Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Paulo alimaanisha nini aliposema hivi: “Mara nyingi kwa kadiri mlavyo mkate huu na kunywa kikombe hiki”?

Akizungumzia kuanzishwa kwa Ukumbusho wa kifo cha Yesu, Paulo aliandika hivi: “Mara nyingi kwa kadiri mlavyo mkate huu na kunywa kikombe hiki, mwafuliza kutangaza kifo cha Bwana, mpaka awasilipo.” (1 Wakorintho 11:25, 26) Wengine hufikiri kwamba neno “mara nyingi” katika andiko hilo humaanisha kwamba kifo cha Kristo kinapasa kuadhimishwa mara nyingi. Hivyo, wao huadhimisha kifo hicho zaidi ya mara moja kila mwaka. Je, Paulo alimaanisha hivyo?

Sasa miaka 2,000 hivi imepita tangu Yesu aanzishe Ukumbusho wa kifo chake. Kwa hiyo, Ukumbusho huo umesherehekewa mara nyingi tangu mwaka wa 33 W.K. hata kama umekuwa ukisherehekewa mara moja kila mwaka. Hata hivyo, kulingana na habari inayozunguka andiko la 1 Wakorintho 11:25, 26, Paulo hakuwa akizungumzia ni mara nyingi kadiri gani, bali jinsi gani Ukumbusho unapaswa kuadhimishwa. Katika Kigiriki cha awali, Paulo hakutumia neno pol·laʹkis, linalomaanisha “mara nyingi,” bali alitumia neno ho·saʹkis, linalomaanisha “mara nyingi kwa kadiri” mlavyo, usemi unaomaanisha “wakati wowote” mlapo au “kila mara” mlapo. Paulo alikuwa akimaanisha hivi: ‘Kila mara mnapofanya hivyo, mnaendelea kutangaza kifo cha Bwana.’ *

Basi, Ukumbusho wa kifo cha Yesu wapaswa kuadhimishwa mara nyingi kadiri gani? Inafaa kuadhimishwa mara moja kila mwaka. Kwa kweli huo ni ukumbusho, na kwa kawaida ukumbusho huadhimishwa mara moja tu kila mwaka. Zaidi ya hayo, Yesu alikufa wakati wa Sikukuu ya Kupitwa ya Wayahudi iliyoadhimishwa mara moja kila mwaka. Kwa kufaa, Paulo alimtaja Yesu kuwa “Kristo kafara wetu wa sikukuu ya kupitwa,” kwa kuwa kifo cha kidhabihu cha Yesu kiliwawezesha Waisraeli wa kiroho kupata uhai. Vivyo hivyo, dhabihu iliyotolewa wakati wa Sikukuu ya kwanza ya Kupitwa huko Misri iliokoa wazaliwa wa kwanza Waisraeli na kukomboa taifa hilo kutoka utumwani. (1 Wakorintho 5:7; Wagalatia 6:16) Ulingano huo kati ya Ukumbusho wa kifo cha Yesu na Sikukuu ya Kupitwa ya Wayahudi iliyofanywa kila mwaka, ni uthibitisho mwingine kwamba Ukumbusho huo unapaswa kuadhimishwa mara moja kila mwaka.

Isitoshe, Paulo alihusianisha kifo cha Yesu na sherehe nyingine ya Siku ya Kufunika ambao Wayahudi walifanya kila mwaka. Kwenye andiko la Waebrania 9:25, 26, tunasoma: “Wala si ili [Yesu] ajitoe mwenyewe mara nyingi, kwa kweli kama vile kuhani wa cheo cha juu huingia katika mahali patakatifu kutoka mwaka hadi mwaka [kwenye Siku ya Kufunika] kwa damu isiyo yake mwenyewe. . . . Lakini sasa amejidhihirisha mwenyewe mara moja kwa wakati wote kwenye umalizio wa mifumo ya mambo ili kuweka mbali dhambi kupitia dhabihu yake mwenyewe.” Kwa kuwa dhabihu ya Yesu ilichukua mahali pa Siku ya Kufunika iliyoadhimishwa mara moja kila mwaka, kwa kufaa Ukumbusho wa kifo chake unaadhimishwa mara moja kila mwaka. Hakuna sababu ya Kimaandiko ya kuadhimisha Ukumbusho huo zaidi ya mara moja kila mwaka.

Kupatana na hilo, mwanahistoria John Laurence von Mosheim anaripoti kwamba Wakristo wa karne ya pili huko Asia Ndogo walikuwa wakiadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu “siku ya kumi na nne ya mwezi wa kwanza wa Wayahudi [Nisani].” Ni katika miaka ya baadaye tu kwamba dini zinazojiita za Kikristo zilianza kuadhimisha Ukumbusho huo zaidi ya mara moja kila mwaka.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Linganisha masimulizi kwenye 1 Samweli 1:3, 7, BHN. Andiko hilo linatumia usemi “kila mara” (kulingana na tafsiri ya kisasa ya Kiebrania) unaomaanisha matukio yaliyotokea “mwaka baada ya mwaka,” au mara moja kila mwaka, wakati Elkana na wake zake wawili walipoenda kwenye hema la kukutania huko Shilo.