Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tunahitaji Majengo ya Ibada?

Je, Tunahitaji Majengo ya Ibada?

Je, Tunahitaji Majengo ya Ibada?

‘Maelfu ya mahujaji waliovaa nguo zenye kupendeza kutoka sehemu mbalimbali za nchi, vikundi vya Wahindi wanaoigiza mdundo wa ngoma za Wahispania wa kale, na waumini wanaojitahidi kwa uchungu kutembea kwa magoti katikati ya umati ili wafikie mahali patakatifu walijaa barazani na barabarani karibu na basilika.’

HIVYO ndivyo gazeti El Economista lilivyofafanua umati mkubwa wa watu mnamo Desemba 2001. Wakati huo, watu wapatao milioni tatu walizuru basilika ya Mexico City ili kudhihirisha imani yao kwa Bikira wa Guadalupe. Wageni wengi sana pia hutembelea majengo mengine ya kidini kama vile Basilika ya Mtakatifu Petro huko Roma.

Watu wengi walio na tamaa ya kumwabudu Mungu huhisi kwamba majengo ya kidini ni muhimu na yanapaswa kuheshimiwa sana. “Mimi niliona kanisa kuwa mahali ambapo ningeweza kumkaribia Mungu,” asema Maria kutoka Brazili. “Palikuwa mahali patakatifu. Niliamini kwamba kwenda kanisani kulitakasa nafsi na kwamba ni dhambi kutohudhuria Misa na kuungama dhambi kila Jumapili.” Consuelo kutoka Mexico asema: “Kanisa lilichochea sana hisia zangu; nililithamini sana. Nilipokuwa huko, nilihisi ni kana kwamba niko mbinguni.”

Ingawa watu fulani huona makanisa kuwa muhimu sana, wengine hawayaoni kuwa mahali pa lazima pa kwenda kuabudia. Akizungumzia kuhusu kupungua kwa idadi ya watu wanaoenda makanisani, Peter Sibert, kasisi Mkatoliki huko Uingereza, anasema: “[Watu] huchagua mambo fulani yanayowapendeza katika dini yao. Watu wengi wenye umri mkubwa ni Wakatoliki nao huishi kupatana na imani yao—lakini vijana hawawajibiki sana.” Gazeti Daily Telegraph la London la Novemba 20, 1998, lilisema hivi: “Tangu mwaka wa 1979 makanisa yapatayo 1,500 yamefungwa nchini Uingereza huku makanisa 495 yakizinduliwa na mengine 150 kujengwa upya.”

Mnamo mwaka wa 1997 gazeti Süddeutsche Zeitung la Munich, Ujerumani, liliripoti hivi: “Makanisa yanageuzwa kuwa majumba ya sinema na nyumba za kuishi: Waumini hawahudhurii ibada, majengo ya ibada hayatumiwi tena kwa ibada. . . . Jambo ambalo ni la kawaida nchini Uholanzi au Uingereza sasa linatukia Ujerumani.” Gazeti hilo liliongeza kusema: “Mtu anaweza kuona makanisa makubwa 30 au 40 yaliyouzwa nchini Ujerumani katika miaka michache iliyopita.”

Je, majengo ya ibada ni ya lazima ili kumwabudu Mungu? Je, Maandiko yanaonyesha kwamba kulikuweko na basilika na makanisa yenye fahari? Ni majengo ya aina gani yaliyohusianishwa na ibada ya Mungu wa kweli aliye hai? Majengo hayo yanatufunza nini kuhusu uhitaji wa kuwa na mahali pa kuabudia, nayo yanapaswa kutumiwa kwa kusudi gani?