Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Itieni Mikono Yenu Nguvu

Itieni Mikono Yenu Nguvu

Itieni Mikono Yenu Nguvu

KATIKA Biblia, mikono imetajwa mara nyingi sana. Misemo inayohusu mikono imetumiwa kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, mikono safi inamaanisha kutokuwa na hatia. (2 Samweli 22:21; Zaburi 24:3, 4) Kufungua mkono humaanisha kuwa mkarimu kwa wengine. (Kumbukumbu la Torati 15:11; Zaburi 145:16) Mtu anayehatarisha uhai wake husemekana kuwa anatia uhai wake mikononi mwake. (1 Samweli 19:5) Kulegeza mikono humaanisha kuvunjika moyo. (2 Mambo ya Nyakati 15:7) Na kuitia mikono nguvu humaanisha kuimarishwa kufanya jambo fulani.—1 Samweli 23:16.

Ni muhimu sana leo kuitia nguvu mikono yetu. Tunaishi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Sisi wanadamu tuna mwelekeo wa kukata tamaa au kulegeza mikono tunapovunjika moyo. Ni jambo la kawaida kuona vijana wakiacha shule, waume wakiacha familia zao, na mama wakiwaacha watoto wao. Tukiwa Wakristo, tunahitaji kuitia nguvu mikono yetu ili kuvumilia majaribu tunayokabili tunapomtumikia Mungu. (Mathayo 24:13) Kwa kufanya hivyo, tunaufurahisha moyo wa Yehova.—Mithali 27:11.

Jinsi Mikono Inavyotiwa Nguvu

Wayahudi wa siku za Ezra walihitaji kuitia nguvu mikono yao ili wamalize kujenga upya hekalu la Yehova huko Yerusalemu. Mikono yao ilitiwaje nguvu? Biblia inasema: “Wakaifanya sikukuu ya mikate isiyotiwa chachu kwa furaha, kwa muda wa siku saba; kwa kuwa BWANA amewafurahisha, na kumgeuza moyo mfalme wa Ashuru, awaelekee, ili awatie nguvu mikono yao katika kazi hiyo ya nyumba ya Mungu, Mungu wa Israeli.” (Ezra 6:22) Ni wazi kwamba Yehova alitumia nguvu yake ya utendaji kumchochea “mfalme wa Ashuru” ili awaruhusu watu Wake warudi kwao. Yehova pia aliwachochea watu wakamaliza kazi waliyokuwa wameanza.

Baadaye, kuta za Yerusalemu zilipohitaji kujengwa upya, Nehemia aliitia nguvu mikono ya ndugu zake ili wafanye kazi hiyo. Tunasoma hivi: “Nikawaeleza habari ya mkono wa Mungu wangu ulivyokuwa mwema juu yangu; pia na maneno ya mfalme aliyoniambia. Nao wakasema, Haya! Na tuondoke tukajenge. Basi wakaitia mikono yao nguvu kwa kazi hiyo njema.” Kwa mikono iliyotiwa nguvu, Nehemia na Wayahudi wenzake waliweza kujenga upya kuta za Yerusalemu kwa siku 52 tu!—Nehemia 2:18; 6:9, 15.

Vivyo hivyo, Yehova huitia nguvu mikono yetu ili tuhubiri habari njema za Ufalme. (Mathayo 24:14) Yeye hufanya hivyo ‘kwa kutupatia vifaa kwa kila jambo jema ili tufanye mapenzi yake.’ (Waebrania 13:21) Yeye ametupatia vifaa bora sana. Tuna Biblia na vitabu vinavyozungumzia Biblia, magazeti, broshua, trakti, na kanda na video zilizorekodiwa ili zitumiwe kuwafikia watu kote ulimwenguni. Vichapo vyetu vinapatikana katika lugha zipatazo 380. Isitoshe, kupitia mikutano ya kutaniko na makusanyiko, Yehova huandaa elimu ya kimungu na hutuzoeza kutumia vifaa hivyo bora katika kutimiza huduma yetu.

Ingawa Yehova hutia nguvu mikono yetu kwa njia nyingi sana, yeye pia hutarajia tujitahidi. Kumbuka mambo ambayo nabii Elisha alimwambia Mfalme Yehoashi, aliyekuja kumwomba Elisha msaada wa kupambana na wavamizi kutoka Shamu. Elisha alimwambia mfalme huyo achukue mishale na kupiga chini. Masimulizi ya Biblia yanasema: “Akaipiga mara tatu, akaacha. Yule mtu wa Mungu akamkasirikia, akasema, Ingalikupasa kupiga mara tano au mara sita; ndipo ungaliipiga Shamu hata kuiangamiza; bali sasa utaipiga Shamu mara tatu tu.” (2 Wafalme 13:18, 19) Kwa kuwa hakuonyesha bidii, Yehoashi alifanikiwa kidogo tu katika vita vyake na Washami.

Tunaweza kutumia kanuni hiyo iwapo tunataka kutimiza kazi ambayo Yehova ametupatia. Badala ya kuhangaika kuhusu vizuizi tunavyokabili au kuhusu ugumu wa kazi tuliyopewa, tunapaswa kuifanya kwa bidii na kwa moyo wote. Tunahitaji kuitia nguvu mikono yetu na kumtegemea Yehova atusaidie.—Isaya 35:3, 4.

Yehova Ataitia Nguvu Mikono Yetu

Yehova hatashindwa kutusaidia na kuitia nguvu mikono yetu ili kufanya mapenzi yake. Bila shaka, Mungu hatafanya muujiza au kutufanyia kila kitu. Yeye hutazamia tufanye sehemu yetu—kusoma Biblia kila siku, kujitayarisha kwa ajili ya mikutano na kuihudhuria kwa ukawaida, kushiriki katika huduma mara nyingi iwezekanavyo, na kusali kwake daima. Tukifanya sehemu yetu kwa bidii tunapokuwa na nafasi, Yehova atatupatia nguvu ya kufanya yale anayotarajia tufanye.—Wafilipi 4:13.

Fikiria kisa cha Mkristo mmoja aliyefiwa na mkewe na mama yake katika kipindi cha mwaka mmoja. Akiwa bado na huzuni hiyo, mwanaye aliachwa na mkewe ambaye pia aliacha njia ya Kikristo. “Nilijifunza kwamba hatuwezi kuchagua matatizo yatakayotupata, wala kuchagua wakati yatakapotupata, wala kuchagua ni mara ngapi matatizo hayo yatatupata,” akasema ndugu huyo. Yeye hupata wapi nguvu za kuendelea? “Sala na funzo la kibinafsi zimenitegemeza sana. Nao utegemezo wa ndugu na dada zangu wa kiroho umenifariji sana. Zaidi ya yote, nimetambua umuhimu wa kusitawisha uhusiano mzuri na Yehova kabla ya kupatwa na magumu.”

Hata hali yako iweje maishani, azimia kumtumaini Yehova kabisa na kutumia ifaavyo maandalizi yake yote ya kuitia nguvu mikono yako. Kisha utaweza kumtolea Yehova utumishi bora na hivyo kulisifu na kulitukuza jina lake lililotukuka sana.—Waebrania 13:15.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kwa kuwa hakuonyesha bidii, Yehoashi alifanikiwa kidogo tu katika vita vyake na Washami