Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msiache Kukusanyika Pamoja

Msiache Kukusanyika Pamoja

Msiache Kukusanyika Pamoja

‘Tusiache kukusanyika pamoja, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri tuonavyo siku ikikaribia,’ yanasema Maandiko. (Waebrania 10:25) Bila shaka, waabudu wa kweli wanapaswa kukusanyika pamoja kwenye mahali pa ibada ili “kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora.”—Waebrania 10:24.

MTUME Paulo alipoandika maneno hayo katika karne ya kwanza Wakati wa Kawaida, kulikuwa na hekalu lenye kuvutia huko Yerusalemu ambalo Wayahudi walikutanikia ili kuabudu. Pia kulikuweko masinagogi. Yesu alikuwa ‘akifundisha katika sinagogi na katika hekalu, ambapo Wayahudi wote walikuja pamoja.’—Yohana 18:20.

Paulo alikuwa akifikiria majengo gani ya kukutania alipowashauri Wakristo wakusanyike pamoja na kutiana moyo? Je, majengo makubwa ya dini zinazojiita eti za Kikristo yanalingana na hekalu la Yerusalemu? Majengo makubwa ya kidini yalianza kutumiwa wakati gani na watu wanaojidai kuwa Wakristo?

‘Nyumba kwa Ajili ya Jina la Mungu’

Maagizo ya kwanza kutolewa kuhusu mahali pa kumwabudu Mungu yanapatikana katika kitabu cha Biblia cha Kutoka. Yehova Mungu aliwaagiza Waisraeli—watu wake waliochaguliwa—wajenge “maskani,” au “hema ya kukutania.” Sanduku la agano na vyombo vingine vitakatifu vilipaswa kuwekwa humo. ‘Utukufu wa Bwana ulijaza maskani’ ilipokamilishwa mwaka wa 1512 K.W.K. Hema hiyo ambayo ingeweza kuhamishwa ilikuwa sehemu kuu ya mpango wa Mungu wa kumfikia ambao aliuweka kwa zaidi ya karne nne. (Kutoka, sura ya 25-27; 40:33-38) Pia Biblia huita hema hiyo “hekalu la BWANA” na ‘nyumba ya BWANA.’—1 Samweli 1:9, 24.

Baadaye, Daudi alipokuwa mfalme huko Yerusalemu, alitamani sana kumjengea Yehova nyumba ya kudumu ambayo ingemletea Yehova utukufu. Hata hivyo, kwa kuwa Daudi alipigana vita vingi sana, Yehova alimwambia hivi: “Hutajenga nyumba kwa ajili ya jina langu.” Badala yake, alimchagua Solomoni, mwana wa Daudi, amjengee hekalu. (1 Mambo ya Nyakati 22:6-10) Solomoni alizindua hekalu hilo mwaka wa 1026 K.W.K., baada ya kulijenga kwa muda wa miaka saba u nusu. Yehova alilikubali jengo hilo na kusema: “Nimeitakasa nyumba hii uliyoijenga ili niweke jina langu humo milele; tena macho yangu na moyo wangu utakuwapo hapo sikuzote.” (1 Wafalme 9:3) Nyumba hiyo ingeendelea kuwa na kibali cha Yehova maadamu Waisraeli wangedumu wakiwa waaminifu. Lakini iwapo wangeacha kutenda mema, Yehova angeondoa kibali chake kutoka mahali hapo, na ‘nyumba hiyo ingebomoka na kuwa magofu.’—1 Wafalme 9:4-9, NW; 2 Mambo ya Nyakati 7:16, 19, 20.

Baada ya muda, Waisraeli waliacha ibada ya kweli. (2 Wafalme 21:1-5) ‘Kwa hiyo Yehova akaleta juu yao mfalme wa Wakaldayo, aliyeiteketeza nyumba ya Mungu, akaubomoa ukuta wa Yerusalemu, akayataketeza kwa moto majumba yake yote, akaviharibu vyombo vyake vya thamani. Na wale waliookoka na upanga akawachukua mpaka Babeli; wakamtumikie yeye na wanawe.’ Kulingana na Biblia, hilo lilitukia mwaka wa 607 K.W.K.—2 Mambo ya Nyakati 36:15-21; Yeremia 52:12-14.

Kama ilivyotabiriwa na nabii Isaya, Mungu alitokeza Mfalme Koreshi awakomboe Wayahudi kutoka kwa utawala wa Babiloni. (Isaya 45:1) Baada ya kukaa uhamishoni kwa miaka 70, walirudi Yerusalemu mwaka wa 537 K.W.K. kwa kusudi la kujenga upya hekalu. (Ezra 1:1-6; 2:1, 2; Yeremia 29:10) Baada ya kazi ya ujenzi kucheleweshwa mara kadhaa, hatimaye hekalu lilikamilishwa mwaka wa 515 K.W.K., na ibada safi ya Yehova ikarudishwa. Ingawa jengo hilo halikuwa na utukufu kama hekalu la Solomoni, lilidumu kwa muda wa miaka 600 hivi. Hata hivyo, jengo hilo halikufanyiwa ukarabati kwa sababu Waisraeli walipuuza ibada ya Yehova. Yesu alipokuja duniani, hekalu hilo lilikuwa likijengwa upya na Mfalme Herode. Hekalu hilo lingepatwa na nini?

“Halitaachwa Jiwe juu ya Jiwe”

Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi kuhusu hekalu la Yerusalemu: “Kwa vyovyote halitaachwa jiwe juu ya jiwe hapa na lisiangushwe chini.” (Mathayo 24:1, 2) Kupatana na maneno hayo, mahali hapo ambapo palikuwa pametambuliwa kwa karne nyingi kuwa kituo cha ibada ya Mungu paliharibiwa mwaka wa 70 W.K. na majeshi ya Roma yaliyokuja kukomesha uasi wa Wayahudi. * Hekalu hilo halikupata kujengwa tena. Katika karne ya saba, kihekalu cha Waislamu kinachoitwa Kuba la Mwamba kilijengwa, na hadi leo hii kingali kipo mahali ambapo Wayahudi wa kale walikutania kuabudu.

Wafuasi wa Yesu wangefuata mpango gani wa ibada? Je, Wakristo wa mapema waliolelewa katika mazingira ya Wayahudi wangeendelea kumwabudu Mungu kwenye hekalu ambalo lingeharibiwa baada ya muda mfupi? Wakristo ambao hawakuwa Wayahudi wangemwabudu Mungu wapi? Je, majengo ya dini zinazojiita eti za Kikristo yangechukua mahali pa hekalu? Mazungumzo kati ya Yesu na mwanamke Msamaria hutusaidia kuelewa jambo hilo.

Kwa karne nyingi, Wasamaria walimwabudu Mungu kwenye hekalu kubwa lililokuwa katika Mlima Gerizimu huko Samaria. “Baba zetu wa zamani waliabudu katika mlima huu; lakini nyinyi watu husema kwamba katika Yerusalemu ndipo penye mahali ambapo watu wapaswa kuabudia,” mwanamke Msamaria akamwambia Yesu. Yesu alijibu kwa kusema: “Niamini mimi, mwanamke, Saa inakuja wakati ambapo wala si katika mlima huu wala katika Yerusalemu nyinyi watu mtamwabudu Baba.” Hekalu halisi halingehitajiwa ili kumwabudu Yehova, kwa kuwa Yesu alisema: “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yeye lazima waabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:20, 21, 24) Baadaye Mtume Paulo aliwaambia Waathene hivi: “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyo katika huo, akiwa, kama Huyu alivyo, Bwana wa mbingu na dunia, hakai katika mahekalu yaliyofanywa kwa mikono.”—Matendo 17:24.

Ni wazi kwamba, majengo ya kidini ya dini zinazojiita eti za Kikristo hayana uhusiano wowote na mpango uliokuwako wa kuwa na hekalu kabla ya Ukristo. Nao Wakristo wa karne ya kwanza hawakuwa na sababu ya kujenga majengo kama hayo. Hata hivyo, baada ya mitume kufa, kukengeuka kutoka kwa mafundisho ya kweli, yaani ule uasi-imani, ulitukia. (Matendo 20:29, 30) Miaka mingi kabla Maliki Mroma Konstantino hajageuzwa imani kuwa Mkristo mwaka wa 313 W.K., watu waliodai kuwa Wakristo walianza kuacha mafundisho ya Yesu.

Konstantino alichangia kuchanganya “Ukristo” na dini ya kipagani ya Roma. Kichapo The Encyclopædia Britannica kinasema: “Konstantino mwenyewe aliagiza kujengwa kwa basilika tatu kubwa za Kikristo huko Roma: Basilika ya Mtakatifu Petro, S. Paolo Fuori le Mura, na S. Giovanni huko Laterano. Ndiye . . . aliyechora ramani za ujenzi za makanisa yenye muundo wa msalaba ambayo yalijengwa huko Ulaya magharibi katika Enzi za Kati.” Basilika ya Mtakatifu Petro ya Roma ambayo imejengwa upya bado huonwa kuwa kituo muhimu cha Kanisa Katoliki.

“Kanisa lilianza kufuata desturi na namna fulani za ibada zilizokuwako huko Roma kabla ya Ukristo,” asema mwanahistoria Will Durant. Pia “ramani za kujenga basilika” zilikuwa miongoni mwa mambo waliyofuata. Kuanzia karne ya 10 hadi ya 15, makanisa na makathedro mengi sana yalijengwa, huku ramani za ujenzi zikikaziwa zaidi. Wakati huo ndipo majengo mengi ya dini zinazojiita eti za Kikristo ambayo sasa huonwa kuwa ya kiusanii yalipoanza kujengwa.

Je, watu hupata burudiko na kitia-moyo cha kiroho kwa kuabudu kanisani? “Nilianza kuona mambo ya kanisa kuwa yenye kuchosha sana,” asema Francisco kutoka Brazili. “Misa haikuwa na maana yoyote, ilikuwa sherehe inayofanywa kwa kurudiwa-rudiwa na haikutosheleza mahitaji yangu. Nilifurahi misa ilipoisha.” Hata hivyo, waamini wa kweli wanaamriwa wakusanyike pamoja. Wanapaswa kukusanyika kwa kufuata utaratibu gani?

“Kutaniko Lililo Katika Nyumba Yao”

Wakristo wa kweli hufuata kielelezo cha waamini wa karne ya kwanza wanapokusanyika pamoja. Maandiko yanaonyesha kwamba kwa kawaida walikusanyika pamoja katika nyumba za faragha. Kwa mfano, mtume Paulo aliandika hivi: “Wapeni salamu zangu Priska na Akila wafanyakazi wenzangu katika Kristo Yesu, . . . na salimuni kutaniko lililo katika nyumba yao.” (Waroma 16:3, 5; Wakolosai 4:15; Filemoni 2) Neno la Kigiriki linalomaanisha “kutaniko” (ek·kle·siʹa) linatafsiriwa “kanisa” katika tafsiri fulani za Kiingereza, kama vile King James Version. Lakini neno hilo halimaanishi jengo fulani bali linamaanisha kikundi cha watu waliokusanyika pamoja wakiwa na kusudi moja. (Matendo 8:1; 13:1) Ibada ya Wakristo wa kweli haihitaji majengo ya kidini yenye fahari.

Mikutano ilifanywaje katika makutaniko ya Kikristo ya mapema? Mwanafunzi Yakobo anatumia namna fulani ya neno la Kigiriki sy·na·go·geʹ kurejelea mkutano wa Kikristo. (Yakobo 2:2, kielezi-chini) Neno hilo la Kigiriki linamaanisha “kukusanya pamoja” nalo lina maana sawa na neno ek·kle·siʹa. Hata hivyo, baada ya muda, neno “sinagogi” likaja kumaanisha mahali au jengo ambapo kusanyiko lilifanyiwa. Wakristo wa kwanza Wayahudi walielewa mambo yaliyofanyika kwenye sinagogi. *

Ingawa Wayahudi walikutanika kwenye hekalu huko Yerusalemu kwa ajili ya sherehe zilizofanywa kila mwaka, masinagogi yalikuwa mahali pa kujifunza juu ya Yehova na kuelimishwa kuhusu Sheria. Yaonekana mambo yaliyofanywa kwenye masinagogi yalitia ndani sala na kusoma Maandiko, na vilevile mazungumzo ya kindani kuhusu Maandiko na kuhimizana. Paulo na wenzake walipoingia kwenye sinagogi huko Antiokia, “maofisa-wasimamizi wa sinagogi wa[li]tuma watu kwao, wakisema: ‘Wanaume, akina ndugu, ikiwa kuna neno lolote la kitia-moyo mlilo nalo kwa ajili ya watu, lisemeni.’” (Matendo 13:15) Wakristo Wayahudi wa kwanza walipokusanyika pamoja kwenye nyumba za faragha, yaonekana walifuata mfano huo, na wakafanya mikutano yenye kujenga kiroho ambapo Maandiko yalitumiwa kufundisha.

Makutaniko kwa Ajili ya Kutiana Moyo

Kama Wakristo wa mapema, Mashahidi wa Yehova leo hukusanyika pamoja katika majengo mbalimbali ya ibada ili kupokea mafundisho ya Biblia na kufurahia ushirika ujengao. Kwa miaka mingi walikusanyika katika nyumba za faragha nao hufanya hivyo katika sehemu fulani leo. Lakini sasa idadi ya makutaniko imefikia zaidi ya 90,000, na majengo yao ya kukutania yanaitwa Majumba ya Ufalme. Majengo yao hayana madoido mengi, nayo hayafanani na makanisa. Ni majengo yanayofaa na sahili, nayo hutumiwa na makutaniko ya watu 100 hadi 200 ambao hukutanika kila juma ili kusikiliza na kujifunza Neno la Mungu.

Makutaniko mengi ya Mashahidi wa Yehova hufanya mikutano yao mara tatu kwa juma. Mkutano mmoja ni hotuba ya watu wote inayohusu habari ya kisasa iliyo muhimu. Mkutano huo hufuatwa na funzo linalozungumzia habari fulani au unabii wa Biblia, kwa kutumia gazeti Mnara wa Mlinzi. Mkutano mwingine ni shule inayokusudiwa kusaidia watu waeleze wengine ujumbe wa Biblia. Inafuatwa na mkutano ambao umekusudiwa kuandaa madokezo yanayofaa kuhusu huduma ya Kikristo. Mashahidi pia hukusanyika mara moja kwa juma katika vikundi vidogo kwenye nyumba za faragha kwa ajili ya funzo la Biblia. Watu wote wanakaribishwa kwenye mikutano hiyo. Kiingilio ni bure.

Francisco, aliyetajwa hapo awali, aliona kwamba mikutano inayofanywa katika Jumba la Ufalme inanufaisha sana. Anasema: “Nilihudhuria mkutano wangu wa kwanza kwenye jengo moja zuri lililokuwa katikati mwa jiji, na niliondoka huko nikiwa nimevutiwa na mahali hapo. Wahudhuriaji walikuwa na urafiki, na nilihisi upendo miongoni mwao. Nilitamani sana kurudi huko. Kwa kweli, sijakosa mkutano tangu wakati huo. Mikutano hiyo ya Kikristo inachochea, nayo hutosheleza mahitaji yangu ya kiroho. Hata ninapohisi kuwa nimevunjika moyo kwa sababu fulani, mimi huenda kwenye Jumba la Ufalme nikiwa na uhakika kwamba nitarudi nyumbani nikiwa nimetiwa moyo.”

Utapata elimu ya Biblia, ushirika ujengao, na fursa ya kumsifu Mungu kwenye mikutano ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova. Tunakukaribisha kwa uchangamfu uhudhurie mikutano kwenye Jumba la Ufalme lililo karibu na nyumbani kwako. Utafurahi sana ukifanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Hekalu hilo lilibomolewa kabisa na Waroma. Ukuta wa Kilio, ambapo Wayahudi wengi kutoka sehemu za mbali huja kusali, si sehemu ya hekalu hilo. Ni sehemu ya ukuta wa ua wa hekalu.

^ fu. 20 Inaonekana kwamba masinagogi yalianza kutumiwa wakati wa ile miaka 70 ya utekwa huko Babiloni wakati ambapo hakukuwa na hekalu au muda mfupi baada ya Wayahudi kurudi kutoka utekwani, hekalu lilipokuwa likijengwa upya. Kufikia karne ya kwanza, kila mji wa Palestina ulikuwa na sinagogi lake, miji mikubwa zaidi ilikuwa na masinagogi kadhaa.

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Maskani na baadaye mahekalu yalitumiwa kuwa vituo vinavyofaa vya kumwabudia Yehova

[Picha katika ukurasa wa 6]

Basilika ya Mtakatifu Petro huko Roma

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wakristo wa mapema walikusanyika pamoja katika nyumba za faragha

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Mashahidi wa Yehova hufanya mikutano yao ya Kikristo katika nyumba za faragha na kwenye Majumba ya Ufalme