Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kabla na Baada ya Kujifunza Biblia—Neno la Mungu Lina Matokeo

Kabla na Baada ya Kujifunza Biblia—Neno la Mungu Lina Matokeo

“Mkaribieni Mungu, Naye Atawakaribia”

Kabla na Baada ya Kujifunza Biblia—Neno la Mungu Lina Matokeo

TONY alikuwa kijana mvulana mjeuri asiye na adabu, aliyetembelea mitaa iliyochakaa huko Sydney, Australia, kwa ukawaida. Baadhi ya marafiki wake walikuwa washiriki wa magenge ya mitaani. Mara nyingi walihusika katika wizi, mapigano kati ya magenge, na kufyatuliana risasi mitaani.

Tony alianza kuvuta sigara alipokuwa na miaka tisa. Alipokuwa na miaka 14 alikuwa akitumia bangi kwa ukawaida na aliishi maisha mapotovu kiadili. Alipokuwa na miaka 16, alitumia dawa ya kulevya aina ya heroini kwa ukawaida, na jambo hilo lilifanya aanze kutumia kokeini, LSD, “nilitumia dawa yoyote ile ambayo ingefanya nilewe,” Tony anaeleza. Kisha alianza kufanya magendo ya dawa za kulevya kwa kushirikiana na mashirika mawili ya wahalifu yaliyokuwa mabaya sana. Muda si muda, Tony akawa mmojawapo wa walanguzi wanaotegemeka zaidi wa dawa za kulevya kwenye pwani ya mashariki ya Australia.

Utumizi wa dawa za kulevya aina ya heroini na bangi ulimgharimu Tony dola 160 hadi dola 320 (za Marekani) kila siku. Lakini familia yake ilipata madhara makubwa zaidi. Anasema hivi: “Mimi na mke wangu tulitishwa mara nyingi na wahalifu wenye bunduki na visu waliotafuta fedha na dawa za kulevya tulizokuwa nazo nyumbani.” Baada ya kufungwa gerezani mara tatu, Tony aliona uhitaji wa kuchunguza maisha yake.

Ijapokuwa alienda kanisani kwa ukawaida, Tony hakuweza kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu anayesemekana kuwa anawaadhibu wakosaji kwa kuwateketeza katika moto wa mateso milele na milele. Hata hivyo, alipotembelewa na Mashahidi wawili wa Yehova, Tony alishangaa kujua kwamba Mungu hatesi watu. Na Tony alifurahi kujua kwamba angeweza kurekebisha maisha yake na kupata baraka za Mungu. Tony alivutiwa na maneno haya ya Yesu Kristo: “Mambo yote yawezekana kwa Mungu.” (Marko 10:27) Tony aliguswa hasa na maneno haya yenye kutia moyo: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.”—Yakobo 4:8.

Sasa ikambidi Tony arekebishe maisha yake ili yapatane na kanuni za Biblia. Anasema hivi: “Kwanza niliacha kuvuta sigara. Nilikuwa nimeshindwa kuacha zoea hilo ijapokuwa nilikuwa nimejaribu mara nyingi. Yehova alinipa nguvu ya kuacha kutumia dawa za kulevya za heroini na bangi ambazo nilikuwa nimezitumia kwa miaka 15 iliyopita. Sikuamini kwamba ningeweza kuacha mazoea hayo.”

Badala ya kuamini kwamba Mungu huwatesa watu milele katika moto, jambo ambalo Biblia haifundishi, Tony na mke wake walikuja kuamini kwamba wataweza kuishi milele katika paradiso duniani. (Zaburi 37:10, 11; Mithali 2:21) Tony anasema hivi: “Ilichukua muda mrefu na ilikuwa vigumu kwangu kurekebisha maisha yangu ili yapatane na kanuni za Mungu, lakini Yehova amenibariki na nimefaulu.”

Naam, mtu huyo aliacha kutumia dawa za kulevya, akawa Mkristo. Yeye na mke wake wametumia maelfu ya saa na mali zao katika kazi ya kufundisha Biblia bila malipo. Pia wanajitahidi kulea watoto wao wawili katika njia ya Mungu. Badiliko hilo kubwa liliwezekana kwa nguvu isiyozuilika ya Neno la Mungu, Biblia. Ni kama mtume Paulo anavyosema: “Neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu.”—Waebrania 4:12.

Baadhi ya watu huteta bila msingi kwamba kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kufundisha Biblia inaharibu familia na maadili ya vijana. Bila shaka kisa cha Tony kinaonyesha kwamba shtaka hilo ni la uwongo.

Sawa na Tony, wengi wameona kwamba wanaweza kuacha mazoea yenye kufisha. Jinsi gani? Kwa kumwamini Mungu na kumtegemea yeye na Neno lake, na vilevile kwa msaada wa marafiki Wakristo wenye upendo wanaojali. Tony anamalizia kusema hivi kwa furaha: “Nimeona jinsi kanuni za Biblia zimewalinda watoto wangu. Mafundisho ya Biblia yameokoa ndoa yangu. Na majirani wangu hulala salama kwa kuwa hawaniogopi tena.”

[Blabu katika ukurasa wa 9]

‘Kwa nguvu ya Yehova, nilifaulu kuacha kutumia dawa za kulevya ambazo nilikuwa nimezitumia kwa miaka 15’

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Kanuni za Biblia Zinazosaidia

Kanuni mbalimbali za Biblia zimewasaidia watu wengi kuacha kutumia dawa za kulevya. Zifuatazo ni baadhi ya kanuni hizo:

“Tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na wa roho, tukikamilisha utakatifu katika hofu ya Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Kutumia dawa za kulevya kunavunja sheria ya Mungu.

“Kumcha BWANA ni mwanzo wa hekima; na kumjua Mtakatifu ni ufahamu.” (Mithali 9:10) Staha kwa Yehova na ujuzi sahihi kumhusu yeye na njia zake umewasaidia wengi kuacha kutumia dawa za kulevya.

“Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:5, 6) Inawezekana kuacha mazoea yenye kudhuru kwa kumwamini Mungu kwa moyo wote na kumtegemea kabisa.