Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Aliyokumbuka Yoshua

Aliyokumbuka Yoshua

Aliyokumbuka Yoshua

YEHOVA alimwambia Yoshua hivi: “Musa mtumishi wangu amekufa; haya basi, ondoka, vuka mto huu wa Yordani; wewe na watu hawa wote, mkaende hata nchi niwapayo.” (Yoshua 1:2) Yoshua alikuwa na mgawo mgumu kama nini! Alikuwa amemhudumia Musa kwa miaka 40 hivi, kisha akaambiwa achukue mahali pa bwana wake na kuwaongoza wana wa Israeli, ambao mara kwa mara walikuwa wagumu, hadi Nchi ya Ahadi.

Alipofikiria mambo ambayo angekabili baadaye, huenda Yoshua alikumbuka majaribu aliyokuwa amekabili na kuyashinda. Bila shaka, mambo aliyokumbuka yalimsaidia sana wakati huo, na yanaweza pia kuwasaidia Wakristo leo.

Mtumwa Awa Kamanda

Yoshua alikumbuka miaka mingi aliyokuwa mtumwa. (Kutoka 1:13, 14; 2:23) Tunaweza kuwazia tu mambo yaliyompata Yoshua wakati huo kwa kuwa Biblia haielezi mambo hayo kwa undani. Huenda Yoshua alijifunza kupanga mambo vizuri wakati wa utumishi wake huko Misri, na yawezekana alisaidia kupanga safari ya Waebrania na “kundi kubwa la watu waliochangamana” kutoka nchini humo.—Kutoka 12:38.

Yoshua alikuwa wa familia ya kabila la Efraimu. Babu yake Elishama alikuwa mkuu wa kabila hilo na yaelekea aliwaongoza wanaume 108,100 wenye silaha wa mojawapo ya migawanyo ya makabila matatu ya Israeli. (Hesabu 1:4, 10, 16; 2:18-24; 1 Mambo ya Nyakati 7:20, 26, 27) Hata hivyo, wakati Waamaleki walipowashambulia Waisraeli muda mfupi baada ya Waisraeli kutoka Misri, Musa alimwomba Yoshua apange jinsi ya kujikinga. (Kutoka 17:8, 9a) Kwa nini Yoshua alichaguliwa, na si babu yake au baba yake? Wazo moja ni: “Musa aliona kwamba [Yoshua] ndiye kiongozi aliyefaa zaidi kuchagua na kupanga askari kwa ajili ya vita kwa kuwa mbali na kuwa mkuu wa kabila muhimu la Efraimu, Yoshua alijulikana kwa ustadi wake katika kupanga mambo na alitumainiwa kabisa na watu.”

Hata sababu iwe nini, baada ya kuchaguliwa, Yoshua alifanya sawasawa na vile Musa alivyomwamuru. Ingawa Waisraeli hawakuwa na uzoefu wa vita, Yoshua alikuwa na hakika kwamba Mungu angewasaidia. Kwa hiyo, Musa alipomwambia, “kesho nitasimama juu ya kilele kile, na ile fimbo ya Mungu nitakuwa nayo mkononi mwangu,” Yoshua hakuhitaji uhakikisho zaidi. Bila shaka Yoshua alikumbuka kwamba Yehova alikuwa tu amemaliza kuiangamiza serikali kuu ya kijeshi ya wakati huo. Siku iliyofuata, Musa alipoinua mikono yake juu hadi jua lilipotua, hakuna adui aliyeweza kuwashinda Waisraeli, hata Waamaleki walishindwa. Kisha Yehova akamwamuru Musa aandike katika kitabu na ‘kuhubiri masikioni mwa Yoshua’ agizo hili: “Nitaufuta ukumbusho wa Amaleki kabisa, usiwe tena chini ya mbingu.” (Kutoka 17:9b-14) Naam, bila shaka Yehova angetekeleza hukumu hiyo.

Akiwa Mhudumu wa Musa

Lazima vita hivyo kati ya Waisraeli na Waamaleki viwe viliimarisha uhusiano kati ya Yoshua na Musa. Yoshua alikuwa na pendeleo la kuwa mhudumu wa kibinafsi wa Musa, “tangu ujana wake” hadi Musa alipokufa. Alimhudumia kwa miaka 40 hivi.—Hesabu 11:28.

Cheo hicho kilimaanisha kwamba angekuwa na mapendeleo na madaraka mbalimbali. Kwa mfano, yaelekea Yoshua alikuwa pamoja na Musa, Aroni, wana wa Aroni, na wazee 70 wa Israeli wakati walipokwea Mlima Sinai na kuona utukufu wa Yehova katika maono. Kwa kuwa alikuwa mhudumu, Yoshua aliandamana na Musa alipokwea juu zaidi na yaonekana aliachwa mbali kidogo Musa alipoingia katika wingu lililowakilisha kuwapo kwa Yehova. Hata yaonekana Yoshua alikaa mlimani siku 40, mchana na usiku. Yoshua alingojea kwa uaminifu kurudi kwa bwana wake Musa, naye alikuwapo kumlaki alipoanza safari ya kuteremka kutoka mlimani akiwa na yale mabamba ya Ushuhuda.—Kutoka 24:1, 2, 9-18; 32:15-17.

Baada ya Waisraeli kuabudu sanamu ya ndama ya dhahabu, Yoshua aliendelea kumhudumia Musa kwenye hema la kukutania, nje ya kambi. Huko Yehova alisema na Musa uso kwa uso. Lakini hata baada ya Musa kurudi kambini, Yoshua “hakutoka mle hemani.” Labda alihitajika awe huko ili awazuie Waisraeli wasiingie hemani wakiwa najisi. Yoshua alichukua daraka lake kwa uzito kama nini!—Kutoka 33:7, 11.

Lazima imani ya Yoshua iwe iliimarika sana kwa kushirikiana na Musa ambaye kulingana na Josephus, umri wake ulikuwa mkubwa kuliko wa Yoshua kwa miaka 35. Uhusiano wao umeelezwa kuwa “urafiki kati ya mtu aliyekomaa na kijana, kati ya bwana na mwanafunzi,” nao ulifanya Yoshua awe “mwanamume imara, mwenye kutegemeka.” Hatuna manabii kama Musa leo, lakini katika makutaniko ya watu wa Yehova kuna watu wazee wenye ustadi na hali nzuri ya kiroho ambao huwaimarisha wengine na kuwatia moyo sana. Je, unawathamini? Na je, unanufaika kutokana na ushirika wao?

Mpelelezi Kanaani

Jambo muhimu zaidi katika maisha ya Yoshua lilitukia muda mfupi baada ya Waisraeli kupewa Sheria. Alichaguliwa kuwakilisha kabila lake walipoenda kupeleleza Nchi ya Ahadi. Masimulizi hayo yanajulikana sana. Wapelelezi wote 12 walikubali kwamba nchi ya Kanaani ilikuwa na “wingi wa maziwa na asali,” kama vile Yehova alivyokuwa ameahidi. Hata hivyo, wapelelezi kumi wasio na imani walihofia kwamba Waisraeli hawangeweza kuiteka nchi hiyo kutoka kwa wakazi wake. Yoshua na Kalebu tu ndio waliowatia watu moyo wasiasi kwa sababu ya woga, kwa kuwa pasipo shaka Yehova angekuwa pamoja nao. Ndipo mkutano wote ukawalalamikia na kusema utawapiga wote wawili kwa mawe. Huenda wangalifanya hivyo kama Yehova hangaliingilia kwa wonyesho wa utukufu wake. Kwa sababu walikosa imani, Mungu aliagiza kwamba hakuna Mwisraeli aliyesajiliwa kuanzia umri wa miaka 20 au zaidi angeruhusiwa kuingia Kanaani. Kati ya Waisraeli hao, Yoshua, Kalebu, na Walawi tu ndio waliookoka.—Hesabu 13:1-16, 25-29; 14:6-10, 26-30.

Je, si Waisraeli wote walioona matendo makuu ya Yehova katika nchi ya Misri? Ni nini basi kilichomsaidia Yoshua kuwa na imani kwamba Mungu angewasaidia ingawa walio wengi walikuwa na shaka? Ni lazima Yoshua awe alikumbuka vizuri mambo yote ambayo Yehova alikuwa ameahidi na kufanya, naye aliyatafakari. Miaka mingi baadaye aliweza kusema, ‘halikupunguka hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena BWANA kwa Israeli, yote yametimia.’ (Yoshua 23:14) Hivyo, Yoshua alikuwa na imani kwamba ahadi zote ambazo Yehova alikuwa ametoa kuhusu wakati ujao zingetimizwa. (Waebrania 11:6) Jambo hilo linapasa kumfanya mtu ajiulize: ‘Namna gani mimi? Je, kujifunza kwa bidii na kutafakari juu ya ahadi za Yehova kumenihakikishia kwamba zinatumainika? Je, ninaamini kwamba Mungu anaweza kunilinda pamoja na watu wake wakati wa dhiki kubwa inayokuja?’

Mbali na imani, Yoshua pia alikuwa jasiri katika kufanya lililo jema. Yoshua na Kalebu walisimama imara upande wa Yehova, nao mkutano wote ukasema utawapiga kwa mawe. Ungehisije? Ungeogopa? Yoshua hakuogopa. Yeye na Kalebu walisema kwa uthabiti yale waliyoamini. Huenda siku moja tutalazimika kufanya vivyo hivyo kwa sababu ya uaminifu wetu kwa Yehova.

Masimulizi kuhusu wapelelezi hao pia hutufahamisha kwamba jina la Yoshua lilibadilishwa. Jina lake la awali lilikuwa Hoshea, linalomaanisha “Wokovu,” lakini Musa akaongeza herufi zinazowakilisha jina la Mungu na kumwita Yehoshua, au Yoshua linalomaanisha “Yehova Ni Wokovu.” Katika tafsiri ya Septuagint anaitwa “Yesu.” (Hesabu 13:8, 16) Na ili atimize maana ya jina hilo, Yoshua alitangaza kwa ujasiri kwamba Yehova ni wokovu. Jina la Yoshua halikubadilishwa kivivi hivi tu. Kubadilishwa kwa jina hilo kulionyesha kwamba Musa aliheshimu sifa za Yoshua na pia daraka la heshima ambalo angetimiza katika kuongoza kizazi kipya kuingia Nchi ya Ahadi.

Waisraeli walitangatanga nyikani kwa miaka 40 yenye kuchosha huku baba zao wakiendelea kufa mmoja baada ya mwingine. Hatujui lolote kumhusu Yoshua wakati huo. Hata hivyo, lazima awe alijifunza mambo mengi pindi hiyo. Yaelekea alishuhudia hukumu ya Mungu juu ya Kora, Dathani, na Abiramu waliokuwa waasi na juu ya wafuasi wao na wale walioshiriki ibada chafu ya Baali wa Peori. Yaelekea Yoshua alihuzunika sana kujua kwamba hata Musa hangeingia katika nchi ya ahadi kwa sababu ya kutomtakasa Yehova kuhusiana na maji ya Meriba.—Hesabu 16:1-50; 20:9-13; 25:1-9.

Achaguliwa Kuchukua Mahali pa Musa

Musa alipokaribia kufa, alimwomba Mungu achague mtu ambaye angechukua mahali pake ili Waisraeli wasiwe “kama kondoo wasio na mchungaji.” Yehova aliitikiaje? Yoshua, “mtu mwenye roho ndani yake,” angechaguliwa mbele ya mkutano wote nao walipaswa kumsikiliza. Hilo lilikuwa pendekezo lililoje! Yehova alikuwa ameona imani na uwezo wa Yoshua. Yeye ndiye aliyestahili kuchaguliwa kuwaongoza Waisraeli. (Hesabu 27:15-20) Hata hivyo, Musa alijua kwamba Yoshua angekuwa na kazi ngumu. Kwa hiyo, Musa akamtia moyo awe ‘hodari na mwenye moyo wa ushujaa,’ kwa kuwa Yehova angeendelea kuwa pamoja naye.—Kumbukumbu la Torati 31:7, 8.

Mungu mwenyewe alimpa Yoshua kitia-moyo hichohicho na kuongeza kusema: “Uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume, au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako. Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana. Je! Si mimi niliyekuamuru? Uwe hodari na moyo wa ushujaa; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa BWANA, Mungu wako, yu pamoja nawe kila uendako.”—Yoshua 1:7-9.

Yoshua hangeweza kuwa na shaka, kwa kuwa alikuwa na uzoefu na pia alikuwa bado anakumbuka maneno ya Yehova. Alikuwa na hakika kwamba angeiteka nchi ya Kanaani. Bila shaka kungekuwa na matatizo, na la kwanza kabisa lingekuwa kuvuka Mto Yordani ukiwa umefurika. Hata hivyo, Yehova mwenyewe alikuwa amemwamuru: “Ondoka, vuka mto huu wa Yordani.” Basi, hakuna jambo ambalo lingemzuia Yoshua.—Yoshua 1:2.

Mambo yaliyotukia baadaye maishani mwa Yoshua— ambayo ni kutekwa kwa Yeriko, kutiishwa hatua kwa hatua kwa maadui wao, na kugawanywa kwa nchi—yanaonyesha kwamba hakusahau ahadi za Mungu. Alipokaribia kufa, wakati ambapo Yehova alikuwa amewaondolea Waisraeli maadui wao, Yoshua aliwakusanya Waisraeli ili watafakari mambo ambayo Mungu alikuwa amewatendea na akawatia moyo wamtumikie Yeye kwa moyo wote. Kwa sababu hiyo, Waisraeli walifanya upya agano lao pamoja na Yehova, na yaelekea kielelezo cha kiongozi wao kiliwachochea ‘kumtumikia BWANA siku zote za Yoshua.’—Yoshua 24:16, 31.

Yoshua ni kielelezo bora sana kwetu. Wakristo leo wanapata majaribu mengi ya imani. Ni muhimu kuyashinda ili kuendelea kuwa na kibali cha Yehova na mwishowe kuona utimizo wa ahadi zake. Yoshua alifanikiwa kwa sababu alikuwa na imani yenye nguvu. Ni kweli kwamba hatujaona matendo makuu ya Mungu kama yale ambayo Yoshua aliona, lakini ikiwa yeyote ana shaka, basi kitabu cha Biblia cha Yoshua kina masimulizi ya mtu aliyejionea kwamba Yehova hutimiza anayosema. Sisi, kama Yoshua, tumehakikishiwa kwamba tutapata hekima na tutafanikiwa tukisoma Neno la Mungu kila siku na kuhakikisha kwamba tunalifuata maishani.

Je, mara kwa mara unaumizwa na mwenendo wa Wakristo wenzako? Fikiria uvumilivu wa Yoshua alipolazimika kutangatanga nyikani pamoja na Waisraeli wasio na imani, ingawa yeye hakuwa na kosa. Je, wewe huona ni vigumu kutetea imani yako? Kumbuka jinsi Yoshua na Kalebu walivyofanya. Walipokea thawabu nzuri kwa sababu ya imani na utii wao. Naam, Yoshua alikuwa na imani kwamba Yehova angetimiza ahadi zake zote. Na tuwe na imani kama hiyo.—Yoshua 23:14.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kushirikiana na Musa kuliimarisha imani ya Yoshua

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yoshua na Kalebu walikuwa na uhakika katika uwezo wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 10]

Uongozi wa Yoshua uliwachochea watu kushikamana na Yehova