Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endeleeni Kutumikia Bega kwa Bega

Endeleeni Kutumikia Bega kwa Bega

Endeleeni Kutumikia Bega kwa Bega

“[Nitawarudishia] mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la BWANA, wamtumikie kwa nia moja [“bega kwa bega,” “NW”].” —SEFANIA 3:9.

1. Andiko la Sefania 3:9 linatimizwaje?

KUNA lugha 6,000 hivi zinazozungumzwa sasa ulimwenguni pote. Mbali na lugha hizo, kuna lahaja tofauti-tofauti zinazozungumzwa katika maeneo mbalimbali. Lakini, hata kama watu wanazungumza lugha nyingi zilizo tofauti kama vile Kiarabu na Kizulu, Mungu amefanya jambo la kipekee sana. Amewawezesha wanadamu kila mahali wajifunze na kuzungumza ile lugha moja tu iliyo safi. Jambo hilo linatukia ili kutimiza ahadi iliyotolewa kupitia nabii Sefania: ‘Nitawarudishia mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la BWANA, wamtumikie bega kwa bega.’—Sefania 3:9.

2. “Lugha iliyo safi” ni nini, nayo imefanya jambo gani liwezekane?

2 “Lugha iliyo safi” ni kweli ya Mungu inayopatikana katika Neno lake Biblia. Kweli hiyo inahusu hasa Ufalme wa Mungu, ambao utatakasa jina la Yehova, kutetea haki yake ya kutawala, na kuwaletea wanadamu baraka. (Mathayo 6:9, 10) Lugha hiyo ambayo ndiyo tu safi kiroho duniani, inazungumzwa na watu wa mataifa na jamii zote. Inawawezesha wamtumikie Yehova “bega kwa bega.” Hivyo, wanamtumikia kwa umoja au kwa “nia moja.”

Watu wa Mungu Hawapaswi Kuwa na Ubaguzi

3. Ni nini hutuwezesha kumtumikia Yehova kwa umoja?

3 Tukiwa Wakristo, tunashukuru kwa ushirikiano uliopo kati ya watu wa lugha mbalimbali miongoni mwetu. Ingawa tunahubiri habari njema za Ufalme katika lugha mbalimbali, tunamtumikia Mungu kwa umoja. (Zaburi 133:1) Hilo linawezekana kwa sababu popote tunapoishi duniani, tunazungumza ile lugha safi ili kumsifu Yehova.

4. Kwa nini watu wa Mungu hawapaswi kuwa na ubaguzi?

4 Watu wa Mungu hawapaswi kuwa na ubaguzi. Mtume Petro alifafanua jambo hilo alipohubiri nyumbani kwa Kornelio, ofisa wa jeshi asiyekuwa Myahudi, mwaka wa 36 W.K. Petro alichochewa kusema: “Kwa hakika nahisi kwamba Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Kwa kuwa maneno hayo ni kweli, hatupaswi kuwa wabaguzi, kujitenga katika vikundi-vikundi, au kuonyesha upendeleo katika kutaniko la Kikristo.

5. Kwa nini ni kosa kuchochea watu wajitenge katika vikundi-vikundi kutanikoni?

5 Mwanafunzi mmoja wa chuo alisema hivi baada ya kutembelea Jumba fulani la Ufalme: “Kwa kawaida makanisa huvutia waumini wa jamii fulani au kabila fulani. . . . Lakini Mashahidi wa Yehova walikuwa wameketi wote pamoja, hakuna waliojitenga katika vikundi-vikundi.” Hata hivyo, washiriki fulani wa kutaniko la Korintho la kale walikuwa wanasababisha mafarakano. Kwa kufanya hivyo, walikuwa wakiipinga roho takatifu ya Mungu ambayo huchangia amani na umoja. (Wagalatia 5:22) Iwapo tutachochea watu wajitenge katika vikundi-vikundi kutanikoni, tutakuwa tukipinga mwongozo wa roho takatifu. Kwa hiyo, na tukumbuke maneno ya mtume Paulo kwa Wakorintho: “Nawahimiza nyinyi kwa bidii, akina ndugu, kupitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kwamba nyote mseme kwa upatano, na kwamba kusiwe na migawanyiko miongoni mwenu, bali kwamba mpate kuunganishwa kwa kufaa katika akili ileile na katika mstari uleule wa fikira.” (1 Wakorintho 1:10) Paulo pia alikazia umoja katika barua yake kwa Waefeso.—Waefeso 4:1-6, 16.

6, 7. Yakobo alitoa ushauri gani kuhusu upendeleo, na maneno yake yanatuhusuje?

6 Sikuzote Wakristo wameagizwa wasiwe na ubaguzi. (Waroma 2:11) Wengine katika kutaniko la karne ya kwanza waliwaonyesha matajiri upendeleo, hivyo mwanafunzi Yakobo akaandika: “Ndugu zangu, nyinyi hamshiki imani ya Bwana wetu Yesu Kristo, utukufu wetu, kwa matendo ya upendeleo, je, mnafanya hivyo? Kwa maana, ikiwa mwanamume mwenye pete za dhahabu kwenye vidole vyake na aliyevaa mavazi maridadi aingia ndani ya kusanyiko lenu, lakini mtu maskini aliyevaa mavazi yenye uchafu wa kuchukiza aingia pia, lakini mwamtazama kwa upendeleo yule aliyevaa mavazi maridadi na kumwambia: ‘Wewe kalia kiti hiki hapa mahali bora,’ nanyi mwamwambia aliye maskini: ‘Wewe fuliza kusimama,’ au: ‘Kalia kiti kile pale chini ya kibago cha miguu yangu,’ nyinyi mna tofauti za kitabaka miongoni mwenu wenyewe nanyi mmekuwa mahakimu mkitoa maamuzi maovu, je, sivyo ilivyo?”—Yakobo 2:1-4.

7 Waamini matajiri waliovaa pete za dhahabu na mavazi maridadi walipohudhuria mikutano ya Kikristo pamoja na waamini maskini wenye mavazi machafu, matajiri walipendelewa. Walipewa viti “mahali bora,” huku walio maskini wakiambiwa wasimame au wakae chini penye miguu ya mtu. Lakini Mungu alitoa dhabihu ya fidia ya Yesu kwa ajili ya matajiri na maskini, bila kubagua. (Ayubu 34:19; 2 Wakorintho 5:14) Kwa hiyo ikiwa tunataka kumpendeza Yehova na kumtumikia bega kwa bega, hatupaswi kuonyesha upendeleo au ‘kuwasifu watu mashuhuri kwa ajili ya manufaa yetu wenyewe.’—Yuda 4, 16.

Usiwe Mnung’unikaji

8. Waisraeli walipatwa na nini kwa sababu ya kunung’unika?

8 Ili kudumisha umoja wetu na kuendelea kuwa na kibali cha Mungu, lazima tutii ushauri huu wa Paulo: “Fulizeni kufanya mambo yote bila manung’uniko.” (Wafilipi 2:14, 15) Waisraeli wasio na imani ambao walikombolewa utumwani Misri waliwanung’unikia Musa na Aroni na hivyo hata kumnung’unikia Yehova Mungu. Kwa sababu hiyo, wanaume wote wenye umri wa miaka 20 na zaidi hawakuingia katika Nchi ya Ahadi bali walikufa wakati wa ile miaka 40 waliyotangatanga nyikani. Walioingia humo ni wanaume waaminifu, Yoshua na Kalebu pamoja na Walawi. (Hesabu 14:2, 3, 26-30; 1 Wakorintho 10:10) Walipata adhabu iliyoje kwa kunung’unika!

9. Miriamu alipatwa na nini kwa sababu ya kunung’unika?

9 Hiyo inaonyesha kile kinachoweza kulipata taifa zima lenye kunung’unika. Namna gani wanung’unikaji mmoja-mmoja? Miriamu, dada ya Musa, pamoja na ndugu yake Aroni walinung’unika hivi: “Je! Ni kweli BWANA amenena na Musa tu? Hakunena na sisi pia?” Masimulizi hayo yanaendelea kusema: “BWANA akasikia maneno yao.” (Hesabu 12:1, 2) Matokeo yakawaje? Miriamu, ambaye yaelekea ndiye aliongoza manung’uniko hayo, aliaibishwa na Mungu. Jinsi gani? Kwa kupigwa kwa ukoma na kulazimishwa kukaa nje ya kambi kwa siku saba hadi alipotakaswa.—Hesabu 12:9-15.

10, 11. Manung’uniko yasipozuiwa yanaweza kutokeza nini? Toa mfano.

10 Kunung’unika si kulalamika tu kuhusu kosa fulani. Wale wanaonung’unika wakati wote huona hisia na cheo chao kuwa cha maana sana, hivyo kuvuta fikira kwao wenyewe badala ya kwa Mungu. Hali hiyo isipozuiwa, huleta migawanyiko miongoni mwa akina ndugu na huzuia jitihada zao za kumtumikia Yehova bega kwa bega. Hali inakuwa hivyo kwa sababu wanung’unikaji hulalamika daima, yaelekea wakitumaini kuungwa mkono na wengine.

11 Kwa mfano, huenda mtu akachambua jinsi mzee fulani anavyotoa hotuba au jinsi anavyoshughulikia migawo yake kutanikoni. Iwapo tutamsikiliza mlalamikaji huyo, huenda tukaanza kufikiri kama yeye. Kabla mawazo hayo ya kutoridhika hayajaingizwa akilini mwetu, huenda hatukuudhiwa na jinsi ambavyo mzee huyo hushughulikia mambo, lakini sasa tunaudhika. Hatimaye, tutaona mambo yote afanyayo mzee huyo kuwa hayafai, na huenda hata sisi tukaanza kulalamika kumhusu. Mwenendo huo haufai katika kutaniko la watu wa Yehova.

12. Kunung’unika kunaweza kuathirije uhusiano wetu na Mungu?

12 Huenda kunung’unikia wanaume ambao wana kazi ya kuchunga kundi la Mungu kukafanya tuanze kuwatukana. Kunung’unika huko au kusema mambo mabaya kuwahusu kunaweza kuhatarisha uhusiano wetu na Yehova. (Kutoka 22:28) Watukanaji wasiotubu hawataurithi Ufalme wa Mungu. (1 Wakorintho 5:11; 6:10) Mwanafunzi Yuda aliandika kuhusu wanung’unikaji ‘waliopuuza ubwana na kusema kwa maneno yenye kuudhi juu ya watukufu,’ au wanaume wenye madaraka kutanikoni. (Yuda 8) Wanung’unikaji hao hawakuwa na kibali cha Mungu, na kwa hekima sisi huepuka mwenendo wao mwovu.

13. Kwa nini si malalamiko yote yaliyo mabaya?

13 Hata hivyo, si malalamiko yote yanayomchukiza Mungu. Yeye hakupuuza “malalamiko” dhidi ya Sodoma na Gomora lakini aliharibu majiji hayo maovu. (Mwanzo 18:20, 21, Biblia Habari Njema; 19:24, 25) Muda mfupi baada ya Pentekoste 33 W.K., “mnung’uniko ulitokea kwa upande wa Wayahudi wenye kusema Kigiriki dhidi ya Wayahudi wenye kusema Kiebrania, kwa sababu wajane wao walikuwa hawaangaliwi katika ugawanyaji wa kila siku.” Hivyo, “wale kumi na wawili” wakarekebisha hali hiyo kwa kuweka “wanaume saba wenye kuthibitishwa” ili wasimamie ‘shughuli hiyo ya lazima’ ya kugawanya chakula. (Matendo 6:1-6) Wazee wa siku hizi hawapaswi ‘kuziba masikio yao’ wasisikie malalamiko yaliyo halali. (Mithali 21:13) Na badala ya kuwachambua waabudu wenzao, wazee wanapaswa kuwatia moyo na kuwajenga.—1 Wakorintho 8:1.

14. Tunahitaji sifa gani hasa ili tuepuke kunung’unika?

14 Sisi sote tunahitaji kuepuka manung’uniko, kwa kuwa roho ya kulalamika inadhuru kiroho. Roho kama hiyo inaweza kuvuruga umoja wetu. Badala yake, sikuzote na turuhusu roho takatifu itokeze upendo ndani yetu. (Wagalatia 5:22) Kutii ‘sheria ya kifalme ya upendo’ kutatusaidia kuendelea kumtumikia Yehova bega kwa bega.—Yakobo 2:8; 1 Wakorintho 13:4-8; 1 Petro 4:8.

Epuka Uchongezi

15. Unaweza kutofautishaje porojo na uchongezi?

15 Kwa kuwa kulalamika kunaweza kutokeza porojo zinazodhuru, ni lazima tuwe waangalifu kuhusu yale tusemayo. Porojo ni mazungumzo ya kupisha wakati tu kuhusu watu na shughuli zao. Lakini, uchongezi ni habari za uwongo zinazokusudiwa kumharibia mtu mwingine sifa. Mazungumzo kama hayo ni maovu na hayampendezi Mungu. Kwa hiyo, Mungu aliwaambia Waisraeli hivi: “Usiende huko na huko katikati ya watu wako, kama mchongezi.”—Mambo ya Walawi 19:16.

16. Paulo alisema nini kuhusu wapiga-porojo fulani, nasi twapaswa kuuonaje ushauri wake?

16 Kwa kuwa mazungumzo hayo ya kupisha wakati yanaweza kugeuka na kuwa uchongezi, Paulo aliwakemea kwa ujasiri wapiga-porojo fulani. Baada ya kutaja wajane waliostahili kupewa msaada kutanikoni, Paulo alizungumza juu ya wajane waliojifunza “kuwa wasio na shughuli, wakizurura huku na huku kwenye nyumba; ndiyo, si wakiwa wasio na shughuli tu, bali pia wapiga-porojo na wajiingizaji katika mambo ya watu wengine, wakiongea juu ya mambo yasiyowapasa.” (1 Timotheo 5:11-15) Mwanamke Mkristo akigundua kwamba ana udhaifu wa kuzungumzia mambo yanayoweza kumfanya awe mchongezi, anapaswa kutii ushauri wa Paulo wa ‘kuchukua mambo kwa uzito na asiwe mwenye uchongezi.’ (1 Timotheo 3:11) Bila shaka, wanaume Wakristo wanapaswa pia kuepuka porojo zenye kudhuru.—Mithali 10:19.

Acha Kuhukumu!

17, 18. (a) Yesu alisema nini kuhusu kumhukumu ndugu yetu? (b) Tunaweza kutumiaje yale ambayo Yesu alisema kuhusu kuhukumu?

17 Hata ikiwa hatumchongei mtu yeyote, huenda tukahitaji kujitahidi sana tusiwahukumu wengine. Yesu alishutumu mtazamo huo aliposema: “Komeni kuhukumu ili msipate kuhukumiwa; kwa maana kwa hukumu mnayohukumu, mtahukumiwa; na kwa kipimo mnachopimia, watawapimia nyinyi. Basi, kwa nini wautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako, lakini hulifikirii boriti lililo katika jicho lako mwenyewe? Au wawezaje kumwambia ndugu yako, ‘Niruhusu niutoe unyasi ulio katika jicho lako’; wakati, tazama! boriti limo katika jicho lako mwenyewe? Mnafiki! Kwanza toa boriti lililo katika jicho lako mwenyewe, na ndipo utaona waziwazi jinsi ya kutoa unyasi ulio katika jicho la ndugu yako.”—Mathayo 7:1-5.

18 Haingefaa kujaribu kuutoa “unyasi” katika jicho la ndugu yetu huku uwezo wetu wenyewe wa kuhukumu vizuri ukiwa umezuiwa na “boriti” la mfano. Ikiwa kwa kweli tunaifahamu rehema ya Mungu, hatutakuwa na mwelekeo wa kuwahukumu ndugu na dada zetu wa kiroho. Hatuwezi kuwaelewa vizuri kama Baba yetu wa mbinguni anavyowaelewa. Si ajabu kwamba Yesu alituonya ‘tukome kuhukumu ili tusipate kuhukumiwa’! Kuchunguza kwa unyofu hali yetu ya kutokamilika kunapaswa kutuzuia kutoa hukumu ambayo Mungu angeiona kuwa isiyo ya uadilifu.

Dhaifu Lakini Vyenye Kuheshimika

19. Tunapaswa kuwaonaje waamini wenzetu?

19 Iwapo tumeazimia kumtumikia Mungu bega kwa bega pamoja na waamini wenzetu, hatutaepuka tu kuwahukumu bali tutachukua hatua ya kwanza kuwaonyesha heshima. (Waroma 12:10) Isitoshe, tutatanguliza masilahi yao badala ya yetu, na kufurahia kuwafanyia mambo madogo-madogo. (Yohana 13:12-17; 1 Wakorintho 10:24) Tunawezaje kudumisha mtazamo huo mzuri? Kwa kukumbuka kwamba kila mwamini ni mwenye thamani kwa Yehova na kwamba tunahitajiana, kama vile viungo vyote vya mwili hutegemeana.—1 Wakorintho 12:14-27.

20, 21. Andiko la 2 Timotheo 2:20, 21 lina maana gani kwetu?

20 Ni kweli kwamba Wakristo ni vyombo dhaifu vya udongo, nao wamepewa hazina tukufu ya huduma. (2 Wakorintho 4:7) Ikiwa tutaendelea kufanya huduma hiyo takatifu ya kumsifu Yehova, ni lazima tudumishe msimamo wenye heshima mbele yake na Mwana wake. Tunaweza tu kuendelea kuwa chombo chenye kuheshimika kwa ajili ya kazi ya Mungu ikiwa tutadumu tukiwa safi kiadili na kiroho. Kuhusu jambo hilo Paulo aliandika: “Katika nyumba kubwa mna vyombo si vya dhahabu na fedha tu bali pia vya mbao na vya udongo, na baadhi yavyo ni kwa kusudi lenye kuheshimika lakini vingine ni kwa kusudi lenye kukosa heshima. Kwa hiyo, ikiwa yeyote ajiepusha kabisa na hawa wa mwisho, atakuwa chombo kwa kusudi lenye kuheshimika, kilichotakaswa, chenye mafaa kwa mmiliki wacho, kilichotayarishwa kwa kila kazi njema.”—2 Timotheo 2:20, 21.

21 Watu wasiojiendesha kupatana na matakwa ya Mungu ni ‘vyombo visivyo na heshima.’ Hata hivyo, kwa kufuata mwenendo unaompendeza Mungu, tutakuwa ‘vyombo kwa kusudi lenye kuheshimika, vilivyotakaswa, au vilivyotengwa, kwa utumishi wa Yehova na kutayarishwa kwa kila kazi njema.’ Kwa hiyo huenda tukajiuliza: ‘Je, mimi ni “chombo chenye kuheshimika”? Je, mimi nina uvutano ufaao kuelekea waamini wenzangu? Je, mimi ni mshiriki wa kutaniko ninayefanya kazi bega kwa bega pamoja na waabudu wenzangu?’

Endeleeni Kutumikia Bega kwa Bega

22. Kutaniko la Kikristo linaweza kulinganishwa na nini?

22 Kutaniko la Kikristo ni kama familia. Familia ambayo washiriki wake wote wanamwabudu Yehova, inakuwa yenye upendo, yenye kusaidiana, na inapendeza. Huenda familia ikawa na watu kadhaa wenye nyutu zinazotofautiana, lakini kila mmoja wao anastahili heshima. Hali iko hivyo kutanikoni. Ingawa sisi sote ni tofauti—na wasio wakamilifu—Mungu ametuvuta kwake kupitia Kristo. (Yohana 6:44; 14:6) Yehova na Yesu wanatupenda, na kama familia yenye umoja, bila shaka tunahitaji kupendana.—1 Yohana 4:7-11.

23. Tunapaswa kukumbuka na pia kuazimia kufanya nini?

23 Kutaniko la Kikristo lililo kama familia pia ni mahali ambapo kwa kufaa tunatarajia kupata watu waaminifu-washikamanifu. Mtume Paulo aliandika: “Nataka kwamba katika kila mahali wanaume waendeleze sala, wakiinua mikono yenye uaminifu-mshikamanifu, bila hasira ya kisasi na mashindano ya maneno.” (1 Timotheo 2:8) Hivyo Paulo alihusianisha uaminifu-mshikamanifu na sala za hadharani zinazotolewa “kila mahali” ambapo Wakristo wamekutana. Wanaume waaminifu-washikamanifu tu ndio wanaopaswa kuliwakilisha kutaniko katika sala ya hadharani. Bila shaka, Mungu anatarajia sisi sote tuwe waaminifu-washikamanifu kwake na kwa mmoja na mwenzake. (Mhubiri 12:13, 14) Basi na tuazimie kufanya kazi kwa upatano, kama vile viungo vya mwili wa binadamu. Na tutumikie kwa umoja tukiwa washiriki wa familia ya waabudu wa Yehova. Zaidi ya yote, na tukumbuke kwamba tunahitajiana na tutapata kibali na baraka za Yehova tukiendelea kumtumikia bega kwa bega.

Ungejibuje?

• Ni nini kinachowawezesha watu wa Yehova wamtumikie bega kwa bega?

• Kwa nini Wakristo huepuka ubaguzi?

• Kuna ubaya gani kunung’unika?

• Kwa nini tunapaswa kuwaheshimu waamini wenzetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Petro alihisi kwamba ‘Mungu hana ubaguzi’

[Picha katika ukurasa wa 16]

Je, unajua ni kwa nini Mungu alimwaibisha Miriamu?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wakristo waaminifu-washikamanifu humtumikia Yehova bega kwa bega