Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, nadhiri zinazowekwa kwa Mungu zinaweza kuvunjwa?

Kulingana na Maandiko, nadhiri ni ahadi nzito ambayo mtu huweka kwa Mungu kufanya tendo fulani, kujitoa kwa njia fulani, kuanza utumishi fulani wa pekee au kutwaa daraka fulani, au kujiepusha na vitu fulani ambavyo havipingani na sheria. Biblia inasimulia kuhusu nadhiri zilizowekwa kwa masharti na ambazo zilihusisha kiapo cha kuchukua hatua fulani iwapo Mungu angefanya jambo fulani kwanza. Kwa mfano, Hana, mama yake nabii Samweli, ‘aliweka nadhiri, akasema: “Ee BWANA wa majeshi, ikiwa . . . [huta]nisahau mimi mjakazi wako, na kunipa mimi mjakazi wako mtoto mume, ndipo mimi nitakapompa BWANA huyo mtoto siku zote za maisha yake, wala wembe hautamfikilia kichwani kamwe.” ’(1 Samweli 1:11) Pia Biblia hutaja kwamba nadhiri huwekwa kwa hiari. Je, nadhiri zinazowekwa kwa Mungu zinaweza kuvunjwa?

Mfalme Solomoni wa Israeli la kale asema: “Ukimwekea Mungu nadhiri, usikawie kuitimiza.” Anaongeza kusema: “Tekeleza ulichoahidi. Ni afadhali kutoweka nadhiri kuliko kuweka nadhiri kisha usiitimize.” (Mhubiri 5:4, 5, BHN) Sheria ambayo taifa la Israeli lilipewa kupitia Musa ilisema: “Utakapoweka nadhiri kwa BWANA, Mungu wako, usiwe mlegevu katika kuiondoa [“kuitekeleza,” BHN]; kwa kuwa BWANA, Mungu wako, hataacha kuitaka kwako; nayo hivi itakuwa dhambi kwako.” (Kumbukumbu la Torati 23:21) Bila shaka, kuweka nadhiri kwa Mungu ni jambo zito. Inapaswa kuwekwa kwa nia nzuri, na mtu anayeiweka anapaswa kuwa na uhakika kwamba ataweza kutimiza nadhiri hiyo. Ikiwa sivyo, ni afadhali asiweke nadhiri. Hata hivyo, je, kuna nadhiri zinazoweza kuvunjwa?

Namna gani ikiwa nadhiri fulani inamtaka mtu afanye jambo ambalo baadaye anatambua kwamba linapingana na mapenzi ya Mungu? Tuseme ni nadhiri ambayo ingechanganya ibada ya kweli na uasherati. (Kumbukumbu la Torati 23:18) Bila shaka, nadhiri kama hiyo inaweza kuvunjwa. Isitoshe, chini ya Sheria ya Musa, nadhiri iliyowekwa na mwanamke ingeweza kuvunjwa na baba yake au mume wake.—Hesabu 30:3-15.

Pia fikiria mtu ambaye ameweka nadhiri kwa Mungu ya kubaki mseja lakini sasa anajikuta katika hali ya kutatanisha. Nadhiri yake imemwingiza katika hali ambayo anahisi kwamba kuitimiza kutamfanya awe karibu kuvunja viwango vya Mungu vya maadili. Je, bado anapaswa kujitahidi kutimiza nadhiri hiyo? Je, si afadhali ajilinde na hatia ya uasherati kwa kutotimiza nadhiri yake na badala yake atafute rehema ya Mungu na kumsihi amsamehe? Yeye tu ndiye anayeweza kuamua atakalofanya. Hakuna mtu mwingine anayeweza kumwamulia.

Namna gani mtu akiweka nadhiri na baadaye atambue kwamba aliiweka haraka bila kufikiri? Je, bado anapaswa kujitahidi kutimiza nadhiri hiyo? Haikuwa rahisi kwa Yeftha kutimiza nadhiri aliyoweka kwa Mungu, lakini alitimiza yote aliyoahidi. (Waamuzi 11:30-40) Mtu anapokosa kutimiza nadhiri, anaweza kufanya Mungu ‘akasirike’ na kuharibu kazi ambazo mtu huyo alikuwa amefanya. (Mhubiri 5:6) Mtu anaweza kukosa kibali cha Mungu kwa sababu ya kukosa kuchukua kwa uzito nadhiri aliyoweka.

Yesu Kristo alisema: “Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, La yenu, La; kwa maana lizidilo hayo ni kutoka kwa yule mwovu.” (Mathayo 5:37) Mkristo anapaswa kuhangaikia jinsi anavyoweza kutimiza nadhiri zake kwa Mungu na vilevile kuwa mwaminifu katika mambo yote anayosema kwa Mungu na wanadamu. Namna gani akijikuta katika hali ya kutatanisha ambapo alifanya maagano na mtu mwingine ambayo hapo mwanzoni yalionekana kuwa mazuri lakini baada ya kuyachunguza zaidi yakaonekana kuwa ya kipumbavu? Hapaswi kuchukua mambo hayo kivivihivi tu. Lakini baada ya kuzungumza mambo kwa njia iliyo wazi, huenda mtu aliyefanya maagano naye akaamua kuyavunja.—Zaburi 15:4; Mithali 6:2, 3.

Tunapaswa kuhangaikia nini hasa kuhusiana na nadhiri na mambo mengine yote? Sikuzote na tujitahidi kudumisha uhusiano mzuri pamoja na Yehova Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 30, 31]

Hana hakusita kutimiza nadhiri yake

[Picha katika ukurasa wa 30, 31]

Yeftha alitimiza nadhiri yake, ingawa ilikuwa vigumu kufanya hivyo