Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Huu Ndio Wakati Muhimu Zaidi wa Kukaa Macho!

Huu Ndio Wakati Muhimu Zaidi wa Kukaa Macho!

Huu Ndio Wakati Muhimu Zaidi wa Kukaa Macho!

“Acheni tusiendelee kulala usingizi kama wengine, bali acheni tukae macho na kutunza hisi zetu.”—1 WATHESALONIKE 5:6.

1, 2. (a) Pompeii na Herculaneum yalikuwa majiji ya aina gani? (b) Wakazi wa jiji la Pompeii na Herculaneum walipuuza onyo gani, nao wakapatwa na nini?

KATIKA karne ya kwanza Wakati wa Kawaida, kulikuweko majiji mawili ya Roma yenye ufanisi yaliyoitwa Pompeii na Herculaneum yaliyokuwa karibu na Mlima Vesuvius. Matajiri wa Roma walipenda kwenda likizo kwenye majiji hayo. Viwanja vya maonyesho vya majiji hayo vilitoshea watu zaidi ya elfu moja, na katika jiji la Pompeii kulikuwa na uwanja mkubwa sana ambao ungeweza kutoshea karibu watu wote wa mji huo. Watu wanaochimbua vitu vya kale walipata baa 118 zilizokuwa katika jiji la Pompeii. Baadhi ya baa hizo zilitumiwa kuchezea kamari au kufanyia ukahaba. Ukosefu wa maadili na ufuatiaji wa vitu vya kimwili ulienea sana, kama inavyoonyeshwa na michoro ya ukutani na vitu vya kale.

2 Siku ya Agosti 24, 79 W.K., Mlima Vesuvius ulianza kulipuka. Wataalamu wa volkeno wanaamini kwamba mlipuko wa kwanza uliorusha jivu na mawe ya volkeno kwenye majiji hayo mawili, labda usingaliwazuia wakazi kutoroka. Kwa kweli, yaonekana wengi walitoroka. Hata hivyo, wengine hawakuchukua kwa uzito hatari hiyo, au walipuuza tu dalili za onyo na wakaamua kubaki katika majiji hayo. Kisha, mwendo wa saa sita usiku, maporomoko ya gesi moto sana na mawe ya volkeno yalifunika jiji la Herculaneum, na kuangamiza wakazi wote waliosalia jijini humo. Asubuhi na mapema siku iliyofuata, maporomoko kama hayo yaliua wakazi wote waliokuwa katika jiji la Pompeii. Walipatwa na msiba ulioje kwa sababu ya kupuuza dalili za onyo!

Mwisho wa Mfumo wa Mambo wa Kiyahudi

3. Uharibifu wa Yerusalemu unafananaje na wa majiji ya Pompeii na Herculaneum?

3 Uharibifu wenye kuogopesha wa jiji la Pompeii na Herculaneum haukuwa mkubwa kama ule wa Yerusalemu uliotukia miaka tisa mapema, na ambao ulisababishwa na watu. Uharibifu huo unaotajwa kuwa “mazingiwa mabaya zaidi katika historia,” ulisababisha vifo vya Wayahudi zaidi ya milioni moja. Hata hivyo, msiba uliopata jiji la Pompeii na Herculaneum ulitanguliwa na onyo na ndivyo na uharibifu uliopata jiji la Yerusalemu.

4. Yesu alitoa ishara gani ya unabii ili kuonya wafuasi wake kwamba mwisho wa mfumo wa mambo ulikuwa umekaribia, na ishara hiyo ilitimizwaje mara ya kwanza katika karne ya kwanza?

4 Yesu Kristo alikuwa ametabiri kwamba jiji hilo lingeharibiwa na kutaja matukio ambayo yangetangulia uharibifu huo—mambo ya kuogopesha kama vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya ardhi, na uvunjaji wa sheria. Kungekuwa na manabii wasio wa kweli, lakini habari njema ya Ufalme wa Mungu ingehubiriwa ulimwenguni pote. (Mathayo 24:4-7, 11-14) Ingawa maneno ya Yesu yanatimizwa kwa kiwango kikubwa leo, yalitimizwa kwa kiwango kidogo wakati huo. Historia inaonyesha kwamba kulikuwa na njaa kali huko Yudea. (Matendo 11:28) Mwanahistoria Myahudi Josephus anaripoti kwamba kulikuwa na tetemeko la ardhi huko Yerusalemu kabla tu ya jiji hilo kuharibiwa. Uharibifu wa Yerusalemu ulipokaribia, mara nyingi kulikuwa na maasi yasiyokoma, vita ya wenyewe kwa wenyewe kati ya vikundi vya kisiasa vya Wayahudi, na mauaji katika majiji kadhaa ambayo wakazi wake walikuwa Wayahudi na watu wasio Wayahudi. Licha ya hayo, habari njema ya Ufalme ilikuwa ikihubiriwa “katika viumbe vyote chini ya mbingu.”—Wakolosai 1:23.

5, 6. (a) Ni unabii gani wa Yesu uliotimizwa mwaka wa 66 W.K.? (b) Kwa nini watu wengi sana walikufa Yerusalemu lilipoharibiwa mwaka wa 70 W.K.?

5 Hatimaye, mnamo mwaka wa 66 W.K., Wayahudi waliasi dhidi ya Roma. Wakati Cestius Gallus alipoongoza majeshi yake yazingire Yerusalemu, wafuasi wa Yesu walikumbuka maneno haya ya Yesu: “Wakati mwonapo Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwalo kumekaribia. Ndipo waacheni wale walio katika Yudea waanze kukimbia hadi kwenye milima, na waacheni wale walio katikati yalo waondoke, na waacheni wale walio katika sehemu za mashambani wasiingie ndani yalo.” (Luka 21:20, 21) Wakati wa kuondoka Yerusalemu ulikuwa umefika. Lakini wangeondokaje? Gallus na majeshi yake yaliondoka kwa ghafula, hivyo Wakristo huko Yerusalemu na Yudea wakapata fursa ya kutii maneno ya Yesu na kukimbilia milimani.—Mathayo 24:15, 16.

6 Miaka minne baadaye, yapata wakati wa Sikukuu ya Kupitwa, jeshi la Roma lilirudi likiongozwa na Jenerali Titus, aliyekuwa ameazimia kukomesha kabisa uasi wa Wayahudi. Majeshi yake yalizingira Yerusalemu na kujenga “boma lenye miti iliyochongoka,” na hivyo kuzuia mtu yeyote asiweze kutoroka. (Luka 19:43, 44) Licha ya tisho la vita, Wayahudi kutoka Milki yote ya Roma walikuwa wamekuja Yerusalemu kwa ajili ya Sikukuu ya Kupitwa. Sasa wakawa wamenaswa. Kulingana na Josephus, idadi kubwa ya waliokufa wakati Roma lilipozingirwa ni wageni hao wa kusikitikiwa. * Wakati Yerusalemu lilipoharibiwa, karibu Myahudi mmoja kati ya kila Wayahudi saba alikufa katika Milki ya Roma. Kuharibiwa kwa Yerusalemu na hekalu lake kulimaanisha kukomeshwa kwa taifa la Kiyahudi na mfumo wake wa kidini uliotegemea Sheria ya Musa. *Marko 13:1, 2.

7. Kwa nini Wakristo waaminifu waliokoka uharibifu wa Yerusalemu?

7 Mnamo mwaka wa 70 W.K., Wakristo Wayahudi wangaliuawa au kupelekwa utumwani pamoja na watu wote waliokuwa Yerusalemu. Hata hivyo, historia inathibitisha kwamba walitii onyo la Yesu lililokuwa limetolewa miaka 37 mapema. Walikuwa wameondoka jijini na hawakuwa wamerudi.

Maonyo ya Mitume ya Wakati Unaofaa

8. Petro alitambua uhitaji gani, na yaelekea alikumbuka maneno gani ya Yesu?

8 Leo, uharibifu mkubwa sana unakaribia, yaani, kuharibiwa kwa mfumo wote wa mambo. Miaka sita kabla Yerusalemu halijaharibiwa, mtume Petro alitoa shauri muhimu na la wakati unaofaa ambalo linahusu hasa Wakristo wa leo: Kaeni chonjo! Petro aliona kwamba Wakristo wanahitaji kuchochea ‘uwezo wao mwangavu wa kufikiri’ ili wasipuuze “amri ya Bwana,” Yesu Kristo. (2 Petro 3:1, 2) Akiwahimiza Wakristo wawe chonjo, yaelekea Petro alikumbuka maneno ambayo Yesu aliwaambia mitume Wake siku chache kabla hajafa: “Fulizeni kutazama, fulizeni kuwa macho, kwa maana hamjui ni lini ulio wakati uliowekwa rasmi.”—Marko 13:33.

9. (a) Watu fulani wangesitawisha mtazamo gani hatari? (b) Kwa nini ni hatari hasa kuwa na shaka?

9 Leo, wengine husema hivi kwa dhihaka: “Kuko wapi kuwapo kwake huku kulikoahidiwa?” (2 Petro 3:3, 4) Bila shaka, watu hao huhisi kwamba mambo hayabadiliki hata kidogo bali yanaendelea kama kawaida tangu dunia iumbwe. Ni hatari kuwa na shaka kama hiyo. Shaka inaweza kufanya tusitambue umuhimu wa nyakati tunamoishi, na kutuchochea tuzingatie mno kutimiza tamaa za kimwili. (Luka 21:34) Mbali na hayo, Petro anasema kwamba wadhihaki hao wanasahau Furiko la siku za Noa lililoharibu mfumo wote wa mambo. Kwa kweli, mambo yalibadilika wakati huo!—Mwanzo 6:13, 17; 2 Petro 3:5, 6.

10. Petro anawatia moyo kwa maneno gani wale ambao huenda wakakosa subira?

10 Petro anawasaidia wasomaji wake wasitawishe subira kwa kuwakumbusha sababu ambayo mara nyingi hufanya Mungu asichukue hatua mara moja. Kwanza, Petro anasema: “Siku moja kwa Yehova ni kama miaka elfu na miaka elfu kama siku moja.” (2 Petro 3:8) Kwa kuwa Yehova huishi milele, anaweza kufikiria mambo yote yanayohusika na kuamua wakati unaofaa kabisa kuchukua hatua. Kisha, Petro anataja kwamba Yehova anatamani watu kila mahali watubu. Subira ya Mungu itafanya wengi waokoke ambao wangeangamia kama angechukua hatua haraka. (1 Timotheo 2:3, 4; 2 Petro 3:9) Hata hivyo, subira ya Yehova haimaanishi kwamba hatachukua hatua kamwe. “Siku ya Yehova itakuja kama mwizi,” asema Petro.—2 Petro 3:10.

11. Ni nini kitakachotusaidia tukae macho kiroho, na kufanya hivyo ‘kutaharakishaje’ kwa njia ya mfano siku ya Yehova?

11 Ulinganisho wa Petro unafaa. Si rahisi kuwakamata wezi, lakini mlinzi aliye macho usiku kucha anaweza kumwona mwizi kwa urahisi kuliko yule anayesinzia-sinzia. Mlinzi anawezaje kukaa macho? Ni rahisi mlinzi kuwa chonjo anapotembea-tembea kuliko anapoketi usiku kucha. Vivyo hivyo, kwa kuendelea kuwa na bidii katika mambo ya kiroho kutatusaidia kukaa macho tukiwa Wakristo. Kwa hiyo, Petro anatuhimiza tujishughulishe na “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.” (2 Petro 3:11) Utendaji huo utatusaidia tuendelee “kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “kuweka karibu akilini” linaweza kutafsiriwa kihalisi kuwa “kuharakisha.” (2 Petro 3:12) Ni kweli kwamba hatuwezi kubadili ratiba ya Yehova. Siku yake itakuja wakati wake barabara. Lakini tutaona kana kwamba wakati uliobaki unapita haraka iwapo tuna mengi ya kufanya katika utumishi wake.—1 Wakorintho 15:58.

12. Tunawezaje kunufaika na subira ya Yehova?

12 Kwa hiyo, mtu yeyote anayehisi kwamba siku ya Yehova inachelewa anatiwa moyo kutii shauri la Petro la kungojea kwa subira wakati uliowekwa wa Yehova. Kwa kweli, tunaweza kutumia kwa hekima wakati huu ambao Mungu ameruhusu kwa sababu ya subira yake. Kwa mfano, tunaweza kuendelea kusitawisha sifa muhimu za Kikristo na vilevile kuhubiri habari njema kwa watu wengi zaidi. Hatungeweza kufanya hivyo iwapo Yehova hangeonyesha subira. Tukikaa macho, Yehova atatupata tukiwa “bila doa na bila waa na katika amani” mwishoni mwa mfumo huu wa mambo. (2 Petro 3:14, 15) Hiyo itakuwa thawabu iliyoje!

13. Paulo aliwaandikia Wakristo wa Thesalonike maneno gani yanayofaa sana leo?

13 Pia Paulo anazungumzia uhitaji wa kukaa macho katika barua yake ya kwanza kwa Wakristo wa Thesalonike. Anashauri hivi: “Acheni tusiendelee kulala usingizi kama wengine, bali acheni tukae macho na kutunza hisi zetu.” (1 Wathesalonike 5:2, 6) Leo, ni muhimu sana kukaa macho kwa kuwa mwisho wa mfumo wote wa mambo unakaribia. Watumishi wa Yehova wanaishi katika ulimwengu usiojali mambo ya kiroho, na hilo linaweza kuwaathiri. Kwa hiyo, Paulo anashauri hivi: “Acheni tutunze hisi zetu na kuwa tumevaa bamba la kifuani la imani na upendo na kama kofia ya chuma lile tumaini la wokovu.” (1 Wathesalonike 5:8) Kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida na kushirikiana na ndugu zetu mikutanoni kutatusaidia kutii shauri la Paulo na kutambua umuhimu wa nyakati hizi.—Mathayo 16:1-3.

Mamilioni Wanafuliza Kulinda

14. Ni takwimu gani zinazoonyesha kwamba wengi leo wanatii shauri la Petro la kukaa macho?

14 Je, leo wengi wanatii shauri hilo lililoongozwa na roho ya Mungu la kukaa macho? Ndiyo. Katika mwaka wa utumishi wa 2002, kilele cha wahubiri 6,304,645—ongezeko la asilimia 3.1 kuliko mwaka wa 2001—walithibitisha kwamba walikuwa chonjo kiroho kwa kutumia saa 1,202,381,302 wakizungumza na watu kuhusu Ufalme wa Mungu. Wahubiri hao walifurahia kazi hiyo. Ilikuwa kazi muhimu maishani mwao. Mtazamo wa wengi wao ni kama ule wa Eduardo na Noemi wanaoishi nchini El Salvador.

15. Ni jambo gani lililoonwa linaloonyesha kwamba wengi wanaendelea kukaa chonjo kiroho nchini El Salvador?

15 Miaka kadhaa iliyopita, Eduardo na Noemi walizingatia maneno haya ya Paulo: “Mandhari ya ulimwengu huu inabadilika.” (1 Wakorintho 7:31) Walifanya maisha yao kuwa sahili na kuanza kazi ya upainia, yaani, utumishi wa wakati wote. Muda uliposonga walibarikiwa katika njia mbalimbali hata wakawa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya. Licha ya kupatwa na matatizo magumu, Eduardo na Noemi wanaamini kwamba walifanya uamuzi unaofaa walipoacha vitu vya kimwili na kuanza huduma ya wakati wote. Wengi wa wahubiri 29,269—kutia ndani mapainia 2,454—nchini El Salvador wameonyesha roho hiyo ya kujidhabihu. Kwa sababu hiyo, nchi hiyo ilikuwa na ongezeko la wahubiri la asilimia 2 mwaka jana.

16. Ndugu fulani mchanga alionyesha mtazamo gani nchini Côte d’Ivoire?

16 Nchini Côte d’Ivoire, Mkristo mchanga alionyesha mtazamo kama huo alipoandikia ofisi ya tawi hivi: “Mimi ni mtumishi wa huduma. Lakini siwezi kuwaambia akina ndugu wawe mapainia kwa sababu sijawawekea kielelezo kizuri. Kwa hiyo nimeacha kazi yenye mshahara mzuri na sasa nimejiajiri, na ninapata wakati zaidi wa kuhubiri.” Kijana huyo alikuwa miongoni mwa mapainia 983 wanaotumikia katika nchi ya Côte d’Ivoire, ambayo iliripoti wahubiri 6,701 mwaka jana, ongezeko la asilimia 5.

17. Shahidi mchanga nchini Ubelgiji alionyeshaje kwamba hakuogopeshwa na ubaguzi?

17 Hali ya kutovumiliana, upendeleo na ubaguzi unazidi kusababisha matatizo kwa wahubiri wa Ufalme 24,961 nchini Ubelgiji. Hata hivyo, wahubiri hao ni wenye bidii na hawana woga. Wakati Shahidi mwenye umri wa miaka 16 aliposikia Mashahidi wa Yehova wakiitwa madhehebu wakati wa somo la maadili shuleni, aliomba ruhusa ya kueleza maoni ya Mashahidi wa Yehova. Akitumia video Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name na broshua Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Akina Nani?, aliweza kueleza ukweli kuhusu Mashahidi. Wanafunzi walifurahia sana habari hiyo na juma lililofuata wanafunzi wakapewa mtihani ambao walipaswa kujibu maswali kuhusu dini ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova.

18. Kuna uthibitisho gani kwamba wahubiri nchini Argentina na Msumbiji hawakuacha kumtumikia Yehova kwa sababu ya magumu ya kiuchumi?

18 Wakristo wengi wanalazimika kukabili matatizo magumu katika siku hizi za mwisho. Hata hivyo, wanajitahidi wasiache utumishi wao. Licha ya magumu ya kiuchumi, Argentina iliripoti kilele kipya cha Mashahidi 126,709 mwaka jana. Bado kuna umaskini mwingi nchini Msumbiji. Hata hivyo, kulikuwa na ongezeko la asilimia 4 na wahubiri 37,563 walishiriki kazi ya kuhubiri. Maisha ni magumu kwa watu wengi nchini Albania, hata hivyo, nchi hiyo iliripoti ongezeko la asilimia 12, na kufikia kilele cha wahubiri 2,708. Ni wazi kwamba roho ya Yehova haizuiwi na hali ngumu wakati watumishi wake wanapotanguliza Ufalme.—Mathayo 6:33.

19. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba bado kuna watu wenye mfano wa kondoo ambao wanatamani kweli ya Biblia? (b) Ni mambo gani mengine katika ripoti ya kila mwaka yanayoonyesha kwamba watumishi wa Yehova wanaendelea kukaa macho kiroho? (Ona chati kwenye ukurasa wa 12-15.)

19 Wastani wa mafunzo ya Biblia 5,309,289 ulimwenguni pote yaliyoripotiwa mwaka jana unaonyesha kwamba bado kuna watu wengi wenye mfano wa kondoo wanaotamani kweli ya Biblia. Miongoni mwa kilele kipya cha watu 15,597,746 waliohudhuria Ukumbusho, wengi wao hawamtumikii Yehova. Na waendelee kuzidisha ujuzi na upendo kwa Yehova na kwa ndugu zao. Inafurahisha kuona kwamba “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” unaendelea kupata matokeo mazuri huku wakimtumikia Muumba “mchana na usiku katika hekalu lake” pamoja na ndugu zao waliotiwa mafuta kwa roho.—Ufunuo 7:9, 15; Yohana 10:16.

Tunayojifunza Kutoka kwa Loti

20. Mfano wa Loti na mke wake unatufunza nini?

20 Bila shaka, hata watumishi waaminifu wa Mungu wanaweza kusahau kwa muda umuhimu wa nyakati wanamoishi. Mfikirie Loti, mtoto wa ndugu ya Abrahamu. Alijulishwa na malaika wawili kwamba Mungu alikuwa karibu kuharibu Sodoma na Gomora. Loti hakushangazwa na habari hizo kwa sababu ‘alitaabishwa sana na kujitia mno kwa watu wanaokaidi sheria katika mwenendo mlegevu.’ (2 Petro 2:7) Hata hivyo, malaika wawili walipokuja kumtoa Sodoma, ‘alikawia-kawia.’ Karibu malaika wamkokote yeye na familia yake kutoka katika jiji hilo. Baadaye, mke wa Loti alipuuza onyo la malaika kwamba wasitazame nyuma. Alipoteza maisha yake kwa sababu ya mtazamo wake wa kutojali. (Mwanzo 19:14-17, 26) “Mkumbukeni mke wa Loti,” Yesu akaonya.—Luka 17:32.

21. Kwa nini huu ndio wakati muhimu zaidi wa kukaa macho?

21 Msiba uliopata jiji la Pompeii na Herculaneum, mambo yaliyotukia wakati Yerusalemu lilipoharibiwa, na vilevile wakati wa Furiko la Noa na siku za Loti yanaonyesha umuhimu wa kuchukua maonyo kwa uzito. Tukiwa watumishi wa Yehova, tunatambua ishara ya wakati wa mwisho. (Mathayo 24:3) Tumejitenga na dini isiyo ya kweli. (Ufunuo 18:4) Kama Wakristo wa karne ya kwanza, tunahitaji “kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” (2 Petro 3:12) Naam, huu ndio wakati muhimu zaidi wa kukaa macho! Tunaweza kuchukua hatua gani, na tunaweza kusitawisha sifa gani ili tukae macho? Makala inayofuata itazungumzia mambo hayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Haielekei kwamba Yerusalemu lilikuwa na wakazi zaidi ya 120,000 katika karne ya kwanza. Eusebius anakadiria kwamba wakazi 300,000 kutoka mkoa wa Yudea walisafiri hadi Yerusalemu kusherehekea Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 70 W.K. Bila shaka, wengine waliokufa walitoka sehemu nyingine za milki hiyo.

^ fu. 6 Bila shaka, kulingana na maoni ya Yehova, agano jipya lilichukua mahali pa Sheria ya Musa mwaka wa 33 W.K.—Waefeso 2:15.

Ungejibuje?

• Ni nini kilichowawezesha Wakristo Wayahudi kutoroka uharibifu wa Yerusalemu?

• Shauri linalopatikana katika maandishi ya mtume Petro na mtume Paulo hutusaidiaje kukaa macho?

• Ni nani leo walio macho kabisa?

• Tunajifunza nini kutokana na simulizi la Loti na mke wake?

[Maswali ya Funzo]

[Chati katika ukurasa wa 12-15]

2002 REPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE

(Ona buku lililojalidiwa)

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mnamo mwaka wa 66 W.K., Wakristo huko Yerusalemu walitii onyo la Yesu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kuwa na bidii katika mambo ya kiroho huwasaidia Wakristo wakae macho