Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Lichungeni Kundi la Mungu”

“Lichungeni Kundi la Mungu”

“Njoni Kwangu, . . . Nami Hakika Nitawaburudisha Nyinyi”

“Lichungeni Kundi la Mungu”

“Nyinyi huwa tayari sikuzote kutusikiliza na kututia moyo kwa kutumia Biblia.”—Pamela.

“Asanteni kwa ajili ya mambo yote mnayofanya kwa niaba yetu sote. Mnatusaidia sana.”—Robert.

MIOYO ya Pamela na Robert iliwachochea kuwaandikia wazee Wakristo katika makutaniko yao maneno hayo ya shukrani. Watumishi wengine wa Mungu ulimwenguni pote wanashukuru pia kwa sababu ya kutunzwa na kutegemezwa na wale ‘wanaolichunga kundi la Mungu.’ (1 Petro 5:2) Kwa kweli, watu wa Yehova wanashukuru sana kwa ajili ya mambo mengi ambayo wazee hufanya kwa ajili yao na jinsi wanavyoyafanya.

‘Wana Mengi ya Kufanya’

Wazee Wakristo wamepewa madaraka mengi sana. (Luka 12:48) Wao hutayarisha hotuba za kutoa kutanikoni nao hushiriki kazi ya kuhubiri hadharani habari njema za Ufalme wa Mungu. Madaraka yao yanatia ndani kuwatembelea waamini wenzao katika ziara za uchungaji. Wazee huwatembelea pia watu wote wenye mahitaji ya pekee—waliozeeka na wengineo—bila kupuuza hali ya kiroho na ya kimwili ya familia zao wenyewe. (Ayubu 29:12-15; 1 Timotheo 3:4, 5; 5:8) Wazee wengine husaidia kujenga Majumba ya Ufalme. Wengine hutumikia kwenye Halmashauri za Uhusiano na Hospitali au wamepewa mgawo wa kuwatembelea Mashahidi waliolazwa hospitalini. Na wengi wao hujitolea kufanya kazi kwenye makusanyiko. Naam, wazee wana “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Wakorintho 15:58) Ndiyo sababu wazee hao wanaofanya kazi kwa bidii wanathaminiwa sana na wale walio chini yao.—1 Wathesalonike 5:12, 13.

Wazee wanaowatembelea kwa ukawaida Wakristo wenzao nyumbani au kwingineko ili kuwaimarisha kiroho ni vyanzo vya kitia-moyo. Thomas, aliyetunzwa na mama peke yake, alisema hivi: “Kama wazee hawangenitia moyo kwa upendo, sidhani ningekuwa mtumishi wa Yehova wa wakati wote leo.” Vijana wengi waliolelewa na mzazi mmoja wanakubali kwamba wazee waliwasaidia kusitawisha uhusiano mzuri na Mungu.

Ziara za uchungaji huthaminiwa sana pia na washiriki wa kutaniko walio wazee kwa umri. Wenzi wawili mishonari wenye umri wa miaka 80 na kitu waliandika hivi baada ya kutembelewa na wazee wawili: “Tungependa kuwashukuru kwa ziara yenu iliyotufaa sana. Mlipoondoka, tulisoma tena maandiko mliyotuonyesha. Hatutasahau kamwe maneno yenu yenye kutia moyo.” Mjane mmoja mwenye umri wa miaka 70 aliwaandikia hivi wazee: “Nimekuwa nikimwomba Yehova msaada, naye akawatuma nyinyi ndugu wawili nyumbani kwangu. Ziara yenu ilikuwa baraka kutoka kwa Yehova!” Je, umenufaika kwa kutembelewa na wazee wa kutaniko lenu hivi karibuni? Bila shaka sote tunathamini jitihada zao za kulichunga kundi walilopewa!

Wachungaji Wanaomwiga Mungu na Kristo

Yehova ni Mchungaji mwenye upendo. (Zaburi 23:1-4; Yeremia 31:10; 1 Petro 2:25) Yesu Kristo pia ni Mchungaji bora anayetutunza kiroho. Anaitwa “mchungaji mwema,” “mchungaji mkubwa,” na “mchungaji mkuu.” (Yohana 10:11; Waebrania 13:20; 1 Petro 5:4) Yesu aliwatendeaje wale waliotaka kuwa wanafunzi wake? Aliwaalika kwa uchangamfu: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi.”—Mathayo 11:28.

Leo, wazee hujitahidi vivyo hivyo kuliburudisha na kulilinda kundi. Wanaume hao ‘huwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.’ (Isaya 32:2) Walinzi hao wenye fadhili huburudisha, huheshimiwa na kundi, na wanampendeza Mungu.—Wafilipi 2:29; 1 Timotheo 5:17.

Msaada Muhimu Kutoka kwa Wake Zao

Watu wa Mungu wanashukuru kwa ajili ya wazee Wakristo na kwa ajili ya msaada wenye upendo ambao wake zao wanawapa. Kwa kawaida wanawake hao hujidhabihu sana ili kuwaunga mkono waume zao. Nyakati nyingine, wao hubaki nyumbani waume zao wanaposhughulikia mambo ya kutaniko au wanapofanya ziara za uchungaji. Nyakati nyingine, mipango muhimu ya familia huahirishwa kunapotokea tatizo la dharura kutanikoni. “Hata hivyo, ninapomwona mume wangu akitayarisha mikutano kwa bidii au akifanya ziara za uchungaji, mimi hukumbuka kwamba anafanya kazi ya Yehova, nami hujaribu kumuunga mkono kadiri niwezavyo,” akasema Michelle.

Cheryl, ambaye pia ameolewa na mzee alisema hivi: “Ninajua kwamba akina ndugu na dada kutanikoni wanahitaji kuzungumza na wazee, nami hutaka wahisi kwamba wako huru kuja kumwona mume wangu wakati wowote wanapomhitaji.” Wanawake kama vile Michelle na Cheryl, wanaowaunga mkono waume zao, hujinyima mambo mengi kwa hiari ili waume zao wawatunze kondoo wa Mungu. Wake wa wazee wanathaminiwa kwa ajili ya kuwaunga mkono kwa hiari waume zao.

Hata hivyo, mzee mwenye shughuli nyingi hapaswi kupuuza mahitaji ya kiroho na mahitaji mengineyo ya mke na watoto wake. Mzee aliyeoa hapaswi ‘kuwa na shtaka, anahitaji kuwa mume wa mke mmoja, mwenye watoto wanaoamini ambao [hawako] chini ya shtaka la ufasiki wala kuwa wasiotawalika.’ (Tito 1:6) Ni lazima aitunze familia yake kwa kupatana na maagizo ya Mungu yaliyo katika Maandiko kwa ajili ya waangalizi Wakristo.—1 Timotheo 3:1-7.

Mzee mwenye shughuli nyingi humthamini sana mke anayemuunga mkono! Wazee wanaowajali wake zao wanahisi hivyo. Ni kama Biblia inavyosema: “Apataye mke [mwema] apata kitu chema.” (Mithali 18:22) Wazee hao huwaonyesha wake zao kwa maneno na matendo kwamba wanawatha-mini sana. Mbali na kusali pamoja kwa bidii na kuwa na funzo lenye kufurahisha, wenzi hao Wakristo hutenga wakati wa kufanya mambo pamoja kama vile kutembea ufuoni, msituni, kwenye bustani na kufanya mambo mengine. Naam, wazee hufurahia kuwatunza wake zao kwa upendo.—1 Petro 3:7.

Wazee wanaolichunga kundi la Mungu bila ubinafsi huwaburudisha kiroho watu wa Yehova. Wao kwa kweli ni “zawadi zikiwa wanadamu,” baraka kwa kutaniko!—Waefeso 4:8, 11-13.