Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitihada za Kutafsiri Biblia Katika Kigiriki cha Kisasa

Jitihada za Kutafsiri Biblia Katika Kigiriki cha Kisasa

Jitihada za Kutafsiri Biblia Katika Kigiriki cha Kisasa

Huenda ukashangaa kusikia kwamba kwa muda mrefu kumekuwa na mapambano ya kutafsiri Biblia kwa lugha ya kawaida katika nchi ya Ugiriki, nchi ambayo nyakati nyingine imeitwa chanzo cha uhuru wa usemi. Lakini ni nani angezuia kazi ya kutafsiri Biblia katika Kigiriki kinachoeleweka kwa urahisi? Mbona mtu azuie kazi hiyo?

HUENDA mtu akafikiri kwamba watu wanaozungumza Kigiriki wana pendeleo kwa sababu vitabu vingi vya Maandiko Matakatifu viliandikwa kwanza kwa lugha yao. Hata hivyo, Kigiriki cha kisasa ni tofauti sana na Kigiriki kilichotumiwa kwenye tafsiri ya Septuagint ya Maandiko ya Kiebrania na ni tofauti pia na kile kilichotumiwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kwa kweli, katika karne sita zilizopita, watu wengi wanaozungumza Kigiriki wameshindwa kuelewa Kigiriki cha Biblia kana kwamba ni lugha ya kigeni. Maneno mapya yanatumiwa badala ya maneno yaliyotumiwa hapo zamani, msamiati, sarufi na mtiririko wa maneno umebadilika.

Hati kadhaa za Kigiriki zilizoandikwa kuanzia karne ya 3 hadi ya 16 zinaonyesha jitihada zilizofanywa ili kutafsiri Septuagint kwa Kigiriki cha baadaye. Katika karne ya 3, Gregory, askofu wa Neocaesarea (karibu mwaka wa 213-270 W.K.), alitumia Kigiriki sahili kutafsiri kitabu cha Mhubiri cha Septuagint. Katika karne ya 11, Myahudi aliyeitwa Tobias ben Eliezer, aliyeishi Makedonia alitafsiri baadhi ya vitabu vitano vya kwanza vya Septuagint kwa Kigiriki cha kawaida. Hata alitumia herufi za Kiebrania ili kuwafaidi Wayahudi wa Makedonia ambao walizungumza Kigiriki peke yake na kusoma Kiebrania. Vitabu vitano vya kwanza vya Biblia vilivyoandikwa kwa lugha hiyo vilichapishwa huko Constantinople mwaka wa 1547.

Nuru Gizani

Baada ya Waturuki kuteka maeneo ya Kigiriki ya Miliki ya Byzantium katika karne ya 15, wakazi wengi wa maeneo hayo walihitaji kuelimishwa. Ingawa Kanisa Othodoksi lilikuwa na mapendeleo ya pekee katika Miliki ya Uturuki, liliwapuuza waumini wake walioendelea kuwa maskini na wasio na elimu. Mwandishi Mgiriki Thomas Spelios alisema hivi: “Lengo kuu la Kanisa Othodoksi na la mfumo wake wa elimu lilikuwa kulinda waumini wake kutokana na Uislamu na uvumi wa Kanisa Katoliki. Hivyo hakukuwa na maendeleo yoyote ya kielimu nchini Ugiriki.” Licha ya hali hiyo yenye kusikitisha, watu wanaopenda Biblia waliona kwamba kulikuwa na uhitaji wa kuwatuliza na kuwafariji watu walioshuka moyo kwa kutumia kitabu cha Biblia cha Zaburi. Kuanzia mwaka wa 1543 hadi 1835, kulikuwa na tafsiri 18 za kitabu cha Zaburi katika Kigiriki cha kawaida.

Tafsiri ya kwanza ya Kigiriki ya Maandiko yote ya Kigiriki ya Kikristo ilitafsiriwa mwaka wa 1630 na Maximus Callipolites, mtawa Mgiriki wa Callipolis. Alifanya kazi hiyo chini ya mwongozo wa Cyril Lucaris, kiongozi mashuhuri kutoka Constantinople aliyeleta mabadiliko katika Kanisa Othodoksi. Hata hivyo, Lucaris alikuwa na wapinzani kanisani, ambao hawangekubali mabadiliko yoyote au kutafsiriwa kwa Biblia katika lugha ya kawaida. * Alinyongwa kwa madai ya kuwa msaliti. Isitoshe, nakala 1,500 za tafsiri ya Maximus zilichapishwa mwaka wa 1638. Miaka 34 baadaye, viongozi wa Kanisa Othodoksi waliokutana huko Jerusalem ili kujadiliana kuhusu tafsiri hiyo, walitangaza kwamba Maandiko “hayapaswi kusomwa na mtu yeyote yule, lakini yanapasa kusomwa na watu wanaochunguza mambo mazito sana ya kiroho baada ya kufanya utafiti ufaao.” Walimaanisha kwamba Maandiko yanapaswa kusomwa tu na makasisi wenye elimu.

Seraphim, mtawa Mgiriki kutoka kisiwa cha Lesbos, alijaribu kuchapisha tafsiri mpya ya Maximus huko London mnamo mwaka wa 1703. Wakuu wa serikali walipokataa kumpa msaada wa kifedha ambao walimwahidi, alitumia fedha zake mwenyewe kuchapisha tafsiri hiyo mpya. Seraphim aliandika maneno makali katika utangulizi wake, akikazia kwamba “kila Mkristo anayempenda Mungu” anapaswa kusoma Biblia. Aliwashutumu makasisi wenye vyeo vya juu kanisani ambao “walijaribu kuficha uovu wao kwa kutowaelimisha watu.” Kama ilivyotarajiwa, adui zake Waothodoksi walipanga njama, naye akakamatwa huko Urusi na kupelekwa uhamishoni huko Siberia, ambako alifia mwaka wa 1735.

Akizungumzia njaa kali ya kiroho ambayo watu waliozungumza Kigiriki walikuwa nayo, kasisi mmoja Mgiriki alisema hivi kuhusu tafsiri ya baadaye ya Maximus: “Wagiriki na wengineo walipokea Biblia hii Takatifu kwa hamu na uchangamfu sana. Nao wanaisoma. Uchungu waliokuwa nao moyoni ulitulizwa, na imani yao katika Mungu . . . iliongezeka.” Hata hivyo, viongozi wao wa kidini waliogopa kwamba matendo ya makasisi na mafundisho yao yasiyo ya kimaandiko yangejulikana kama watu wangeanza kuielewa Biblia. Kwa hiyo, katika mwaka wa 1823 na pia mwaka wa 1836, askofu mkuu wa Constantinople aliagiza tafsiri hizo zote ziteketezwe.

Mtafsiri Jasiri

Licha ya upinzani mkali, watu walikuwa na hamu kubwa ya kujifunza Biblia. Hivyo mtu mmoja mashuhuri alijitokeza kufanya kazi muhimu ya kutafsiri Biblia katika Kigiriki cha kisasa. Mtu huyo jasiri alikuwa Neofitos Vamvas, mtaalamu wa lugha na msomi maarufu wa Biblia, ambaye alionwa na wengi kuwa miongoni mwa “Walimu wa Taifa.”

Vamvas aliamini kwamba Kanisa Othodoksi ndilo lililowatumbukiza watu katika giza la kiroho. Aliamini kabisa kwamba Biblia ilihitaji kutafsiriwa katika Kigiriki cha kawaida ili kuwaamsha watu kiroho. Mnamo mwaka wa 1831, yeye pamoja na wasomi wengine, walianza kutafsiri Biblia kwa Kigiriki cha wasomi. Tafsiri yake nzima ilichapishwa mwaka wa 1850. Alishirikiana na Chama cha Biblia cha Uingereza na cha Lugha za Kigeni (BFBS) katika kuchapisha na kugawanya tafsiri yake kwa kuwa Kanisa Othodoksi la Ugiriki lilikataa kumsaidia. Kanisa lilimwita “Mprotestanti,” na baada ya muda alitengwa na kanisa.

Tafsiri ya Vamvas ilitegemea kabisa tafsiri ya King James Version na hivyo ilikuwa na kasoro kama tafsiri hiyo kwa sababu wakati huo watu hawakujua vyema lugha wala kazi ya kutafsiri Biblia. Hata hivyo, kwa miaka mingi, hiyo ndiyo iliyokuwa Biblia pekee iliyotafsiriwa katika Kigiriki cha kisasa. Jambo la kuvutia ni kwamba jina la Mungu likiwa limeandikwa “Ieová” linapatikana mara nne ndani ya tafsiri hiyo.—Mwanzo 22:14; Kutoka 6:3; 17:15; Waamuzi 6:24.

Watu walikuwa na maoni gani kuhusu Biblia hii na Biblia nyingine zilizotafsiriwa kwa lugha rahisi? Walisisimuka ajabu! Kwenye mashua iliyokuwa karibu na ufuo wa kisiwa kimoja cha Ugiriki, muuzaji mmoja wa Biblia wa chama cha BFBS “alizingirwa na mashua zilizojaa watoto waliotaka [Biblia], hivi kwamba alilazimika . . . kumwagiza nahodha afunge safari” la sivyo, angegawa nakala zote alizokuwa nazo mahali hapo. Lakini wapinzani walichukua hatua mara moja.

Makasisi Waothodoksi waliwaonya watu wasichukue tafsiri hizo. Kwa mfano, katika jiji la Athens, Biblia zote zilikusanywa kwa nguvu. Katika mwaka wa 1833, askofu Mwothodoksi wa Crete aliteketeza Biblia za “Agano Jipya” alizopata kwenye nyumba moja ya watawa. Kasisi mmoja na wakazi wa vijiji vya karibu walificha nakala zao hadi askofu huyo alipoondoka kisiwani.

Miaka kadhaa baadaye, kwenye kisiwa cha Corfu, tafsiri ya Biblia ya Vamvas ilipigwa marufuku na Sinodi Takatifu ya Kanisa Othodoksi la Ugiriki. Uuzaji wa Biblia hiyo ulipigwa marufuku, na nakala zilizosalia zikaharibiwa. Biblia ziliteketezwa kwenye visiwa vya Chios, Síros, na Mykonos kwa sababu ya upinzani wa makasisi. Lakini kazi ya kutafsiri Biblia ilikumbwa na upinzani mwingi baadaye.

Malkia Apendezwa na Biblia

Katika miaka ya 1870, Malkia Olga wa Ugiriki aligundua kwamba Wagiriki wengi hawakuijua vizuri Biblia. Alijitahidi kuhakikisha kwamba Biblia imetafsiriwa kwa lugha rahisi kuliko tafsiri ya Vamvas kwa sababu aliamini kwamba ujuzi wa Maandiko ungeliimarisha na kulitia nguvu taifa hilo.

Askofu mkuu wa Athens na msimamizi wa Sinodi Takatifu, Prokopios, alimtembelea kwa faragha malkia na kumtia moyo aendelee na jitihada zake. Hata hivyo, malkia alipoomba idhini rasmi kutoka kwa Sinodi Takatifu, ombi lake lilikataliwa. Lakini hakukata tamaa, alitoa ombi jingine, na likakataliwa tena mnamo mwaka wa 1899. Alipuuza katazo hilo, akaamua kugharimia uchapishaji wa nakala chache. Alimaliza kazi hiyo mwaka wa 1900.

Wapinzani Sugu

Mnamo mwaka wa 1901, gazeti maarufu la Athens, The Acropolis, lilichapisha Injili ya Mathayo katika Kigiriki cha kawaida. Injili hiyo iliandikwa na Alexander Pallis, mtafsiri aliyekuwa akifanya kazi huko Liverpool, Uingereza. Pallis na wenzake walikuwa na nia ya ‘kuwaelimisha Wagiriki’ na “kuliokoa taifa” lisizorote.

Wanafunzi wa theolojia wa Othodoksi na maprofesa wao walisema tafsiri hiyo “iliaibisha vitu vitakatifu vya taifa hilo,” na ilikufuru Biblia. Askofu mkuu wa Constantinople, Joakim wa Tatu aliandika barua ya kupinga tafsiri hiyo. Ubishi huo uligeuka kuwa wa kisiasa, na vyama vya kisiasa vyenye kuzozana viliutumia kwa ujanja.

Magazeti maarufu ya Athens yalianza kushambulia tafsiri ya Pallis. Yalisema kwamba watu waliounga mkono tafsiri hiyo “hawakumwamini Mungu,” walikuwa “wasaliti,” na “vibaraka wa serikali za kigeni” ambao walitaka kuvuruga amani nchini Ugiriki. Makundi yasiyopenda kamwe mabadiliko katika Kanisa Othodoksi la Ugiriki yaliwachochea wanafunzi wafanye ghasia jijini Athens kuanzia Novemba 5 hadi 8, mwaka wa 1901. Walishambulia ofisi za gazeti la The Acropolis, wakaandamana kwenye makao ya mfalme, wakateka Chuo Kikuu cha Athens huku wakidai serikali ijiuzulu. Watu wanane waliuawa katika mapambano hayo baina ya wanafunzi na wanajeshi. Siku iliyofuata, mfalme alimwagiza Askofu Mkuu Prokopios ajiuzulu, na siku mbili baadaye Baraza lote la Mawaziri likajiuzulu.

Baada ya mwezi mmoja, wanafunzi waliandamana tena na kuiteketeza tafsiri moja ya Pallis hadharani. Waliazimia kukomesha ugawanyaji wa tafsiri hiyo na wakapendekeza kwamba mtu yeyote atakayejaribu kufanya hivyo wakati ujao aadhibiwe vikali. Kusudi lao lilikuwa kupiga marufuku matumizi ya tafsiri yoyote ya kisasa ya Kigiriki. Ulikuwa wakati mwovu sana.

“Usemi wa Yehova Hudumu Milele”

Amri iliyopiga marufuku Biblia ya kisasa ya Kigiriki ilifutiliwa mbali mwaka wa 1924. Tangu wakati huo, Kanisa Othodoksi la Ugiriki limeshindwa kabisa kuwazuia watu kuisoma Biblia. Kwa sasa, Mashahidi wa Yehova wanaongoza katika kazi ya kuwafundisha watu Biblia nchini Ugiriki kama wanavyofanya katika nchi nyingine nyingi. Tangu mwaka wa 1905, wametumia tafsiri ya Vamvas kufundisha maelfu ya watu wanaozungumza Kigiriki kuhusu ujuzi juu ya kweli ya Biblia.

Kwa miaka mingi, wasomi wengi na maprofesa wamejitahidi sana kutafsiri Biblia kwa Kigiriki cha kisasa. Leo, kuna tafsiri 30 hivi za Biblia nzima au sehemu-sehemu ambazo zinaweza kusomwa na Mgiriki wa kawaida. Biblia bora sana ambayo wanayo ni Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko Matakatifu katika Kigiriki. Ilitolewa mwaka wa 1997 ili kuwafaidi watu milioni 16 wanaozungumza Kigiriki ulimwenguni pote. Biblia hiyo inayochapishwa na Mashahidi wa Yehova ni tafsiri ya Neno la Mungu iliyo sahili na inayoeleweka. Nayo hushikamana kwa uaminifu na maandishi ya awali.

Jitihada za kutafsiri Biblia katika Kigiriki cha kisasa zinathibitisha jambo moja muhimu, kwamba “usemi wa Yehova hudumu milele,” licha ya upinzani mkali wa wanadamu.—1 Petro 1:25.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kwa habari zaidi kumhusu Cyril Lucaris, ona Mnara wa Mlinzi, Februari 15, 2000, ukurasa 26-29.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Cyril Lucaris aliongoza kazi ya kutafsiri Biblia ya kwanza ya Kigiriki ya Maandiko yote ya Kigiriki ya Kikristo mwaka wa 1630

[Hisani]

Bib. Publ. Univ. de Genève

[Picha katika ukurasa wa 28]

Baadhi ya tafsiri za Kigiriki cha kawaida: Tafsiri ya Zaburi iliyochapishwa mwaka wa: (1) 1828 na Ilarion, (2) 1832 na Vamvas, (3) 1643 na Julianus. Tafsiri ya “Agano la Kale” iliyochapishwa mwaka wa: (4) 1840 na Vamvas

Malkia Olga

[Hisani]

Biblia: National Library of Greece; Malkia Olga: Culver Pictures

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]

Mafunjo: Reproduced by kind permission of The Trustees of the Chester Beatty Library, Dublin

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 29]

Mafunjo: Reproduced by kind permission of The Trustees of the Chester Beatty Library, Dublin