Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utoaji Unaoleta Furaha

Utoaji Unaoleta Furaha

Utoaji Unaoleta Furaha

GENIVAL anayeishi katika mtaa wa mabanda huko kaskazini-mashariki mwa Brazili, alimruzuku mke na watoto wake kwa mshahara mdogo aliopata akiwa askari mlinda-usalama kwenye hospitali moja. Licha ya magumu aliyokuwa nayo, Genival aliendelea kutoa fungu lake la kumi kwa uaminifu. “Wakati mwingine familia yangu ilikosa chakula,” anasema huku akishika-shika tumbo lake, “lakini nilitaka kumpa Mungu kilicho bora, haidhuru kungenigharimu nini.”

Hata baada ya kupoteza kazi yake, Genival aliendelea kutoa fungu la kumi. Kasisi wake alimhimiza amjaribu Mungu kwa kutoa mchango mkubwa, akimhakikishia kwamba Mungu angembariki sana kama angefanya hivyo. Kwa hiyo, Genival akaamua kuuza nyumba yake na kupeleka pesa zote kanisani.

Mbali na Genival watu wengi walio maskini sana hutoa fungu la kumi kwa unyofu. Wanafanya hivyo kwa sababu wanafundishwa na makanisa yao kwamba hilo ni takwa la Biblia. Ndivyo ilivyo?

Kutoa Fungu la Kumi na Sheria

Amri ya kutoa fungu la kumi ilikuwa takwa moja la Sheria ambayo Yehova Mungu aliyapa makabila 12 ya Israeli la kale zaidi ya miaka 3,500 iliyopita. Sheria hiyo iliagiza kwamba fungu la kumi la mazao na matunda ya nchi na fungu la kumi la wanyama wote waliozaliwa katika mifugo yao litolewe kwa kabila la Lawi ili kutegemeza utumishi wao kwenye hema la kukutania.—Mambo ya Walawi 27:30, 32; Hesabu 18:21, 24.

Yehova aliwahakikishia Waisraeli kwamba Sheria ‘haingekuwa nzito mno kwao.’ (Kumbukumbu la Torati 30:11) Yehova aliwaahidi kwamba wangepata mavuno mengi iwapo wangefuata kwa uaminifu sheria zake, kutia ndani kutoa fungu la kumi. Na ili kusiwe na upungufu, fungu la kumi la ziada lilitolewa kila mwaka, na kwa kawaida lilitumiwa wakati taifa hilo lilipofanya sherehe za kidini. Hivyo, ‘mgeni, yatima, na mjane’ wangeweza kushiba.—Kumbukumbu la Torati 14:28, 29; 28:1, 2, 11-14.

Sheria haikuonyesha adhabu ambayo mtu angepata kwa kukosa kutoa fungu la kumi, lakini kila Mwisraeli alikuwa na daraka zito la kutegemeza ibada ya kweli kwa njia hiyo. Kwa kweli, Yehova aliwashutumu Waisraeli waliopuuza utoaji wa fungu la kumi siku ya Malaki kwa ‘kumwibia fungu la kumi na dhabihu.’ (Malaki 3:8, New International Version) Je, tunaweza kusema kwamba Wakristo wasiotoa fungu la kumi wanamwibia Mungu?

Ona kwamba si kawaida kwa sheria za nchi moja kutumika katika nchi nyingine. Kwa mfano, sheria ambayo huwataka madereva wa magari nchini Uingereza wafuate upande wa kushoto wa barabara haitumiki nchini Ufaransa. Vivyo hivyo, sheria iliyowataka watu watoe fungu la kumi ilikuwa sehemu ya agano kati ya Mungu na taifa la Israeli pekee. (Kutoka 19:3-8; Zaburi 147:19, 20) Waisraeli tu ndio waliopaswa kufuata sheria hiyo.

Isitoshe, ingawa Mungu habadiliki, matakwa yake hubadilika mara kwa mara. (Malaki 3:6) Biblia inasema waziwazi kwamba kifo cha kidhabihu cha Yesu mwaka wa 33 W.K., ‘kilifuta kabisa,’ au ‘kubatilisha,’ Sheria pamoja na ‘amri ya kukusanya sehemu za kumi.’—Wakolosai 2:13, 14; Waefeso 2:13-15; Waebrania 7:5, 18.

Utoaji wa Kikristo

Hata hivyo, michango ya kutegemeza ibada ya kweli bado ilihitajiwa. Yesu aliwatuma wanafunzi wake ‘wawe mashahidi hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.’ (Matendo 1:8) Uhitaji wa kuwa na walimu Wakristo na waangalizi wa kutembelea na kuyatia nguvu makutaniko uliongezeka kadiri idadi ya waamini ilivyoongezeka. Wajane, mayatima, na watu wengine wenye uhitaji walipaswa kutunzwa nyakati nyingine. Wakristo wa karne ya kwanza waligharimiaje mambo hayo?

Mnamo mwaka wa 55 W.K., Wakristo wasio Wayahudi wa Ulaya na Asia Ndogo waliombwa wasaidie kutaniko maskini la Yudea. Katika barua zake kwa kutaniko la Korintho, mtume Paulo anaeleza jinsi ukusanyaji wa ‘mchango kwa ajili ya watakatifu’ ulivyopangwa. (1 Wakorintho 16:1) Huenda ukashangazwa na yale Paulo aliyosema kuhusu utoaji wa Kikristo.

Mtume Paulo hakuwabembeleza waamini wenzake watoe. Kwa kweli Wakristo wa Makedonia waliokuwa “chini ya taabu kubwa” na katika “umaskini wa kina kirefu” walilazimika ‘kufuliza kumwomba kwa kusihi sana ili wapate pendeleo la kutoa kwa fadhili na kuwa na ushiriki katika huduma waliyokusudiwa watakatifu.’—2 Wakorintho 8:1-4.

Ni kweli kwamba Paulo aliwatia moyo Wakorintho waliokuwa matajiri waige ndugu zao wa Makedonia waliokuwa wakarimu. Hata hivyo, kitabu kimoja cha kitaalamu kinasema kwamba ‘alikataa kutoa maagizo, na badala yake akawaomba, akawatolea madokezo, akawatia moyo, na kuwasihi. Wakorintho hawangetoa kwa hiari wala kwa uchangamfu kama wangelazimishwa.’ Paulo alijua kwamba “Mungu hupenda mpaji mchangamfu,” hapendi yule anayetoa “kwa kinyongo au kwa shurutisho.”—2 Wakorintho 9:7.

Imani yao kubwa, ujuzi, pamoja na upendo wa kweli kwa Wakristo wenzao ungewachochea Wakorintho watoe kwa hiari.—2 Wakorintho 8:7, 8.

“Kama Vile Ameazimia Moyoni Mwake”

Badala ya kutaja kiasi hususa cha pesa, Paulo alipendekeza tu kwamba ‘kila mmoja atenge kiasi cha fedha kadiri ya mapato yake’ katika siku ya kwanza ya juma. (1 Wakorintho 16:2, Biblia Habari Njema) Kwa kupanga na pia kutenga kando kiasi fulani kwa ukawaida, Wakorintho hawangehisi kwamba wanashurutishwa kutoa michango yao, wala hawangeitoa kwa sababu ya msisimuko tu wakati Paulo alipofika. Kila Mkristo angeamua kibinafsi ni kiasi gani angetoa, kulingana na ‘alichokuwa ameazimia moyoni mwake.’—2 Wakorintho 9:5, 7.

Wakorintho walihitaji kupanda kwa wingi ili wavune kwa wingi. Paulo hakusema lolote kuhusu kutoa kupita uwezo wa mtu. ‘Sikusudii iwe vigumu kwenu,’ Paulo akawahakikishia. Michango ‘ilikubalika hasa kulingana na alicho nacho mtu, si kulingana na kile ambacho mtu hana.’ (2 Wakorintho 8:12, 13; 9:6) Katika barua fulani aliyoandika baadaye, mtume alionya: “Ikiwa yeyote hawaandalii kitu . . . wale walio washiriki wa nyumbani mwake, ameikana imani naye ni mbaya zaidi kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Paulo hakuwahimiza watu watoe kwa njia iliyovunja kanuni hiyo.

Inafaa kuona kwamba Paulo alisimamia ukusanyaji wa ‘mchango kwa ajili ya watakatifu’ waliokuwa na uhitaji. Maandiko hayasemi popote pale kwamba Paulo au mitume wengine walipanga michango itolewe au walipokea fungu la kumi ili kugharimia huduma zao wenyewe. (Matendo 3:6) Paulo alishukuru daima kwa zawadi ambazo makutaniko yalimpelekea, naye alikuwa mwangalifu asiwatwike ndugu zake “mzigo ulemeao wenye gharama.”—1 Wathesalonike 2:9; Wafilipi 4:15-18.

Kutoa kwa Hiari Leo

Ni wazi kwamba wafuasi wa Kristo katika karne ya kwanza walitoa michango ya hiari, wala si fungu la kumi. Hata hivyo, huenda ukajiuliza kama utoaji huo bado ni njia bora ya kugharimia kazi ya kuhubiri habari njema na kuwatunza Wakristo walio na uhitaji.

Fikiria yafuatayo. Mnamo mwaka wa 1879, wahariri wa gazeti hili walitaja hadharani kwamba “hawataombaomba wala kusihi wanadamu walitegemeze.” Je, uamuzi huo unazuia Mashahidi wa Yehova wasieneze kweli ya Biblia?

Leo, Mashahidi hugawanya Biblia, vitabu vya Kikristo, na vichapo vinginevyo katika nchi 235. Mwanzoni, nakala 6,000 za gazeti la Mnara wa Mlinzi, linalotumiwa kufundisha Biblia, zilikuwa zikigawanywa katika lugha moja tu. Tangu wakati huo, nakala zaidi ya 24,000,000 za gazeti hilo huchapwa mara mbili kwa mwezi katika lugha 146. Ili kupanga kazi ya ulimwenguni pote ya kufundisha Biblia, Mashahidi wamejenga au kununua majengo ya ofisi katika nchi 110. Kuongezea hayo, wamejenga mamia ya majumba ya kukutania na majumba ya kusanyiko ili kuwe na nafasi ya kutosha kwa wale wanaopendezwa kupokea mafundisho zaidi ya Biblia.

Ingawa ni muhimu kushughulikia mahitaji ya kiroho ya watu, Mashahidi wa Yehova hawapuuzi mahitaji ya kimwili ya waamini wenzao. Ndugu zao wanapokumbwa na vita, matetemeko ya ardhi, ukame, na dhoruba, wao huchukua hatua mara moja kupeleka dawa, chakula, mavazi, na vitu vingine vinavyohitajika. Vitu hivyo hugharimiwa kwa michango inayotolewa na Mkristo mmoja-mmoja au makutaniko.

Kutoa michango kwa hiari kunaleta matokeo mazuri na huwaondolea mzigo watu maskini kama Genival aliyetangulia kutajwa. Inafurahisha kwamba, kabla ya kuuza nyumba yake, Genival alitembelewa na Maria, mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. “Mazungumzo yangu na Shahidi huyo yaliokoa familia yangu na magumu mengi yasiyo ya lazima,” akumbuka Genival.

Genival alitambua kwamba kazi ya Mungu haitegemei fungu la kumi na kwamba kutoa fungu la kumi si takwa la Kimaandiko. Alijifunza kwamba Wakristo hubarikiwa wanapotoa kwa ukarimu lakini si lazima watoe kupita uwezo wao.

Kutoa kwa hiari kumemletea Genival furaha ya kweli. Anasema hivi kuhusu jambo hilo: “Huenda nitoe au nisitoe sehemu ya kumi ya mapato yangu, lakini mimi ninafurahia kutoa michango, na nina hakika kwamba Yehova anafurahi pia.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Je, Waandishi wa Kanisa wa Mapema Walifundisha Kuhusu Kutoa Fungu la Kumi?

“Wale walio matajiri kati yetu huwasaidia walio na uhitaji . . . Walio na mali na wanaotaka, hutoa wanachoona kinafaa.”—Kichapo The First Apology cha Justin Martyr, cha mwaka wa 150 hivi W.K.

“Wayahudi waliweka wakfu kwa Mungu fungu la kumi la mali zao, lakini wale walio huru huweka kando mali zao zote kwa ajili ya kazi za Mungu, . . . kama yule mjane maskini ambaye alitia katika sanduku la hazina ya Mungu riziki yake yote.”—Kichapo Against Heresies, cha Irenaeus cha mwaka wa 180 hivi W.K.

“Ingawa tuna sanduku la michango, pesa tunazochanga si za kununua wokovu kama ilivyo katika dini nyingine. Kila mmoja hutoa mchango mdogo mara moja kwa mwezi; lakini hufanya hivyo akipenda, na ikiwa tu anaweza: kwa kuwa watu hawalazimishwi; wanatoa kwa hiari.”—Kichapo Apology cha Tertullian cha mwaka wa 197 hivi W.K.

“Kanisa lilipopanuka na mashirika mengi yakatokea, sheria zilihitajika ambazo zingehakikisha kwamba makasisi wametegemezwa ifaavyo na kwa muda wote. Hivyo mpango wa kutoa fungu la kumi ukaanzishwa kupatana na Sheria ya Zamani . . . Yaonekana sheria hususa ya kwanza kuhusu utoaji huo imeandikwa katika barua ya maaskofu waliokutana jijini Tours mwaka wa 567 W.K. na pia katika [maandishi] ya Baraza la Macon la mwaka wa 585 W.K.”—Kichapo The Catholic Encyclopedia.

[Hisani]

Coin, top left: Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Utoaji wa hiari huleta furaha

[Picha katika ukurasa wa 7]

Michango ya hiari inagharimia kazi ya kuhubiri, kutoa misaada ya dharura, na ujenzi wa majengo ya kukutania