Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tulikotumwa Kuwa Mishonari Kumekuwa Nyumbani

Tulikotumwa Kuwa Mishonari Kumekuwa Nyumbani

Simulizi la Maisha

Tulikotumwa Kuwa Mishonari Kumekuwa Nyumbani

LIMESIMULIWA NA DICK WALDRON

Ilikuwa Jumapili alasiri, mnamo mwezi wa Septemba 1953, nasi tulikuwa bado wageni katika nchi moja ya Kusini-Magharibi ya Afrika (ambayo sasa inaitwa Namibia). Juma moja halikuwa limepita tangu tulipowasili nchini humo, nasi tulikuwa tukijiandaa kufanya mkutano wa watu wote katika mji wake mkuu, Windhoek. Kwa nini tulitoka Australia na kuhamia nchi hii ya Afrika? Mimi na mke wangu, pamoja na wanawake watatu vijana, tulikuwa tumekuja kutangaza habari njema za Ufalme wa Mungu tukiwa mishonari.—Mathayo 24:14.

NILIZALIWA katika mwaka wa kihistoria wa 1914 katika nchi ya Australia iliyo mbali sana na Namibia. Nilikuwa tineja wakati wa ule Mshuko Mkubwa wa Kiuchumi, hata hivyo, nililazimika kuisaidia familia yetu kupata riziki. Hakukuwa na kazi ya kuajiriwa, lakini nilijifunza mbinu ya kuwinda sungura wa porini, ambao walikuwa wengi mno nchini Australia. Kwa hiyo, niliisaidia familia yetu kwa kuleta nyama ya sungura kwa ukawaida.

Kabla ya vita vya pili vya ulimwengu kuzuka mwaka wa 1939, nilifaulu kupata kazi kwenye mabasi na treni za umeme katika jiji la Melbourne. Watu 700 walikuwa wakifanya kazi kwa zamu kwenye mabasi hayo, na kila zamu nilifanya kazi na dereva au kondakta tofauti. Mara nyingi niliwauliza hivi, “Wewe ni mfuasi wa dini gani?” kisha niliwaomba wanieleze mambo wanayoamini. Shahidi mmoja wa Yehova ndiye peke yake aliyenipa majibu yenye kuridhisha. Alinieleza fundisho la Biblia kuhusu paradiso duniani, ambamo wanadamu wanaomcha Mungu wataishi milele.—Zaburi 37:29.

Wakati huohuo, mama yangu alikutana pia na Mashahidi wa Yehova. Mara nyingi, niliporudi nyumbani baada ya zamu ya usiku, alinipa chakula pamoja na nakala ya gazeti la Consolation (ambalo sasa ni Amkeni!). Nilivutiwa mno na mambo niliyosoma. Muda si muda, niliamua kwamba hii ndiyo dini ya kweli, hivyo nilishirikiana nao kwa bidii na nikabatizwa mnamo Mei mwaka wa 1940.

Kulikuwa na makao ya mapainia huko Melbourne, ambako Mashahidi wa Yehova 25 hivi waliokuwa wahudumu wa wakati wote waliishi. Nilianza kuishi nao. Kila siku nilifurahia mazungumzo yao yenye kusisimua kuhusu kazi ya kuhubiri, hivyo nikawa na hamu kubwa ya kuwa painia. Mwishowe, niliomba kuwa painia. Nilikubaliwa na nikaalikwa kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Australia. Nikawa mshiriki wa familia ya Betheli.

Kifungo na Marufuku

Moja ya kazi nilizopewa Betheli ni kupasua mbao kwenye kiwanda cha kupasulia mbao. Tulipasua mbao ambazo ziliteketezwa ili kufanyiza gesi iliyotumiwa kuendesha magari ya ofisi ya tawi, kwa sababu vita vilisababisha uhaba wa petroli. Tulikuwa 12 kwenye kiwanda hicho, na sote tulikabiliwa na hatari ya kuandikishwa jeshini. Muda si muda, tulifungwa gerezani miezi sita kwa kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya msimamo wetu unaotegemea Biblia. (Isaya 2:4) Tulipelekwa kufanya kazi ngumu kwenye shamba la gereza. Tulipewa kazi gani? Jambo la kushangaza ni kwamba tulipewa kazi ya kupasua mbao, kazi tuliyokuwa tumezoezwa kufanya Betheli!

Tulipasua mbao kwa ustadi sana hivi kwamba msimamizi wa gereza alitupatia Biblia na vichapo vyetu vya Biblia, licha ya sheria kali zilizokataza vichapo hivyo. Wakati huo nilijifunza umuhimu wa kuwa na uhusiano mzuri na wengine. Kuna ndugu mmoja ambaye sikupatana naye kamwe nilipokuwa nikifanya kazi Betheli. Nyutu zetu zilikuwa tofauti sana. Sasa, unafikiri nilikaa na nani katika chumba changu gerezani? Ni ndugu huyohuyo. Sasa tulikuwa na wakati mwingi wa kufahamiana, na hivyo tukakuza urafiki wa karibu sana na wenye kudumu.

Baada ya muda, kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku nchini Australia. Ndugu waliokuwa Betheli hawakuwa na pesa nyingi kwa sababu pesa zote zilichukuliwa. Siku moja, ndugu fulani alinijia na kuniambia: “Dick, nataka kwenda kuhubiri kidogo mjini, lakini sina viatu vingine, ila viatu vya kazi.” Nilifurahi kumpa viatu vyangu, naye akaenda mjini akiwa amevivalia.

Baadaye, tulisikia kwamba alikamatwa na kufungwa gerezani kwa sababu ya kuhubiri. Nilimwandikia barua fupi iliyosema hivi: “Pole sana. Angalau sikuwa nimevaa viatu vyangu.” Baada ya muda mfupi, mimi pia nilikamatwa na nikafungwa gerezani kwa mara ya pili kwa sababu ya msimamo wangu wa kutounga mkono upande wowote. Baada ya kuachiliwa, nilipewa mgawo wa kutunza shamba ambamo chakula cha kulisha familia ya Betheli kilikuzwa. Wakati huo tulikuwa tumeshinda kesi mahakamani, na marufuku ikaondolewa kwa kazi ya Mashahidi wa Yehova.

Nafunga Ndoa na Mhubiri Mwenye Bidii

Nilipokuwa nikifanya kazi kwenye shamba la Betheli, nilianza kufikiria sana ndoa na nikavutiwa na dada mmoja kijana aitwaye Coralie Clogan, aliyekuwa painia. Nyanya ya Coralie ndiye aliyeanza kupendezwa na ujumbe wa Biblia katika jamaa yao. Alipokuwa karibu kufa, alimwambia hivi Vera, mama ya Coralie: “Walee watoto wako ili wampende Mungu na kumtumikia, na siku moja tutakutana katika Paradiso duniani.” Baadaye, painia mmoja alipomtembelea Vera na kumwonyesha kichapo Millions Now Living Will Never Die, alianza kuelewa maana ya maneno hayo. Kijitabu hicho kilimsadikishia Vera kwamba Mungu alikusudia wanadamu wafurahie maisha katika paradiso duniani. (Ufunuo 21:4) Alibatizwa mapema miaka ya 1930, na akaanza kuwasaidia binti zake watatu—Lucy, Jean, na Coralie—wampende Mungu kama alivyohimizwa na mama yake. Hata hivyo, baba ya Coralie alichukia mno dini ya familia yake. Yesu alikuwa ameonya kwamba familia zingekumbwa na hali hiyo.—Mathayo 10:34-36.

Familia ya Clogan ilipenda sana muziki; kila mtoto alijua kucheza ala fulani ya muziki. Coralie alicheza fidla, naye alipata shahada ya diploma katika muziki mwaka wa 1939, akiwa na umri wa miaka 15. Kuzuka kwa Vita vya Pili vya Ulimwengu kulimfanya Coralie afikirie sana maisha yake ya wakati ujao. Wakati ulikuwa umewadia wa kuamua jambo ambalo angefanya maishani. Angeweza kuwa mchezaji wa muziki kwa kuwa tayari alikuwa amealikwa kujiunga na Melbourne Symphony Orchestra, au angeweza kutumia wakati wake katika kazi tukufu ya kuhubiri habari njema za Ufalme. Baada ya kufikiria kwa uzito jambo hilo, Coralie na dada zake wawili walibatizwa mwaka wa 1940 na wakajitayarisha kuwa wahubiri wa wakati wote wa habari njema.

Mara tu baada ya Coralie kuamua kuwa mhudumu wa wakati wote, alifikiwa na ndugu mwenye madaraka katika ofisi ya tawi ya Australia, Lloyd Barry, ambaye alitumikia baadaye akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Baada tu ya kutoa hotuba huko Melbourne, Barry alimwambia hivi Coralie: “Narudi Betheli. Mbona usisafiri nami kwa gari la moshi ukajiunge na familia ya Betheli?” Coralie alikubali mara moja.

Coralie na dada wengine wa familia ya Betheli walifanya kazi muhimu ya kupeleka vichapo vya Biblia kwa akina ndugu nchini Australia wakati wa marufuku na vita. Kwa kweli, walichapisha vichapo vingi chini ya usimamizi wa Ndugu Malcolm Vale. Kitabu The New World na kitabu Children vilikuwa vikichapishwa na kutiwa majalada, na akina ndugu hawakukosa toleo lolote la Mnara wa Mlinzi kwa zaidi ya miaka miwili ya marufuku.

Walilazimika kuhamisha ofisi ya uchapishaji mara 15 ili kuepuka polisi. Pindi moja, vichapo vya Biblia vilikuwa vikichapishiwa kwenye chumba cha ardhini cha jengo ambamo uchapishaji mwingine wa kuwahadaa polisi ulikuwa ukifanywa. Dada aliyekuwa kwenye sehemu ya mapokezi angeweza kubonyeza kidude fulani na kupiga kengele iliyokuwa katika chumba hicho cha ardhini alipoona hatari yoyote, na hivyo akina dada waliokuwa katika chumba hicho wangeweza kuficha vichapo kabla mtu yeyote hajaanza kufanya msako.

Siku moja wakati wa msako, baadhi ya dada walishtuka sana walipogundua kwamba nakala ya gazeti Mnara wa Mlinzi ilikuwa imeachwa juu ya meza ambapo ilionekana waziwazi. Polisi mmoja aliingia ndani, akauwekelea mkoba wake juu ya gazeti hilo, na akaanza kufanya msako. Hakupata chochote, hivyo akachukua mkoba wake na akaenda zake!

Baada ya marufuku kuondolewa na ndugu kurudishiwa tena vifaa vya ofisi ya tawi, wengi wao walipewa nafasi ya kuwa mapainia wa pekee. Ndipo Coralie alipojitolea kwenda Glen Innes. Nilijiunga naye huko baada ya kumwoa mnamo Januari 1, 1948. Wakati tulipoondoka huko, kutaniko kubwa lenye maendeleo lilikuwa limeanzishwa.

Mgawo wetu wa pili ulikuwa Rockhampton, lakini hatukupata mahali pa kuishi. Kwa hiyo tulipiga hema katika uwanja uliokuwa katika shamba la mtu mmoja mwenye kupendezwa. Tuliishi kwenye hema hilo kwa muda wa miezi tisa. Tungaliishi humo kwa muda mrefu zaidi, lakini mvua ilipoanza kunyesha, dhoruba kali ilirarua kabisa hema hilo na kulifagilia mbali. *

Twatumwa Nchi Nyingine

Tulipokuwa Rockhampton, tulialikwa kuhudhuria darasa la 19 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower ili kupata mazoezi ya mishonari. Hapo ndipo tulipotumwa kwenye nchi ya Kusini-Magharibi ya Afrika, baada tu ya kufuzu mwaka wa 1952.

Punde si punde, makasisi wa dini zinazojiita za Kikristo walionyesha chuki kwa kazi yetu ya mishonari. Kila Jumapili kwa majuma sita mfululizo, waliwaonya wafuasi wao kanisani kutuhusu. Waliwaambia watu wasitukaribishe nyumbani mwao wala kuturuhusu kuwasomea Biblia, kwa sababu ingewavuruga. Katika sehemu moja, tuliwaachia watu vichapo kadhaa, lakini kasisi alitufuata nyumba hadi nyumba na kukusanya vichapo hivyo. Siku moja tulipokuwa tukizungumza na kasisi huyo nyumbani mwake tuligundua kwamba alikuwa na vitabu vyetu vingi.

Muda si muda, wenye mamlaka walianza pia kuwa na wasiwasi kuhusu kazi yetu. Hapana shaka kwamba kwa sababu ya uchochezi wa makasisi, walitushuku kuwa na uhusiano na Wakomunisti. Kwa hiyo walichukua alama zetu za vidole, na baadhi ya watu tuliowatembelea walihojiwa. Licha ya upinzani huo wote, hudhurio la mikutano yetu lilizidi kuongezeka.

Tangu tulipowasili nchini, tulikuwa na hamu kubwa ya kueneza ujumbe wa Biblia kwa wenyeji wa makabila ya Ovambo, Herero, na Nama. Lakini haikuwa rahisi. Nyakati hizo, nchi ya Kusini-Magharibi ya Afrika ilikuwa chini ya utawala wa serikali ya Afrika Kusini iliyozingatia ubaguzi wa rangi. Hatukuruhusiwa kuhubiri kwenye makazi ya watu weusi bila kibali cha serikali kwa sababu tulikuwa wazungu. Tuliomba kibali mara kwa mara, lakini wenye mamlaka walikataa kutupatia.

Baada ya kutumikia kwa miaka miwili katika nchi ya kigeni, jambo tusilotarajia lilitukia. Coralie alikuwa mja-mzito. Binti yetu Charlotte alizaliwa mnamo Oktoba 1955. Ijapokuwa hatungeweza kuendelea kuwa mishonari, nilipata kazi ya muda na nikaendelea kupainia kwa muda fulani.

Jibu kwa Sala Zetu

Tulikumbwa na tatizo jingine mwaka wa 1960. Coralie alipokea barua iliyosema kwamba mama yake alikuwa mgonjwa sana na kama Coralie hangerudi nyumbani, huenda hangemwona mamaye tena. Kwa hiyo tulipanga kuondoka nchi ya Kusini-Magharibi ya Afrika na kurudi Australia. Lakini juma lilelile ambalo tulipanga kuondoka, wenye mamlaka walinipa kibali cha kwenda kwenye eneo la watu weusi la Katutura. Sasa tungefanya nini? Je, tungerudisha kibali hicho baada ya kukitafuta kwa miaka saba? Ilikuwa rahisi kusema kwamba wengine wataendelea na kazi hiyo. Lakini je, hii haikuwa zawadi kutoka kwa Yehova na jibu kwa sala zetu?

Nilifanya uamuzi mara moja. Ningebaki nchini, kwa sababu niliogopa kwamba ombi letu la kibali chetu cha uraia lingetupiliwa mbali kama tungeondoka sote na kurudi Australia. Siku iliyofuata, nilirudisha tiketi yangu ya kusafiri kwa meli, na nikawaruhusu Coralie na Charlotte waende Australia kwa likizo ndefu.

Walipokuwa Australia, nilianza kuhubiri eneo la watu weusi. Watu wengi sana walipendezwa. Coralie na Charlotte waliporudi, watu kadhaa wa eneo hilo walikuwa wakihudhuria mikutano yetu.

Wakati huo nilikuwa na gari zee nililotumia kuwapeleka mikutanoni watu wenye kupendezwa. Nilisafiri mara nne au tano hivi wakati wa kila mkutano, na nilibeba watu saba, wanane, au tisa. Mtu wa mwisho aliposhuka, Coralie alikuwa akiniuliza hivi kwa utani: “Ni wangapi waliobaki chini ya kiti?”

Ili tuwe na matokeo zaidi katika kazi ya kuhubiri, tulihitaji vichapo katika lugha ya wenyeji. Kwa hiyo nilikuwa na pendeleo la pekee la kufanya mpango wa kutafsiriwa kwa trakti ya Uzima Katika Ulimwengu Mpya katika lugha nne za wenyeji: Kiherero, Kinama, Kindonga, na Kwanyama. Watu wenye elimu tuliokuwa tukijifunza nao Biblia ndio waliokuwa watafsiri, lakini nilifanya kazi nao ili kuhakikisha kwamba kila sentensi ilitafsiriwa kwa usahihi. Lugha ya Kinama haina maneno mengi. Kwa mfano, nilikuwa nikijaribu kueleza wazo hili: “Hapo mwanzo Adamu alikuwa mtu mkamilifu.” Mtafsiri alijikuna-kuna kichwani na kusema kwamba hangeweza kukumbuka neno “mkamilifu” katika lugha ya Kinama. Mwishowe alisema, “nimelipata.” “Hapo mwanzo Adamu alikuwa kama tunda la pichi lililoiva.”

Tumefurahia Tulikotumwa

Miaka 49 imepita tangu tulipowasili katika nchi hii, ambayo sasa inaitwa Namibia. Leo si lazima kuwa na kibali ili kuingia maeneo ya watu weusi. Namibia inatawaliwa na serikali mpya ambayo inafuata katiba isiyozingatia ubaguzi wa rangi. Leo, kuna makutaniko manne makubwa yanayokutana kwenye Majumba mazuri ya Ufalme katika jiji la Windhoek.

Mara nyingi tumekumbuka maneno tuliyoambiwa kwenye Shule ya Gileadi: “Fanyeni nchi mnakotumwa kuwa nyumbani.” Tunapoona jinsi ambavyo Yehova ametusaidia, tunasadiki kwamba yalikuwa mapenzi yake kwetu kufanya nchi hii ya kigeni kuwa nyumbani kwetu. Tumewapenda akina ndugu, pamoja na tamaduni zao mbalimbali zenye kuvutia. Tumecheka pamoja nao na kulia pamoja nao wanapokumbwa na mambo yenye kuhuzunisha. Baadhi ya wale wapya tuliokuwa tukiwasomba kwa gari letu kwenda mikutanoni, sasa ni nguzo katika makutaniko. Tulipowasili katika nchi hii kubwa mwaka wa 1953, wahubiri wa habari njema hawakuzidi kumi. Sasa idadi ya wahubiri imeongezeka kutoka idadi hiyo ndogo sana hadi zaidi ya wahubiri 1,200. Kupatana na ahadi yake, Yehova ametokeza ukuzi katika eneo ambalo sisi na wengine ‘tulipanda na kutia maji.’—1 Wakorintho 3:6.

Mimi na Coralie tunaridhika sana tunapofikiria miaka mingi ambayo tumekuwa tukitumika, kwanza nchini Australia na sasa nchini Namibia. Tunatumaini na kusali ili Yehova aendelee kutupatia nguvu za kufanya mapenzi yake sasa na milele.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 22 Mnara wa Mlinzi wa Desemba 1, 1952, ukurasa wa 707-708, unasimulia jinsi Waldron na mkewe walivyovumilia katika mgawo huo mgumu, lakini majina yao hayatajwi.

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Tukielekea kwenye mgawo wetu huko Rockhampton, Australia

[Picha katika ukurasa wa 27]

Tukiwa bandarini kuelekea Shule ya Gileadi

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kuhubiri nchini Namibia hutuletea shangwe nyingi sana