliandika pia kwamba kila mtu alipaswa kutoa “kadiri ya mapato yake.” (1 Wakorintho 16:2b, BHN) Yaani, mtu anayetaka kutoa kwa hiari anaweza kufanya hivyo kulingana na uwezo wake. Hata ingawa Mkristo ana mapato ya chini, kiasi kidogo anachoweza kuchanga kinathaminiwa na Yehova. (Luka 21:1-4) (3) Paulo aliongeza hivi: “Acheni kila mmoja afanye kama vile ameazimia moyoni mwake, si kwa kinyongo au kwa shurutisho, kwa maana Mungu hupenda mpaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Wakristo wa kweli hutoa kwa moyo na kwa furaha.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nehemia alikuwa mwanamume mtendaji na mwenye huruma

[Picha katika ukurasa wa 30]

Michango ya hiari hutumiwa kuendeleza uchapishaji, kutoa misaada wakati wa misiba, kujenga Majumba ya Ufalme, na huduma nyinginezo zenye faida kotekote duniani