Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunawezaje Kuishi Maisha Yanayompendeza Yehova?

Tunawezaje Kuishi Maisha Yanayompendeza Yehova?

Tunawezaje Kuishi Maisha Yanayompendeza Yehova?

‘Jana, kati ya mapambazuko na machweo, saa mbili muhimu sana zilipotea, kila saa ikiwa na muda wa dakika sitini. Dakika hizo haziwezi kupatikana kamwe, zimetokomea kabisa!’—Lydia H. Sigourney, mwandishi Mmarekani (1791-1865).

SIKU za maisha yetu zinaonekana kuwa chache sana na zinapita haraka. Mtunga-zaburi Daudi alitafakari mno kuhusu ufupi wa maisha na hilo lilimfanya asali hivi: “BWANA, unijulishe mwisho wangu, na kiasi cha siku zangu ni kiasi gani; nijue jinsi nilivyo dhaifu. Tazama, umefanya siku zangu kuwa mashubiri; maisha yangu ni kama si kitu mbele zako.” Daudi alitaka kuishi maisha yanayompendeza Mungu kwa maneno na kwa matendo yake. Alionyesha anamtegemea Mungu kwa kusema hivi: “Matumaini yangu ni kwako.” (Zaburi 39:4, 5, 7) Yehova alimsikiliza. Alichunguza matendo ya Daudi na kumthawabisha.

Ni rahisi sana kuwa na shughuli nyingi kila dakika na kunaswa katika hekaheka za maisha ya kila siku. Hekaheka hizo zinaweza kutuletea mahangaiko kwa sababu ya kuwa na mambo mengi ya kufanya na kukosa wakati wa kuyafanya. Je, tunajitahidi kuishi maisha yanayompendeza Mungu kama Daudi alivyofanya? Bila shaka Yehova humchunguza kwa makini kila mmoja wetu. Yapata miaka 3,600 iliyopita, Ayubu, aliyemcha Mungu alikiri kwamba Yehova aliona njia zake na kuhesabu hatua zake zote. Ayubu alijiuliza hivi: “Naye atakapozuru, nitamjibuje?” (Ayubu 31:4-6, 14) Tunaweza kuishi maisha yanayompendeza Mungu kwa kutanguliza mambo ya kiroho, kutii amri zake, na kutumia wakati wetu kwa hekima. Hebu tuchunguze mambo hayo kwa makini.

Tanguliza Mambo ya Kiroho

Maandiko yaliyoandikwa kwa mwongozo wa Mungu yanatuhimiza tutangulize mambo ya kiroho, yanaposema hivi: ‘Hakikisheni mambo yaliyo ya maana zaidi.’ Mambo yaliyo ya maana zaidi ni yapi? Yanahusiana na “ujuzi sahihi na ufahamu kamili.” (Wafilipi 1:9, 10) Ni lazima tutumie wakati wetu kwa hekima ili tupate kujua kusudi la Yehova. Hata hivyo, tukitanguliza mambo ya kiroho tutaishi maisha yenye kuridhisha na yenye kuthawabisha.

Mtume Paulo anatukumbusha ‘tufulize kuhakikisha ni nini lililo lenye kukubalika kwa Bwana.’ Tutahakikisha mambo hayo kwa kuchunguza nia na mwelekeo wetu wa moyoni. Mtume huyo aendelea kusema: “Endeleeni kufahamu mapenzi ya Yehova ni nini.” (Waefeso 5:10, 17) Basi, ni nini kinachompendeza Yehova? Mithali moja ya Biblia inajibu: “Bora hekima, basi jipatie hekima; naam, kwa mapato yako yote jipatie ufahamu. Umtukuze, naye atakutukuza.” (Mithali 4:7, 8) Yehova hupendezwa sana na mtu anayejipatia hekima ya kimungu na kuitumia. (Mithali 23:15) Hekima hiyo ni bora sana kwa sababu haiwezi kuibiwa au kuharibiwa. Kwa kweli, inamlinda na kumhifadhi mtu kutokana na “njia ya uovu na  watu wanenao yaliyopotoka.”—Mithali 2:10-15.

Basi ni jambo la hekima kuepuka mwelekeo wa kutojali mambo ya kiroho! Tunahitaji kusitawisha mwelekeo wa kuthamini maagizo ya Yehova na kuwa na hofu inayofaa kumwelekea. (Mithali 23:17, 18) Ingawa tunaweza kukuza mwelekeo huo wakati wowote maishani, ni vyema zaidi kukuza mwelekeo huo unaofaa na kufuata kabisa kanuni za Biblia ujanani. “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako,” asema Mfalme Solomoni mwenye hekima.—Mhubiri 12:1.

Njia bora ya kuwa na uhusiano wa karibu sana na Yehova ni kusali faraghani kila siku. Daudi alitambua umuhimu wa kumwambia Yehova mambo yaliyo moyoni mwake, kwa kuwa alimsihi hivi: “Ee BWANA, usikie maombi yangu, utege sikio lako niliapo, usiyanyamalie machozi yangu.” (Zaburi 39:12) Je, nyakati nyingine uhusiano wetu wa karibu pamoja na Mungu hutugusa moyo kiasi cha kutufanya tulie machozi? Kwa kweli, kadiri tunavyomfunulia Yehova mambo yaliyo moyoni mwetu na kutafakari Neno lake, ndivyo anavyozidi kutukaribia.—Yakobo 4:8.

Jifunze Kutii

Musa pia alikuwa na imani na alitambua kwamba uhai wake unamtegemea Mungu. Kama Daudi, Musa aliona jinsi maisha yalivyojaa taabu. Kwa hiyo alimsihi Mungu amwonyeshe jinsi ya ‘kuzihesabu siku zake, na kujipatia moyo wa hekima.’ (Zaburi 90:10-12) Angejipatia moyo wa hekima kwa kujifunza na kuishi tu kupatana na sheria na kanuni za Yehova. Musa alijua hilo na hivyo alijitahidi sana kukazia kweli hiyo muhimu kwa taifa la Israeli kwa kuwasomea tena na tena sheria na maagizo ya Mungu muda mfupi kabla ya kuingia katika Bara Lililoahidiwa. Mwanadamu yeyote ambaye angeteuliwa na Yehova kutawala Waisraeli alipaswa kujiandikia nakala yake ya Sheria na kuisoma siku zote za maisha yake. Kwa nini? Ili ajifunze kumhofu Mungu. Mfalme angeonyesha kwamba yeye ni mtiifu kwa kufanya hivyo. Sheria hiyo ingemlinda ili asiuinue moyo wake juu ya ndugu zake na pia ingefanya siku za utawala wake ziwe nyingi. (Kumbukumbu la Torati 17:18-20) Yehova alirudia ahadi hiyo alipomwambia Solomoni, mwana wa Daudi hivi: “Ukienda katika njia zangu, na kuyashika mausia yangu, na amri zangu, kama baba yako Daudi alivyokwenda, basi nitazifanya siku zako kuwa nyingi.”—1 Wafalme 3:10-14.

Kutii ni muhimu sana machoni pa Mungu. Kama tukipuuza na kudharau matakwa na amri fulani za Yehova, bila shaka ataona mwelekeo huo. (Mithali 15:3) Kujua hivyo kunapasa kutufanya tutii kabisa amri zote za Yehova, hata ingawa huenda isiwe rahisi kufanya hivyo sikuzote. Tunapojitahidi kutii sheria na amri za Mungu, Shetani anafanya yote awezayo ‘kukatiza pito letu.’—1 Wathesalonike 2:18.

Ni muhimu hasa kutii shauri la Maandiko la kukutana pamoja kwa ajili ya ibada na ushirika. (Kumbukumbu la Torati 31:12, 13; Waebrania 10:24, 25) Kwa hiyo tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, nimeazimia kabisa-kabisa kufanya jambo linalofaa?’ Kupuuza ushirika na mafundisho yanayotolewa kwenye mikutano ya Kikristo ili kujaribu kutafuta usalama wa kifedha kutaharibu uhusiano wetu na Yehova. Mtume Paulo aliandika hivi: “Acheni namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa fedha, huku nyinyi mkiridhika na vitu vilivyopo. Kwa maana [Yehova] amesema: ‘Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote.’” (Waebrania 13:5) Kutii amri za Yehova kwa hiari kunaonyesha tunatumaini kabisa kwamba atatutunza.

Yesu alijifunza utii na alifaidika. Sisi pia tunaweza kufanya hivyo. (Waebrania 5:8) Kadiri tunavyozidi kujifunza utii, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kutii hata mambo madogo-madogo. Huenda tukalazimika kuvumilia mnyanyaso kwa sababu ya uaminifu wetu, hasa kazini, shuleni, au katika familia iliyogawanyika kidini. Lakini, tunafarijiwa na ahadi ambayo Waisraeli walipewa kwamba kama ‘wangempenda Yehova kwa kuitii sauti yake na kushikamana naye; angekuwa uzima wao na wingi wa siku zao.’ (Kumbukumbu la Torati 30:20) Tumepewa ahadi hiyohiyo.

Tumia Wakati kwa Hekima

Kutumia wakati kwa hekima kutatusaidia pia kuishi maisha yanayompendeza Yehova. Wakati si kama pesa ambazo zinaweza kuwekwa akiba, ni lazima utumiwe la sivyo utapotea. Kila saa inayopita inatokomea kabisa. Kwa kuwa hatuna wakati wa kutosha kufanya mambo yote tunayotaka, je, tunatumia wakati wetu kutimiza malengo yetu maishani? Lengo kuu la Wakristo wote lapasa kuwa kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

Tutatumia wakati wetu kwa hekima tukitambua tu umuhimu wake. Ndiyo sababu andiko la Waefeso 5:16 linatuhimiza ‘tujinunulie kabisa wakati unaofaa,’ na hilo lamaanisha kuacha mambo yasiyo na maana sana. Lamaanisha kupunguza mambo yanayopoteza wakati. Kutazama televisheni au kutumia Internet kwa muda mrefu, kusoma vichapo vya kilimwengu visivyo na faida, au kutumia wakati mwingi katika tafrija na burudani huchosha. Isitoshe, kurundika mali nyingi mno kunaweza kupoteza wakati tunaohitaji kutumia ili kujipatia moyo wa hekima.

Watu wanaotoa mashauri kuhusu jinsi ya kuokoa wakati wanasema: “Huwezi kamwe kutumia wakati wako vizuri usipokuwa na miradi hususa.” Wanadokeza mambo matano ya kuzingatia unapoweka miradi: weka miradi hususa, miradi ambayo maendeleo yanaweza kukadiriwa, inayoweza kutimizwa, inayofaa, iliyoratibiwa.

Mradi mmoja unaofaa ni kuboresha usomaji wetu wa Biblia. Hatua ya kwanza ni kuwa na mradi hususa—kusoma Biblia nzima. Hatua ya pili ni kuweza kukadiria maendeleo ya mradi wetu. Tukifanya hivyo, tunaweza kujua mambo ambayo tunatimiza. Miradi inapasa kutuchochea tufanye maendeleo na kukua. Ni lazima pia iwe miradi inayofaa na inayoweza kutimizwa. Ni lazima utilie maanani uwezo wako, ustadi na wakati ulio nao. Huenda wengine wakahitaji muda zaidi ili kutimiza mradi wao. Mwishowe, tunahitaji kuratibu mradi wetu. Kupanga tarehe ya kutimiza jambo fulani kunaweza kutuchochea tulitimize.

Washiriki wote wa familia ya Betheli ulimwenguni pote, ambao wanatumikia kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova au katika mojawapo ya ofisi za tawi ulimwenguni pote, wana mradi hususa wa kusoma Biblia nzima mwaka wao wa kwanza Betheli. Wanatambua kwamba usomaji mzuri wa Biblia huwasaidia kufanya maendeleo ya kiroho na kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova, ambaye anawafundisha ili wafaidike. (Isaya 48:17) Je, tunaweza pia kuweka mradi wa kusoma Biblia kwa ukawaida?

Faida za Kuishi Maisha Yanayompendeza Yehova

Tutapata baraka nyingi sana tukitanguliza mambo ya kiroho maishani. Kwanza, kunatusaidia kutimiza mambo mengi na kuwa na kusudi maishani. Kuzungumza na Yehova kwa ukawaida kupitia sala inayotoka moyoni hufanya tumkaribie. Tunaposali tunaonyesha kwamba tunamtumaini. Kusoma Biblia kila siku na kusoma vichapo vinavyozungumzia Biblia ambavyo vinatayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kunaonyesha kwamba tuko tayari kumsikiliza Mungu anapozungumza nasi. (Mathayo 24:45-47) Hilo linatusaidia kujipatia moyo wa hekima unaotuwezesha kufanya maamuzi na machaguzi yanayofaa maishani.—Zaburi 1:1-3.

Tunafurahia kutii amri za Yehova, kwa sababu si zenye kulemea. (1 Yohana 5:3) Tunapojitahidi kuishi maisha yanayompendeza Yehova kila siku, tunaimarisha uhusiano wetu naye. Tunawategemeza kwelikweli kiroho Wakristo wenzetu. Mambo hayo yanamfurahisha Yehova Mungu. (Mithali 27:11) Hakuna jambo lenye kuthawabisha kama kupata kibali cha Yehova sasa na milele!

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wakristo wanaona mambo ya kiroho kuwa muhimu sana

[Picha katika ukurasa wa 22]

Je, unatumia wakati wako kwa hekima?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tunapojitahidi kuishi maisha yanayompendeza Yehova kila siku, tunaimarisha uhusiano wetu naye