Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Furahia Kujifunza Kibinafsi Neno la Mungu

Furahia Kujifunza Kibinafsi Neno la Mungu

Furahia Kujifunza Kibinafsi Neno la Mungu

“Nitaitafakari kazi yako yote; nitaziwaza habari za matendo yako.”—ZABURI 77:12.

1, 2. (a) Kwa nini tutenge wakati wa kutafakari? (b) Kutafakari kunamaanisha nini?

TUKIWA wanafunzi wa Yesu Kristo, mambo yaliyo muhimu zaidi kwetu ni uhusiano wetu pamoja na Mungu na sababu zinazofanya tumtumikie. Hata hivyo, leo, watu wengi wana shughuli nyingi mno hivi kwamba hawapati wakati wa kutafakari. Wanajishughulisha kabisa na ufuatiaji wa vitu vya kimwili, ununuzi wa bidhaa, na kufuatia anasa bila kusudi lolote. Tunawezaje kuepuka shughuli hizo zisizo na kusudi? Kama vile tunavyotenga wakati kila siku kufanya shughuli za lazima, kama kula na kulala, tunapaswa pia kutenga wakati kila siku kutafakari juu ya kazi na matendo ya Yehova.—Kumbukumbu la Torati 8:3; Mathayo 4:4.

2 Je, kuna wakati unapotulia na kutafakari? Kutafakari kunamaanisha nini? Kamusi ya Kiswahili Sanifu inafasiri neno -tafakari kuwa ‘kuzama katika fikira juu ya jambo fulani; kuwaza, kuzingatia.’ Kutafakari ni muhimu kadiri gani kwetu?

3. Kufanya maendeleo ya kiroho kunahusiana moja kwa moja na nini?

3 Kwanza, kutafakari kunapaswa kutukumbusha maneno ambayo mtume Paulo alimwandikia mtumishi mwenzake Timotheo: “Ninapokuwa nikija, endelea kujitahidi mwenyewe kusoma mbele ya watu wote, kuhimiza kwa bidii, kufundisha. . . . Fikiri kwa uzito juu ya mambo haya; vama katika hayo, ili kusonga mbele kwako kupate kuwa dhahiri kwa watu wote.” Naam, Timotheo alitarajiwa asonge mbele, nayo maneno ya Paulo yalionyesha kwamba kufikiri kwa uzito juu ya mambo ya kiroho kunahusiana moja kwa moja na kusonga mbele. Ndivyo ilivyo leo. Ili kupata uradhi unaotokana na kufanya maendeleo ya kiroho, lazima ‘tufikiri kwa uzito juu ya’ na ‘kuvama’ katika mambo yanayohusiana na Neno la Mungu.—1 Timotheo 4:13-15.

4. Ni vifaa gani unavyoweza kutumia ili vikusaidie kutafakari Neno la Yehova kwa ukawaida?

4 Wakati unaokufaa zaidi wa kutafakari hutegemea ratiba yako na ya familia yako. Wengi hutafakari juu ya andiko la Biblia asubuhi wanaposoma kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. Wajitoleaji wapatao 20,000 katika makao ya Betheli ulimwenguni pote huanza siku kwa kuzungumzia andiko la Biblia kwa muda wa dakika 15. Ingawa ni washiriki wachache wa Betheli ambao hutoa maelezo kila asubuhi, wengine hutafakari habari inayosemwa na kusomwa. Mashahidi wengine hutafakari juu ya Neno la Yehova wanaposafiri kuelekea kazini. Wao husikiliza kaseti za usomaji wa Biblia na za gazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ambazo hupatikana katika lugha fulani. Wake wengi wa nyumbani husikiliza usomaji huo wanapofanya kazi nyumbani. Kwa kweli, wanamwiga mtunga-zaburi Asafu, aliyeandika hivi: “Nitayakumbuka matendo ya BWANA; naam, nitayakumbuka maajabu yako ya kale. Pia nitaitafakari kazi yako yote; nitaziwaza habari za matendo yako.”—Zaburi 77:11, 12.

Mtazamo Unaofaa Huwa na Matokeo Mema

5. Kwa nini tuone funzo la kibinafsi kuwa muhimu?

5 Katika nyakati zetu za kisasa ambapo kuna televisheni, video, na kompyuta watu wengi hawasomi sana. Mashahidi wa Yehova hawapaswi kuwa hivyo. Kwa kweli, kusoma Biblia ni kama kamba ya kuokolea inayotuunganisha na Yehova. Maelfu ya miaka iliyopita, Yoshua alichukua mahali pa Musa kuwaongoza Waisraeli. Ili kupata baraka za Yehova, ilimbidi Yoshua asome Neno la Mungu. (Yoshua 1:8; Zaburi 1:1, 2) Tunatakiwa kufanya hivyo hata wakati huu. Hata hivyo, kwa sababu ya elimu ya chini, huenda watu fulani wakaona ugumu kusoma au wakachoshwa na kusoma. Kwa hiyo, ni nini kinachoweza kuchochea hamu yetu ya kusoma na kujifunza Neno la Mungu? Jibu linapatikana katika maneno ya Mfalme Solomoni kwenye andiko la Mithali 2:1-6. Tafadhali fungua Biblia yako na usome mistari hiyo. Kisha tutaizungumzia pamoja.

6. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuelekea kumjua Mungu?

6 Kwanza, tunahimizwa hivi: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; . . .” (Mithali 2:1, 2) Tunajifunza nini kutokana na maneno hayo? Kwamba kila mmoja wetu ana daraka la kujifunza Neno la Mungu. Ona sharti ambalo limewekwa hapa “kama ukiyakubali maneno yangu.” Sharti hilo ni muhimu kwa sababu watu wengi hawajishughulishi kusoma Neno la Mungu. Ili tupate shangwe ya kujifunza Neno la Mungu, lazima tuwe tayari kupokea maneno ya Yehova na kuyaona kama kitu chenye thamani kubwa hivi kwamba hatungependa kukipoteza. Hatupaswi kuruhusu shughuli zetu za kila siku au mambo fulani yatukengeushe fikira na hivyo tukose kupendezwa na Neno la Mungu, au hata kuwa na shaka nalo.—Waroma 3:3, 4.

7. Inapowezekana, kwa nini tunapaswa kuhudhuria na kusikiliza mikutano ya Kikristo?

7 Je, kweli ‘tunatega sikio’ na kusikiliza kwa makini wakati Neno la Mungu linapofafanuliwa katika mikutano yetu ya Kikristo? (Waefeso 4:20, 21) Je, ‘tunauelekeza moyo wetu’ ili tupate ufahamu? Labda msemaji hana uzoefu mwingi, lakini tunapaswa kumsikiliza kwa makini anapozungumzia Neno la Mungu. Bila shaka, ili kusikiliza hekima ya Yehova, lazima tuhudhurie mikutano ya Kikristo wakati wote inapowezekana. (Mithali 18:1) Hebu wazia jinsi mtu yeyote aliyekosa ule mkutano uliofanywa katika chumba cha juu huko Yerusalemu, Pentekoste 33 W.K. alivyovunjika moyo! Ingawa mikutano yetu si ya pekee kama mkutano huo, Biblia, ambayo ni kitabu chetu kikuu cha mafundisho, huzungumziwa. Kwa hiyo, tunaweza kunufaishwa kiroho na kila mkutano ikiwa tutasikiliza na kufungua maandiko yanayosomwa katika Biblia zetu.—Matendo 2:1-4; Waebrania 10:24, 25.

8, 9. (a) Tunapaswa kufanya nini kuhusiana na funzo la kibinafsi? (b) Ungetofautishaje dhahabu na kumjua Mungu?

8 Mfalme mwenye hekima aendelea kusema: “Naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu; . . .” (Mithali 2:3) Maneno hayo hufanya tuwe na mtazamo gani? Bila shaka, yanafanya tuwe na tamaa kubwa ya kuelewa Neno la Yehova! Yanadokeza nia ya kujifunza kwa kusudi la kupata ufahamu, kuelewa mapenzi ya Yehova. Bila shaka, jitihada inahitajiwa ili kufanya hivyo, kama inavyoonyeshwa na maneno na mfano ufuatao wa Solomoni.—Waefeso 5:15-17.

9 Aendelea kusema: “Ukiutafuta [ufahamu] kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; . . .” (Mithali 2:4) Hilo lafanya tufikirie mafanikio ambayo wachimba-migodi wamepata kwa karne nyingi wakitafuta madini yanayoitwa eti yenye thamani kama vile fedha na dhahabu. Watu wamewaua wengine kwa sababu ya dhahabu. Wengine wametumia maisha yao yote wakitafuta dhahabu. Hata hivyo, dhahabu ina thamani gani? Ikiwa ungepotea jangwani na una kiu kali sana, ungechagua nini: kipande cha dhahabu au kikombe cha maji? Hata hivyo, watu wametafuta dhahabu kwa bidii licha ya kwamba thamani yake ni ya kijuujuu tu na hubadilika-badilika! * Tunapaswa kujitahidi sana kutafuta hekima, ufahamu, na uelewevu wa mapenzi ya Mungu! Lakini tutapata manufaa gani kwa kutafuta mambo hayo?—Zaburi 19:7-10; Mithali 3:13-18.

10. Tunaweza kupata nini tukijifunza Neno la Mungu?

10 Solomoni aendelea hivi na maelezo yake: “Ndipo utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu.” (Mithali 2:5) Ni jambo la kushangaza kama nini—kwamba sisi wanadamu wenye dhambi tunaweza kupata ‘kumjua Yehova Mungu,’ Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu! (Zaburi 73:28; Matendo 4:24) Kwa karne nyingi wanafalsafa na wale wanaoitwa eti watu wenye hekima wa ulimwengu wamejaribu kuelewa mambo yenye kutatanisha kuhusu uhai na ulimwengu. Hata hivyo, wameshindwa “kumjua Mungu.” Kwa nini? Ingawa ujuzi huo umekuwako kwa maelfu ya miaka katika Neno la Mungu, Biblia, wanaikataa wakidai kwamba ina habari za kijuujuu tu na hivyo kukosa kuielewa.—1 Wakorintho 1:18-21.

11. Funzo la kibinafsi lina manufaa gani?

11 Solomoni akazia jambo jingine lenye kuchochea: “BWANA huwapa watu hekima; kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu.” (Mithali 2:6) Yehova hutoa hekima, ujuzi, na ufahamu bila malipo kwa yeyote aliye na nia ya kutafuta mambo hayo. Bila shaka, tuna sababu nzuri za kuthamini funzo la kibinafsi la Neno la Mungu, hata kama kufanya hivyo kutahitaji jitihada, nidhamu, na kujidhabihu. Angalau tuna Biblia zilizochapishwa na hatuhitaji kuandika nakala kwa mkono kama watu wa kale walivyofanya!—Kumbukumbu la Torati 17:18, 19.

Kutembea kwa Kumstahili Yehova

12. Tunapaswa kuwa na lengo gani tunapotafuta kumjua Mungu?

12 Tunapaswa kujifunza kibinafsi tukiwa na lengo gani? Je, tunajifunza ili tuonekane kuwa bora kuliko wengine? Je, ni ili tuonekane tuna ujuzi mwingi? Ni ili tuonekane kana kwamba tunajua kila kitu katika Biblia? La. Lengo letu linapaswa kuwa kujizoeza Ukristo kwa maneno na matendo, sikuzote tukiwa tayari kusaidia wengine, kwa kuiga mtazamo wenye kuburudisha wa Kristo. (Mathayo 11:28-30) Mtume Paulo alionya hivi: “Ujuzi hututumuka, lakini upendo hujenga.” (1 Wakorintho 8:1) Kwa hiyo, tunapaswa kuwa wanyenyekevu kama Musa wakati alipomwambia Yehova hivi: “Unionyeshe njia zako, nipate kukujua, ili nipate neema mbele zako.” (Kutoka 33:13) Naam, tunapaswa kutamani kuwa na ujuzi ili tumpendeze Mungu, si wanadamu. Tungependa kuwa watumishi wa Mungu walio wanyenyekevu na wanaostahili. Tunawezaje kutimiza mradi huo?

13. Ni nini kinachohitajiwa ili mtu awe mtumishi wa Mungu anayestahili?

13 Paulo alimshauri Timotheo hivi kuhusu jinsi ya kumpendeza Mungu: “Fanya yote uwezayo kabisa ili ujionyeshe mwenyewe kuwa mwenye kukubaliwa na Mungu, mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli.” (2 Timotheo 2:15) Usemi ‘kutumia sawasawa’ unatokana na kitenzi-ambatani cha Kigiriki ambacho hapo awali kilimaanisha “kukata kwa kunyooka.” (Kingdom Interlinear) Kulingana na wasomi fulani, usemi huo hudokeza wazo la fundi anayekata kitambaa kwa kufuata mshono fulani, au mkulima anayechimba mitaro, na kadhalika. Vyovyote vile, lazima kitambaa kinachokatwa au mtaro unaochimbwa uwe umenyooka. Jambo kuu ni kwamba ili Timotheo awe mtumishi wa Mungu aliyekubaliwa na anayestahili, alipaswa ‘kufanya yote awezayo’ ili kuhakikisha kwamba mafundisho na mwenendo wake ulipatana na neno la kweli.—1 Timotheo 4:16.

14. Funzo letu la kibinafsi linapaswa kuathirije maneno na matendo yetu?

14 Paulo alitaja jambo hilo alipowahimiza Wakristo wenzake huko Kolosai ‘watembee kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili’ kwa “kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.” (Wakolosai 1:10) Hapa Paulo anahusianisha kumstahili Yehova na “kuzaa matunda katika kila kazi njema” na vilevile “kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.” Yaani, jambo ambalo Yehova huliona kuwa muhimu si jinsi tunavyothamini ujuzi bali ni jinsi tunavyotii Neno lake kwa maneno na matendo. (Waroma 2:21, 22) Hii inamaanisha kwamba funzo letu la kibinafsi linapaswa kuathiri fikira zetu na mwenendo wetu iwapo tunataka kumpendeza Mungu.

15. Tunawezaje kulinda na kudhibiti akili na mawazo yetu?

15 Leo, Shetani ameazimia kuharibu hali yetu ya kiroho kwa kuchochea vita inayohusisha akili. (Waroma 7:14-25) Kwa hiyo, lazima tulinde na kudhibiti akili na mawazo yetu ili tustahili mbele za Yehova, Mungu wetu. Tuna silaha ya “ujuzi wa Mungu,” ambao unaweza ‘kuingiza kila fikira katika utekwa ili kuifanya iwe tiifu kwa Kristo.’ Hii ni sababu nyingine inayofanya tuzingatie kujifunza Biblia kila siku, kwa kuwa tunataka kuondoa mawazo ya ubinafsi na ya kimwili kutoka akilini mwetu.—2 Wakorintho 10:5.

Vifaa vya Kutusaidia Tupate Uelewevu

16. Tunaweza kupata manufaa gani kwa kufundishwa na Yehova?

16 Mafundisho ya Yehova hutokeza manufaa ya kiroho na ya kimwili. Si theolojia isiyopendeza na isiyoweza kutumika. Kwa hiyo, tunasoma hivi: “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.” (Isaya 48:17) Yehova hutusaidiaje tutembee katika njia yake inayonufaisha? Kwanza, tuna Neno lake lililoongozwa kwa roho, Biblia Takatifu. Hiki ndicho kitabu chetu kikuu cha mafundisho, tunachokisoma daima ili kupata msaada. Ndiyo sababu inafaa kusikiliza kwa makini na kusoma maandiko wakati wa mikutano ya Kikristo. Tunaweza kuona manufaa ya kufanya hivyo kutokana na simulizi la towashi Mwethiopia linalopatikana katika Matendo sura ya 8.

17. Ni nini kilichotokea kwa towashi Mwethiopia, na jambo hilo linatufunza nini?

17 Towashi Mwethiopia alikuwa amebadili imani yake akawa mfuasi wa Dini ya Kiyahudi. Alikuwa mwamini mnyofu wa Mungu, naye alijifunza Maandiko. Alikuwa akisafiri katika gari lake, huku akisoma andiko la Isaya wakati Filipo alipomfikia na kumwuliza: “Je, wewe kwa hakika wajua unayoyasoma?” Towashi alimjibuje? “‘Kwa kweli, ningewezaje kufanya hivyo, isipokuwa mtu fulani angeniongoza?’ Naye akamsihi Filipo kwa bidii apande na kuketi pamoja naye.” Kisha Filipo, akiongozwa na roho takatifu, akamsaidia towashi huyo aelewe unabii wa Isaya. (Matendo 8:27-35) Jambo hilo linatufunza nini? Kwamba haitoshi tu kujifunza Biblia kibinafsi. Yehova, kupitia roho yake, hutumia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara kutusaidia tuelewe Neno lake kwa wakati unaofaa. Anafanyaje hivyo?—Mathayo 24:45-47; Luka 12:42.

18. Jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara hutusaidiaje?

18 Ingawa jamii ya mtumwa inafafanuliwa kuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” Yesu hakusema kwamba mtumwa huyo hangeweza kukosea. Wakristo hao waaminifu waliotiwa mafuta si wakamilifu. Hata wanapokuwa na makusudi mazuri, wanaweza kueleweka vibaya, kama wenzao katika karne ya kwanza. (Matendo 10:9-15; Wagalatia 2:8, 11-14) Hata hivyo, wana nia safi, naye Yehova anawatumia kutuandalia vifaa vya kutusaidia kujifunza Biblia na kuimarisha imani yetu katika Neno la Mungu na ahadi zake. Kifaa kikuu ambacho mtumwa huyo ametupatia kwa ajili ya funzo la kibinafsi ni tafsiri ya New World Translation of the Holy Scriptures. Sasa inapatikana ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 42, na nakala milioni 114 zimechapishwa katika tafsiri mbalimbali. Tunaweza kuitumiaje kwa njia yenye matokeo tunapojifunza kibinafsi?—2 Timotheo 3:14-17.

19. Ni sehemu gani za tafsiri ya New World Translation—With References zinazoweza kutusaidia katika funzo la kibinafsi?

19 Kwa mfano, fikiria tafsiri ya New World Translation of the Holy Scriptures—With References. Ina safu za marejeleo yanayolingana, vielezi-chini, konkodansi ndogo ambayo imepangwa kama “Faharisi ya Maneno ya Biblia” na “Faharisi ya Vielezi-chini,” na Nyongeza yenye vichwa na habari mbalimbali 43, kutia ndani ramani na chati. Pia kuna “Utangulizi,” wenye maelezo kuhusu vichapo mbalimbali vilivyotumiwa katika tafsiri hii ya pekee ya Biblia. Iwapo inapatikana katika lugha unayoweza kuelewa, jitahidi kadiri uwezavyo kufahamu sehemu hizo na kuzitumia. Vyovyote vile, tunapaswa kuanza programu yetu ya funzo kwa kujifunza Biblia, na tafsiri ya New World Translation, hukazia ifaavyo jina la Mungu na utawala wa Ufalme wa Mungu.—Zaburi 149:1-9; Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10.

20. Ni maswali gani kuhusu funzo la kibinafsi yanayohitaji kujibiwa sasa?

20 Sasa, huenda tukauliza: ‘Ni msaada gani zaidi tunaohitaji ili kuielewa Biblia? Tunawezaje kupata wakati wa kujifunza kibinafsi? Tunawezaje kufanya funzo letu liwe lenye matokeo zaidi? Funzo letu linapaswa kuwaathirije wengine?’ Makala inayofuata itazungumzia mambo hayo muhimu yanayohusu maendeleo yetu ya Kikristo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Tangu mwaka wa 1979 thamani ya dhahabu imeshuka kutoka dola za Marekani 850.00 kwa gramu 31 mwaka wa 1980 hadi dola za Marekani 252.80 kwa gramu 31 mwaka wa 1999.

Je, Unakumbuka?

• Kutafakari kunamaanisha nini?

• Tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuelekea kujifunza Neno la Mungu?

• Tunapaswa kuwa na lengo gani tunapojifunza kibinafsi?

• Tuna vifaa gani vya kutusaidia kuielewa Biblia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Washiriki wa familia ya Betheli huona kwamba wanaimarishwa kiroho wanapoanza kila siku kwa kuchunguza andiko la Biblia

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tunaweza kukomboa wakati wenye thamani kwa kusikiliza kaseti za usomaji wa Biblia tunaposafiri

[Picha katika ukurasa wa 16]

Watu walifanya kazi kwa bidii na kwa muda mrefu ili kupata dhahabu. Unajitahidi kadiri gani kujifunza Neno la Mungu?

[Hisani]

Courtesy of California State Parks, 2002

[Picha katika ukurasa wa 17]

Biblia ni hazina inayoweza kuongoza kwenye uhai udumuo milele