Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Funzo la Kibinafsi Ambalo Hutuandaa Kuwa Walimu Bora

Funzo la Kibinafsi Ambalo Hutuandaa Kuwa Walimu Bora

Funzo la Kibinafsi Ambalo Hutuandaa Kuwa Walimu Bora

“Fikiri kwa uzito juu ya mambo haya; vama katika hayo, ili kusonga mbele kwako kupate kuwa dhahiri kwa watu wote. Daima kaza uangalifu kwako mwenyewe na kwa kufundisha kwako.”—1 TIMOTHEO 4:15, 16.

1. Ukweli ni nini kuhusu wakati na funzo la kibinafsi?

“KWA kila jambo kuna majira yake,” yasema Biblia katika andiko la Mhubiri 3:1. Bila shaka, hilo lahusu pia funzo la kibinafsi. Wengi huona vigumu kutafakari mambo ya kiroho wakati usiofaa au mahali pasipofaa. Kwa mfano, baada ya kufanya kazi ngumu na kula chakula kingi jioni, je, utataka kujifunza, hasa iwapo umejinyoosha kwenye kiti chako cha kustarehe ukitazama televisheni? La. Kwa hiyo suluhisho ni nini? Bila shaka, tunapaswa kuchagua mahali na wakati wa kujifunza tukiwa na kusudi la kunufaika kikamili na funzo letu.

2. Ni wakati upi unaofaa zaidi kufanya funzo la kibinafsi?

2 Wengi huona kwamba wakati unaofaa zaidi kujifunza ni asubuhi na mapema wakati akili yao inapokuwa chonjo. Wengine hujifunza kwa muda mfupi wakati wa mapumziko ya mchana. Ona wakati unaotajwa wa kufanya mambo muhimu ya kiroho katika mifano inayofuata. Mfalme Daudi wa Israeli la kale aliandika hivi: “Unifanye kusikia fadhili zako asubuhi, kwa maana nimekutumaini Wewe. Unijulishe njia nitakayoiendea, kwa maana nakuinulia nafsi yangu.” (Zaburi 143:8) Nabii Isaya alionyesha uthamini kama huo aliposema: “Bwana MUNGU amenipa ulimi wa hao wafundishwao, nipate kujua jinsi ya kumtegemeza kwa maneno yeye aliyechoka, huniamsha asubuhi baada ya asubuhi; huniamsha, sikio langu lipate kusikia kama watu wafundishwao.” Jambo kuu ni kwamba tunapaswa kujifunza na kuwasiliana na Yehova kindani wakati akili zetu ziko chonjo, hata iwe ni saa ngapi.—Isaya 50:4, 5; Zaburi 5:3; 88:13.

3. Ni hali zipi zinazofaa ili kunufaika na funzo?

3 Jambo jingine linalofanya funzo liwe lenye matokeo ni kutoketi katika kiti chenye kustarehesha sana. Hatuwezi kuwa chonjo tukifanya hivyo. Tunapojifunza, akili yetu inapaswa kuwa chonjo, na hatuwezi kuwa chonjo iwapo tumestarehe sana. Pia inafaa kuwa mahali patulivu pasipo na vikengeusha-fikira ili kujifunza na kutafakari. Huwezi kunufaika na funzo iwapo fikira zako zinakengeushwa na redio, televisheni, au watoto. Yesu alipotaka kutafakari, alienda mahali patulivu. Pia alitaja umuhimu wa kutafuta mahali pa faragha ili kusali.—Mathayo 6:6; 14:13; Marko 6:30-32.

Funzo la Kibinafsi Ambalo Hutuandaa Kujibu Maswali

4, 5. Broshua Anataka inasaidia katika njia gani?

4 Funzo la kibinafsi huridhisha tunapotumia vichapo mbalimbali vinavyoifafanua Biblia ili kufanya utafiti zaidi kuhusu habari fulani, hasa tunapofanya hivyo ili kujibu maswali ambayo mtu ameuliza kwa unyofu. (1 Timotheo 1:4; 2 Timotheo 2:23) Wapya wengi huanza kwa kujifunza broshua Mungu Anataka Tufanye Nini?, * ambayo sasa hupatikana katika lugha 261. Ni kichapo rahisi kueleweka lakini sahihi, nacho kinategemea kabisa Biblia. Kinasaidia wasomaji waelewe upesi matakwa ya Mungu kuhusu ibada ya kweli. Hata hivyo, kwa kuwa hiyo ni broshua, haiwezekani kuzungumzia kila habari kindani. Ikiwa mwanafunzi wako wa Biblia auliza maswali kwa unyofu kuhusu habari fulani za Biblia, utapata wapi habari zaidi itakayomsaidia kujibu maswali hayo?

5 Wale ambao wana Watchtower Library kwenye CD-ROM katika lugha yao, wanaweza kupata habari nyingi kwenye kompyuta. Lakini namna gani wale ambao hawana kifaa hiki? Na tuchunguze masomo mawili katika broshua Anataka ili tuone jinsi tunavyoweza kuzidisha uelewevu wetu na kuweza kujibu kindani zaidi—hasa mtu anapouliza, Mungu ni nani? na kwa kweli Yesu alikuwa mtu wa aina gani?—Kutoka 5:2; Luka 9:18-20; 1 Petro 3:15.

Mungu Ni Nani?

6, 7. (a) Ni swali gani linalotokea kumhusu Mungu? (b) Kasisi mmoja alifanya kosa gani kubwa alipokuwa akitoa hotuba?

6 Somo la 2 katika broshua Anataka hujibu swali hili muhimu, Mungu Ni Nani? Hili ni fundisho muhimu kwa sababu mtu hawezi kumwabudu Mungu wa kweli ikiwa Hamjui au ikiwa labda anatilia shaka kuwepo Kwake. (Waroma 1:19, 20; Waebrania 11:6) Hata hivyo, watu ulimwenguni pote wana maoni mbalimbali kuhusu Mungu. (1 Wakorintho 8:4-6) Kila dini hutoa jibu tofauti kuhusu Mungu ni nani. Dini nyingi zinazojiita eti za Kikristo huamini kwamba Mungu ni Utatu. Kasisi mmoja mashuhuri huko Marekani alitoa hotuba iliyokuwa na kichwa “Je, Unamjua Mungu?” lakini hakutaja jina la Mungu hata kidogo katika hotuba yake, licha ya kwamba alinukuu Maandiko ya Kiebrania mara kadhaa. Bila shaka, alikuwa akisoma tafsiri ya Biblia inayotumia neno “Bwana” ambalo ni neno lililo na maana nyingi na si jina la mtu binafsi badala ya kutumia jina Yehova au Yahweh.

7 Kasisi huyo alikosa kuona jambo muhimu sana aliponukuu andiko la Yeremia 31:33, 34: “Wala hawatamfundisha kila mtu jirani yake, na kila mtu ndugu yake, wakisema, Mjue BWANA [Kiebrania, “Mjue Yehova”]; kwa maana watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema BWANA [Kiebrania, Yehova].” Tafsiri aliyotumia haikutaja jina Yehova, linalomtambulisha Mungu.—Zaburi 103:1, 2.

8. Ni nini kinachoonyesha umuhimu wa kutumia jina la Mungu?

8 Andiko la Zaburi 8:9, NW linaonyesha kwa nini ni muhimu sana kutumia jina la Yehova: “Ee Yehova Bwana wetu, jina lako ni lenye utukufu kama nini katika dunia yote!” Linganisha tafsiri hiyo na: “Ee BWANA, Bwana wetu, jina lako ni lenye utukufu duniani mwote!” (Zaire Swahili Bible) Hata hivyo, kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, tunaweza kupata “kumjua Mungu” tukiruhusu Neno lake lituelimishe. Lakini ni kifaa gani cha kujifunzia Biblia kitakachojibu maswali yetu moja kwa moja kuhusu umuhimu wa jina la Mungu?—Mithali 2:1-6.

9. (a) Ni kichapo gani kinachoweza kutusaidia kueleza umuhimu wa kutumia jina la Mungu? (b) Watafsiri wengi wamekosaje kuonyesha heshima kwa jina la Mungu?

9 Tunaweza kupata msaada katika broshua Jina la Mungu Litakaloendelea Milele, ambayo imetafsiriwa katika lugha 69. * Sehemu yenye kichwa “Jina la Mungu—Maana Yalo na Linavyotamkwa” (ukurasa wa 6-11) inaonyesha waziwazi kwamba ile Tetragramatoni ya Kiebrania (Tetragramatoni inamaanisha “herufi nne” katika Kigiriki) inapatikana karibu mara 7,000 katika maandishi ya awali ya Kiebrania. Hata hivyo, makasisi na watafsiri wa Dini ya Kiyahudi na dini zinazojiita eti za Kikristo wameliondoa kimakusudi katika tafsiri zao za Biblia. * Wanawezaje kudai kwamba wanamjua Mungu na wawe na uhusiano mzuri pamoja naye ikiwa hawataki kumwita kwa jina lake? Jina lake la kweli husaidia watu waelewe makusudi yake na utu wake. Zaidi ya hayo, ile sehemu katika sala ya kielelezo ya Yesu “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako litakaswe” ina thamani gani ikiwa jina la Mungu halitumiwi?—Mathayo 6:9; Yohana 5:43; 17:6.

Yesu Kristo Ni Nani?

10. Tunawezaje kupata habari kamili kuhusu maisha na huduma ya Yesu?

10 Somo la 3 katika broshua Anataka lina kichwa “Yesu Kristo Ni Nani?” Katika mafungu sita tu, inatoa muhtasari mfupi kuhusu Yesu, mwanzo wake, na kusudi lake la kuja duniani. Hata hivyo, mbali na vitabu vya Injili unaweza pia kupata habari kamili kuhusu maisha yake katika kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi ambacho kinapatikana katika lugha 111. * Kitabu hiki kinatoa habari kamili kwa kufuata utaratibu wa miaka na matukio kuhusu maisha na mafundisho ya Kristo, kupatana na zile Injili nne. Sura zake 133 zinazungumzia maisha na huduma ya Yesu. Ukitaka habari inayochanganua kindani Yesu Kristo, unaweza kusoma kitabu Insight, Buku la 2, chini ya kichwa “Jesus Christ.”

11. (a) Imani ya Mashahidi wa Yehova kuhusu Yesu inatofautianaje na ya wengine? (b) Ni maandiko gani ya Biblia ambayo hupinga fundisho la Utatu waziwazi, na ni kichapo gani ambacho hutusaidia kuelewa habari hiyo?

11 Katika dini zinazojiita eti za Kikristo kuna ubishi wa kama Yesu ni “Mwana wa Mungu” na vilevile “Mungu Mwana”—yaani, ubishi ambao kichapo Catechism of the Catholic Church huuita “fumbo kuu la imani ya Kikristo,” Utatu. Mashahidi wa Yehova ambao ni tofauti na dini zinazojiita eti za Kikristo wanaamini kwamba Yesu aliumbwa na Mungu, naye si Mungu. Maelezo mazuri sana kuhusu habari hii yanapatikana katika broshua Je, Uamini Utatu?, ambayo imetafsiriwa katika lugha 95. * Baadhi ya maandiko mengi ambayo yametumiwa katika broshua hiyo kupinga fundisho la Utatu ni Marko 13:32 na 1 Wakorintho 15:24, 28.

12. Ni swali gani jingine tunalopaswa kulifikiria?

12 Habari iliyotajwa juu kuhusu Mungu na Yesu Kristo inaonyesha njia mbalimbali tunazoweza kutumia kufanya funzo la kibinafsi tukiwa na kusudi la kusaidia wale ambao hawafahamu kweli ya Biblia wapate ujuzi sahihi. (Yohana 17:3) Hata hivyo, namna gani wale ambao wamekuwa wakishirikiana na kutaniko la Kikristo kwa miaka mingi? Kwa kuwa wana ujuzi mwingi wa Biblia, je, bado wanahitaji kujifunza Neno la Yehova kibinafsi?

Kwa Nini ‘Tukaze Uangalifu Daima’?

13. Ni maoni gani yasiyofaa ambayo huenda watu wengine wakawa nayo kuhusu funzo la kibinafsi?

13 Huenda wengine ambao wamekuwa washiriki wa kutaniko kwa miaka mingi wakawa na zoea la kutegemea tu ujuzi wa Biblia waliopata miaka michache ya kwanza wakiwa Mashahidi wa Yehova. Ni rahisi mtu kuwaza hivi: “Si lazima nijifunze kwa bidii kama wapya. Kwani, kwa miaka mingi nimeisoma Biblia na vichapo vinavyozungumzia Biblia mara nyingi.” Hii ingekuwa sawa na kusema: “Kwa kweli sihitaji kukazia uangalifu sana kiasi cha chakula ninachokula sasa, kwani nimekula mara nyingi sana muda uliopita.” Tunajua kwamba mwili unapaswa kulishwa kwa ukawaida chakula kinachofaa, kilichopikwa vizuri, ili uwe na nguvu na afya. Tunapaswa kufanya vivyo hivyo iwapo tunataka kuendelea kuwa wenye afya na nguvu kiroho.—Waebrania 5:12-14.

14. Kwa nini tunapaswa kukaza uangalifu daima kwetu wenyewe?

14 Kwa hiyo, sisi sote, tuwe tumejifunza Biblia kwa muda mrefu au la, tunahitaji kutii shauri la Paulo kwa Timotheo, ambaye wakati huo alikuwa mwangalizi aliyekomaa kiroho: “Kaza uangalifu kwako mwenyewe na kwa kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivi utajiokoa wewe mwenyewe na wale wakusikilizao pia.” (1 Timotheo 4:15, 16) Kwa nini tuzingatie sana shauri la Paulo? Kumbuka, pia kwamba Paulo alisema tuna pigano dhidi ya “mbinu [“matendo ya hila”] za Ibilisi” na “dhidi ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” Naye mtume Petro alionya kwamba Ibilisi ‘anatafuta sana kunyafua mtu fulani,’ na ‘mtu’ huyo anaweza kuwa yeyote kati yetu. Anaweza kupata fursa ya kutushambulia iwapo hatujali hatari hiyo.—Waefeso 6:11, 12; 1 Petro 5:8.

15. Ni kinga gani ya kiroho tuliyo nayo, nasi tunaweza kuidumishaje?

15 Kwa hiyo, tuna kinga gani? Mtume Paulo anatukumbusha hivi: “Chukueni suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu, ili mpate kuweza kukinza katika siku ya uovu na, baada ya nyinyi kuwa mmefanya mambo yote kikamili, kusimama imara.” (Waefeso 6:13) Ili suti hiyo kamili ya silaha itukinge, tunapaswa kuitunza kwa ukawaida badala ya kuiachilia katika hali yake ya awali. Kwa hiyo, suti hiyo kamili ya silaha kutoka kwa Mungu lazima itie ndani ujuzi wa sasa kutoka kwa Neno la Mungu. Hilo lakazia umuhimu wa kwenda sambamba na uelewevu wa ile kweli ambao Yehova hufunua kupitia Neno lake na kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Ili tudumishe suti yetu ya silaha kamili za kiroho, tunapaswa kujifunza Biblia kwa ukawaida pamoja na vichapo vinavyozungumzia Biblia.—Mathayo 24:45-47; Waefeso 6:14, 15.

16. Tunaweza kufanya nini ili tuhakikishe kwamba “ngao [yetu] kubwa ya imani” imetunzwa vizuri?

16 Paulo anakazia sehemu muhimu ya silaha zetu za ulinzi “ngao kubwa ya imani,” inayoweza kutusaidia kuzuia na kuzima mishale yenye moto ya Shetani ambayo ni mashtaka bandia na mafundisho ya waasi-imani. (Waefeso 6:16) Kwa hiyo ni muhimu kuchunguza ngao yetu ya imani ina nguvu kadiri gani na ni hatua gani tunazopaswa kuchukua ili kuitunza na kuiimarisha. Kwa mfano, huenda ukajiuliza: ‘Ninatayarishaje funzo la Biblia la kila juma kwa kutumia Mnara wa Mlinzi? Je, nimejifunza vya kutosha kuweza ‘kuwachochea wengine kwenye upendo na kazi zilizo bora’ kwa kutoa majibu yaliyofikiriwa vizuri wakati wa mkutano? Je, mimi hufungua Biblia na kusoma maandiko yaliyotajwa tu bila kunukuliwa? Je, ninawatia moyo wengine kwa kutoa maelezo kwa shauku?’ Chakula chetu cha kiroho ni kigumu, na kinahitaji kusagwa ifaavyo ili tunufaike kikamili.—Waebrania 5:14; 10:24.

17. (a) Shetani anatumia sumu gani kudhoofisha hali yetu ya kiroho? (b) Dawa ya sumu ya Shetani ni nini?

17 Shetani anajua udhaifu wetu sisi wanadamu wasio wakamilifu, naye hutumia mbinu za hila. Mojawapo ya mbinu anazotumia kueneza uvutano wake mwovu ni kufanya ponografia (picha na habari chafu) ipatikane kwa urahisi kwenye televisheni, Internet, video, na vichapo. Wakristo fulani wameruhusu sumu hiyo ipenye na kuwadhoofisha, na imefanya wapoteze mapendeleo kutanikoni au hata kupatwa na madhara mabaya zaidi. (Waefeso 4:17-19) Dawa ya sumu hiyo ya Shetani ni nini? Hatupaswi kuacha kujifunza Biblia kwa ukawaida, wala mikutano yetu ya Kikristo, na suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu. Mambo hayo yote hutupatia uwezo wa kutofautisha kati ya mema na mabaya na kuchukia mambo ambayo Mungu huchukia.—Zaburi 97:10; Waroma 12:9.

18. “Upanga wa roho” unaweza kutusaidiaje katika vita yetu ya kiroho?

18 Tukiendelea kujifunza Biblia kwa ukawaida, ujuzi sahihi wa Neno la Mungu utatupatia nguvu za kujikinga, na pia tutafanikiwa kufanya mashambulizi tukitumia “upanga wa roho, yaani, neno la Mungu.” Neno la Mungu ni “lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili na hudunga hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na uloto wavyo, na ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.” (Waefeso 6:17; Waebrania 4:12) Tukiwa stadi katika kutumia “upanga,” huo basi tunapokabili vishawishi, tutaweza kutambua waziwazi mambo ambayo huenda yakaonekana kuwa hayana madhara, au hata yanayoonekana kuwa yenye kuvutia, na kuyaona kuwa mtego wa waovu unaoweza kusababisha kifo. Ujuzi wa Biblia pamoja na uelewevu tulio nao utatusaidia kukataa maovu na kutenda mema. Kwa hiyo sote tunapaswa kujiuliza: ‘Je, upanga wangu ni mkali, au una kutu? Je, mimi huona ni vigumu kukumbuka maandiko ya Biblia yanayoweza kunipa nguvu za kushambulia?’ Na tudumishe mazoea mazuri ya kujifunza Biblia kibinafsi na hivyo kumpinga Ibilisi.—Waefeso 4:22-24.

19. Tunaweza kupata manufaa gani kwa kujifunza kibinafsi kwa bidii?

19 Paulo aliandika hivi: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.” Tukizingatia maneno ambayo Paulo alimwambia Timotheo, tunaweza kuimarisha hali yetu ya kiroho na kufanya huduma yetu iwe yenye matokeo zaidi. Wazee na watumishi wa huduma wanaweza kunufaisha sana kutaniko, na sisi sote tunaweza kudumu tukiwa thabiti katika imani.—2 Timotheo 3:16, 17; Mathayo 7:24-27.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kwa kawaida, mtu mwenye kupendezwa anayejifunza broshua Anataka atajifunza kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, baada ya kumaliza broshua hiyo. Vichapo vyote viwili vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova. Madokezo yaliyotolewa hapa yatasaidia kuondoa mambo yoyote yanayoweza kumzuia mtu asifanye maendeleo ya kiroho.

^ fu. 9 Kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova. Wale ambao wana kitabu Insight on the Scriptures katika lugha yao wanaweza kutazama Buku la 2, chini ya kichwa, “Jehovah.”

^ fu. 9 Baadhi ya tafsiri za Kiswahili zinatumia Tetragramatoni za Kiebrania “Yahweh” na “Yehova.”

^ fu. 10 Imechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 11 Imechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Ni hali gani zinazofaa ili kuwa na funzo la kibinafsi lenye matokeo?

• Tafsiri nyingi za Biblia hufanya kosa gani kuhusiana na jina la Mungu?

• Ni maandiko gani ya Biblia unayoweza kutumia ili kupinga fundisho la Utatu?

• Tunapaswa kufanya nini ili kujikinga na mbinu za Shetani, hata kama tumekuwa Wakristo wa kweli kwa miaka mingi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 19]

Ili kuwa na funzo la kibinafsi lenye matokeo, unahitaji kuwa mahali panapofaa pasipo na vikengeusha-fikira

[Picha katika ukurasa wa 23]

Je, “upanga” wako ni mkali au una kutu?