Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Barua Iliyobadili Maisha Yangu

Barua Iliyobadili Maisha Yangu

Simulizi la Maisha

Barua Iliyobadili Maisha Yangu

LIMESIMULIWA NA IRENE HOCHSTENBACH

Ilikuwa Jumanne jioni mwaka wa 1972. Nilikuwa na umri wa miaka 16 nami nilikuwa nimeambatana na wazazi wangu kwenye mkutano wa kidini katika jiji la Eindhoven, ambalo liko katika mkoa wa Brabant huku Uholanzi. Sikustarehe. Ndipo wasichana wawili wakanipatia barua fupi iliyosema: “Irene Mpendwa, tungependa sana kukusaidia.” Sikujua kwamba barua hiyo ingebadili maisha yangu kabisa. Lakini kabla ya kueleza mambo yaliyofuata, acha nieleze kidogo kuhusu maisha yangu ya utotoni.

NILIZALIWA katika kisiwa cha Belitung, huko Indonesia. Bado ninakumbuka sauti mbalimbali za kisiwa hicho chenye joto jingi. Nakumbuka sauti ya minazi iliyowayawaya upeponi, mtiririko wa mto uliokuwa karibu, kicheko cha watoto waliocheza karibu na nyumba yetu, na vilevile muziki tuliocheza nyumbani. Mwaka wa 1960, nilipokuwa na umri wa miaka minne, familia yetu ilihama Indonesia na kwenda Uholanzi. Tulisafiri kwa meli na sauti ambayo ninakumbuka hasa katika safari hiyo ni mwanasesere wangu aliyepiga ngoma zake. Nilipokuwa na umri wa miaka saba nikawa mgonjwa, na nilipoteza uwezo wangu wa kusikia. Tangu wakati huo sijaweza kusikia sauti zozote, ninazikumbuka tu.

Maisha ya Mtoto Kiziwi

Wazazi wangu walinitunza kwa upendo mwingi, kwa hiyo, mwanzoni sikuelewa kikamili jinsi ambavyo kutoweza kusikia kungeniathiri maishani. Nilipokuwa mtoto nilifurahia chombo changu kikubwa cha kunisaidia kusikia, ijapokuwa hakikunisaidia sana. Watoto majirani walizoea kuandika hadithi kwenye lami njiani ili kuwasiliana nami, nami niliwajibu ijapokuwa sikuweza kusikia sauti yangu mwenyewe.

Hatua kwa hatua nilitambua kwamba nilikuwa tofauti na watu wengine. Pia niliona kwamba watu wengine walinifanyia mzaha kwa sababu nilikuwa kiziwi, huku wengine wakikataa kushirikiana nami. Nilianza kuhisi upweke. Nilianza pia kuelewa magumu ambayo kiziwi hukabili maishani, na nilizidi kuwaogopa watu wasio viziwi.

Ili niweze kwenda shule ya viziwi, wazazi wangu waliamua tuhame kijiji cha mkoa wa Limburg ambako tulikuwa tukiishi na kuhamia jiji la Eindhoven. Baba yangu alitafuta kazi huko na ndugu yangu na dada zangu wakaenda shule mpya. Ninawashukuru kwa marekebisho yote waliyofanya kwa ajili yangu. Shuleni nilifundishwa jinsi ya kuongeza na kupunguza sauti kulingana na hali na jinsi ya kutamka maneno vizuri zaidi. Na ijapokuwa walimu hawakutumia lugha ya ishara, wanafunzi wenzangu walinifundisha lugha hiyo.

Sikuelewa Kile Kilichoendelea

Wazazi wangu walijitahidi sana kuwasiliana nami nilipokuwa mtoto, hata hivyo, mambo mengi yalinipita. Kwa mfano, sikuelewa kwamba wazazi wangu walikuwa wakijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Lakini ninakumbuka kwamba siku moja tulikwenda mahali ambapo watu wengi walikuwa wameketi kwenye viti. Wote walikazia macho huko mbele, nyakati nyingine walipiga makofi, na mara kwa mara walisimama. Sikuelewa ni kwa nini watu hao walifanya hayo yote. Muda mrefu baadaye, nilielewa kwamba nilikuwa nimehudhuria kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. Pia, nilizoea kwenda na wazazi wangu kwenye jumba dogo jijini Eindhoven. Sikuona ubaya wowote kwenda huko kwa maana wote walinitendea kwa fadhili na watu wa familia yetu walionekana kuwa na furaha. Lakini sikuelewa ni kwa nini tulikwenda huko kwa ukawaida. Sasa ninajua kwamba jumba lile dogo lilikuwa Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova.

Jambo la kusikitisha ni kwamba, hakukuwa na mtu yeyote aliyeweza kunifasiria habari zilizozungumziwa kwenye mikutano hiyo. Sasa ninajua kwamba wale waliohudhuria mikutano hiyo walitaka kunisaidia lakini hawakujua jinsi ya kuwasiliana nami. Nilipokuwa kwenye mikutano hiyo nilihisi upweke na niliwaza, ‘Laiti ningekuwa shuleni wala si hapa.’ Lakini mara nilipoanza kuwaza hivyo, wasichana wawili waliandika habari fulani kwenye kikaratasi, wakanipa. Hiyo ilikuwa ile barua niliyotaja awali. Sikujua kwamba barua hiyo fupi ilikuwa mwanzo wa urafiki wa karibu ambao ungeondoa upweke wangu.

Kukuza Urafiki wa Karibu

Colette na Hermine, walionipa barua hiyo, walikuwa na umri wa miaka 20 hivi. Baadaye nilijua kwamba walikuwa mapainia wa kawaida, yaani wahubiri wa wakati wote, na walikuwa wamekuja kutumikia katika kutaniko letu la Mashahidi wa Yehova. Ijapokuwa Colette na Hermine hawakujua lugha ya ishara, nilifaulu kusoma midomo yao walipoongea nami, na kwa njia hiyo tuliweza kuwasiliana vizuri.

Wazazi wangu walifurahi Colette na Hermine walipowaomba ruhusa kujifunza Biblia pamoja nami. Lakini wasichana hao walifanya mengi zaidi. Walijitahidi pia kunifasiria habari zilizozungumziwa kwenye mikutano katika Jumba la Ufalme na walinisaidia kushirikiana na wengine kutanikoni. Tulifanya mazoezi ili niweze kutumia Biblia vizuri katika kazi ya kuhubiri, na walinisaidia pia kutayarisha hotuba za Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Wazia, nilikuwa na ujasiri wa kutosha kutoa hotuba mbele ya kundi la watu wasio viziwi!

Isitoshe, nilihisi kwamba niliweza kuwategemea Colette na Hermine. Walikuwa wenye subira na walinisikiliza. Ijapokuwa tulicheka mara nyingi kwa sababu ya makosa niliyofanya, hawakunifanyia mzaha kamwe; wala hawakuona aibu kushirikiana nami. Walijitahidi kuelewa hisia zangu na hawakunipuuza. Wasichana hao wenye fadhili walinipa zawadi nzuri sana, upendo na urafiki wao.

Jambo muhimu zaidi ni kwamba Colette na Hermine walinisaidia kujua kwamba Mungu wetu, Yehova, ni rafiki anayetegemeka. Walinieleza kwamba Yehova alikuwa ameniona nikiketi katika Jumba la Ufalme na kwamba anajua matatizo ambayo kiziwi hukabili maishani. Ninashukuru sana kwamba upendo wetu kwa Yehova ulitufanya sisi watatu tuwe marafiki. Nilivutiwa kuona kwamba Yehova ananijali, na nilisukumwa na upendo kwake kujiweka wakfu, na nikabatizwa katika maji Julai 1975.

Kuambatana na Rafiki wa Pekee

Katika miaka iliyofuata nilikuja kuwajua ndugu na dada Wakristo wengi. Ndugu mmoja akawa rafiki yangu wa pekee, nasi tukaoana mwaka wa 1980. Muda mfupi baadaye nilianza kutumikia kama painia, na mwaka wa 1994 mimi na mume wangu Harry tulitumwa kama mapainia wa pekee kuwahubiria watu wanaotumia Lugha ya Ishara ya Uholanzi. Mwaka uliofuata nilipata pendeleo gumu la kuambatana na mume wangu, asiye kiziwi, alipotembelea makutaniko mbalimbali akiwa mwangalizi wa mzunguko wa badala.

Mimi hufanya hivi: Tunapotembelea kutaniko fulani kwa mara ya kwanza, mara moja mimi huwaendea ndugu na dada wengi iwezekanavyo na kujitambulisha. Mimi huwaambia kwamba mimi ni kiziwi na kuwaomba waangalie uso wangu wanapoongea nami na kwamba waongee polepole. Ninajitahidi pia kutoa maelezo mara moja kwenye mikutano ya kutaniko. Pia mimi humwomba mtu mmoja awe mfasiri wangu kwenye mikutano na katika kazi ya kuhubiri kwa muda wa juma lile.

Njia hiyo ina matokeo mazuri sana hivi kwamba mara kwa mara ndugu na dada husahau kwamba mimi siwezi kusikia. Nyakati nyingine jambo hilo husababisha kicheko. Kwa mfano, wanaponiona mjini, wao hupiga honi ya gari lao ili kunisalimu, lakini mimi siitikii, kwani siwezi kuwasikia. Mimi pia husahau hali yangu. Kwa mfano, ninapotaka kumnong’onezea mume wangu jambo la siri, naye anaaibika kwa ghafula, ninatambua kwamba nilisema kwa sauti kubwa.

Watoto husaidia kwa njia zisizotazamiwa. Katika kutaniko moja tulilotembelea kwa mara ya kwanza, mvulana mmoja mwenye umri wa miaka tisa alitambua kwamba wengine katika Jumba la Ufalme walisitasita kuongea nami, naye akaamua kurekebisha hali hiyo. Alinijia, akanishika mkono na kuniongoza hadi katikati ya Jumba la Ufalme, kisha akasema kwa sauti kubwa kabisa, “Ninataka mmjue Irene, yeye ni kiziwi!” Wale waliokuwapo wakanijia na kujitambulisha.

Ninapoambatana na mume wangu katika kazi ya kutembelea makutaniko, ninaendelea kupata marafiki wengi. Maisha yangu leo ni tofauti sana na wakati nilipokuwa mpweke bila marafiki. Tangu jioni ile ambapo Colette na Hermine waliponipatia ile barua fupi nimejionea jinsi urafiki ulivyo na faida na nimewajua watu ambao ni marafiki wangu wa karibu sasa. Zaidi ya yote, nimemjua Yehova ambaye ni Rafiki bora kuliko wote. (Waroma 8:38, 39) Barua ile fupi ilibadili maisha yangu kwelikweli!

[Picha katika ukurasa wa 24]

Ninakumbuka sauti ya mwanasesere wangu aliyepiga ngoma zake

[Picha katika ukurasa wa 25]

Katika kazi ya kuhubiri na nikiwa pamoja na mume wangu, Harry