Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakristo Wanahitajiana

Wakristo Wanahitajiana

Wakristo Wanahitajiana

“Sisi ni viungo vya mtu na mwenzake.”—WAEFESO 4:25.

1. Kichapo kimoja kinasema nini kuhusu mwili wa binadamu?

MWILI wa binadamu umeumbwa kwa njia ya ajabu sana! Kichapo The World Book Encyclopedia kinasema: “Nyakati nyingine watu huuita mwili wa binadamu mashine—mashine bora zaidi kuwahi kutengenezwa. Bila shaka, mwili wa binadamu si mashine. Lakini unaweza kulinganishwa na mashine katika njia mbalimbali. Kama mashine, mwili una viungo vingi. Kila kiungo cha mwili, kama vile ilivyo na kila sehemu ya mashine, hufanya kazi fulani hususa. Lakini viungo au sehemu hizo zote hushirikiana na hivyo kufanya mwili au mashine ifanye kazi vizuri.”

2. Ni katika njia gani mwili wa binadamu na kutaniko la Kikristo zinafanana?

2 Naam, mwili wa binadamu una viungo vingi na kila kiungo hutimiza kazi fulani muhimu. Hakuna hata mshipa mmoja, msuli, au kiungo chochote cha mwili kisichokuwa cha maana. Vivyo hivyo, kila mmoja katika kutaniko la Kikristo anaweza kuchangia kwa kadiri fulani hali nzuri ya kiroho ya kutaniko. (1 Wakorintho 12:14-26) Hakuna mshiriki wa kutaniko anayepaswa kujiona kuwa bora kuliko wengine, wala hakuna mmoja anayepaswa kujiona kuwa hafai kitu.—Waroma 12:3.

3. Andiko la Waefeso 4:25 linaonyeshaje kwamba Wakristo wanahitajiana?

3 Kama vile viungo vya mwili vinavyotegemeana, Wakristo wanahitajiana. Mtume Paulo aliwaambia waamini wenzake watiwa-mafuta hivi: “Sasa kwa kuwa mmeweka mbali ukosefu wa lililo kweli, semeni kweli kila mmoja wenu pamoja na jirani yake, kwa sababu sisi ni viungo vya mtu na mwenzake.” (Waefeso 4:25) Kwa kuwa wao ni viungo “vya mtu na mwenzake,” washiriki wa Israeli wa kiroho—“mwili wa Kristo”—husema kweli kila mmoja na mwenzake na hushirikiana kabisa. Naam kila mmoja wao ni sehemu ya wale wengine wote. (Waefeso 4:11-13) Israeli hao wa kiroho wana umoja na Wakristo walio na tumaini la kuishi duniani ambao pia husema kweli na kushirikiana nao kwa furaha.

4. Wapya wanaweza kusaidiwa katika njia zipi?

4 Kila mwaka, mamia ya walio na tumaini la kuishi katika dunia paradiso hubatizwa. Washiriki wengine wa kutaniko huwasaidia kwa furaha ‘wasonge mbele kwenye ukomavu.’ (Waebrania 6:1-3) Huenda wao huwasaidia kwa kujibu maswali ya Biblia wanayouliza au kwa kuwaunga mkono katika kazi ya kuhubiri. Tunaweza kuwasaidia wapya kwa kuwawekea kielelezo bora kwa kutoa maelezo kwa ukawaida katika mikutano ya Kikristo. Tunaweza pia kuwatia moyo au labda kuwafariji wakati wa msiba. (1 Wathesalonike 5:14, 15) Tunapaswa kutafuta njia za kuwasaidia wengine ‘waendelee kutembea katika kweli.’ (3 Yohana 4) Tuwe wachanga au wazee, tuwe tumeanza tu kutembea katika kweli au tumefanya hivyo kwa muda mrefu, tunaweza kuboresha hali ya kiroho ya waamini wenzetu—nao kwa kweli wanatuhitaji.

Walitoa Msaada Uliohitajiwa

5. Akila na Prisila walimsaidiaje Paulo?

5 Wakristo waliofunga ndoa ni baadhi ya wale wanaofurahia kuwasaidia waamini wenzao. Kwa mfano Akila na mkewe Prisila (Priska), walimsaidia Paulo. Walimkaribisha nyumbani kwao, wakafanya pamoja naye kazi ya kutengeneza mahema, na kumsaidia kuliimarisha kutaniko jipya la Korintho. (Matendo 18:1-4) Kwa njia fulani ambayo haikutajwa, hata walihatarisha uhai wao kwa niaba ya Paulo. Walikuwa wakiishi Roma wakati Paulo alipowaambia Wakristo wa Roma hivi: “Wapeni salamu zangu Priska na Akila wafanyakazi wenzangu katika Kristo Yesu, ambao wamehatarisha shingo zao wenyewe kwa ajili ya nafsi yangu, ambao si mimi tu bali pia makutaniko yote ya mataifa yawashukuru.” (Waroma 16:3, 4) Kama Akila na Prisila, baadhi ya Wakristo wa siku hizi huimarisha makutaniko na kuwasaidia waamini wenzao katika njia mbalimbali, nyakati nyingine hata wakihatarisha uhai wao ili wawalinde watumishi wengine wa Mungu wasitendwe kikatili au kuuawa na wanyanyasaji.

6. Apolo alipokea msaada gani?

6 Akila na Prisila pia walimsaidia Apolo, Mkristo mwenye ufasaha aliyekuwa akiwafundisha wakazi wa Efeso juu ya Yesu Kristo. Wakati huo, Apolo alifahamu tu ubatizo uliofanywa na Yohana ambao ulikuwa ishara ya toba kwa dhambi dhidi ya agano la Sheria. Walipotambua kwamba Apolo alihitaji msaada, Akila na Prisila “walimfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.” Inaelekea kwamba walimweleza kuhusu ubatizo wa Kikristo uliotia ndani kuzamishwa majini na kupokea roho takatifu. Apolo alitenda kupatana na yale aliyojifunza. Baadaye akiwa huko Akaya, Apolo “aliwasaidia sana wale waliokuwa wameamini kwa sababu ya fadhili isiyostahiliwa ya Mungu; kwa maana kwa juhudi nyingi alithibitisha kikamili hadharani kuwa Wayahudi ni wenye makosa, huku akionyesha kwa Maandiko kwamba Yesu alikuwa ndiye Kristo.” (Matendo 18:24-28) Mara nyingi maelezo yanayotolewa na waabudu wenzetu yanaweza kutusaidia kulielewa Neno la Mungu vyema zaidi. Hivyo, tunahitajiana pia katika jambo hilo.

Kutoa Msaada wa Kimwili

7. Wafilipi walitendaje wakati Wakristo wenzao walipohitaji msaada wa kimwili?

7 Washiriki wa kutaniko la Kikristo la Filipi walimpenda sana Paulo nao walimpelekea vitu vya kimwili alivyohitaji alipokuwa akiishi Thesalonike. (Wafilipi 4:15, 16) Wakati ndugu huko Yerusalemu walipohitaji msaada wa kimwili, Wafilipi walikuwa tayari hata kuchanga zaidi ya uwezo wao. Paulo alishukuru sana kwa roho ambayo ndugu na dada hao wa Filipi walionyesha hivi kwamba aliwataja kuwa mfano kwa waamini wengine.—2 Wakorintho 8:1-6.

8. Epafrodito alionyesha mtazamo gani?

8 Paulo alipokuwa kifungoni, Wafilipi walimpelekea zawadi za kimwili na pia wakatuma mjumbe wao, Epafrodito. Paulo alisema, “Kwa ajili ya kazi ya Bwana [Epafrodito] alikaribia sana kifo, akihatarisha nafsi yake, ili apate kujazia kikamili kutokuwapo kwenu hapa ili kutoa utumishi wa faragha kwangu.” (Wafilipi 2:25-30; 4:18) Hatuambiwi kama Epafrodito alikuwa mzee au mtumishi wa huduma. Hata hivyo, alikuwa Mkristo mwenye kujitolea na mwenye kusaidia, naye Paulo alimhitaji kwelikweli. Je, kuna mtu aliye kama Epafrodito katika kutaniko lenu?

Walikuwa ‘Misaada Yenye Kutia Nguvu’

9. Aristarko anatuwekea kielelezo gani?

9 Ndugu na dada wenye upendo kama Akila, Prisila, na Epafrodito, wanathaminiwa sana katika kutaniko lolote lile. Huenda baadhi ya waabudu wenzetu wakawa kama Aristarko, Mkristo wa karne ya kwanza. Yeye na wengine walikuwa “msaada wenye kutia nguvu.” Yawezekana kuwa waliwafariji au kuwasaidia wengine katika mambo fulani ya msingi. (Wakolosai 4:10, 11) Kwa kumsaidia Paulo, Aristarko alikuwa rafiki wa kweli wakati wa uhitaji. Alikuwa na sifa zinazotajwa kwenye Mithali 17:17: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” Je, haitupasi sote kujitahidi kuwa ‘misaada yenye kutia nguvu’ kwa Wakristo wenzetu? Tunapaswa hasa kuwasaidia wale waliopatwa na msiba.

10. Petro aliweka kielelezo gani kwa wazee Wakristo?

10 Wazee Wakristo hasa wanapaswa kuwa misaada yenye kutia nguvu kwa ndugu na dada zao wa kiroho. Kristo alimwambia mtume Petro hivi: “Watie nguvu ndugu zako.” (Luka 22:32) Petro aliweza kufanya hivyo kwa sababu alikuwa imara sana, hasa baada ya Yesu kufufuliwa. Wazee, jitahidini kadiri mwezavyo kufanya vivyo hivyo bila kulazimishwa na kwa wororo, kwa kuwa waamini wenzenu wanawahitaji.—Matendo 20:28-30; 1 Petro 5:2, 3.

11. Tunaweza kunufaikaje kwa kufikiria mtazamo wa Timotheo?

11 Timotheo aliyeandamana na Paulo katika safari zake alikuwa mzee aliyejali sana Wakristo wengine. Ingawa alikuwa na matatizo fulani ya kiafya, Timotheo alionyesha imani thabiti naye ‘alitumikia pamoja na Paulo katika kuendeleza habari njema.’ Kwa hiyo mtume huyo angeweza kuwaambia hivi Wafilipi: “Kwa maana sina mwingine yeyote mwenye mwelekeo kama wake atakayejali kihalisi mambo yanayohusiana nanyi.” (Wafilipi 2:20, 22; 1 Timotheo 5:23; 2 Timotheo 1:5) Tunaweza kuwanufaisha wale wanaoabudu Yehova pamoja nasi kwa kuwa na mtazamo kama wa Timotheo. Ni kweli kwamba ni lazima tupambane na udhaifu wetu wenyewe na majaribu mbalimbali, lakini sisi pia tunaweza na tunapaswa kuonyesha imani yenye nguvu na kuwahangaikia kwa upendo ndugu na dada zetu wa kiroho. Tunapaswa kukumbuka sikuzote kwamba wanatuhitaji.

Wanawake Waliowajali Wengine

12. Tunaweza kujifunza nini kutokana na kielelezo cha Dorkasi?

12 Dorkasi alikuwa mmoja wa wanawake wenye kumwogopa Mungu waliowajali wengine. Alipokufa, wanafunzi walimwita Petro na kumpeleka katika chumba fulani cha juu. Humo, “wajane wote wakajitokeza kwake wakitoa machozi na kuonyesha mavazi mengi ya ndani na mavazi ya nje ambayo Dorkasi alikuwa na kawaida ya kuyafanya alipokuwa pamoja nao.” Dorkasi alifufuliwa na pasipo shaka akaendelea ‘kuzidi katika vitendo vyema na zawadi za rehema.’ Katika kutaniko la Kikristo leo, kuna wanawake kama Dorkasi ambao huenda wanashonea wengine mavazi au kuwatendea watu walio na uhitaji mambo fulani yanayoonyesha upendo. Bila shaka, matendo yao mazuri yanahusiana hasa na kuendeleza masilahi ya Ufalme na kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi.—Matendo 9:36-42; Mathayo 6:33; 28:19, 20.

13. Lidia alionyeshaje kwamba anawajali Wakristo wenzake?

13 Mwanamke mwenye kumwogopa Mungu aitwaye Lidia aliwajali wengine pia. Mwanamke huyo aliyezaliwa Thiatira alikuwa akiishi Filipi wakati Paulo alipohubiri huko yapata mwaka wa 50 W.K. Yaelekea Lidia alikuwa amebadili imani akawa mfuasi wa dini ya Wayahudi, lakini huenda hakukuwa na Wayahudi wengi wala sinagogi huko Filipi. Yeye na wanawake wengine waliomwogopa Mungu walikusanyika kwa ajili ya ibada kando ya mto wakati Paulo alipowatangazia habari njema. Masimulizi hayo yanasema: ‘Yehova alifungua wazi moyo wa Lidia ukazie uangalifu mambo yaliyokuwa yakisemwa na Paulo. Basi wakati yeye na watu wa nyumbani mwake walipobatizwa, alisema hivi kwa kusihi sana: “Ikiwa nyinyi watu mmenihukumu mimi kuwa mwaminifu kwa Yehova, ingieni ndani ya nyumba yangu mkae.” Naye akatushurutisha kwelikweli tuingie.’ (Matendo 16:12-15) Kwa kuwa Lidia alitaka kuwatendea wengine mema, alifanikiwa kuwashawishi Paulo na wenzake wakae naye. Tunathamini kama nini wakati Wakristo wenye fadhili na upendo wanapoonyesha sifa hiyo ya ukaribishaji leo!—Waroma 12:13; 1 Petro 4:9.

Tunawahitaji Enyi Vijana Pia

14. Yesu Kristo aliwatendeaje vijana?

14 Kutaniko la Kikristo lilianzishwa na Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliyekuwa mwenye fadhili na upendo. Watu hawakumwogopa kwa kuwa alikuwa mwenye upendo na huruma. Pindi moja, watu walipoanza kumletea Yesu watoto wao, wanafunzi wake walijaribu kuwafukuza. Lakini Yesu akawaambia: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwakomesha, kwa maana ufalme wa Mungu ni wa walio kama hao. Kwa kweli nawaambia nyinyi, Yeyote yule asiyeupokea ufalme wa Mungu kama mtoto mchanga hataingia kwa vyovyote ndani ya huo.” (Marko 10:13-15) Ili kupokea baraka za Ufalme, tunapaswa kuwa wanyenyekevu na wenye kufundishika kama watoto. Yesu alionyesha upendo wake kwa watoto kwa kuwakumbatia na kuwabariki. (Marko 10:16) Namna gani nyinyi vijana leo? Mnahakikishiwa kwamba mnapendwa na mnahitajiwa kutanikoni.

15. Andiko la Luka 2:40-52 linasimulia nini kuhusu maisha ya Yesu, naye aliwawekea vijana kielelezo gani?

15 Alipokuwa kijana, Yesu alimpenda Mungu na Maandiko pia. Alipokuwa na umri wa miaka 12, yeye na wazazi wake, Yosefu na Maria, walisafiri kutoka mji wao wa Nazareti kwenda Yerusalemu ili kusherehekea Sikukuu ya Kupitwa. Walipokuwa wakirudi nyumbani, wazazi wa Yesu waligundua kwamba hakuwa miongoni mwa wasafiri wenzao. Mwishowe walimpata ameketi katika jumba moja la hekalu, akiwasikiliza walimu Wayahudi na kuwauliza maswali. Yesu alishangaa kwamba Yosefu na Maria hawakujua mahali ambapo wangempata, hivyo akawauliza: “Je, hamkujua kwamba ni lazima mimi niwe katika nyumba ya Baba yangu?” Yesu alirudi nyumbani na wazazi wake, akajitiisha kwao, na akazidi kuwa na hekima na kukua kimwili. (Luka 2:40-52) Yesu aliwawekea vijana wetu kielelezo kizuri kama nini! Kwa kweli wanapaswa kuwatii wazazi wao na kupendezwa kujifunza mambo ya kiroho.—Kumbukumbu la Torati 5:16; Waefeso 6:1-3.

16. (a) Wavulana fulani walisema nini kwa sauti kubwa Yesu alipokuwa akitoa ushahidi hekaluni? (b) Vijana Wakristo wana pendeleo gani leo?

16 Ukiwa kijana, huenda ukawa unatoa ushahidi kumhusu Yehova shuleni na nyumba kwa nyumba pamoja na wazazi wako. (Isaya 43:10-12; Matendo 20:20, 21) Yesu alipokuwa akitoa ushahidi na kuwaponya watu kwenye hekalu muda mfupi kabla ya kifo chake, wavulana fulani walisema hivi kwa sauti kubwa: “Okoa Mwana wa Daudi, twasihi!” Makuhani wakuu na waandishi walikasirishwa sana na maneno hayo na kulalamika: “Je, wasikia yale wanayosema hawa?” “Ndiyo,” Yesu akajibu. “Je, nyinyi hamkusoma kamwe hili, ‘Kutoka kinywani mwa vitoto na watoto wanyonyao umetoa sifa’?” (Mathayo 21:15-17) Kama watoto hao, nyinyi vijana kutanikoni mna pendeleo zuri la kumsifu Mungu na Mwana wake. Tunataka na tunahitaji kushirikiana nanyi katika kutangaza Ufalme.

Msiba Unapotokea

17, 18. (a) Kwa nini Paulo alipanga michango itolewe kwa ajili ya Wakristo wa Yudea? (b) Michango ya hiari kwa ajili ya waamini kutoka Yudea ilikuwa na matokeo gani kwa Wakristo Wayahudi na wale wasio Wayahudi?

17 Hata hali yetu iweje, sisi huchochewa na upendo kuwasaidia Wakristo wenzetu walio na uhitaji. (Yohana 13:34, 35; Yakobo 2:14-17) Kwa kuchochewa na upendo kwa ndugu na dada zake huko Yudea, Paulo alipanga michango itolewe na makutaniko ya Akaya, Galatia, Makedonia, na wilaya ya Asia kwa ajili yao. Huenda mnyanyaso, msukosuko wa raia, na njaa iliyowapata wanafunzi huko Yerusalemu ilisababisha yale ambayo Paulo aliyaita “mateso,” “dhiki,” na ‘kuporwa kwa mali yao.’ (Waebrania 10:32-34; Matendo 11:27–12:1) Kwa hiyo alisimamia michango iliyotolewa kwa ajili ya Wakristo maskini wa Yudea.—1 Wakorintho 16:1-3; 2 Wakorintho 8:1-4, 13-15; 9:1, 2, 7.

18 Michango ya hiari kwa ajili ya watakatifu huko Yudea ilithibitisha kwamba kulikuwa na uhusiano wa kidugu kati ya waabudu wa Yehova—Wayahudi na watu wasio Wayahudi. Michango hiyo pia iliwawezesha Wakristo wasio Wayahudi kuonyesha shukrani zao kwa utajiri wa kiroho waliopokea kutoka kwa waabudu wenzao huko Yudea. Hivyo, walishiriki vitu vyao vya kimwili na vya kiroho. (Waroma 15:26, 27) Leo, michango kwa ajili ya waamini wenzetu wenye uhitaji hutolewa pia kwa hiari na huchochewa na upendo. (Marko 12:28-31) Tunahitajiana katika jambo hilo pia ili kuwe na usawaziko ‘na mtu aliye na vichache asiwe na vichache mno.’—2 Wakorintho 8:15.

19, 20. Toa mfano kuonyesha jinsi watu wa Yehova hutoa misaada wakati wa misiba.

19 Kwa kuwa tunajua kwamba Wakristo wanahitajiana, sisi huwa tayari kuwasaidia ndugu na dada zetu katika imani. Kwa mfano, fikiria yaliyotukia wakati tetemeko na maporomoko ya ardhi yaliyosababisha uharibifu mkubwa yalipoikumba El Salvador mapema mwaka wa 2001. Ripoti moja ilisema: “Ndugu katika sehemu zote za El Salvador walianza kutoa misaada. Vikundi vya akina ndugu kutoka Guatemala, Marekani, na Kanada walikuja kutusaidia. . . . Nyumba zaidi ya 500 na Majumba ya Ufalme 3 yenye kuvutia yalijengwa haraka. Ushahidi mkubwa umetolewa kupitia kazi ambayo ndugu hao wenye kujitolea walifanya kwa bidii na kwa ushirikiano.”

20 Ripoti moja kutoka Afrika Kusini ilisema: “Mafuriko mabaya sana yaliyokumba sehemu kubwa za Msumbiji yaliathiri pia wengi wa ndugu zetu Wakristo. Ofisi ya tawi huko Msumbiji ilipanga kushughulikia mahitaji yao. Lakini ndugu katika ofisi hiyo wakatuomba tuwatumie ndugu hao wenye uhitaji mavazi yaliyotumika ambayo hayakuwa yamechakaa. Tulikusanya mavazi yaliyojaa kontena yenye urefu wa meta 12 (ukubwa ulio sawa na vyumba vitatu vya kawaida) na kuwapelekea ndugu zetu huko Msumbiji.” Naam, hata katika mambo hayo pia, tunahitajiana.

21. Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

21 Kama ilivyotajwa awali, viungo vyote vya mwili wa binadamu ni muhimu. Bila shaka, hivyo ndivyo kutaniko la Kikristo lilivyo. Washiriki wote wanahitajiana. Wanahitaji pia kuendelea kutumikia kwa umoja. Makala ifuatayo itazungumzia mambo fulani yanayowawezesha kuwa na umoja.

Ungejibuje?

• Kuna ufanani gani kati ya mwili wa binadamu na kutaniko la Kikristo?

• Wakristo wa mapema walitendaje wakati waamini wenzao walipohitaji msaada wa kimwili?

• Ni mifano gani ya Kimaandiko inayoonyesha kwamba Wakristo wanahitaji kusaidiana?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Akila na Prisila waliwajali wengine

[Picha katika ukurasa wa 12]

Watu wa Yehova husaidiana na kuwasaidia wengine pia wakati wa msiba