Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, andiko la Ufunuo 20:8 linamaanisha kwamba watu watakaopotoshwa na Shetani wakati wa jaribu la mwisho watakuwa wengi sana?

Andiko la Ufunuo 20:8 linaeleza jinsi ambavyo Shetani atawashambulia mara ya mwisho watu watakaokuwa duniani baada ya utawala wa miaka elfu wa Ufalme wa Kimesiya. Mstari huo unasema hivi kumhusu Shetani: “Atatoka kwenda kuyaongoza vibaya yale mataifa katika pembe nne za dunia, Gogu na Magogu, kuyakusanya pamoja kwa ajili ya vita. Hesabu yayo ni kama mchanga wa bahari.”

Licha ya maendeleo ya kisayansi na pia kuwepo kwa vifaa vya kufanyia hesabu, hakuna awezaye kuhesabu “mchanga wa bahari.” Kwa hiyo, inaweza kusemwa kwamba usemi huo unawakilisha idadi isiyojulikana, isiyoweza kuhesabiwa. Lakini je, ni idadi kubwa mno, isiyoweza kuhesabiwa, au ni idadi kubwa tu lakini isiyojulikana?

Katika Biblia, usemi “mchanga wa bahari” umetumiwa kwa njia kadhaa. Kwa mfano, twasoma hivi kwenye Mwanzo 41:49: “Yusufu akakusanya nafaka kama mchanga wa pwani, nyingi mno, hata akaacha kuhesabu, maana ilikuwa haina hesabu.” Andiko hilo lakazia kwamba nafaka hiyo haikuwa na hesabu. Vivyo hivyo, Yehova alisema hivi: “Kama vile jeshi la mbinguni haliwezi kuhesabiwa, wala mchanga wa bahari kupimwa; ndivyo nitakavyoongeza wazao wa Daudi, mtumishi wangu.” Kama vile nyota za mbinguni na mchanga wa bahari usivyoweza kuhesabiwa, vivyo hivyo Yehova atatimiza ahadi yake kwa Daudi.—Yeremia 33:22.

Mara nyingi usemi “mchanga wa bahari” humaanisha kitu kikubwa ajabu au kingi mno. Waisraeli waliokuwa Gilgali waliogopeshwa sana na jeshi la Wafilisti lililokusanyika Mikmashi, ambalo lilikuwa “kama mchanga ulio ufuoni mwa bahari kwa wingi wao.” (1 Samweli 13:5, 6; Waamuzi 7:12) Naye “Mungu akampa Sulemani hekima, na akili nyingi sana, na moyo mkuu, kama mchanga ulioko pwani.” (1 Wafalme 4:29) Ijapokuwa kila kitu kinachotajwa hapo juu kilikuwa kingi, bado kilikuwa na mipaka.

“Mchanga wa bahari” unaweza pia kuwakilisha idadi isiyojulikana, bila kuonyesha kwamba ni idadi kubwa mno. Yehova alimwambia Abrahamu hivi: “Nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani.” (Mwanzo 22:17) Yehova aliporudia ahadi hiyo kwa Yakobo, mjukuu wa Abrahamu, alitumia usemi “mavumbi ya nchi,” naye Yakobo akatumia usemi, “mchanga wa bahari.” (Mwanzo 28:14; 32:12) Mwishowe “uzao” wa Abrahamu ulijumlisha watu 144,000 mbali na Yesu Kristo. Yesu aliwaita watu hao “kundi dogo.”—Luka 12:32; Wagalatia 3:16, 29; Ufunuo 7:4; 14:1, 3.

Mifano hiyo inatufundisha nini? Inatufundisha kwamba usemi, “kama mchanga wa bahari” sikuzote haumaanishi idadi kubwa mno, isiyohesabika; wala hautumiwi sikuzote kumaanisha kitu kilicho kikubwa sana au kingi mno. Mara nyingi huwakilisha idadi isiyojulikana lakini inayoweza kuwa kubwa. Kwa hiyo, ni jambo la busara kuamini kwamba umati wenye kuasi unaomuunga Shetani mkono anapowashambulia watu wa Mungu kwa mara ya mwisho, si mkubwa mno, lakini ni mkubwa vya kutosha kuwa tisho. Hata hivyo, kwa sasa bado idadi yao haijulikani.