Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Fulizeni Kulinda”!

“Fulizeni Kulinda”!

“Fulizeni Kulinda”!

“Lile niwaambialo nyinyi nawaambia wote, Fulizeni kulinda.”—MARKO 13:37.

1, 2. (a) Mtu mmoja alijifunza nini kuhusu kulinda mali zake? (b) Kielezi cha Yesu kuhusu mwizi kinatufunza nini kuhusu kukaa macho?

JUAN aliweka vitu vyake vyenye thamani nyumbani. Aliviweka mahali alipodhani ni salama zaidi, yaani, mvunguni mwa kitanda chake. Hata hivyo, usiku mmoja alipokuwa amelala usingizi pamoja na mke wake, mwizi aliingia kwenye chumba cha kulala. Ni wazi kwamba mwizi huyo alijua kabisa mahali ambapo angepata kutafuta vitu hivyo. Alichukua kila kitu chenye thamani kutoka mvunguni mwa kitanda pamoja na pesa ambazo Juan alikuwa ameziweka kwenye droo ya meza iliyokuwa kando ya kitanda. Aligundua asubuhi iliyofuata kwamba pesa na vitu vyake vyenye thamani vimeibwa. Atakumbuka kwa muda mrefu jambo lenye kuhuzunisha alilojifunza: Mtu ambaye amelala usingizi hawezi kulinda mali zake.

2 Ndivyo ilivyo katika maana ya kiroho. Hatuwezi kulinda tumaini na imani yetu iwapo tumelala. Kwa hiyo, Paulo anatuhimiza hivi: “Acheni tusiendelee kulala usingizi kama wengine, bali acheni tukae macho na kutunza hisi zetu.” (1 Wathesalonike 5:6) Ili kuonyesha umuhimu wa kukaa macho, Yesu alitumia kielezi cha mwizi. Alitaja matukio ambayo yangetangulia kuja kwake akiwa Hakimu, kisha akaonya hivi: “Kwa hiyo, fulizeni kulinda kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu anakuja. Lakini jueni jambo moja, kwamba ikiwa mwenye nyumba angalijua ni katika lindo gani mwizi anakuja, angalifuliza kuwa macho na hangaliruhusu nyumba yake ivunjwe na kuingiwa. Kwa sababu hiyo nyinyi pia jithibitisheni wenyewe kuwa tayari, kwa sababu kwenye saa msiyoifikiri kuwa hiyo, Mwana wa binadamu anakuja.” (Mathayo 24:42-44) Mwizi hasemi wakati atakapokuja. Yeye angependa kuja wakati asipotarajiwa. Vivyo hivyo, kama Yesu alivyosema, mwisho wa mfumo huu utakuja kwenye ‘saa tusiyoifikiri kuwa hiyo.’

“Kaeni Macho, Simameni Imara Katika Imani”

3. Yesu alionyeshaje umuhimu wa kukaa macho kwa kutumia kielezi cha watumwa wanaomsubiri bwana wao arudi kutoka kwenye arusi?

3 Katika maneno ya Injili ya Luka, Yesu aliwafananisha Wakristo na watumwa wanaomsubiri bwana wao arudi kutoka kwenye arusi. Wanahitaji kuwa chonjo ili ajapo wawe macho, tayari kumpokea. Kwa njia hiyohiyo, Yesu alisema: “Kwenye saa msiyofikiri yaelekea kuwa, Mwana wa binadamu anakuja.” (Luka 12:40) Huenda wengine ambao wamemtumikia Yehova kwa miaka mingi wakakosa kutambua umuhimu wa nyakati tunamoishi. Huenda hata wakakata kauli kwamba mwisho uko mbali sana. Lakini kufikiri kwa njia hiyo kunaweza kufanya tupuuze mambo ya kiroho na kuzingatia miradi ya kimwili, mambo yanayoweza kutufanya tusinzie kiroho.—Luka 8:14; 21:34, 35.

4. Ni nini kitakachotusadikisha na kutuchochea tuendelee kulinda, na Yesu alionyeshaje jambo hilo?

4 Kielezi cha Yesu kinaweza kutufunza jambo jingine. Ijapokuwa watumwa hao hawakujua saa ambayo bwana wao angewasili, yaonekana walijua usiku ambao angewasili. Haingekuwa rahisi kukaa macho usiku kucha ikiwa wangefahamu kwamba bwana wao hangewasili usiku huo. Lakini sivyo, walijua usiku ambao angewasili, na jambo hilo likawachochea kukaa macho. Kwa njia kama hiyo, unabii wa Biblia huonyesha waziwazi kwamba tunaishi wakati wa mwisho; lakini hautuambii siku au saa ya mwisho. (Mathayo 24:36) Tukiamini kwamba mwisho unakuja tutakaa macho, lakini tukiwa na uhakika kwamba siku ya Yehova imekaribia kweli, tutachochewa hata zaidi kuendelea kulinda.—Sefania 1:14.

5. Tunaweza kuitikiaje himizo la Paulo la ‘kukaa macho’?

5 Paulo aliwaandikia Wakorintho na kuwahimiza hivi: “Kaeni macho, simameni imara katika imani.” (1 Wakorintho 16:13) Naam, kukaa macho kunahusiana na kuwa na msimamo imara katika imani ya Kikristo. Tunawezaje kukaa macho? Kwa kujifunza Neno la Mungu kwa kina zaidi. (2 Timotheo 3:14, 15) Mazoea mazuri ya kujifunza na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida hutusaidia kuimarisha imani yetu na kuiweka akilini siku ya Yehova na hilo ni jambo muhimu kuhusiana na imani yetu. Tukisoma mara kwa mara uthibitisho wa kimaandiko kwamba mfumo huu unakaribia kwisha, hatutasahau kweli muhimu kuhusu mwisho huo. * Pia ni vizuri kufikiria matukio ya ulimwengu yanayotimiza unabii wa Biblia. Ndugu mmoja nchini Ujerumani aliandika hivi: “Kila wakati ninapotazama habari—vita, matetemeko ya ardhi, jeuri, na kuchafuliwa kwa sayari yetu—mambo hayo hukazia kwamba mwisho umekaribia.”

6. Yesu alionyeshaje kwamba tunaweza kushindwa kuendelea kukaa macho kiroho kadiri muda unavyosonga?

6 Katika Marko sura ya 13, tunaona simulizi lingine la Yesu akiwasihi wafuasi wake wakae macho. Kulingana na sura hiyo, Yesu analinganisha hali yao na ya mtunza-mlango anayesubiri bwana wake arudi kutoka safari ya ng’ambo. Mtunza-mlango hakujua saa ambayo bwana wake angerudi. Alipaswa kufuliza kulinda. Yesu alitaja malindo manne ambayo bwana angeweza kuwasili. Lindo la nne lilianza mwendo wa saa tisa za usiku hadi jua linapochomoza. Kwenye lindo hilo la nne, ni rahisi mtunza-mlango aanze kusinzia. Inasemekana kwamba, askari wanaona kuwa wakati unaofaa kumkamata adui ni kabla ya mapambazuko. Vivyo hivyo, wakati huu wa mwisho, ambapo ulimwengu umelala kabisa kiroho, huenda ikatubidi tujitahidi hata zaidi kukaa macho. (Waroma 13:11, 12) Kwa hiyo, katika kielezi chake, Yesu anatusihi hivi mara kadhaa: “Fulizeni kutazama, fulizeni kuwa macho . . . Kwa hiyo fulizeni kulinda . . . Lile niwaambialo nyinyi nawaambia wote, Fulizeni kulinda.”—Marko 13:32-37.

7. Tunakabili hatari gani, na kwa kufikiria hatari hiyo, tunapata kitia-moyo gani mara kwa mara tunaposoma Biblia?

7 Katika huduma yake, na baada ya kufufuliwa, mara nyingi Yesu alikazia umuhimu wa kukaa macho. Kwa kweli, karibu kila mara Maandiko yanapotaja mwisho wa mfumo huu wa mambo, tunaona onyo la kukaa macho au kufuliza kulinda. * (Luka 12:38, 40; Ufunuo 3:2; 16:14-16) Ni wazi kwamba, kuna hatari kubwa ya kusinzia kiroho. Sisi sote tunahitaji maonyo hayo!—1 Wakorintho 10:12; 1 Wathesalonike 5:2, 6.

Mitume Watatu Walioshindwa Kukaa Macho

8. Katika bustani ya Gethsemane, mitume watatu wa Yesu waliitikiaje ombi lake kwamba wafulize kulinda?

8 Kukaa macho kunahitaji mengi zaidi ya kuwa na nia njema, kama vile kielelezo cha Petro, Yakobo, na Yohana kinavyoonyesha. Wanaume hao watatu walikuwa watu wa kiroho waliomfuata Yesu kwa uaminifu na waliompenda sana. Hata hivyo, usiku wa Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., walishindwa kukaa macho. Walipoondoka kwenye chumba cha juu ambapo walikuwa wakisherehekea Sikukuu ya Kupitwa, mitume hao watatu waliambatana na Yesu hadi kwenye bustani ya Gethsemane. Wakiwa huko, Yesu aliwaambia hivi: “Nafsi yangu ina kihoro sana, hata kufikia kifo. Kaeni hapa na kufuliza kulinda pamoja nami.” (Mathayo 26:38) Yesu alisali kwa bidii mara tatu kwa Baba yake wa mbinguni, naye alirudi mara tatu mahali rafiki zake walipokuwa na kukuta wamelala.—Mathayo 26:40, 43, 45.

9. Yaelekea ni nini kilichofanya mitume wasinzie?

9 Kwa nini wanaume hao wenye imani walimkatisha Yesu tamaa usiku huo? Walikuwa wamechoka. Ilikuwa usiku sana, labda baada ya saa sita usiku, na “macho yao yalikuwa mazito” kwa usingizi. (Mathayo 26:43) Hata hivyo, Yesu alisema: “Fulizeni kulinda na kusali kwa kuendelea, ili msipate kuingia ndani ya jaribu. Bila shaka, roho ni yenye hamu, lakini mwili ni dhaifu.”—Mathayo 26:41.

10, 11. (a) Licha ya uchovu, ni nini kilichomsaidia Yesu kufuliza kulinda katika bustani ya Gethsemane? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na jambo lililowapata mitume watatu Yesu alipowaomba wafulize kulinda?

10 Bila shaka, Yesu pia alikuwa amechoka usiku huo muhimu. Hata hivyo, badala ya kulala, Yesu alitumia wakati huo muhimu wa mwisho akiwa huru kusali kwa bidii. Siku chache zilizotangulia, alikuwa amewahimiza wafuasi wake wasali hivi: “Basi, fulizeni kuwa macho wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.” (Luka 21:36; Waefeso 6:18) Tukitii onyo la Yesu na kuiga kielelezo chake kizuri kuhusiana na sala, sala zetu za kutoka moyoni tunazomtolea Yehova zitatusaidia kukaa macho kiroho.

11 Bila shaka, Yesu alielewa—ingawa wakati huo wafuasi wake hawakuelewa jambo hilo—kwamba baada ya muda mfupi angekamatwa na kuuawa. Angejaribiwa na hatimaye kufa kifo chenye maumivu makali kwenye mti wa mateso. Yesu alikuwa amewaonya mitume wake kuhusu mambo hayo, lakini hawakuelewa. Kwa hiyo, walilala alipokuwa macho akisali. (Marko 14:27-31; Luka 22:15-18) Kama vile mitume, mwili wetu pia ni dhaifu na kuna mambo ambayo bado hatuyajui. Hata hivyo, tusipotambua kwamba tunaishi nyakati muhimu, tunaweza kulala usingizi wa kiroho. Tunaweza kukaa macho tu kwa kuwa chonjo.

Sifa Tatu Muhimu

12. Ni sifa gani tatu ambazo Paulo anahusianisha na kutunza hisi zetu?

12 Tunawezaje kutambua umuhimu wa nyakati tunamoishi? Tayari tumeona umuhimu wa sala na uhitaji wa kuweka akilini siku ya Yehova. Kwa kuongezea, Paulo anataja sifa tatu muhimu tunazopaswa kusitawisha. Anasema: “Kwa habari yetu sisi tulio wa mchana, acheni tutunze hisi zetu na kuwa tumevaa bamba la kifuani la imani na upendo na kama kofia ya chuma lile tumaini la wokovu.” (1 Wathesalonike 5:8) Na tuchunguze kifupi jinsi ambavyo imani, tumaini, na upendo hutusaidia kuendelea kukaa macho kiroho.

13. Imani hutusaidiaje tuendelee kukaa chonjo?

13 Lazima tuwe na imani isiyotikisika kwamba Yehova yuko na kwamba “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Kutimizwa kwa mara ya kwanza kwa unabii wa Yesu unaohusu mwisho katika karne ya kwanza kunaimarisha imani yetu kwamba unabii huo utatimizwa kwa kiwango kikubwa wakati wetu. Nayo imani yetu hufanya tutazamie kwa hamu siku ya Yehova, tukiwa na uhakika kwamba “[njozi ya kiunabii] haina budi kuja, haitakawia.”—Habakuki 2:3.

14. Kuwa na tumaini kunawezaje kutusaidia sana kukaa macho?

14 Tumaini letu ni kama “nanga ya nafsi” ambayo hutusaidia tuvumilie magumu hata kama itatubidi kungojea kutimizwa kwa ahadi hakika za Mungu. (Waebrania 6:18, 19) Margaret, dada aliyetiwa mafuta kwa roho ambaye ana umri wa miaka 90 na kitu na ambaye alibatizwa miaka 70 iliyopita, asema hivi: “Mume wangu alipokuwa mahututi kwa ugonjwa wa kansa mwaka wa 1963, nilitamani mwisho ufike upesi. Lakini sasa ninaona kwamba nilikuwa nikijifikiria tu. Wakati huo hatukujua kazi ingeenea hadi sehemu gani za dunia. Hata sasa, kuna maeneo mengi ambapo kazi imeanza kufanywa hivi karibuni tu. Kwa hiyo ninafurahi kwamba Yehova ameonyesha subira.” Mtume Paulo anatuhakikishia hivi: “Uvumilivu, [hutokeza] hali yenye kukubaliwa; nayo hali yenye kukubaliwa, tumaini, nalo tumaini haliongozi kwenye kukata tamaa.”—Waroma 5:3-5.

15. Upendo utatuchocheaje hata ikionekana kana kwamba tumengoja kwa muda mrefu?

15 Upendo wa Kikristo ni sifa ya pekee kwa sababu ndiyo msingi wa mambo yote tunayofanya. Tunamtumikia Yehova kwa sababu tunampenda, si kwa kufikiria tu ratiba yake. Upendo kwa jirani hutuchochea tuhubiri habari njema ya Ufalme, hata kama Mungu atataka tufanye hivyo muda mrefu kadiri gani au turudi kwa nyumba zilezile mara ngapi. Kama Paulo alivyoandika, “kwabaki imani, tumaini, upendo, matatu haya; lakini lililo kubwa zaidi sana kati ya haya ni upendo.” (1 Wakorintho 13:13) Upendo hutusaidia kuvumilia na kukaa macho. “[Upendo] hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.”—1 Wakorintho 13:7, 8.

“Fuliza Kushika Sana Lile Ulilo Nalo”

16. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani badala ya kupunguza bidii?

16 Tunaishi nyakati muhimu ambapo matukio ya ulimwengu hutukumbusha daima kwamba tuko kwenye umalizio wa siku za mwisho. (2 Timotheo 3:1-5) Sasa si wakati wa kupunguza bidii yetu bali ‘kufuliza kushika sana lile tulilo nalo.’ (Ufunuo 3:11) Kwa “kukesha katika sala” na kusitawisha imani, tumaini, na upendo, tutakuwa tayari kuvumilia majaribu. (1 Petro 4:7) Tuna mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana. Kwa kujihusisha na matendo ya ujitoaji-kimungu tutakuwa macho kabisa.—2 Petro 3:11.

17. (a) Kwa nini hatupaswi kuvunjika moyo tunapotamauka mara kwa mara? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 21.) (b) Tunawezaje kumwiga Yehova, na wale wanaomwiga watapata baraka gani?

17 Yeremia aliandika, “BWANA ndiye fungu langu, kwa hiyo nitamtumaini yeye. BWANA ni mwema kwa hao wamngojeao, kwa hiyo nafsi imtafutayo. Ni vema mtu autarajie wokovu wa BWANA.” (Maombolezo 3:24-26) Baadhi yetu tumengoja kwa muda mfupi tu. Wengine wamengoja kwa miaka mingi kuona wokovu wa Yehova. Hata hivyo, muda huo wa kungoja ni mfupi kama nini unapolinganishwa na umilele! (2 Wakorintho 4:16-18) Na tunapongoja wakati wa Yehova unaofaa, tunaweza kusitawisha sifa muhimu za Kikristo na kuwasaidia wengine wanufaike na subira ya Yehova na kukubali kweli. Kwa hiyo, sote na tufulize kulinda. Na tumwige Yehova kwa kuwa wenye subira, na kushukuru kwa tumaini ambalo ametupatia. Na tuendeleapo kwa uaminifu kukaa macho, na tushike kabisa tumaini la uhai udumuo milele. Kisha, ahadi hizi za kiunabii zitatimia kwetu: “[Yehova] atakutukuza uirithi nchi, wasio haki watakapoharibiwa utawaona.”—Zaburi 37:34.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Huenda ikafaa kupitia mambo sita yanayothibitisha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” ambayo yameonyeshwa kwenye gazeti Mnara wa Mlinzi, Januari 15, 2000 ukurasa wa 12-13.—2 Timotheo 3:1.

^ fu. 7 Akizungumzia kitenzi cha Kigiriki kilichotafsiriwa “kaa macho,” mtaalamu wa kuandika kamusi W. E. Vine asema kwamba kitenzi hicho kihalisi kinamaanisha ‘kuondoa usingizi,’ na pia ‘kinakazia jinsi ambavyo watu wanaokusudia kufanya jambo fulani hukaa macho na kulinda.’

Ungejibuje?

• Tunawezaje kuimarisha uhakika wetu kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo u karibu?

• Kielelezo cha Petro, Yakobo, na Yohana kinaonyesha nini?

• Ni sifa gani tatu zitakazotusaidia tuendelee kuwa chonjo kiroho?

• Kwa nini huu ndio wakati wa ‘kufuliza kushika sana lile tulilo nalo’?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

“Heri Angojaye.”—Danieli 12:12

Ebu wazia kwamba mlinzi anashuku kwamba mwizi anapanga kuiba katika jengo analolinda. Usiku unapowadia, mlinzi anasikiliza kwa makini kelele yoyote inayoweza kutambulisha mwizi. Anajitahidi kutumia masikio na macho yake kwa kadiri awezavyo. Unaweza kuelewa jinsi anavyoweza kudanganywa kwa urahisi na kelele ya miti inayosababishwa na upepo unaovuma au paka ambaye amegonga kitu fulani.—Luka 12:39, 40.

Jambo kama hilo linaweza kuwapata wale ambao ‘wanangoja kwa hamu ufunuo wa Bwana wetu Yesu Kristo.’ (1 Wakorintho 1:7) Mitume walifikiri kwamba Yesu ‘angerudishia Israeli ufalme’ mara tu baada ya kufufuliwa. (Matendo 1:6) Miaka kadhaa baadaye, Wakristo huko Thesalonike walikumbushwa kwamba kuwapo kwa Yesu kungetukia wakati ujao. (2 Wathesalonike 2:3, 8) Hata hivyo, wafuasi hao wa mapema wa Yesu hawakuiacha njia iongozayo kwenye uzima kwa sababu matumaini yao hayakutimizwa kuhusu siku ya Yehova. —Mathayo 7:13.

Katika siku zetu, hatupaswi kulegeza bidii yetu kwa kukata tamaa kwamba mwisho wa mfumo wa mambo unakawia. Huenda mlinzi aliye chonjo akadanganywa na kelele, hata hivyo lazima afulize kulinda! Hiyo ndiyo kazi yake. Wakristo wanapaswa kufanya hivyo.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, una uhakika kwamba siku ya Yehova imekaribia?

[Picha katika ukurasa wa 19]

Mikutano, sala, na mazoea mazuri ya kujifunza hutusaidia tufulize kulinda

[Picha katika ukurasa wa 22]

Kama Margaret, na tuwe na subira na kufuliza kulinda